Machaku, Yondani chali, Dihile, Kazimoto waula Send to a friend Tuesday, 15 March 2011 21:13
kocha wa timu ya taifa,Taifa Stars, Jan Poulsen
Sosthenes NyoniKOCHA wa timu ya taifa,Taifa Stars, Jan Poulsen ametangaza kikosi cha wachezaji 23 kitakachojiandaa kwa mchezo dhidi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati na kuwaacha Salum Machaku na Kelvin Yondani.
Mbali ya kuwaacha nyota hao Poulsen amewaita kwa mara ya kwanza nyota wa JKT Ruvu kiungo Mwinyi Kazimoto na kipa Shaaban Dihile waliokuwa nje ya kikosi hicho kwa zaidi ya miezi 8 tangu kuoondoka Mbrazil Marcio Maximo.
Akitangaza kikosi hicho kwenye ofisi za Shirikisho la Soka nchini TFF, Poulsen alitetea uamuzi wake wa kumuita mshambuliaji mkongwe Athuman Machupa kwa kusema uzoefu wake una umuhimu katika kujenga ari ya kikosi kwa kuwa anajua nini anachokifanya.
"Tunahitaji kuchanganya wachezaji ili kuwapa uzoefu wale chipukizi ili waweze kujifunza kwa wale wachezaji wazoefu,"alisema Poulsen.
Mdenmark huyo amemwacha beki wa Simba, Kelvin Yondan, kipa wa Majimaji, Said Mohamed na mshambuaji wa Mtibwa Sugar, Salum Machaku aliyekuwa moja ya nguzo muhimu kwenye kikosi cha Kilimanjaro Stars kilichotwaa ubingwa wa Kombe la Chalenji mwishoni mwaka jana.
Pia, amewachagua Shaban Kado na Mbwana Samata katika kikosi chake ili hali anajua wazi wachezaji hao wamo katika kikosi cha timu ya taifa ya vijana chini ya miaka 23, Ngorongoro Heroes kinachojiandaa na mechi dhidi ya Cameroon.Poulsen alisema kuwa timu zote hizo ni muhimu, lakini duniani kote timu ya taifa ya wakubwa ni muhimu zaidi.
Kwa mara ya kwanza Mdenmark huyo amewaita Kazimato na Dihile ambao waliwahi kuichezea Taifa Stars ilipokuwa ikinolewa na Marcio Maximo.Akizungumzia uamuzi wa Poulsen, kocha wa JKT Ruvu, Charles Kilinda alisema amefurahishwa na uteuzi wa wachezaji wake wawili Dihile na Kazimoto na kumtaka kuongeza idadi ya wachezaji kutoka kikosi cha maafande hao.
"Nimefurahi, kwanza nasema alikuwa hatutendei haki, alichelewa sana kuwaita, lakini Poulsen aangalie uwezekano wa kuongeza wengine kwani nina wachezaji wengi mahiri,"alisema Kilinda.
Naye Dihile aliyeiongoza Stars kucheza hatua ya mtoano ya michuano ya CHAN mwaka 2009 alisema; "Nimefurahi kwa sababu mwalimu ameona nafaa na mimi naahidi sitamuangusha nitajitahidi kadri ya uwezo wangu kwa kushirikiana na wenzangu kuhakikisha tunaisaidia timu ifikie malengo yake.
Kwa sababu Mungu ndiye muweza wa yote na kila kitu ni juu yake hata hilo suala zima la ushindani wa makipa katika timu ya taifa yeye mwenyewe ndiye atafanikisha,alieleza Dhile.Akizungumzia mchezo wa Machi 26, Poulsen alisema ni dhahiri utakuwa mgumu ukizingatia uzuri wa wapinzani wao Jamhuri ya Afrika ya Kati ambao wanaongoza kundi hilo na walipata ushindi ugenini dhidi ya Algeria.
"Tunahitaji pointi nne ili tujiweke katika nafasi nzuri ya kufuzu,tunafahamu wazi kwamba Jamhuri ya Afrika ya Kati si timu rahisi, waliifunga Algeria kwao, lakini na sisi tunataka ushindi pia, hivyo tutahakikisha tunashinda mechi hiyo,"alisema Poulsen.
Kikosi kamili kilichotangazwa jana mbele wa Wanahabari ni makipa Shaaban Kado, Juma Kaseja na Shaaban Dihile wakati mabeki ni Shadrack Nsajingwa, Aggrey Morris, Nadir Haroub'Canavaro', Stephano Mwasika,Haruna Shamte, Juma Nyoso na Idrisa Rashid.
Viungo ni Nurdin Bakari, Shaaban Nditi, Jabir Aziz, Henry Joseph, Abdi Kassim na Mwinyi Kazimoto huku washambuliaji ni Dan Mrwanda, Nizar Khalfan, Mrisho Ngassa, Mohamed Banka, Athumam Machupa, John Boko na Mbwana Samata.
Wakati huo huo; Salome Millinga anaripoti kuwa timu ya soka ya vijana U-23, Ngorongoro Heros leo itashuka dimbani uwanja wa Uhuru kucheza mechi yake ya kirafiki dhidi ya Azam FC kabla ya kuifuata Mtibwa Sugar, Machi 18 mjini Morogoro.
Akizungumza na Mwananchi, kocha Ngorongoro Heroes, Jamhuri Kihwelu alisema anategemea mechi hizo mbili zitamsaidia kujua mapungufu ya kikosi chake kabla ya safari ya Cameroon."Pia, tunasubiri majibu kutoka Shirikisho la soka Uganda kama timu yao itakuja huku kwa ajili ya mechi ya kirafiki au tutaenda kwao kucheza na timu ya U23 ya kwao," alisema Kihwelu.