MAMA YANGU ADUI YANGU - 23-
ILIPOISHIA:
BASI mpenzi kuanzia sasa utakaa hapa.
Na ile nyumba unayonijengea Boko?
Hapa nimekupangia kwa muda wakati unasubiri nyumba yako kuisha ili nami nipate muda wa kuwa na wewe kwa nafasi baada ya kazi.
Mmh! Asante mpenzi, nilimshukuru kwa kumkumbatia.
Basi vitu vyote unavyoviona ndani vimenunuliwa juzi na kupangwa jana. Baada ya kuridhika ndiyo nikakuleta ujionee nyumba yako.
Asante sana, nilijikuta nikiwa na furaha ya ajabu moyoni na kuona kama Mungu kaamua kunifanyia muujiza.
Haya ni matunda ya msimamo na tabia zako, sijawahi kuona msichana kama wewe katika kipindi hiki.
Mbona tupo wengi tu basi mmekuwa wavivu kuchagua vinavyongaa barabarani mkadhani vyote ni dhahabu.
Nimekubaliana na kauli yako.
SASA ENDELEA...
Tulirudi ndani, kwa vile muda ulikuwa umekwenda nilimuomba aniwahishe nyumbani.
Bebi kwa nini leo usilale hapa?
Mmh! Peke yangu jumba lote hili?
Tutalala wote.
Hapana siku nyingine, si unajua mimi mtoto wa mama lazima nikaage nyumbani kuwa naanza kujitegemea!
Hakuna tatizo nakusikiliza wewe.
Basi kila kitu kitakwenda kama kilivyopangwa.
Hakuna tatizo.
Tulikubaliana kuondoka tulizima taa na kufunga mlango wa nyumba na geti na kunirudisha nyumbani. Tulipofika maeneo ya Mwembe Yanga alinikodia teksi hadi nyumbani.
Nilifika nyumbani na kuwa na mawazo mengi juu ya mzee Sambi. Baada ya kuoga na kupata chakula cha usiku, nilimfuata mama chumbani kwake na kumweleza siri yangu.
Aliposikia namgongea alitoka na kuniuliza, kwa vile sikuwa na kawaida ya kumfuata muda ule. Toka nilipoanza kazi baada ya kazi nilikuwa chumbani kwangu nikiangalia CD za filamu.
Sikutaka kukaa nje kwa kuhofia kujiingiza kwenye vishawishi vibaya. Mama aliponiona aliniuliza:
Vipi mama?
Nilikuwa na mazungumzo na wewe kidogo.
Sawa, nisubiri sebuleni nakuja.
Hapana mama nataka tuzungumzie chumbani kwako.
Mmh! Makubwa mazungumzo ya chumbani kwangu?
Ndiyo mama.
Haya karibu.
Niliingia chumbani kwa mama na kukaa kitandani kwake karibu yake. Mama alimaliza kuweka vitu vyake vizuri kisha alinigeukia.
Haya mama niambie.
Mama kuna kitu ninacho muda mrefu, ilikuwa vigumu kukueleza mwanzo kwa vile sikuwa na uhakika nacho.
Kitu gani hicho?
Mama nimepata rafiki wa kiume ambaye amejitolea kila kitu katika maisha yangu.
Nilijua, nilisubiri kuambiwa ningekuuliza ningeonekana muongo.
Inawezekana lakini mwanzo ilikuwa ngumu kulisema.
Haya mwanangu ulikuwa unasemaje?
Mama mtu mwenyewe unamfahamu.
Mwanangu nimfahamu vipi bila kunifahamisha.
Mzee Sambi.
Mzee Sambi aliyekuwa mpenzi wa dada yako?
Ndiyo.
Mmh! Makubwa, kwa nini umekubali kuchangia mapenzi na dada yako? nilimshangaa mama kuniuliza swali kama lile.
Hata mimi mwanzo sikutaka kukubali, lakini mzee yule alinieleza mambo mengi kuhusiana na dada kumfukuza na alivyotaka kumfanyia ambavyo vyote dada alivipiga teke.
Vitu gani?
Alitaka awe nyumba yake ndogo na kumuahidi kumjengea nyumba na kumnunulia gari.
Muongo wanaume wa mjini utawaweza, wanataka wakutumie wakitimiza haja zao wanaondoka bila kwa heri. Dada yako aliniambia nikamkatalia.
