Mauaji ya Patrice Lumumba 1961

Mauaji ya Patrice Lumumba 1961

Johnny Sins

JF-Expert Member
Joined
Nov 4, 2019
Posts
2,536
Reaction score
3,883
OPERESHENI BARRACUDA ILIVYOMUUA LUMUMBA - 01


Alhamisi ya Juni 30, 1960, Congo ilijipatia uhuru kutoka kwa Ubelgiji. Waziri Mkuu Patrice Emery Lumumba akiwa na miaka 35, akawa kiongozi wa jamhuri hii mpya. Lakini hali ya amani na utulivu ikatoweka muda mfupi baadaye. Kikosi cha majeshi ya waasi kikazua vurugu kiasi kwamba Ubelgiji ilipeleka jeshi lake kulinda raia wake.

Siku chache baadaye, Jumatatu ya Julai 11, ya mwaka huo, Jimbo la Katanga, lililokuwa likiongozwa na Moise Kapenda Tshombe likajitenga. Umoja wa Mataifa ukaingilia kati kwa kutuma jeshi la kulinda amani.

Jumanne ya Januari 17, 1961, miezi sita tu baada ya uhuru wa Congo, Patrice Lumumba aliuawa katika Jimbo la Katanga. Februari 13, maofisa wa Jimbo la Katanga wakatangaza kifo cha Lumumba, lakini hakuna aliyewaamini. Hata wao hawakuziamini taarifa walizotoa. Lawama zikaanza kumiminika kutoka pande zote za dunia.

Urusi iliwashutumu mabeberu na kuitaka Marekani iondoe watu wake Congo, pia ikamtaka aliyekuwa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dag Hammarskjold, kujiuzulu kwa sababu alionekana kuwa kibaraka wa wakoloni.

Katika jiji la Moscow nchini Urusi watu waliandamana baada ya kupata taarifa za kuuawa kwa Lumumba. Katika jiji la Beijing, China, kulifanyika maandamano makubwa ya watu waliokadiriwa kuwa zaidi ya 100,000. Katika nchi mbalimbali raia walivamia balozi za Ubelgiji na kufanya uharibifu.

Ndani ya mwaka mmoja tangu kuuawa kwa Lumumba, Umoja wa Mataifa ulifanya uchunguzi na baadaye ikabainika kuwa hata Shirika la Kijasusi la Marekani (CIA) lilishiriki katika njama za kumuua Lumumba.

Katika ukurasa wa 198 wa kitabu “The African Liberation Struggle: Reflections” cha Godfrey Mwakikagile, jasusi wa Marekani, Stephen Andrew Lucas, ambaye alikuja Tanzania na kufundisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alikuwa Congo na kufanya kazi chini ya mkuu wa CIA, Larry Devlin, wakati Lumumba alipokamatwa na kuuawa. Mwingine aliyekuwa Congo na baadaye akaenda Zanzibar ni Frank Carlucci.

Pamoja na Lumumba walikuwako wengine wawili waliokamatwa na kuuawa pamoja naye; Joseph Okito (alikuwa Naibu Spika wa Bunge la Congo) na Maurice Mpolo (alikuwa Waziri wa Vijana na Michezo). Watatu hao walisafirishwa kwa ndege kutoka Kinshasa hadi mji mkuu wa Kalonji wa Bakwanga (sasa unaitwa Mbuji-Mayi).

Wakiwa kwenye ndege aina ya DC-3, wote watatu waliteswa kikatili na walinzi wa Congo. Ndege ilipowasili anga la Bakwanga, rubani hakuweza kutua kwa sababu uwanjani hapo kulikuwa kumetapakaa matanki ya ujazo wa galoni 55.

Rubani aliamua kwenda kutua Uwanja wa Elisabethville (sasa Lubumbashi), na ndege ilipotua, Lumumba alikuwa anakaribia kuzirai kutokana na maumivu.

Ndani ya ndege walikuwa wakiteswa mbele ya Kamishna wa Ulinzi wa Congo, Ferdinand Kazadi na Kamishna wa Mambo ya Ndani wa Congo, Jonas Mukamba. Walipofikishwa Lubumbashi walipelekwa kwenye nyumba jirani na Uwanja wa Ndege wa Luano na kuendelea kuteswa.

Lumumba, ambaye uso wake uliharibiwa kiasi cha kutotambulika kutokana na vipigo na nguo zake zikiwa zimetapakaa damu, alisimamishwa kwenye kichuguu kikubwa huku akimulikwa na taa za magari.

