Traxtion
JF-Expert Member
- Dec 10, 2021
- 5,895
- 11,788
Wakuu Tanzania ni nchi kubwa sana na ina resources nyingi sana. Kwa muda mrefu nimekuwa nikiwaza sana hivi tukianza kuwa makini na resources zetu hatuwezi kujikomboa kutoka kwenye umasikini kweli?
Hii Tanzania ina ardhi kubwa sana, kuna madini, ardhi yenye rutuba, vyanzo vya maji, watu wengi, vivutio vya utalii na kadhalika
Mawazo yangu ni kwamba kama serikali ikiamua kushirikiana na wananchi basi umasikini kwisha habari yake, na sasahivi Bongo tuna wasomi wengi sana na ni vijana, hakika kama vijana wakishirikiana na serikali basi tunaweza kuijenga Tanzania mpya.
Serikali inaweza kununua matrekta makubwa hata buku hivi kutoka Marekani, Ujerumani na India na kuwapa vijana wasomi wa Kitanzania wayatumie kulima mashamba makubwa sana ambayo yatakuwa yanamilikiwa na serikali.
Kuna matrekta yana nguvu sana na ni ya kisasa kabisa, mfano trekta la Maxxum 150 hp lina uwezo wa kubeba majembe 50 kwa wakati mmoja unakuta trekta limeenda round chache umeshalima hekari kibao
Mashamba yakiwa mengi na makubwa Watanzania wengi sana watanufaika. Mfano Kilombero kuna mashamba mengi ya miwa na yameajiri Watanzania 4000, ili kuweza kupata miwa inayotumika kiwanda cha sukari Kilombero.
Leo hii serikali ikianzisha mashamba ya pamba au miwa au koroshi nk itaajiri vijana waliohitimu Agricultural Engineering, Computer Science, Chemical Engineering, watu wa biashara, arts nk na wasomi tunao wengi. Aidha na wale watu wasiosoma wanahitajika pia katika mashamba hayo.
Unakuta kama shamba la miwa Kilombero limeajiri Watanzania 4000 maana yake tukiwa na mashamba mia moja kama hayo tutaajiri Watanzania laki 4.
Fikiria hii, Tanzania ina mpango wa kuwa Tanzania ya viwanda, kama tukianza kuzalisha pamba kwa wingi kule Kanda ya Ziwa tunaweza pia kuanzisha viwanda vya nguo hapahapa nchini na kwa kuwa malighafi tunayo basi tunaweza kutengeneza nguo nyingi na watu waliosomea Industrial Engineering, Mechanical, sijui Business Administration, Electrical Engineering wote watanufaika na kuanzishwa kwa viwanda hivi
Tukiwa na mashamba makubwa ya miwa tutaongeza viwanda vya sukari, tukiwa na mashamba mengi ya alizeti tutaongeza viwanda vya kukamua mafuta ya alizeti, tukiwa na mashamba makubwa ya karanga tutaongeza viwanda vya siagi na kukamua mafuta ya karanga nk
Kuna mikoa kama Mbeya hapa Tanzania mazao mengi ya chakula yanastawi vizuri sana kuanzia mpunga, mahindi, maharage, kunde, mboga za majani kila kitu kinastawi. Huu mkoa na maeneo mengine yanayofanana na Mbeya tunaweza kuitumia vizuri sana kulisha Tanzania na nchi jirani. Serikali inaweza kutuma wanauchumi nchi nyingine za Africa kama DRC, Kenya, Burundi, Malawi, Zambia, Botswana, Mozambique, Botswana nk kwenda kuongea biashara vizuri na kusaini mikataba ili kupata ruhusa ya kuwauzia bidhaa zetu nyingi za kilimo na kupata soko kirahisi. Kwa hali hii utasaidia hata kupunguza njaa nchi jirani na kuongezea kipato Watanzania
Mkoa wa Morogoro una mito mingi sana. Maana yake ni kwamba kuna vyanzo vya maji kila kona hususani vijijini. Maji haya tunaweza kuyatumia kufanya kilimo cha kisasa cha umwagiliaji kwa kutumia teknolojia ya hali ya juu. Hii itatuwezesha kulima hadi kiangazi bila kutegemea mvua. Itasaidia kwa kiasi kikubwa na kama Tanzania tutakuwa na mazao mengi tutafungua fursa nyingine nyingi za kiuchumi
Kwa sasa kwenye kilimo kuna changamoto nyingi, mfano Lindi na Mtwara wakulima wanalima korosho wanauza kwenye vyama vya kilimo halafu serikali inanunua kilo moja ya korosho kwa bei ya chini, hii inakatisha sana wakulima tamaa kwa sababu faida inakuwa ndogo na inafanya wengine kukata tamaa ya kuingia kwenye kilimo.
Serikali ya Tanzania inapaswa kuwa namba moja kwenye ku support efforts za wakulima na pia kuhamasisha matumizi ya teknolojia kwenye kilimo ili tuanze kuwa na KILIMO CHA KISASA. Tuache kutegemea mvua na tuifanye ardhi yetu kubwa ya Tanzania iliyo na rutuba itumike kuongeza ajira kwa raia wa taifa letu pendwa
Kama tukiwekeza vizuri kwenye Kilimo basi fursa nyingi za Kiuchumi zitaongezeka
Idadi ya magari yanayosafirisha mazao kutoka eneo moja hadi lingine itaongezeka kwa hiyo Watanzania wengi wataajiriwa kama madereca wa magari haya na wengine watamiliki makampuni ya kusafirisha mazao
Idadi ya wakulima successful itaongezeka, na watu wakitajirika nchini ndio mwanzo wa kufungua fursa nyingine mfano baadhi ya watu wakipata pesa za kutosha watajenga hoteli, lodges mbalimbali, wengine watanunua mabasi, wengine wataanzisha supermarket, wengine watajenga shule na private sector itakuwa nchini maana haya yote watakayojenga maana yake ni kwamba wamesaidia watu wengi kupata ajira pia maana hoteli zinahitaji kuajiri watu, mabasi yanahitaji madereva, supermarket zinahitaji watu pia yani kazi zitaongezeka
Na serikali ikiajiri watu milioni 4 kwenye kilimo kwa haraka haraka unaweza ukadhani umeokoa watu milioni 4 kutoka kwenye umasikini, ila kiuhalisia umeokoa watu zaidi ya milioni 10 kutoka kwenye umasikini, kwa sababu hawa watu wana familia zao zinazowategemea maana yake wakipata kipato inasaidia watu kama watano hivi kuwa na maisha mazuri maana unakuta nyumbani wana watoto, unakuwa umeeakomboa hawa watoto kutoka kwenye umasikini pia, na kupitia ajira nyingine za usafirishaji, viwanda, biashara nk ambavyo vinakuwa facilitated na kilimo basi unakuwa umesaidia kundi kubwa la watu kupata ajira
Hiko ni kilimo tu, Tanzania inaweza kuwekeza uchumi wake kwa asilimia kubwa kwenye rasilimali mbalimbali kama rasilimali watu, madini, vyanzo vya maji, ardhi nk
Hii itasaidia sana nchi yetu kukua kwa kasi kiuchumi na kusaidia sekta nyingine za kiuchumi nazo zifanye vizuri. Watu wengi wakiona wanaweza kupata maisha mazuri hapahapa Tanzania basi yale mawazo ya kuikimbia nchi hii yatapungua, wengi watabaki hapa huku wanalisaidia taifa kimaendeleo
Mimi nahisi kama tatizo la ajira tukiwa serious kuna namna nyingi tu tunaweza kulipunguza tukitumia vizuri rasilimali zetu