Mama yangu adui yangu

Mama yangu adui yangu

story imeshaanza kunoga ... nahofia upatikanaji wa mtoto kweli ... this mzee seems to have a lot under his sleeves .. thanks brother
 
MAMA YANGU ADUI YANGU - 26-

ILIPOISHIA:
“Kwangu ilikuwa ngumu kutokana na masharti ya mke wangu. Ndipo nilipokutana na dada yako ambaye nilimuahidi kama atakubali kunizalia mtoto ningempa zawadi kubwa.
Tatizo lingine ambalo lilimtibua dada yako na ndiyo chanzo cha kunifukuza lilikuwa kumwambia kama atakuwa tayari tukapime. Hicho ndicho kilichosababisha mi na dada yako tukosane.
“Lakini nashukuru sasa hivi nimeangukia kwenye mikono salama.”
SASA ENDELEA...


“Kama mlikubaliana na mkeo kupata mtoto, kwa nini unatumia fedha nyingi kunijengea nyumba na kuninunulia gari wakati ningekuzalia mtoto tu na kuachana?”
“Pamoja na yote niliyokueleza, mke wangu mkorofi sana kiasi cha kunifanya nyumba niichukie, jambo dogo anaomba talaka.”
“Labda unamnyanyasa kutokana na hali yake.”
“Haijatokea hata siku moja, basi siku hizi kabadilika amekuwa mtu wa kukasirika bila sababu.”
“Sasa akijua umenifanyia vitu hivi tofauti na makubaliano yenu unafikiri itakuwaje, si ndiyo kuuana?” nilijikuta nikiingia woga.
“Hawezi kufahamu hata siku moja.”
“Sababu ya kuuliza hivyo inatokana na mimi kukutega siku zangu za hatari bila mafanikio.”
“Kwa hiyo ulitaka tufanyeje?”
“Tukacheki afya zetu tujue sababu ya kuchelewa kupata mimba ni nini.”
“Hakuna tatizo.”
Tulikubaliana siku ya pili kwenda hospitali kuangalia tatizo la kuchelewa kupata mimba linatokana na nini au kati yetu kuna mwenye tatizo linalosababisha nisishike ujauzito.
***
Siku ya pili alinipitia kazini mapema na kwenda naye kwenye moja ya hospitali kubwa jijini. Tulipofika tulipokelewa na daktari ambaye alionesha anamfahamu sana mzee Sambi aliyekuwa maarufu jijini.
“Karibu mzee Sambi.”
“Asante John.”
“Karibu dada,” alinikaribisha na mimi.
“Asante.”
“Ndiyo mzee za siku?”
“Nzuri tu ndugu yangu.”
“Naona mmefika hapa mna shida?”
“Ndiyo.”
“Mna shida gani?”
“Nina imani unajua raha ya nyumba mtoto?” mzee Sambi alisema.
“Ndiyo, lakini mtoto ni majaliwa.”
“Ni kweli, lakini lazima ujue kama una tatizo na kama unalo linatatulika vipi?”
“Kwa hiyo mna shida gani?”
“Tunataka tuangalie afya zetu ili tujue kwa nini tunalima lakini hatupati mazao.”
“Hakuna tatizo mtajua kila kitu.”
Daktari alituandikia karatasi ya kwenda kuchukua vipimo. Tulikwenda hadi kwenye chumba cha maabara. Tulipofika tulichukuliwa, nilitangulia mimi ndani na kufanya uchunguzi kwa kuangaliwa kwa Ultra Sound kuangalia mirija ya uzazi na uwezo wa mayai kukomaa na kubeba mimba.
Kwa upande wa mwenzangu sikujua kwa vile kila mmoja alipimwa peke yake. Baada ya kumaliza kupimwa nilielekezwa kwenda kukaa sehemu kusubiri.
Baada ya muda mzee Sambi naye alikuja nilipokuwa nimekaa. Tulikaa sehemu ile kusubiri kuitwa, kwa upande wangu sikuwa na wasiwasi kwa vile niliishawahi kupata ujauzito na kutoka.
Wasiwasi wangu mkubwa ulikuwa kwa mzee Sambi kwa kujua huenda ana tatizo lakini hakutaka kuliweka wazi. Baada ya kukaa zaidi ya saa tatu tuliitwa kwa daktari.
Baada ya kuingia tulitulia kusubiri majibu ya daktari kuhusiana na afya zetu.
“Jamani majibu yenu yamerudi, vipimo vyetu vinatazama kwa umakini mkubwa na majibu yake hayana ubabaishaji. Hivyo basi majibu yanaonesha kila kona haina tatizo kila mtu ana uwezo wa kupata mtoto.”
“Sasa tatizo nini?” niliuliza.
“Hii huwa ni hali ya kawaida tu wala haina tatizo kwa mtu kuchelewa kupata mtoto. Muda ukifika mtapata tu.”
“Sasa mpaka lini?” mzee Sambi naye aliuliza.
“Kwani mna muda gani kwenye uhusiano?”
“Mwezi wa pili sasa.”
“Mbona mapema, kuna watu hupata mtoto ndani ya miaka sita mpaka kumi ya ndoa.”
“Okay, tumekuelewa daktari.”
Baada ya kupata ukweli wa afya zetu tulirudi kuendelea kumtega mtoto kwa kuzitumia siku zote za hatari ili niweze kumzalia mtoto mzee Sambi. Alionesha ana hamu na mtoto kama uzima kwa mtu aliyesimama mbele ya malaika mtoa roho.
Wakati huo, ujenzi wa nyumba yangu ulikuwa ukiendelea vizuri. Kutokana na ujenzi wake wa kisasa isingewezekana kukamilika kwa miezi miwili. Mafundi walinieleza mpaka nahamia kwangu itachukua miezi saba mpaka nane.
Mwezi wa nne nilifikiria kumpeleka mama kwenye ‘saiti’ yangu. Sikutaka kufanya kosa kama la awali la kumpeleka mama bila idhini ya mpenzi wangu.
Nilipomuuliza mzee Sambi alikubali nimpeleke kwa vile yule ni mama yangu hata ikiisha lazima angefika. Mwisho wa wiki nilimpeleka nikiwa na mzee Sambi.
Mama alishtuka kuliona jumba lililokuwa kwenye hatua za mwishomwisho. Nilimuona akishtuka lakini aliuficha mshtuko wake. Wakati mzee Sambi akizungumza na mafundi mama alinivuta pembeni na kuniuliza.
“Unasema hii nyumba ya nani?”
“Yangu.”
“Wewe?”
“Ndiyo mama, huamini?”
“Muongo! Unataka kuniambia mzee Sambi ndiye aliyekujengea?”
“Ndiyo mama, mbona mambo mazuri yanakuja, muda si mrefu nitaacha kazi na kufungua duka langu ambalo lipo katika matengenezo.
Mwezi ujao litajazwa vitu na kulifanyia matangazo kisha nitalifungua.”
“Mmh! Wapi?”
“Maeneo ya sehemu ninayokaa.”
“Hongera.”
“Asante mama.”
Wakati huo mzee Sambi alikuwa amemaliza kuzungumza na mafundi alikuja tuliposimama na kusema:
“Mama si ungezunguka kuliona jengo la m wanao?”