Mama makubaliano yetu ni kuwa naye baada ya kunikamilishia kila alichoniahidi.
Atawahi muongo mkubwa, atakuletea nyaraka za uongo ili uamini lakini mwishoni atazichukua.
Kwangu tofauti, hivi ninavyo kwambia ameisha ninunulia kiwanja na ujenzi utaanza mara moja.
Muongo? mama alishtuka.
Tena mama nyumba ikiisha litakuwa bonge la jumba pia amesema ataninunulia gari la kifahari.
Mmh! Hongera.
Asante na sasa hivi amenipangia nyumba nzima hivi ndiyo nimetoka kuiona yenye kila kitu ndani.
Dada yako akijua itakuwaje si unaujua ukorofi wake.
Yeye ndiye aliyeniambia kama namtaka nimchukue.
Basi mimi sina tatizo, kwa hiyo nyumba aliyokupangia itakuwaje?
Nitahamia wakati wowote.
Kwa hiyo utakuwa unakaa naye?
Hapana, hatujakubaliana hilo bali ametaka niwe huru na kuweza kuonana naye na kupanga mambo yetu kwa uhuru mkubwa.
Sawa, umeona ulijifanya mlokole yote haya ungeyapatia wapi?
Mama nilitaka kusahau, amesema eti nikimzalia mtoto wa kike atanipa milioni kumi na kiume ishirini.
Masuala ya nyumba na gari yanakufa?
Walaa hiyo ni bonasi ya furaha ya kupata mtoto.
Mmh! Makubwa.
Mama mbona unaguna.
Ndiyo nasikia kwako kumzalia mtu mtoto akulipe fedha.
Mama amesema mkewe hana kizazi hivyo anategemea kwangu.
Wewe ndiyo unacho?
Mama maneno gani hayo? maneno ya mama yalinivunja nguvu.
Siyo maneno gani, kwani huyo mkewe alilokosa kwa Mungu nini?
Sasa mama yeye kukosa kizazi na mimi kunaingiaje?
Siyo kuingiaje bali nenda na mawili, isije ahadi ya milioni kumi na ishirini ikayeyukia hewani ukachanganyikiwa bure. Mtoto ni majaliwa ya Mungu na si kwa ahadi ya fedha ingekuwa hivyo mkewe angemzalia.
Sawa mama nimekuelewa, nilikuja kukufahamisha tu.
Hicho kiwanja chenu kipo wapi?
Boko.
Utanipeleka lini nikakione?
Mwisho wa wiki.
Basi mwanangu nakutakia kila la heri.
Asante mama yangu.
Niliagana na mama na kwenda kulala japokuwa nilichelewa kulala kwa kauli ya mama labda sina kizazi kwa kweli iliniumiza sana.
Nilijikuta nikiyadharau yote kwa kuamini kila kitu chini ya jua muwezeshaji wa yote ni Mungu pekee si mwanadamu.
Niliamini hakukuwa na haja ya kuendelea kuwa nyumbani kwa vile sifa ya nyumbani kwetu sikuipenda siku zote. Ilionekana Mungu alisikia kilio changu cha kuishi kwenye nyumba yenye sifa mbaya kilipokelewa.
Pamoja na furaha ya kutoka nyumbani lakini suala la kuanza kuishi na mzee Sambi kama mke na mume sikuliafiki kwa vile ilikuwa mapema sana.
Kukaa peke yangu jumba lile niliona haifai lazima nilitakiwa kuwa na mtu wa karibu. Nilikumbuka kuna msichana mmoja aliyekuwa akifanya kazi za ndani kwa jirani yetu niliye kuwa nimezoeana naye. Kuna siku alinifuata kabla ya kuanza kazi super market kuniomba aje pale kwetu au nimtafutie kazi kutokana na manyanyaso na ugumu wa kazi aliokuwa akikutana nao pale.
Niliamini nikiwa naye angenisaidia kazi pia kunichangamsha nikiwa nyumbani peke yangu. Nilijikuta nikipata tumaini la kuwa na mtu wa kukaa naye. Baada ya kuwaza sana usingizi ulinichukua.
***
Siku ya pili kabla ya kwenda kazini nilibahatika kumuona yule msichana ambaye alikuwa na umri wa miaka kumi na saba.
Kwa kweli alifurahi sana kumpa habari ambazo ilionekana alikuwa akizisubiri kama wokovu.
Itaendelea Jumamosi ijayo....