Kwa amri ya Moise Tshombe, rais wa jimbo la Katanga ambaye naye alikuwa akipokea maelekezo kutoka Brussels, Lumumba aliteswa. Kikosi cha mauaji kilimtoa Lumumba katika nyumba alimokuwa akiteswa na kumsafirisha kwa mwendo wa dakika 45 hadi Katanga.

Hapo aliuawa na kikosi cha mauaji kwa kupigwa risasi kwa amri ya Kapteni wa Ubelgiji, Julien Gat. Aliyemfyatulia risasi ni askari wa Ubelgiji, kanali Carlos Huyghe. Mwingine aliyeshiriki kuwafyatulia risasi na kuwaua Okito na Mpolo ni kapteni Julien Gat.

KUPOTEZA USHAHIDI.
Baada ya kuuawa kwa risasi, miili ya watatu hao ilizikwa eneo walilouawa. Kwa hofu kwamba kaburi la Lumumba lingegundulika na baadaye lingeweza kugeuzwa kuwa eneo la heshima, Wabelgiji na vibaraka wao waliamua kupoteza ushahidi ambao ungeweza kuelekeza uliko mwili wake.

Jumatano ya Januari 18, ikiwa ni siku moja baada ya mauaji hayo, miili ya kina Lumumba ilifukuliwa na kupelekwa ndani zaidi msituni na kuzikwa upya karibu na mpaka wa Rhodesia (Zimbabwe) na Congo.

Usiku wa Jumapili ya Januari 22 ndugu wawili wa Ubelgiji Kamishna wa Polisi wa Ubelgiji, Gerard Soete na ndugu yake walikwenda tena kufukua miili ya Lumumba, Okito na Mpolo. Safari hii walikuwa na shoka na misumeno.

Waliikatakata miili hiyo vipande vipande kabla ya kuyeyusha mabaki yake kwa tindikali iliyokuwa imejaa kwenye pipa la petroli la lita 200. Baadaye Soete alikiri kwamba alitumia koleo kung’oa meno mawili ya Lumumba kwa ajili ya ukumbusho.

OPERESHENI BARRACUDA.
Katika kitabu cha “Encyclopedia of leadership: A-E” (ukurasa 925), George R. Goethals na Georgia Sorenson wanasema mpango wa kumuua Lumumba uliitwa ‘Operesheni Barracuda’ na uliandaliwa na Marekani, hususan CIA, ndipo Lumumba akakamatwa na Kanali Mobutu Oktoba 10, 1960.

Katika kikao kilichofanyika jijini Washington, Marekani iliamriwa Lumumba aondolewe madarakani na awekwe kiongozi ambaye angekubali kulinda maslahi ya Wamarekani nchini Congo.

Maagizo hayo yakatumwa kwa mkuu wa CIA nchini Congo, Lawrence Raymond Devlin. CIA wakaunganisha nguvu zao na Ubelgiji.

Agosti 1960, msaada wa kijeshi kutoka Urusi uliingia Congo, jambo ambalo halikuwapendeza Wamarekani na Wabelgiji. Ilikuwa lazima Lumumba aondoke kwa gharama zozote.

Ndipo wakamshawishi Rais wa Congo, Joseph Kasavubu, lakini waligonga mwamba. Devlin akaripoti taarifa hizo makao makuu ya CIA jijini Langley, Marekani, Agosti 24, 1960.

Dk Sidney Gottlieb, mtaalamu wa dawa, akapewa maagizo ya kutafuta sumu ya kumuua Lumumba na isijulikane kuwa Marekani imehusika, na iwe ni dawa ambayo chanzo chake ni Afrika.
ITAENDELEA
 
LUMUMBA AFUNGWA GEREZANI MARA MBILI.


