Mauaji ya Patrice Lumumba 1961

Mauaji ya Patrice Lumumba 1961

LUMUMBA AONDOLEWA MADARAKANI, ATOROKA - 7


Agosti 21, 1960 Waziri Mkuu wa Congo, Patrice Lumumba aliomba waziwazi msaada wa kijeshi Urusi. Siku tano baadaye, Agosti 26, baada ya kukataliwa na majeshi ya Umoja wa Mataifa (UN) kuishughulikia Kasai Kusini iliyojitenga, Lumumba alituma majeshi ya Congo yanayomtii kwenda Kasai Kusini.

Wanajeshi hao walikuwa katika ndege 15 za kijeshi za Urusi na malori 100. Nia ya Lumumba ni kulirejesha jimbo lililojitenga. Kufikia hatua hiyo, Allen Dulles alimtumia Devlin ujumbe akimwelekeza amuue Lumumba.

Mwishoni mwa Agosti maofisa wa Urusi waliwasili Congo. Kwa kuona Lumumba alikuwa akiegemea sana ushauri na misaada kutoka Urusi, Rais Joseph Kasavubu alianza kuingiwa na wasiwasi.

Septemba 5, Rais Kasavubu akamfukuza kazi Lumumba kama Waziri Mkuu wa Congo. Wakati huo huo Lumumba naye akamfukuza kazi Rais wake, Kasavubu. Kwa hiyo walifukuzana kazi, Kasavubu alimteua Joseph Ileo kuwa waziri mkuu badala ya Lumumba.

Septemba 9, hata baada ya kudaiwa kufukuzwa kazi, Lumumba aliidhinisha malipo ya dola milioni moja kwa wanajeshi wa Leopoldville (sasa Kinshasa). Mgogoro wa uongozi ukaongezeka kati ya Lumumba na Kasavubu.

Baada ya vuta nikuvute kati ya Lumumba na Kasavubu, mgogoro ukafikia kilele chake Septemba 5, 1960. Mgogoro ulisababishwa na kutoelewana kati ya Lumumba na Kasavubu kuhusu namna ya kushughulikia Jimbo la Katanga lililojitenga na Congo.



Siku hiyo serikali ya Congo ikapasuka vipande viwili. Kasavubu akamfukuza Lumumba kazi ya uwaziri mkuu na kuliomba jeshi la UN lichukue madaraka ya utawala Congo. Baraza la Mawaziri la Lumumba nalo likamfukuza Kasavubu kama Rais wa nchi, likimtuhumu kwa uhaini.

Septemba 14, 1960, kikao cha pamoja cha Baraza la Congo kikapiga kura na kumkabidhi Lumumba madaraka ya kuongoza nchi hadi hapo mgogoro wa uongozi utakapomalizika na tume ya kibunge ndiyo ambayo ingemwongoza.

Hadi hapo kulikuwa na kambi mbili za serikali, moja ya Joseph Ileo (baadaye alibadili jina na kujiita Sombo Amba Ileo) ambaye aliteuliwa na Kasavubu kama Waziri Mkuu badala ya Lumumba. Kambi nyingine ni ya Lumumba ikiwa na baraka za tume ya Bunge.

Katika kuhakikisha viwanja vya ndege na redio havitumiwi vibaya, majeshi ya UN yalivitwaa lakini hata baada ya Baraza la Congo kupiga kura kumpa Lumumba mamlaka ya kuendelea kutawala, siku hiyo hiyo, Jumatano ya Septemba 14, Mobutu alitangaza anatwaa madaraka ya nchi hadi Desemba 31 ili kuwapa muda Lumumba na Kasavubu waafikiane. Kisha akateua serikali ya mpito.

“Kuanzia sasa,” alisema Mobutu, “Kasavubu na Lumumba hawako madarakani... ni mpaka mwishoni mwa Desemba watakapokubaliana namna ya kuongoza pamoja.

Baada ya Mobutu kuwatoa madarakani Kasavubu na Lumumba, Kasavubu alikimbilia Brazaville kujificha wakati Lumumba akibaki Leopoldville kwenye nyumba ya makazi ya waziri mkuu akilindwa na majeshi ya Mobutu asitoroke.

Mkono mrefu wa Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA) ulionekana. Mwandishi James Hunter Meriwether katika ukurasa wa 218 wa kitabu chake, ‘Proudly We Can be Africans: Black Americans and Africa, 1935-1961’ anaandika: “Katika kipindi chote cha misukosuko, maofisa wa Serikali ya Marekani walikuwa katika jitihada kubwa ya kumhamisha Mobutu, msaidizi binafsi wa Lumumba kabla bosi wake hajamteua kumfanya mnadhimu wa jeshi, kumhamishia kwenda kambi ya Kasavubu. Saa chache baada ya Kasavubu kutangaza kuliahirisha Bunge, Mobutu alitwaa madaraka kwa jina la jeshi.