Itaendelea Alkhamisi inayo kuja...
 
asante babake MziziMkavu
for some particular reasons I think huyo mama Mchawi.
Ni kweli kabisa mama wa huyo demu ni zinga la mwanga (gagula) halafu binti mwenyewe akili za kushikiwa kwani ana angamia kwa kukosa maarifa. Kwa ujumla binti ni kama ameshastukia kuwa mamake gagula lakini yuko kwenye (denial) kwani hataki kuamini kama ni kweli. Wacha mama gagula ahujumu mimba na kuchafua mambo sasa.
 
Mama yangu adui yangu -27-


ILIPOISHIA:
Wakati mzee Sambi akizungumza na mafundi, mama alinivuta pembeni na kuniuliza.
“Unasema hii nyumba ni ya nani?”
“Yangu.”
“Wewe?”
“Ndiyo mama, huamini?”
“Muongo! Unataka kuniambia mzee Sambi ndiye aliyekujengea?”
“Ndiyo mama, mbona mambo mazuri yanakuja, muda si mrefu nitaacha kazi na kufungua duka langu ambalo lipo katika matengenezo. Mwezi wa kesho litajazwa vitu na kufanyiwa matangazo na mwezi ujao nitalifungua,”
“Mmh! Wapi?”
“Maeneo hayahaya ninayokaa.”
“Hongera.”
“Asante mama.”
Wakati huo mzee Sambi alikuwa amemaliza kuzungumza na mafundi, alikuja tuliposimama na kusema:
“Mama si ungezunguka kuliona jengo la mwanao?”
SASA ENDELEA...


