SEHEMU YA 18
Baada ya kupita miezi sita tena huku akiwa barani Asia ndipo akatumiwa meseji katika akaunti yake ya WhatsApp, harakaharaka akaifungua na kuisoma, alitumiwa kupitia namba ngeni na ujumbe aliotumiwa ulikuwa mfupi tu uliosomeka ‘Miladiva’.
Kitu cha kwanza kabisa kumjia kichwani mwake kilikuwa ni kukumbuka kitu kilichotokea kwenye ufukwe huo. Alikumbuka kwamba mara ya mwisho kwenda katika ufukwe huo ni miezi kadhaa iliyopita ambapo alikwenda pamoja na familia yake.
Hakujua ujumbe huo ulimaanisha nini lakini alipouliza, akatumiwa ujumbe mwingine mfupi uliosomeka ‘Nipigie’, hapo ndipo akakumbuka, picha ya mwanaume tata yule aliyemwambia ampigie ikamjia kichwani mwake, hakutaka kuchelewa, akamtumia meseji ya kulalamika kwamba ilichukua muda mrefu mpaka kumtafuta.
“Nilikuwa bize sana. Ila nimekumiss baba watoto,” aliusoma ujumbe huo, mwili ukamsisimka.
“Kweli?” aliuliza.
“Ndiyo! Naomba nikuone jamani!” aliusoma ujumbe huo ambao uliambatanishwa na sauti iliyorekodiwa, alipoifungua, ilikuwa sauti ya mwanaume huyo iliyokuwa ikilalamika kimahaba, tena mbali na hiyo, alimwambia kwamba alihitaji mpenzi wa kudumu kwani wapenzi wote aliokuwa nao waliishia kumtenda tu, hawakuwa na mapenzi ya dhati.
“Nipo kwa ajili yako! Nitakulinda mpenzi! Naomba kuonana nawe nikifika Tanzania,” alimwambia.
“Kwani upo wapi?”
“Nipo Kuwait, kuna kitu nimefuata.”
“Basi sawa baba watoto! Nakupenda!”
“Nakupenda pia. Mwaaaaah!”
“Mwaaaah!”
Wakaagana, Godfrey hakuamini kama aliwasiliana na mwanaume tata huyo, alibaki hotelini huku akiwa amechanganyikiwa kwa furaha, aliinuka na kuanza kurukaruka, alikuwa na hamu ya kupata mawasiliano na mwanaume huyo na mwisho wa siku alipigiwa na hivyo kuwa na namba yake.
Wakati akiwa anafurahia akasikia simu yake ikilia na alipoifungua akakutana na picha za kihasarahasara alizotumiwa katika akaunti yake ya WhatsApp ambazo zilimuonyesha mwanaume huyo akiwa katika mikao ya hatarihatari.
Japokuwa alikwenda Kuwait kukaa kwa wiki moja na kutakiwa kwenda nchini Uingereza lakini wiki moja akaiona kuwa kama mwaka, kila siku kazi yake ilikuwa ni kuangalia kalenda, hakukuwa na kipindi alichokiona siku kwenda taratibu kama kipindi hicho.