“Aliahidi ‘kubatilisha’ nyadhifa za Kasavubu, Lumumba, Ileo na wanasiasa wengine hadi mwisho wa mwaka (1960). Aliwaita wanafunzi wa Chuo Kikuu Congo na wahitimu wengine wa vyuo kuendesha serikali. Aliwafukuza mabalozi wa Urusi na Czechoslovakia. Siku chache baadaye wakati CIA ilipomtahadharisha Mobutu juu ya njama za kumuua, Mobutu alibadilika, akaanza kuegemea upande wa Kasavubu aliyefuata matakwa ya nchi za Magharibi.

“Aliwaambia maofisa ubalozi wa Marekani kuwa angemkamata Lumumba na kuweka madaraka mikononi mwa serikali ya Ileo-Kasavubu mwishoni mwa Oktoba. Hata hivyo Mobutu hangeweza kumkamata Lumumba kwa sababu Lumumba alikuwa nyumbani kwake akilindwa na UN. Kwa hiyo, majeshi ya Mobutu walimzuia Lumumba asiondoke kwenye nyumba hiyo.”

Septemba 19 ‘Tume ya Wanavyuo’, ikiwa na wahitimu zaidi ya 30, ikaundwa ili kuendesha serikali ya mpito. Kuanzia hapo kamatakamata ilianza. Kasavubu aliondoka kwenda New York, Marekani kuhudhuria mkutano wa Baraza la Usalama la UN. Huko alitoa hotuba yake Novemba 8 na alitambuliwa kama Rais wa Congo licha ya kwamba Mobutu alijitangaza yuko madarakani na serikali ya mpito.

Novemba 27, 1960, siku ambayo Kasavubu alirejea kutoka New York, alikopeleka malalamiko yake UN na kisha akapokewa kwa shangwe na wanasiasa kadhaa wa Congo, ndiyo siku ambayo Lumumba aliondoka Leopoldville kwenda Stanleyville (Kisangani) kuanzisha upya mapambano ya kisiasa.

Hadi Novemba 27 alikuwa chini ya ulinzi wa UN nyumbani kwake Leopoldville lakini aliruhusiwa kutoka na kurudi nyumbani.

Akiwa nyumbani kwake, Lumumba aliona shamrashamra za mapokezi ya Kasavubu zikiendelea. Waliokuwa wamezingira eneo zilipokuwa zikifanyika shangwe hizo ni askari wa Mobutu.

Lumumba aliona atumie fursa hiyo kutoroka na kwenda Stanleyville ambako Antoine Gizenga, aliyekuwa naibu wake, alikuwa akiwaandaa wapambanaji ili kujipanga upya. Alitoroka kwake bila askari wa Mobutu kugundua.

Baada ya kuona kuwa hangeweza tena kurudi madarakani kwa njia za kawaida, hasa baada ya kurejea kwa Kasavubu kutoka UN, Lumumba aliona njia pekee ya kutwaa madaraka ni kuitwaa Leopoldville akitokea Stanleyville.

Wanasiasa wengine saba waliokuwa tayari kujiunga na Lumumba na waliokuwa kwenye baraza lake la mawaziri ni Christophe Gbenye, Joseph Mbuyi, Maurice Mpolo, Anicet Kashamura, Pierre Mulele na aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu, Barthelemy Mujanay. Msafara wao ulikuwa wa magari matatu, mojawapo liliibeba familia yake.

Baada ya Kasavubu na Mobutu na Wamarekani na Wabelgiji kugundua Lumumba ametoroka na familia yake, walianza kumsaka.

Viongozi wa Leopoldville walinuia kumkamata kwa gharama zozote. Shirika la huduma za kijasusi la kikoloni nchini Congo la Surete, chini ya Victor Nendaka Bika, liliingia kazini kumsaka Lumumba. Mkuu wa CIA Congo, Larry Devlin, na mshauri wa Kasavubu wa masuala ya usalama, Andre Lahaye, walishirikiana kikamilifu na taasisi ya Nendaka.

Ubelgiji walitoa ndege ndogo za kuruka karibu na usawa wa ardhi. Mbelgiji mshauri wa Mobutu, kanali Louis Marliere, alisambaza askari wa kuweka vizuizi barabarani na kwenye mito iliyofikiriwa Lumumba angeweza kupitia.

Mvua iliyokuwa inanyesha na vizuizi vya barabarani vilipunguza kasi ya Lumumba kutoroka. Kilichomchelewesha zaidi ni kusimama karibu kila kijiji alipowaona watu na kuanza kuwahutubia.

Huku akiendelea kusalimiana na watu kila alikopita, inaelekea Novemba 30 waliokuwa wanamtafuta wakiwa angani waliuona msafara wake. Kesho asubuhi, Alhamisi, alipita njia-panda ya mji wa Port Francqui karibu na mpaka wa Leopoldville na Kasai.

Itaendelea
 
LUMUMBA AKAMATWA BAADA YA KUTOROKA, ATESWA - 8




Alhamisi ya Desemba mosi, 1960, Patrice Lumumba, alikamatwa na majeshi ya serikali ya Congo baada ya kutoroka. Alikamatiwa eneo la Mweka, Jimbo la Kasai alipokuwa akielekea Stanleyville (sasa Kisangani) baada ya kutoroka Leopoldville (sasa Kinshasa) alikokuwa chini ya ulinzi wa Umoja wa Mataifa (UN), lakini akilindwa na majeshi ya Mobutu.

