Kwenye nchi hii kukamatwa hakutegemei mtu kuwa na kosa la jinai. Kama ni hivyo Kamanda Kamuhanda angekuwa amekamatwa kwa kuwa tume ya haki za binadamu ilimuona amehusika katika mauaji ya Mwangosi. Akili ya kawaida inaweza kukutuma kuamini kuwa kushinda kwake ubunge na kauuli zake za hivi karibuni dhidi ya mkuu wa nchi zinatosha kuwafanya wasaidizi wake kumkamata. Kama tatizo ni yaliyotokea chuoni kulikuwa na sababu gani kwa mfano ya kulichukua gari lake kituoni? Na kama anahusishwa na vurugu za wanachuo ni mtu gani mwenye weledi wa kawaida tu asiyeona ukosefu wa kusoma saikolojia ya watu ulivyosababisha kauli za mkuu wa mkoa kuzua tafrani iliyotokea. Lema anachukiwa, Lema anawindwa, na wanaofanya hivyo wamekosa busara ya kufanya matendo hayo bila kujulikana. Nguvu inayotumika kwa Lema haifanani na kosa linalotajwa. Polisi wetu lini wataacha kushughulika mambo madogo ya kudhaniwa tu na kuanza kushughulikia mamabo halisi yenye ushahidi. Wameshindwa "kuwatambua" na kuwashughulikia wang'oa kucha na meno wa Ulimboka na Kibanda na kuanza kushughulikia video za kwenye Youtube, Wameacha kushughulikia vifo vyenye utata vya wanachuo wawili - (ambalo ndilo dai la wanachuo lililozua yote haya), wanamshughulikia Lema, kana kwamba hiyo ndiyo inayojibu hitaji la wanachuo. Kama wanachuo wasingezuiwa na Lema wakaandamana hadi kwa Mkuu wa mkoa wangekuwa na kosa lipi la kumkamatia Lema? Wangemkamata kwa sababu hakuwazuia waandamanaji? Au kwa kuwa mauaji yametokea kwenye eneo lake? Hawa viongozi wetu kwa nini wanatumia nguvu kubwa zaidi kwa mambo yenye sababu dhaifu na kuacha yenye sababu nzito zilizo wazi? Mungu ibariki Tanzania