Hata mimi nilikuwa na wasi wasi kama wewe, lakini taarifa za vyombo vya Dola zilisema walikuwa watu zaidi ya 800, katika hali ya kawaida hakuna majambazi wanoweza kufikia idadi kama hiyo, maana wataonekana hadharani ilhali majambazi wanatakiwa kujificha ili wasionekane. Ni kweli kwamba mgodi unatakiwa kulindwa kama mabenki au Kampuni yoyote yenye vito vya thamani. Lakini katika historia ya nchi yetu hakuna benki iliyowahi kuvamiwa na majambazi 800 au zaidi.
Kulingana na uelewa wangu hawa waliouwawa Nyamongo, ningeweza kuwaita wavamizi, lakini pia najiuliza kulikoni hadi watu 800 wavamie eneo ambalo wanafahamu kuwa lina ulinzi mkali? Kumbuka kuwa mgodi wa North Mara unalindwa na makundi mawili la kwanza ni Askari Polisi/FFU na la pili ni Askari wa Mgodi tena nao wana sila wanaoitwa "Mobile".
Nilipotafakari mambo yote hayo, nikaona kwamba hadi kufikia watu 800 kwenda kuvamia sehemu kama hiyo hata kama walitaka kuiba, maana yake ni kwamaba wamekata tamaa na wanaenda lolote liwe. Kwa maana nyingine ni kwamba wamefikia kikomo cha uvumilivu na hali ya eneo hilo, hivyo, wanahitaji kusikilizwa na mabadiliko kufanyika. KUFIKIA HAPO, NAMI NIKAWAITA WANAMAPINDUZI.