Ingawa msafara wao ulikuwa na watu kadhaa waliokuwa wakitoroka naye, ni Christophe Gbenye, Anicet Kashamura (aliyekuwa Waziri wa Habari) na Pierre Mulele (Waziri wa Elimu) tu walifanikiwa kumaliza safari yao.

Lumumba, Maurice Mpolo (aliyekuwa Waziri wa Vijana na Michezo) na Joseph Akito (makamu rais wa Baraza la Seneti) walikamatwa na kurejeshwa Kinshasa, lakini Joseph Mbuyi na Barthelemy Mujanay (aliyekuwa Gavana wa Benki Kuuo) waliuawa katika Jimbo la Charlesville.

Siku iliyofuata, wanajeshi 40 walimtoa Lumumba kutoka eneo walilomkamata la Lodi-Mweka na kumsafirisha kwa njia ya barabara hadi uwanja mdogo wa ndege wa Port Francqui ambako alisafirishwa kwa ndege kurudishwa Kinshasa ambapo waliwasili saa 11:00 jioni. Muda wote wakiwa angani, Lumumba na wenzake walikuwa katika mateso makubwa hadi ndege ilipotua na wao kuteremshwa na kupakiwa kwenye lori.

Lumumba alitoroka Kinshasa kwa kutumia gari aina ya Peugeot 403, mali ya mtu aliyeitwa Kamitatu Cleophas na ilikuwa ikiendeshwa na Mungul Diaka.

Johannes Fabian, mwandishi wa kitabu cha “Remembering the Present: Painting and Popular History in Zaire (uk 115)”, anasimulia kuwa Lumumba alikuwa katika gari hiyo ya rangi nyeusi, ingawa mwandishi mwingine, Anna Purna, katika ukurasa wa 285 wa kitabu “Dr. Lumumba’s Dream of Incest”, anasema gari hilo ni Peugeot lakini la rangi nyeupe.



Sehemu ya simulizi ya tukio hilo inasema baada ya kuvuka Mto Sankuru, alirudi kumchukua mkewe Pauline Opango Lumumba, na mtoto wao wa mwisho, Roland, waliokuwa ng’ambo ya mto, na ndipo alipokamatwa.

Wenzake, akiwamo Pierre Mulele, waliovuka mto na Lumumba, walifanikiwa kufika salama Port Francqui Desemba mosi.

Ijumaa, Desemba 2, 1960, muda mfupi kabla ya saa 11:00 jioni, ndege ya Congo DC-3 ilitua uwanja wa ndege wa Ndjili mjini Kinshasa. Ndani yake alikuwamo ofisa usalama wa Congo, Gilbert-Pierre Pongo, Lumumba na wanajeshi.

Pongo ni mmoja wa maofisa usalama wa serikali ya Congo waliomfuatilia Lumumba hadi kumkamata.

Umati wa watu uwanjani hapo ulikuwa ukisubiri kuona wanaoshuka kwenye ndege hiyo. Miongoni mwa waliokuwa kwenye umati huo ni waandishi wa habari, wapigapicha, maofisa wa serikali na wa jeshi la ANC.

Lumumba alikuwa wa pili kushuka, akiwa nyuma ya Pongo ambaye sasa alionekana kama shujaa kwa kuwezesha kukamatwa kwa Lumumba. Mikono ya Lumumba ilifungwa nyuma kwa kamba. Picha zilizopigwa siku hiyo zinamuonyesha alikuwa amevaa shati jeupe.

Lumumba na mateka wengine wawili walisukumwa kuingia kwenye lori kusubiri safari nyingine. Mwandishi wa kitabu cha “The Assassination of Lumumba”, Ludo de Witte anaandika kuwa kwa faida ya wapigapicha, mwanajeshi mmoja alimkamata Lumumba na kunyanyua kichwa chake juu ili apigwe picha.

Kwa mujibu wa kitabu hicho, mwangalizi mmoja wa UN aliyekuwa uwanjani hapo, alisema Lumumba alipoteza miwani yake na shati lake lilitapakaa damu, na kulikuwa na damu iliyovia kwenye shavu lake la kushoto.

Mateka hao walipelekwa kambi ya jeshi ya Binza karibu na makazi ya Mobutu. Waandishi waliokuwa kambini hapo wakati Lumumba anawasili, walisema alikamatwa na kuonyeshwa kwa wapigapicha ili apigwe picha. Wakati huo Mobutu naye alikuwa akiangalia.

Baadaye alitupwa ardhini huku akipigwa na wanajeshi waliomzunguka. Kisha Pongo akapaza sauti kuwataka wanajeshi hao wazidi kumpiga.

Baada ya kumkamata Lumumba, Pongo alipandishwa cheo na kuwa kapteni. Alitumwa kwenda Bukavu, lakini huko alikamatwa.