Katika robo ya mwisho ya karne ya 19, Uingereza, Ufaransa, Ujerumani, Italia na Ureno ziligawana bara la Afrika, lakini Mfalme Leopold II wa Ubelgiji ndiye aliyeichukua Jamhuri ya Congo na kuitawala.
Leopold II alikuwa mfalme wa Ubelgiji Desemba 10, 1865 hadi Desemba 17, 1909. Alimfuata baba yake Leopold I aliyekuwa mfalme wa kwanza baada ya kuanzishwa kwa taifa hilo.
Mwaka 1884, Marekani ililitambua “dola huru la Congo” chini ya mfalme huyo. Msingi wa yote haya uliwekwa katika Mkutano wa Berlin ulioanza Novemba 1884 kujadili kuigawa Afrika katika maeneo ya kiutawala. Ingawa aliitawala Congo na kufaidi utajiri wa rasilimali zake, Leopold hakuwahi kuikanyaga ardhi ya nchi hiyo.
Vuvumko la mataifa ya Kiafrika kujipatia uhuru lilianza katikati ya karne ya 20. Mwanadamu aliyekuja kuwa gumzo kubwa katika historia ya nchi hiyo ni Patrice Emery Lumumba aliyezaliwa Julai 2, 1925, wazazi wake wakiwa Francois Tolenga Otetshima (baba) na Julienne Wamato Lomendja.
Lumumba, aliyezaliwa katika familia ya Kikatoliki, ni wa kabila la Batelela. Alisoma shule za misheni na baada ya kufuzu masomo yake, alipata kazi ya ukarani wa posta.
Kazi hiyo ilimfanya ahame Kinshasa (wakati huo ikiitwa Leopoldville) kutokea Kasai. Baadaye alipanda cheo na kuhamishiwa posta ya Kisangani (wakati huo Kisangani ikijulikana kama Stanleyville). Maisha yake ya kisiasa yalianza 1955 alipoanza kushiriki harakati za kisiasa.

Jina lake halisi ni Elias Okit’ Asombo. Kwa mujibu Jonathan Reynolds katika kitabu chake, “30-Second Twentieth Century: The 50 Most Significant Ideas and Events, Each Explained in Half a Minute” (ukurasa wa 1885), maana ya jina hilo ni “mrithi wa aliyelaaniwa, ambaye atakufa mapema”.
“Baba yake alitaka (Lumumba) awe katekista,” anaandika Johannes Fabian katika kitabu chake cha “Remembering the Present: Painting and Popular History in Zaire”. Lakini baada ya kuelimika kiasi fulani, hakufuata njia hiyo aliyoitaka baba yake.
Alifukuzwa chuo cha kidini kwa sababu hakufuata sana mambo ya dini. Baadaye alijiunga na taasisi ya Kikatoliki ya Tshumbe-Sainte-Marie ambako pia alifukuzwa ndani ya mwaka. Baadaye alijiunga na Chuo cha Kimethodist cha utabibu, lakini huko pia alifukuzwa.
Baada ya hapo alirejea kijijini kwao na kufanya kazi yoyote aliyoipata huku akisoma karibu kila kitu alichokikuta katika maktaba ya Wembo-Nyama aliyokuwa akiitembelea mara kwa mara. Huko alikuwa akikutana na mwalimu wake wa awali, Joseph Logonya.
Baada ya kukaa kijijini muda mrefu, alihamia mjini na ndipo alipobadili jina, badala ya Elias Okit’Asombo, akaanza kuitwa Patrice Lumumba. Maisha yake mjini yalikuwa kati ya 1943 na 1956.
Lumumba alifanya kazi miezi minne katika kampuni ya kuchimba madini ya Symetian mjini Kalima jimbo la Maniema. Julai 1944 aliondoka na kwenda Kisangani.
Akiwa Kisangani alifanya kazi ya ukarani wa posta. Baada ya muda wa kazi alihudhuria masomo Marist Brothers ambayo ni moja ya shule za taasisi ya kidini ya Kikatoliki duniani.
Kwa kuvutiwa na utendaji kazi wake na bidii ya kusoma, wakubwa wake kazini walimpa cheo, kisha kumpeleka kituo cha kilimo cha Yangambi, karibu na mji wa Kisangani.
Mwaka 1947 alikubaliwa kujiunga na Chuo cha Posta cha Leopoldville. Kwa mujibu wa mwandishi Johannes Fabian, Lumumba alifaulu mitihani yake kwa kupata asilimia 94.4 na akapata ajira inayolingana na ya Wazungu waliokuwa wakifanya kazi Posta ya Congo.
Aliporudi Kisangani, akiwa ofisa mwandamizi wa posta, alikuwa akfanya mihadhara na kuandika. Alioa mwanamke kutoka kijiji alichozaliwa, lakini alikuwa na wanawake wawili awali; Mluba na mwingine Mcongo. Mwaka 1952 alikutana na kuanzisha urafiki na mwanasosholojia Mfaransa, Pierre Clement. Kwa mujibu wa kitabu “Lumumba: Africa’s Lost Leader” cha Leo Zeilig, Lumumba na Pierre walishirikiana kufanya tafiti za kijamii zilizomfumbua macho na kumfanya ajihusishe zaidi na harakati za kisiasa.
Mwaka 1954 alikutana na mwanasiasa wa Ubelgiji, Auguste Buisseret na kujiunga na jumuiya yao iliyokuwa Congo.
Katika kujihusisha na siasa, wanasiasa Ubelgiji walianza kuona changamoto kali kutoka kwake. Mawazo ya kuanza kumdhibiti yalianza baada ya ‘umachachari’ wake kuanza kuonekana bayana.
Julai 6, 1956 aliporejea kutoka Ubelgiji alikoalikwa na Buisseret kuzungumza katika jumuiya yao, alikamatwa mara aliposhuka kwenye ndege akituhumiwa kwa matumizi mabaya ya faranga 126,000 za Kifaransa za ofisi ya posta.
Alipopatikana na hatia alihukumiwa kifungo miaka miwili gerezani, lakini baadaye adhabu ilipunguzwa na kuwa miezi 18, lakini mwandishi Willame Jean-Claude katika kitabu chake, “Patrice Lumumba: The Congolese Crisis Revisited” anaamini kufungwa kwa Lumumba kulitokana na chuki na fitina za ajira zilizotengenezwa na Wazungu waliokuwa wakifanya kazi posta walipomwona anaelekea kuwazidi kitaaluma.