“Nimeliona baba inatosha.”
“Hapana mama hebu twende ukakague nyumba ya mwanao.”
Nilimshika mkono mama na kumzungusha sehemu zote za kiwanja changu na nyuma ya nyumba. Mama aliisifia nyumba yangu na kunifanya nifarijike moyoni.
Baada ya kumuonesha mama nyumba yangu, tulimrudisha mpaka Temeke kisha nilirudi nyumbani kwangu kupumzika. Moyoni nilifurahi mama yangu kuona jumba langu la kifahari, mshtuko aliouonesha nilijua ulitokana na kutoamini macho yake.
***
Pamoja na maisha na malezi mazuri kutoka kwa mpenzi wangu, lakini kuchelewa kupata mtoto kulinikosesha raha. Siku moja nikiwa kazini muda mwingi nilikuwa nimetawaliwa na mawazo kitu kilichomshtua da’ Suzy.
“Mwaija mdogo wangu nakuona haupo sawa, nini kinakusibu?”
“Ni kweli.”
“Tatizo nini?”
Sikumficha nilimweleza kila kitu kuhusiana na kuchelewa kumzalia mtoto mzee Sambi.
“Sasa kama mlionekana hamna tatizo kipi kinachelewesha kupata mtoto?”
“Hapo ndipo ninapochanganyikiwa.”
“Mmeshatumia tiba mbadala?”
“Sasa kama huna tatizo tiba mbadala ya nini?”
“Mdogo wangu huenda ni chango, ukipata dawa za asili zitakusaidia.”
“Dada kama lingekuwa chango nisingepata ujauzito.”
“Mdogo wangu, lazima uangalie na jicho la tatu huenda una chango lisilouma na kusababisha mimba isiingie.”
“Mmh! Sijawahi kutumia dawa za asili tangu nizaliwe.”
“Ndiyo unatakiwa ukatumie uone kwani wengi walikuwa na matatizo kama yako leo hii wana watoto.”
“Hizo dawa nitazipata wapi?”
“Nitakupeleka kwa mtaalam.”
“Wapi?”
“Mbagala Maji Matitu.”
“Hiyo dawa itanisaidia kweli?” niliingiwa na wasiwasi japokuwa nilimuamini sana da’ Suzy.
“Dada nakwambia ndani ya wiki ukitumia kitu hicho.”
“Shoga nakuahidi nikishika mimba nitakupa milioni moja.”
“Wee iandae tu, nakuapia mwezi haukatika bila kunasa.”
“Basi dada naomba unipeleke,” nilijikuta nikipata shauku ya kwenda kwa huyo mtaalam ili niweze kumzalia mtoto mzee Sambi.
“Hakuna tatizo.”
Tulikubaliana mwisho wa wiki anipeleke kwa huyo mganga ili anisaidie kupata mtoto. Maneno ya dada Suzy yalinipa faraja kwa asilimia ndogo.
Mwisho wa wiki nilimpitia dada Suzy na kukodi gari mpaka Mbagala Maji Matitu. Tulipofika tulikwenda moja kwa moja kwa mtaalam aliyekuwa akikaa ndani kidogo kupita kituo kidogo cha polisi cha Maji Matitu. Tulifika kwenye nyumba iliyokuwa imezungushiwa uzio wa makuti. Tuliingia ndani tulikuta watu kama sita wakiwa wamekaa kwenye mkeka na ndani kulikuwa na watu wawili.
Mganga alikuwa akitoka ndani alipotuona alitufuata na kutukaribisha. Alikuwa dada mmoja aliyekuwa na umri wa kawaida, pia hata mavazi yake yalikuwa ya kawaida kuonesha si mganga wa kizamani wa kuvaa kaniki na ngozi.
Alikuwa na umbile fupi na alivaa dela lililompendeza, mikononi mwake alikuwa amevaa pete za rangi ya fedha kila kidole na shingoni alikuwa na mkufu wa rangi ya fedha pia, kichwani alikuwa ameseti nywele, ukimuangalia haraka huwezi kuamini kama ni mganga.
“Jamani karibuni,” alitukaribisha kwa uchangamfu mkubwa.