Januari mosi, 1961, siku 16 kabla Lumumba hajauawa, Pongo alitumwa na Mobutu kuongoza shambulio kwenye mji wa mpakani wa Bukavu, ikiwa ni jaribio la kulirejesha eneo hilo kwenye himaya ya Mobutu. Hata hivyo, alikamatwa na kuwekwa mahabusu katika mji wa Kisangani na mahabusu wengine ambako maofisa walitoa sharti la kumuachia kama Lumumba naye angeachiwa. Lumumba hakuachiwa na hivyo Pongo naye hakuachiwa.

Februari 20, 1961, ikiwa ni siku tatu baada ya Lumumba kuuawa, Pongo na wenzake 14 waliuawa na wafuasi wa Lumumba.

Wakati wakiwa bado wanamshikilia na kumtesa Lumumba, mwanajeshi mmoja alisoma ujumbe ulioandikwa kwenye karatasi ukidaiwa kuwa uliandikwa na Lumumba mwenyewe akidai kuwa yeye ndiye kiongozi halali wa serikali ya Congo.

Baada ya kuusoma ujumbe huo, mwanajeshi mmoja aliichukua karatasi hiyo, akaikunjakunja na kuisukumiza mdomoni mwa Lumumba. Baada ya hapo Lumumba alipelekwa chumba kingine ambako mateso dhidi yake yaliendelea.

Siku hiyo usiku, mkuu wa Idara ya Usalama ya Congo, Victor Nendaka, alimpeleka Lumumba mahabusu. Kwa mujibu wa Alfred Cahen, mwanadiplomasia kijana aliyewasili Congo muda mfupi baada ya Lumumba kushushwa kwenye ndege na ambaye alikuwa rafiki wa karibu wa Nendaka, alisema baadaye Nendaka alimwambia kuwa alimfungia Lumumba kwenye gereji ya aliyekuwa mkuu wa ujasusi katika serikali ya kikoloni, Kanali Frederic Vandewall.

Aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Ubelgiji, Pierre Wigny, alikaririwa akisema Desemba 3 alipokea telegramu kutoka ubalozi wa Ubelgiji mjini Brazzaville.

“Alitendwa kikatili sana usiku wa tarehe 2 kuamkia 3 na makomando waliochoma hata ndevu zake,” unasema ujumbe huo.

Bomboko aliingilia kati kutuliza hasira, lakini hakufaulu. Kwa mujibu wa walioshuhudia, “waliomtesa Lumumba ni watu wakatili sana”.

Justin Marie Bomboko Lokumba ni mwanasiasa wa Congo ambaye hakuaminiwa na Lumumba. Akiwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Congo, alishiriki katika kukamatwa kwa Lumumba.

Ujumbe huo kwa njia ya telegramu ulitumwa na Robert Rithschild akiwa ubalozi wa Ubelgiji mjini Kinshasa. Katika ujumbe mwingine alioutuma Brussels siku hiyo, Rothschild alisema: “Hatua muhimu zinachukuliwa kuhakikisha kuwa Kasavubu anawadhibiti mahabusu.”

Vyombo vya habari vya kimataifa vilipiga picha wakati Lumumba akiadhibiwa na askari wa Congo katika uwanja wa ndege wa Ndjili na kisha kwenye kambi ya Binza.

Balozi wa Marekani nchini Congo, Clare Hayes Timberlake, alituma telegramu kwenda kwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Christian Archibald Herter, akimsihi ajitahidi kuzuia kusambaa picha za mateso ya Lumumba kwa sababu “zinaweza kutengeneza bomu la atomiki”.

Picha hizo zilianza kutia simanzi na hasira maeneo mengi ya dunia ambako zilionekana kwenye vyombo vya habari.

Wanasiasa kadhaa walianza kutilia shaka uwezo wa UN, wakihoji wanawezaje kuwalinda Wabelgiji walioko Congo lakini wanashindwa kumlinda Lumumba anayekubaliwa na Bunge na wabunge wa nchi yake.

Nchi kadhaa za Afrika zilitishia hata kuondoa wanajeshi wao katika jeshi la UN lililokuwa Congo, UNOC.

Hata hivyo UN haikushinikiza Lumumba aachiwe, pamoja na kukiri alikuwa na kinga ya Bunge.

Majeshi ya UN hayakufanya chochote zaidi ya kutazama hali ilivyokuwa inakwenda nchini Congo kuhusu Lumumba.

Itaendelea
 
LUMUMBA AANDIKA BARUA UN, AELEZA ANAVYOTESWA - 9



Pamoja na kwamba majeshi ya Umoja wa Mataifa yalikuwa Congo kulinda usalama, hayakuingilia kati kwa muda wote ambao Patrice Lumumba alikuwa akiteswa. Huenda hii ni kwa sababu Ubelgiji na Marekani hazikumtaka Lumumba. Akiwa mahabusu alifanikiwa kuandika barua mbili kwa msaada wa wanajeshi waliokuwa wakimtii. Endelea…



Jumamosi ya Desemba 3, Patrice Lumumba alihamishwa na wanajeshi na kupelekwa kambi ya Hardy iliyoko Thysville. Kwa mujibu wa waandishi wa habari waliokuwapo wakati wa kuhamishwa huko, Lumumba alionekana kuwa na maumivu makali kiasi kwamba alipata shida kupanda lori, na uso wake ulikuwa na alama za vipigo.