UMAARUFU WAONGEZEKA.
Kifungo hicho kilimfanya aanze kupata umaarufu zaidi hata nje ya Kisangani. Akiwa gerezani aliandika kitabu akidai Congo inahitaji ukombozi kamili.
Alitoka gerezani Juni 1958, akiwa tayari amepoteza kazi ya utawala katika Posta ya Congo. Kwa kuwa hakuwa na kazi nyingine Kisangani, aliamua kuhamia Kinshasa na kupata kazi ya usimamizi wa biashara katika kampuni ya bia ya Bas-Congo. Uvumi ukaibuka kuwa bia aina ya Polar inayotengenezwa na Bas-Congo ilikuwa ikiharibu nguvu za kiume. Alipambana na uvumi huo huku akijihusisha na siasa. Baadaye alijiunga na Joseph Ileo na Joseph Ngalula kuanzisha chama cha MNC (National Movement for Congo). Baada ya mwaka mmoja akawa kiongozi MNC. Agosti 1958 alichukua likizo na kwenda Brussels, Ubelgiji katika harakati za kisiasa.
Oktoba 5, 1958 alikiwakilisha chama hicho katika mkutano wa Waafrika uliofanyika Accra, Ghana. Kitendo cha kuhudhuria mkutano huo kilimfanya afahamike kwa wengi waliokuja kuwa viongozi wa nchi za Afrika baada ya uhuru.
Jumapili ya Januari 4, 1959 kulizuka ghasia za kisiasa katika Jimbo la Leopoldville. Ghasia hizo zilisababishwa na Waafrika waliotaka mabadiliko ya haraka. Walitaka uhuru bila kukawia. Vurugu zilizidi kusambaa maeneo mengine.
Vurugu hizo zilizuka katika mkutano wa hadhara wa MNC Oktoba 23, 1959 na kuchukua siku tano kutulia huku watu 30 wakiuawa.
Jumapili ya Novemba Mosi, Lumumba alikamatwa na serikali ya kikoloni na kuhukumiwa kifungo cha miezi sita gerezani. Tofauti na ilivyodhaniwa awali, kifungo hicho kiliongeza umaarufu wa Lumumba.
Itaendelea
 