“Asante dada,” tulijibu kwa pamoja.
“Samahani jamani, vumilieni kidogo sina kazi kubwa nitawaiteni baada ya muda mfupi.”
“Hakuna tatizo.”
Mganga alituachia na kuelekea ndani tukiwa tumekaa kwenye benchi lililokuwa pembeni ya mkeka.
Baada ya muda alituita ndani, tuliingia chumbani ambako ndiko kwenye kilinge, kulikuwa na vitu vyake vya kiganga na dawa. Baada ya sisi kuketi mganga alikaa mbele yetu kwenye kigoda na kutulia kwa muda kisha alisema:
“Ndiyo, karibuni.”
“Asante,” tulijibu kwa pamoja.
‘Mna tatizo gani?”
“Mwenzangu anahitaji mtoto.”
“Anahitaji vipi?” aliuliza huku akitutazama kwa zamu.
“Amekwenda hospitali na kuonekana hana tatizo lakini mtoto hapati,” alisema da’ Suzy aliyeonekana mzoefu wa sehemu zile.
“Na mwenzake naye alikwenda?”
“Ndiyo wote wapo sawa.”
“Basi tumuombe Mungu nina imani dawa nitakazompa zitamsaidia.”
“Halafu tulitaka kujua talaka yake ya mwanzo ilisababishwa na nini?” da’ Suzy aliuliza kwa niaba yangu.
“Hakuna tatizo,” mganga alisema huku akinyanyuka na kuchukua lubega wa Kimasai na kujifunga kisha alivaa taji la Kimasai na chini alivaa viatu vya matairi na kushikilia mkuki, pembeni yake alilaza sime.
Nilijikuta nikiingiwa na hofu na kujiuliza alikuwa akitaka kufanya nini lakini dada Suzy hakuonesha wasiwasi wowote.
Baada ya kutulia kwenye kigoda chake alimwita mwanaume aliyekuwa nje ambaye alikuja kukaa pembeni yetu.
“Jamani nina imani mwalimu atakayepanda kuna maneno yatakushindeni kuyaelewa. Huyu atawasaidia kuwaelewesheni.”
“Hakuna tatizo.”
Baada ya kusema vile alichoma udi na kuuweka pembeni kisha akashika mkuki wake na kuuinamia kwa muda, akatulia kupandisha jini la Kimasai lililokuwa likiitwa Lukuki.
“Heloo habari,” alisema baada ya kupandisha, nilitulia tuli kuangalia kwani jambo lile kwangu lilikuwa ndiyo siku ya kwanza.
“Nzuri,” da’ Suzy aliitikia.
Alianza kwa kutusalimia kwa kutushika mikono na kugusanisha kichwa chake na kila aliyekuwemo mle ndani.
Alianza kuelezea matatizo yangu huku nikibahatisha mawili matatu yaliyonishinda mkalimani alinisaidia kunifafanulia.
“Rafiki una matatizo makubwa sana, matatizo yako si ya leo hata najiuliza maswali mengi yaliyokosa majibu, kweli?”
“Ndiyo,” ndiyo nilijibu.
“Tatizo lako limeanza baada ya ndoa yako, ikiwa pamoja na kuharibikiwa mimba, mume kuharibikiwa maisha na kukosa kazi. Kuharibikiwa maisha na kila kitu kusimama ni kweli?” mganga aliniuliza, yote aliyosema yalikuwa ni ya kweli alikuwa kama mtu anayejua maisha yangu.
“Ni kweli,” nilikubali.
“Mumeo aliondoka na aliporudi alikupa talaka isiyo na maelezo ni kweli?”
“Ndiyo ila alisema mama anajua.”
“Tatizo lako nitakutibu wala sitaki kulichimba sana kwa vile nitazalisha visivyotakiwa, kingine unatafuta mtoto bila mafanikio japo huna tatizo lolote, ni kweli?”
“Kwa nini usinieleze mbaya wangu?” nilitaka kujua.
“Huna moyo huo wa kusikia vitu vizito vilivyo kuzunguka, ila nakuahidi kukutibu na kukuondoa vifungo ulivyofungwa.