Kambi hiyo ilikuwa chini ya Kanali Louis Bobozo. Bobozo, ambaye ni mpwa wa Mobutu, baadaye akawa mkuu wa majeshi ya Congo kuanzia 1965 hadi 1972. Alikuwa ni sajenti tu wakati Congo ikipatia uhuru lakini alipandishwa vyeo haraka.

Katika kambi hiyo kulikuwa na mahabusu wengine wa kisiasa, mmoja wao ni Georges Grenfell ambaye alikuwa waziri katika serikali ya Lumumba.

Aliyekuwa mwakilishi wa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN) nchini Congo, Balozi Rajeshwar Dayal, aliandika kuhusu hali ya Lumumba. “Inasemekana ana maumivu makali yanayotokana na majeraha aliyopata alipowasili. Kichwa kimenyolewa nywele na bado mikono yake imefungwa kwa nyuma. Amefungiwa kwenye mahabusu ambayo haina hadhi ya utu na ni hatari sana kwa afya,” aliandika.

Telegramu ambayo Dayal alimtumia katibu mkuu wa UN, Dag Hammarskjold Desemba 5, iliripoti mazungumzo yaliyofanyika.

“Wanajeshi wa Morocco walioko UN Congo kambi ya Thysville wameripoti kuwapo majadiliano makali kati ya ANC (Jeshi la Congo) kuhusu wanavyomtendea Lumumba. Mabishano hayajatulia,” alisema.


Desemba 22, Dayal alituma ujumbe mwingine kwenda UN ukisema: “Uhalifu unaoendelezwa kwa Lumumba umeanza kuwakera (Kasavubu na Mobutu) kwa sababu umeanza kuwagawa wanajeshi.”

Januari 4, 1961, zikiwa ni siku 13 kabla ya kifo chake, Lumumba alifanikiwa kupenyeza barua mbili kutoka rumande. Ya kwanza ilikuwa ni ujumbe kwa viongozi wa UN, ambayo alieleza hali halisi ya mahabusu ya Camp Hardy.

“Niko hapa na wengine saba waliokuwa wabunge, miongoni mwao ni rais wa seneti, M. Okito (akimaanisha Joseph Okito) mfanyakazi wa serikali na dereva. Jumla yetu tuko 10. Tumewekwa hapa tangu Desemba 2, 1960. Chakula tunacholetewa mara mbili kwa siku ni kibaya sana,” aliandika Lumumba.

“Kwa siku nne sijala zaidi ya ndizi. Nimemweleza daktari wa Msalaba Mwekundu aliyeletwa kuniona; kanali wa Thysville alikuwapo. Nimetaka niletewe matunda ... Ingawa daktari aliruhusu, wanajeshi wa hapa wamekataa wakisema wana amri kutoka juu, kwa Kanali Mobutu.

“Madaktari wameelekeza tutembee [mazoezi] kila jioni nje ya mahabusu, lakini kanali na mkuu wa wilaya wamekataa. Nguo nilizovaa kwa siku 35 hazijaoshwa. Nimezuiwa kuvaa viatu. Kwa ufupi tunaishi katika hali isiyovumilika. Zaidi, sijapata taarifa zozote za mke wangu na familia yangu na sijui waliko. Nilipaswa nitembelewe naye, kama ilivyo katika sheria za Congo.”

Katika barua ya pili aliyomtumia mpwa wake aliyeitwa Albert Onawelo, Lumumba alitoa maelezo ya ziada kuhusu hali yake, pia akaelezea msaada fulani alioupata kutoka kwa baadhi ya wanajeshi.

“Niko hapa na wasaidizi saba, mmoja wao ni Joseph Okito. Tumefungiwa mahabusu gizani mfululizo tangu Desemba 2, 1960. Chakula tunachopewa (chikwangue na wali) unakera na ni kichafu na naweza kukaa siku tatu hadi nne bila kula. Kwa kweli hali ni mbaya kuliko hata wakati wa ukoloni. Kama akitokea askari akatupa ndizi za ziada, anakamatwa na kuadhibiwa. Pamoja na tabu zote kuna baadhi ya wanajeshi wanakuja kwa siri kunisaidia,” aliandika.

Mwisho wa barua hiyo, Lumumba alionyesha pia kuhusu mke wake wa tatu, Pauline Kie “anaendelea vizuri na hufika kila mara na kuwaachia ujumbe (wa Lumumba) wanajeshi walio upande wetu”.

Mwanzoni mwa Januari 1961, katibu mkuu wa UN, Dag Hammarskjold alizuru Congo na kujikuta akipokewa kwa maandamano ya wafuasi wa Lumumba.

Wakati mwanaharakati Cleophas Kamitatu alipojaribu kumpa Hammarskjold barua kutoka kwa Lumumba iliyoelezea hali katika mahabusu walimoshikiliwa, alionyesha kukasirika na kumwelekeza ampatie msaidizi wake.