SIKU 4 BAADA YA UHURU, WANAJESHI WAZUA GHASIA - 3



Januari 1960 Wabelgiji walilazimika kuita mkutano katika jiji la Brussels, Ubelgiji, katika mkutano huo maalum ndipo ilipokubaliwa Congo watapewa uhuru wao Juni 30 ya mwaka huo.
Baada ya ghasia zilizozuka Oktoba 23, 1959 na kudumu hadi Oktoba 28, 1959 na baada ya Patrice Lumumba kukamatwa na kuhukumiwa kifungo gerezani baada ya chama chake kusababisha ghasia hizo, Serikali ya Ubelgiji ilichapisha ripoti kuhusu ghasia hizo.
Jumapili ya Novemba 1, 1959 Lumumba alikamatwa na Serikali ya kikoloni na kumhukumu kifungo cha miezi sita gerezani. Tofauti na ilivyodhaniwa awali, kifungo hicho kiliongeza umaarufu wa Lumumba. Katika ghasia hizo iliripotiwa watu 30 waliuawa.
Theodore Trefon katika kitabu ‘Reinventing Order in the Congo: How People Respond to State Failure in Kinshasa’ anasema ghasia zilizokuwa mbaya zaidi katika historia ya Congo ni zile za kati ya Januari 4 na 6, 1959. “Karibu raia wote Waafrika waliingia mitaani kufanya vurugu”. Ghasia hizo zilianza polisi wa Ubelgiji walipovamia mkutano wa chama cha Abako na kuwatawanya wafuasi wake. Kwa mujibu wa andiko linaloitwa ‘The Congo Operation, 1960—63’ la Birendra Chakravorty, zaidi ya watu 100 waliuawa.
Hata kabla ripoti hiyo haijachapishwa, mkutano uliofanyika mjini Brussels, Ubelgiji na kumalizika Jumanne ya Januari 13, 1959 uliamua kwamba wakati wa Congo kupewa uhuru wake umefika.
Mpango wa kuwakabidhi Wakongo Serikali ya kujitawala wenyewe uliandaliwa tangu Desemba 1955 na kutangazwa Februari 1956. Aliyeifanya kazi hiyo ni Profesa wa Ubelgiji kutoka Chuo Kikuu cha Antwerp aliyeitwa Anton Arnold Jozef “Jef” Van Bilsen.