Itaendelea Jumamosi, usikose.
 
Mama Yangu Adui Yangu -28-

ILIPOISHIA:
“Tatizo lako nitakutibu wala sitaki kulichimba sana kwa vile nitazalisha visivyotakiwa, kingine unatafuta mtoto bila mafanikio japo huna tatizo lolote, ni kweli?”
“Kwa nini usinieleze mbaya wangu?” nilitaka kujua.
SASA ENDELEA...

“Huna moyo huo wa kusikia vitu vizito vilivyokuzunguka, ila nakuahidi kukutibu na kukuondoa vifungo ulivyofungwa. Hivyo ndivyo vilivyosababisha upewe talaka, mshindwe kumaliza nyumba yenu na mumeo awe na maisha magumu, pia usishike ujauzito, ungemeza kila aina ya dawa bila ya mafanikio.”
“Mungu wangu! Na nani?” nilishtuka kusikia habari zile zilizokuwa zinafanana na maneno ya mume wangu.
“Matatizo yako siwezi kukueleza nani ameyasababisha kwa vile najua wanadamu mna mioyo midogo, ila naweza kukutibu. Kwa kukufungua vifungo hivyo kwa uwezo wa Mungu utashika ujauzito tu.”
“Nitashukuru.”
“Leo nitakupa dawa ya kuoga ila kesho njoo asubuhi nitakuosha nuksi, pia kukufungua vifungo na kukupa dawa ya kunywa. Mwezi haufiki utashika ujauzito.”
“Nitashukuru.”
“Kesho njoo na pea mbili za khanga mpya za kukuoshea.”
“Sawa.”
Baada ya kunipa maelezo ya kina kuhusu maisha yangu na kumruhusu jini la Kimasai kuondoka. Yule dada alirudi katika hali ya kawaida na kuelezwa yote aliyosema Lukuki.
Alinipa dawa ya kuoga na kutakiwa siku ya pili asubuhi na mapema sana nifike kwa mganga ili nifanyiwe tiba yangu kwanza. Nilirudi nyumbani nikiwa bado siamini kama kweli kupitia dawa za yule dada nitapona na kupata mtoto.
Nilipofika nyumbani nilijipumzisha kwenye kochi huku msichana wa kazi akiniletea juisi. Baada ya kunywa nilikwenda chumbani na kujifungia ili kupumzisha akili yangu kutokana na kuzongwa na mawazo mengi. Sikutaka kelele za aina yoyote, nilishukuru siku ile mzee wangu alikuwa amesafiri na kupata uhuru mkubwa wa kutulia.
Kichwa kilikuwa kizito kutokana na kugubikwa na mawazo mazito yaliyojifungafunga na kunifanya nishindwe kuelewa niliyoelezwa kama yana ukweli kwa asilimia kubwa.
Swali likabakia nani mtendaji wa ubaya ule. Kila nililoliwaza lilikuwa halikubaliki na kuona kama najichanganya kwa kufikiria vitu ambavyo hata kwa mtutu visingewezekana.
Mpaka usiku unaingia bado nilikuwa kwenye fumbo zito, chakula kilinishinda na kunifanya nipande kitandani mapema. Nilikumbuka nilitakiwa kuoga dawa nilizopewa na mganga. Nilikwenda bafuni na kujimwagia maji ya dawa mwili mzima na kupanda kitandani kujilaza.
Usingizi ulikuwa mbali nilijikuta nikiwa na mawazo mengi kuhusiana na maelezo ya mganga kwa kuijua historia yangu kama vile nilimhadithia na kuona hata ujauzito wangu haukuharibika kwa amri ya Mungu bali kulikuwa na mkono wa mtu.
Hata kuvurugikiwa maisha na kupewa talaka yenye utata na fumbo zito kulikuwa na sababu ambayo bado nilifichwa.
Maneno ya mganga yalizidi kunichanganya sana baada ya kurudia kusema siri nzito za moyoni mwangu ambazo nyingine hata dada Suzy sikuwahi kumwambia.