Kamitatu, kwa kukasirishwa na majibu aliyopewa na Hammarskjold, naye aliandika barua yake yenye maneno yanayofanana na yale ya Lumumba.

“M. Lumumba amekuwa akiteswa kikatili kwa siku 35. Kwa siku zote hizo ameruhusiwa kuoga mara tatu tu. Anapewa chakula kinachostahili kupewa mbwa... Nguo alizovaa zimekaa mwilini kwa siku 35. Anaishi shimoni. Hakuwahi kufikishwa mahakamani, na hata mkewe amezuiwa kumwona,” aliandika.

Ingawa barua hizo ziliwafikia maofisa wa UN nchini Congo, hawakuchukua hatua yoyote kurekebisha hali ya mambo.

Hali ya wasiwasi ilikuwa ikizidi kutanda katika kambi aliyowekwa Lumumba na wenzake. Msaidizi wa Kanali Bobozo, Luteni Jacques Schoonbroot, alikuwa anasisitiza kuwa ghasia zinazozuka zinasababishwa na itikadi za kisiasa na kwamba kulikuwa na kikundi cha wanajeshi wa Congo katika kambi hiyo kilichomtii Lumumba.

Jumanne, Desemba 27 Kanali Bobozo aliarifiwa na msiri wake kuwa huenda Lumumba angetoroka au kutoroshwa. Aliamua mwenyewe kwenda kumfungia Lumumba na kuondoka na funguo.

Siku hiyo usiku alikwenda tena mwenyewe mahabusu alimofungiwa Lumumba kuwazuia makumi ya wanajeshi waliokuwa wamepanga kumtoa.

Kwa mujibu wa Luteni Schoonbroot kama alivyokaririwa na kitabu cha “Assassination of Lumumba”, Kanali Bobozo aliwaambia wanajeshi hao akisema “nyiye hamna la kufanya. Kama mnataka kumuachia mfungwa yeyote, labda muanze kwanza kuniua mimi.” Baada ya kauli hiyo, wanajeshi hao walianza kuondoka mmoja baada ya mwingine.

Siku iliyofuata walikamatwa baadhi ya wanajeshi kutokana na jaribio lao la kumtoa Lumumba mahabusu. Baadaye ukazuka uvumi kwamba Lumumba alikuwa anatendwa vizuri mahabusu na alikula sikukuu ya Krismasi na maofisa wa kambi hiyo.

Luis Lopez Alvarez, raia wa Hispania aliyekuwa rafiki wa karibu na Lumumba, alikaririwa na Stephen Weissman katika kitabu cha “American Foreign Policy in the Congo 1960-1964”, akisema Lumumba alimlaumu sana balozi wa Marekani Congo kwa kuonekana kukaa upande wa watesi wake.

Wakati hayo yakiendelea, serikali ya Ubelgiji ilikuwa na hofu sana na Lumumba kiasi kwamba ilituma ujumbe wa telegramu kwenda Kinshasa ikiwasisitiza “watilie maanani hatari ambayo ingesababishwa na Lumumba ikiwa ataachiwa huru”. Siku iliyofuata ukatumwa ujumbe kwa njia ya telegramu kutoka Congo kwenda Ubelgiji ukisema serikali ya Mobutu isingeruhusu Lumumba kuachiwa huru.

Muda mfupi baadaye, maofisa wa Congo mjini Kinshasa walianza kutafuta namna ya kumpoteza kabisa Lumumba.

Jumapili ya Januari 8, 1961, wanasiasa wawili wa Congo; Albert Delvaux na Cyrille Adoula walikwenda Katanga kuzungumza na rais wa eneo hilo, Moise Tshombe, kuhusu kumhamishia Lumumba huko.

Siku iliyofuata, wanasiasa wa Congo walishauriana na Rais Joseph Kasavubu na mkuu wa majeshi, kumhamisha Lumumba. Kamishna wa Ulinzi wa Congo, Fredinand Kazadi alisema kuhamishwa kwa Lumumba ni kwa muhimu sana ili kuepusha machafuko yaliyokuwa yananukia Thysville.

Siku iliyofuata, kamishna wa mambo ya ndani, Damien Kandolo, aliondoka kwenda Boma kwa ajili ya maandalizi hayo. Ubelgiji ilikuwa ikifuatilia kwa karibu hatua zote hizi.

Kulingana na simulizi za G. Heinz na H. Donnay katika kitabu cha “Lumumba: The Last Fifty Days”, aliyekuwa kiungo kati ya watesi wa Lumumba na serikali ya Ubelgiji ni Andre Lahaye, Mbelgiji aliyekuwa mshauri mkubwa wa mkuu wa Idara ya Usalama ya Congo, Victor Nendaka.

Aliyesaini barua ya kumtaka Nendaka amtoe Lumumba Thysville na kumpeleka Katanga ni Rais Kasavubu. Mpango wa usafiri wa ndege uliandaliwa na Kandolo Damien.

Kuanzia hapo Lahaye alifanya kazi kubwa akituma taarifa za mara kwa mara na hatua kwa hatua kwenda Brussels kwa lengo la kuelezea namna Lumumba alivyokuwa anashughulikiwa.

