Wakati tukijiandaa kwa maadhimisho ya miaka hamsini tangu kupata uhuru wa kisiasa,
inasikitisha kuona sehemu kubwa ya utajiri na rasilimali ya Tanzania iliyopaswa kuwa ni
kwa ajili ya mafao ya wengi, inaendelea kuwanufaisha wachache ndani ya jamii, kinyume
kabisa na mipango na mikakati iliyowekwa na waasisi wa Taifa hili, wakati wa kupigania
uhuru; misingi ya uadilifu, uzalendo na umoja wa kitaifa inazidi kumong'onyoka siku hadi
siku, hali ambayo inasababisha kustawi kwa ubinafsi, ufisadi na kinzani za kijamii.
Tanzania kadiri ya vigezo vya Mashirika ya Fedha ya Kimataifa ni kati ya nchi masikini zaidi
duniani, lakini imekuwa na mvuto mkubwa kwa wawekezaji kutoka sehemu mbalimbali za
dunia, wanaokimbilia nchini kutafuta madini.
Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, Tanzania imefanikiwa kuuza dhahabu yenye thamani
ya zaidi ya dola bilioni mbili nukta tano, lakini, cha kushangaza imeambulia dola milioni mbili
nukta saba, hali inayoonesha kimsingi, ukosefu wa haki na usawa katika soko la kimataifa.
Matajiri wanaendelea kufaidika na mikataba ya madini, wakati kuna mamilioni ya watu wanaokufa
kwa baa la njaa, umasikini na magonjwa, katika maeneo haya yenye rasilimali na utajiri mkubwa
kiasi hiki.
Baadhi ya watu wanaendekeza rushwa na ufisadi; maadui wakuu wa haki na usawa kama
alivyobainisha Mwalimu Nyerere wakati fulani. Masuala haya yameleta mpasuko wa kijamii ambao
kwa sasa ni hatari kubwa kwa ustawi na maendeleo ya Watanzania.
Mikataba ya madini, imeendelea kuwanufaisha wawekezaji kutoka nje ya nchi na wananchi wa
Tanzania kuendelea kuogelea katika umasikini wa kipato, licha ya kuzungukwa na utajiri wa
rasilimali. Uchumi wa Tanzania utaendelea kudidimia, ikiwa kama hatutarudisha uzalendo wa
kuipenda nchi yetu.
Rushwa na ufisadi vinaendelea kuota mizizi katika mioyo ya watu, jambo ambalo itakuwa vigumu
kulifuta kwa kipindi kifupi, kama ilivyo dhana ya udini, iliyoibuliwa na baadhi ya wanasiasa kwa
mafao yao binafsi.
Hivi tufanye nini jamani? Naomba mchango wenu wakuu...