Mpango huo ulipewa jina la “Thirty Year Plan for the Politial Emancipation of Belgian Africa”.
Alipendekeza kuwepo mpango wa miaka 30. Pendekezo hilo la Desemba 1955 aliliita “Mpango wa Miaka 30”. Kwa maneno mengine, ikiwa ushauri wa Profesa Bilsen ungefuatwa, Congo ingejipatia uhuru wake mwaka 1985.
Karibu kipindi chote cha mwaka 1959 Congo iligubikwa na ghasia. Kuona hivyo, Januari 1960 Serikali ya Ubelgiji iliitisha mkutano mjini Brussels ambao vyama vyote vikubwa vya siasa na viongozi wa makabila makubwa ya Congo walihudhuria.
Mkutano huo ulitawaliwa na madai ya “uhuru sasa”. Baada ya shinikizo kuwa kubwa, Ubelgiji waliamua kwa shingo upande kuwapatia Wakongo uhuru wao ifikapo Juni 30 ya mwaka huo.
Wakati wa kampeni za uchaguzi za Aprili 1960 vyama vingi viligombea viti vya ubunge. Vyama vikubwa vilivyoshiriki uchaguzi huo ni MNC cha Patrice Lumumba kilichokuwa na sera ya kuiunganisha Congo yote iwe moja, na kingine ni kile cha Joseph Kasavubu cha Alliance des Bakongo (Abako).
Katika uchaguzi uliofanyika kuanzia Mei 11 hadi 25, 1960, Lumumba na waungaji mkono wake walipata ushindi mkubwa wa viti bungeni akifuatiwa na Kasavubu, wakalazimika kugawana madaraka. Kasavubu alikubali kuwa Rais wa nchi na Lumumba akiwa mtendaji mkuu wa serikali, yaani Waziri Mkuu.
Juni 23, 1960 Lumumba aliapishwa kuwa Waziri Mkuu wa Congo na, Juni 30, 1960, ikawa ndiyo siku ya uhuru wa Congo. Siku hiyo na siku tatu baadaye zikatangazwa kuwa siku za mapumziko ili raia washerehekee uhuru wao.
Katika sherehe hizo kila kitu kilionekana kufanyika katika hali ya amani. Ofisi ya Lumumba ilikuwa na shughuli nyingi huku kukiwa na msururu wa watu kuingia na kutoka huku Lumumba akijishughulisha na ratiba ndefu ya mapokezi ya wageni.
Siku ya uhuru Lumumba alitangaza kuwa Jumapili ya Julai 3 ingekuwa siku ya msamaha wa jumla kwa wafungwa wote. Lakini tangazo hilo halikutekelezwa na Julai 4, Lumumba aliita kikao cha Baraza la Mawaziri kujadili machafuko ya wanajeshi wa Congo.
Wanajeshi wengi waliokuwa na matumaini makubwa kwamba mara baada ya uhuru kupatikana wangepandishwa vyeo na kuongezewa maslahi, walianza kufanya fujo baada ya kuona matarajio yao hayatimii. Ingawa ilikuwa ndani ya wiki moja tu tangu uhuru kupatikana, baadhi yao waliona kuwa Lumumba hatimizi matarajio yao haraka kama walivyotarajia awali.
Bunge lililokutana katika kikao cha kwanza tangu uhuru na kuanza kazi ya kutunga sheria, kilipiga kura ya nyongeza yao ya mishahara. Lumumba alishtushwa na kitendo hicho cha Bunge lake. Kwa kujua hatari ambayo ingesababishwa na kitendo hicho, Lumumba alikiita “upumbavu wa uharibifu.”
Julai 5,, Kamanda wa Jeshi la Congo, Jenerali Emile Janssens, ambaye alikuwa Mbelgiji, aliwaita maofisa wa jeshi na kuwataka wadhibiti hali ya amani. Alisisitiza kuwa hali ilivyokuwa kabla ya uhuru ndivyo itakavyokuwa baada ya uhuru. Lakini tangazo hilo halikutuliza hasira ya baadhi ya wanajeshi.
Siku iliyofuata yaani Julai 6 ambayo ilikuwa siku ya sita tu baada ya uhuru Lumumba aliwapandisha vyeo askari wa Congo kwa ngazi moja lakini hali ya ghasia ilipozidi kuwa mbaya, Lumumba alimfukuza kazi Jenerali Janssens.
Siku mbili baadaye, Ijumaa ya Julai 8, Lumumba aliwaondoa maofisa wote wa kijeshi wa Ubelgiji na kuweka wa Congo ingawa Wazungu kadhaa waliendelea kubaki jeshini kama washauri.
Julai 9 Balozi wa Marekani Congo, Clare Hayes Timberlake, alituma taarifa kwenda Marekani, akidai Ubelgiji wakiingilia mgogoro wa Congo kutakuwa na maafa.
Julai 10 Ubelgiji walituma wanajeshi kwenda Congo kuwalinda raia wao na biashara zao. Kasavubu na Lumumba waliigeukia Marekani kuomba msaada wa kulipanga upya jeshi la Congo.
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Marekani ikasema Marekani iko tayari kusaidia lakini chini ya usimamizi wa Umoja wa Mataifa na uongozi wa Ubelgiji.
Julai 11 Moise Tshombe akatangaza kuwa Jimbo la Katanga limejitenga na Congo na kisha akalitangaza kuwa liko huru huku akiiomba Ubelgiji walitambue na wapewe misaada.
Jumanne, Julai 12 Kasavubu na Lumumba waliiomba Marekani msaada kudhibiti uchokozi wa Wabelgiji na siku hiyo hiyo baraza la mawaziri lilikutana bila Lumumba na Kasavubu kuwapo kwenye kikao, na wakaomba wapewe wanajeshi 3,000 wa Marekani.
Rais wa Marekani, Dwight David Eisenhower, aliamuru vikosi vya nchi yake, vikiwa na zana za kivita, kwenda Congo ikiwa Waziri Mkuu wa Urusi, Nikita Krushchev, angetuma majeshi yake kwenda huko.
Jumatano, Julai 13, Urusi iliutaka Umoja wa Mataifa kuzuia uchokozi wa Ubelgiji nchini Congo. Alhamisi ya Julai 14 Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio la kupeleka jeshi Congo. Siku hiyo hiyo Lumumba na Kasavubu wakawasiliana na Urusi na kuwaomba wafuatilie hali ya Congo. Urusi ilikubali.

Ijumaa, Julai 15, majeshi ya Umoja wa Mataifa yaliwasili Congo. Julai 16, baada ya kukutana na Lumumba, mwakilishi wa Umoja wa Mataifa nchini Congo, Ralph Bunche, aliripoti “Lumumba alikuwa kama kichaa na alitenda mambo kwa tabia za kitoto.” Lumumba na huyo Bunche hawakuelewana vizuri.
Baada ya hali kuzidi kuwa mbaya, Jumapili ya Julai 17 Lumumba alitishia kuwa atayaita majeshi ya Urusi ili yasaidie kuyaondoa majeshi ya Umoja wa Mataifa kama watashindwa kuyaondoa majeshi ya Ubelgiji ndani ya saa 72.
Itaendelea….!
 
Back
Top Bottom