Itaendelea
 
MIPANGO YA KUMHAMISHA LUMUMBA GEREZA YAIVA - 10





Wakati Lumumba akiwa bado mikononi mwa watesi wake, Rais Kasavubu wa Congo alikuwa kwenye shinikizo kali kuhusu hatima ya Lumumba.

Kwa kuona hivyo, Januari 2, 1961, Kasavubu aliitisha mkutano ambao ungewajumuisha wanasiasa mbalimbali wa Congo. Pia wanasiasa wa Afrika na Asia waliokuwa wafuasi na watetezi wa Lumumba, walikuwa wanakutana Casablanca wakitaka aachiwe mara moja.

Kuongezea uzito wa hilo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Dag Hammarskjold alipanga kurudi tena Congo Januari 10. Viongozi wa kisiasa wa Congo waliogopa kwamba kama wangemwachia huru Lumumba, huenda UN wangeshinikiza arudi madarakani.

Mapema asubuhi ya Januari 13, nidhamu katika kambi ya Camp Hardy ilianza kutoweka. Wanajeshi wa kambi hiyo walikataa kupokea amri yoyote kutoka kwa wakubwa zao hadi walipwe stahiki zao, baadhi yao wakitaka Lumumba aachiwe huru.

Baadaye siku hiyo hali ilivyozidi kuwa mbaya Kasavubu, Mobutu, Bomboko na Nendaka waliitana na haraka kuelekea kambini kujadiliana na wanajeshi hao.

Baadaye ukazuka uvumi kwamba Januari 14, Lumumba angekuwa huru na hivyo wanajeshi wanaomtii waliokuwa Katanga wangekuwa njiani kuelekea Kinshasa.

ADVERTISEMENT

Wanajeshi waliokuwa Katanga tayari walishateka eneo lote la kaskazini hata kabla machafuko ya Thysville. Viongozi walishahamishia familia zao Brussels, Ubelgiji.

Januari 13, mkuu wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) nchini Congo, Lawrence Raymond Devlin, alituma ujumbe Marekani akisema serikali ya Congo inaweza kuanguka wakati wowote na kama Marekani hawatachukua hatua za haraka, maslahi yake nchini humo yatakuwa hatarini. Nchini Ubelgiji, mikutano ya haraka ilifanyika kuhusu hali ya kisiasa ya nchi hiyo.

Mwandishi wa habari, Kwame Afadzi Insaidoo katika ukurasa wa sita wa kitabu chake cha “Ghana: A Time to Heal & Renew the Nation” amelikariri jarida la The Economist la Februari 24-Machi 2, 2007, Vol. 382, No. 8517, ukurasa wa 95, kuhusu maendeleo ya hali nchini Congo.

“Bw. (Larry) Devlin alikula njama na mkuu wa jeshi la nchi, Joseph Mobutu, ambaye ni sajini aliyepandishwa cheo hivi karibuni, kumkamata Waziri Mkuu (Lumumba),” ameandika akinukuu jarida hilo.

Wakati Lumumba alipozidi kusababisha matatizo na nchi ikatumbukia kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe, Rais Dwight Eisenhower (wa Marekani) alitoa amri ya kumuua Lumumba, kwa mujibu wa Bw. Devlin.

Kwa mujibu wa kitabu “Betrayal of Trust: The Collapse of Global Public Health” cha Laurie Garrett, uamuzi wa Marekani kumuua Lumumba ulikuja baada ya mawasiliano ya mara kwa mara kati ya mkurugenzi mkuu wa CIA, Allen Dulles na mkuu wake katika kituo cha Congo, Larry Devlin.

Katika taarifa moja ya telegramu iliyotumwa Marekani, Devlin aliripoti kuwa “kuna jitihada za kuifanya Congo kuwa ya kikomunisti”.

Katika mkutano wa Baraza la Usalama wa Taifa la Marekani, ilitengenezwa mipango ya kuivuruga Congo kwa kutengeneza ghasia za mara kwa mara kiasi cha Lumumba kushindwa kutawala.

Kubwa zaidi lililofanyika ni kupandikiza mgogoro wa uongozi ambao hatimaye ulimfanya Lumumba kupoteza cheo chake.

Ghasia zilikuwa za mara kwa mara katika miji mingi ya Congo. Ghasia za Camp Hardy ziliwasukuma maofisa wa Congo kumhamishia Lumumba sehemu nyingine. Baadhi ya wanasiasa wa Katanga, Kasai na Kinshasa walihakikisha wanazuia njia zozote za kumwachia Lumumba.

Mipango ya kumtoa Lumumba mjini Kinshasa kwenda Katanga ilikamilika. Jimbo la Katanga lilikuwa linaongozwa na mmoja wa mahasimu wake kisiasa, Moise Tshombe.

Walioongoza kikao cha mipango ya kumhamisha ni Kandolo Damien na Andre Lahaye, Mbelgiji aliyekuwa mshauri mkubwa wa mkuu wa Idara ya Usalama Congo, Victor Nendaka.