Pamoja na kunieleza sababu ya kuharibikiwa maisha na kuniahidi kunisaidia kwa kunifungua vifungo vyote, bado nilibakia na swali ni nani aliyenifanyia hivyo.
Nilijikuta nikiyakumbuka maneno ya mtalaka wangu na kuamini alichokisema, nikaon alikuwa na sababu ya kunipa talaka. Lakini nilijikuta nikiendelea kumlaumu kama alijua kuna mtu katia mkono kwa nini hakuniambia aliyetenda vile.
Hata kama ni mama yangu mzazi, japokuwa jambo hilo nililipinga kwa nguvu zangu zote, bado niliamini sikuwa na kosa la kupewa talaka.
Nilijikuta nikiwaza peke yangu:
“Mmh! Inawezekana kweli aliyefanya vile ni mama yangu mzazi? Hapana ...hapana... mama yangu mzazi hawezi kufanya kitu hicho, afanye ili iwe nini?” nilijiuliza.
Wazo la mama yangu mzazi ndiye aliyenifanyia mchezo ule nililikataa kwa nguvu zote. Swali lililoniumiza akili lilikuwa kwa nini mtalaka wangu alisema mama ndiye anayejua kila kitu alikuwa na maana gani?
Nilijiuliza nani aliyenifunga au dada zangu kwa wivu wa mimi kuolewa? Lakini mbona wao waliolewa na kuachika iweje wanionee wivu?
Kwa kweli kila nililolifikiria kwangu lilikuwa zito kiasi cha kutaka kunipasua kichwa. Usingizi ulinipitia baada ya kukaa sana kitandani na kushtuka siku ya pili baada ya kupigiwa simu. Nilipoangalia nilikuta ni da’ Suzy ndiye aliyenipigia.
Niliangalia saa ya juu ya droo ya kitanda na kuona kumekucha ilikuwa saa moja kasoro. Niliichukua simu huku kichwa kikiwa kizito kutokana na mawazo kunizidi uwezo, pia kutokana na kuchelewa kulala.
“Haloo da’ Suzy.”
“Abee, vipi umeshatoka nyumbani?”
“Dada wee acha tu, yaani simu yako ndiyo iliyonishtua usingizini, bila hivyo sijui ningeamka saa ngapi?”
“Kwani mzee leo kalala nyumbani?”
“Walaa, mawazo tu dada yangu.”
“Lakini yule dada si kasema atakusaidia?”
“Ni kweli lakini maneno aliyosema mganga na aliyosema Beka yanafanana lazima niseme ukweli nimechanganyikiwa sana ninaposhindwa kumjua mbaya wangu.”
“Mdogo wangu yote hayo yataisha, kwanza mshukuru Mungu umeachwa na Beka lakini sasa hivi una maisha mazuri. Wengine wakiharibikiwa huwa wanachanganyikiwa na kukata tamaa ya maisha, kwani wanaandamwa na mikosi kila kukicha.”
“Mmh! Sawa.”
“Basi usiyape sana nafasi mawazo yanayoumiza, sisi tusingekuwa hapa.”
“Lakini nani kanifanyia hivi?”
“Mwaija hebu kwanza kaoge ili tuwahi kwa mganga.”

Itaendelea Jumatano ijayo......
 
uwiii mbona nahamu ningeisoma yote now, yaani nilianza kusoma hadi sehemu ya 3 nikasema nitarudi mwezi huu mwishoni kusoma itakuwaimeihsa uwiiii unaniumiza roho jamani malizia basi. mara tatu kwa wiki iwe basi?

ninaipendaje, shukurani kwa hadithi hii
 
yaani wewe unamwita mwenzio mjinga, kweli binadamu wengine hamna maana. inabidi umuombe msamaha kwani hadithi kakulazimisha kuisoma.

kweli unaandika maneno machefu hivi FIDELIS PROJESTUS?
 
Last edited by a moderator:
Back
Top Bottom