Nendaka alikuwa ofisini kwake mjini Kinshasa wakati Kandolo alipomwendea akiwa na waraka ulioonyesha ratiba ya ndege itakayotumika. Andre Lahaye naye alikwenda ofisini kwa Nendaka alikokutana tena na Kandolo.

Kabla ya hapo, Jumanne ya Desemba 6, 1960, Kanali Joseph Mobutu aliitisha mkutano na waandishi wa habari na kuwaambia kuwa Lumumba yuko katika mikono salama.

Aliwaonyesha waandishi hao kile alichosema kuwa ni cheti cha daktari kinachoonyesha kuwa Lumumba yuko katika hali njema sana kiafya.

Aliwaambia Lumumba atashtakiwa kwa kosa la kusababisha ghasia katika jeshi na kuwatesa baadhi ya wabunge. Mobutu hakutaja tarehe ambayo Lumumba angeshtakiwa.

Januari 16, mkuu wa kikosi cha usalama, Victor Nendaka Bika, alikutana na wanasiasa wa Congo katika ofisi za Shirika la Ndege la Ubelgiji, Sabena, na kupanga kuwa watamhamisha Lumumba kutoka Bakwanga na kumpeleka Elizabethville.

Operesheni hiyo ingefanyika jioni. Hiyo ilikuwa ni siku moja kabla ya mauaji ya Lumumba. Wanasiasa wawili Fernand Kazadi na Jonas Mukamba walitakiwa washiriki kumsafirisha Lumumba.

Kushikiliwa kwa Lumumba kulianza kuitisha Ubelgiji tangu siku ile majeshi ya Mobutu yalipozingira makazi yake. Uvumi ulisambaa kwamba jimbo la Katanga lilitaka kubadilishana wafungwa na Kinshasa na kwamba Lumumba angekuwemo.

Uliposambaa sana uvumi huo, Waziri wa Mambo ya Afrika nchini Ubelgiji, Harold d’Aspremont Lynden aliwasiliana na maofisa wa serikali yake waliokuwa Congo akiwataka wazuie mazungumzo hayo.

Jumapili ya Januari 14, msiri na mtu wa karibu na Lynden aliyejulikana kwa jina la Meja Jules Loos, na ambaye ni mmoja wa walioshiriki njama za kumuua Lumumba, kwa mujibu wa kitabu “Patrice Lumumba, Ahead of His Time” cha Didier Ndongala Mumbata, alimpelekea Lynden mbinu nyingine za “kumalizana na Lumumba”.

Hiyo ni baada ya kukerwa na magazeti ya Congo kuhusu maasi ya kijeshi ya Thysville ambako Lumumba alikuwa anashikiliwa.

Loos alimshauri Luteni Kanali Louis Marliere, ofisa wa kijeshi wa Ubelgiji nchini Congo kumpeleka Lumumba Katanga kwa hasimu wake, Moise Tshombe.

Lynden alituma ujumbe wa siri kwa Luteni Kanali Marliere na Meja Loos akiwataka wahakikishe Lumumba anaondolewa na wampeleke sehemu nyingine ya siri, lakini yenye ulinzi mkali zaidi.

Januari 16 alimtumia Tshombe ujumbe akimsihi amchukue Lumumba na amshikilie huko Katanga. Hata hivyo ujumbe huo ulifika jioni wakati Tshombe alishafanya uamuzi wake.

Mipango ya kumpeleka Lumumba Katanga iliandaliwa Kinshasa. Tshombe alikubaliana nayo. Mmoja wa maofisa wa serikali aliyeidhinisha kuhamishwa kwa Lumumba na kupelekwa Katanga ni Albert Delvaux, ambaye awali alikuwa waziri wa Lumumba kabla ya mgogoro wa uongozi na alikuwa pia ni mmoja wa maofisa wa Kasavubu waliosaini kuondolewa kwa Lumumba na Justin Marie Bomboko mwaka 1960.

Baadaye Delvaux alikuwa waziri katika baraza la mawaziri la Joseph Ileo ambaye alikuja kuwa Waziri Mkuu wa Congo.

Katika kipindi chote cha mwanzoni mwa Januari 1961, Delvaux alikuwa na harakati nyingi za kuwaweka pamoja akina Kasavubu, Tshombe na Mobutu kuhusu suala zima la Lumumba.

Asubuhi ya Januari 16, wakati mshauri wa Kasavubu wa masuala ya usalama, Andre Lahaye na mkuu wa shirika la huduma za kijasusi la kikoloni, Victor Nendaka, wakijadiliana namna ya kumsafirisha Lumumba kumpeleka Katanga, aliyekuwa akisimamia mawasiliano baina ya Tshombe na Kasavubu ni Delvaux.

Hatimaye jioni ya Jumatatu ya Januari 16, muda mfupi baada ya tafakuri na majadiliano mengi, Nendaka alipanda ndege kuelekea mjini Thysville (sasa ni Mbanza-Ngungu) alikokuwa anashikiliwa Lumumba. Usiku wa siku hiyo alilala katika hoteli mojawapo ya mji huo.

Itaendelea
 
Back
Top Bottom