MAMA YANGU ADUI YANGU - 20-
ILIPOISHIA:
Niliamini kutokana na maneno yake hawezi kushtuka lakini kwa upande wangu niliona ni mapema sana kumwambia jambo lile ambalo bado lilikuwa halijakamilika. Nilijiuliza nini hatima ya maisha yangu kama nitakuwa na mzee Sambi, mwanaume mwenye mke.
SASA ENDELEA...
Niliamua kufanya kwanza siri mpaka kila kitu kitakapokuwa wazi, kwa vile nilikuwa nimechoka na kazi usingizi haukuchelewa kunichukua.
***
Siku ya pili, baada ya muda wa kazi mzee Sambi alinipitia kutokana na makubaliano yetu ya kwenda kuangalia afya zetu, alipofika tu nilimueleza tuliyokubaliana jana yake. Naye hakuwa na pingamizi, alikubali twende tukapime.
Tulikwenda kwenye hospitali moja iliyopo Keko Maduka Mawili. Kama kawaida, tulifika na kupokelewa na dada mmoja aliyekuwa mapokezi.
Baada kuandika kadi, alituelekeza kwa daktari, chumba kilichokuwa mbele kidogo. Tulielekea moja kwa moja kwa vile muda ule hakukuwa na wagonjwa wengi, wengi walionekana wamekuja kupata huduma ya sindano za saa.
Baada ya kuingia ndani ya chumba cha daktari tulipokelewa na kaka mmoja mtanashati.
Karibuni.
Asante, tulijibu kwa pamoja.
Ndiyo niwasaidie nini?
Tunataka kuangalia afya zetu.
Kuangalia kivipi?
Kupima Virusi vya Ukimwi.
Mmh! daktari aliguna kidogo na kututazama wote kwa zamu kisha aliuliza.
Mpo vipi?
Ni marafiki.
Wa kimapenzi?
Ndiyo, alijibu mzee Sambi.
Mna muda gani katika uhusiano wenu?
Mwezi sasa, alijibu mzee Sambi.
Sasa katika huo mwezi mlipokutana mlitumia kinga?
Hatujawahi kukutana, tumekuja hapa kupima ili tujue afya zetu kabla ya kuanza uhusiano rasmi.
Kwa mfano mmoja akikutwa na tatizo mtafanyaje?
Kwa upande wangu hakuna kitakachopungua kwa vile nina mapenzi ya dhati na mpenzi wangu, alijibu mzee Sambi huku akiushika mkono wangu na kuupapasa.
Na dada yangu kama utamkuta mzee ana matatizo?
Kwa upande wangu naamini mapenzi ndiyo yataishia hapa.
Kwa nini?
Kumbuka mi bado msichana mdogo nahitaji kuwa na familia halafu leo mwenzangu awe hivyo unafikiri raha ya ndoa ipo wapi?
Lakini kuna njia ya kuweza kupata mtoto bila tatizo.
Hiyo njia ndiyo siitaki kabisa kwa vile haipo salama asilimia mia moja.
Mzee umemsikia mama? daktari alimuuliza mzee Sambi huku akimtazama.
Kwangu hakuna tatizo, ikiwa hivyo namruhusu aamue chochote anachotaka lakini kama tatizo litakuwa kwake bado nitaendelea kumpenda na kumpa huduma zote muhimu kama nilivyomuahidi.
Sawa, basi nitawapa karatasi mtaingia chumba cha kwanza mkono wa kushoto mkapime damu.
Hakuna tatizo.
Daktari aliinama na kuandika karatasi ya vipimo na kutupa, tulizipokea na kufuata maelekezo. Tulitoka na kuingia chumba cha pili, kwa upande wangu sikuwa na wasiwasi kwa vile sikuwa na tabia ya kurukaruka, pia hata mtalaka wangu naye hakuwa na tabia mbaya japokuwa sikuwa nashinda naye muda wote tulipokuwa pamoja.
Mzee Sambi naye hakuonesha wasiwasi wowote, baada ya kuingia chumba cha maabara tulikaribishwa kwenye kiti. Tulikaa na kumpa vyeti vyetu, baada ya kusoma alichukua vifaa na kutuchukua damu mmoja mmoja. Baada ya kumaliza zoezi lile alituomba tukakae sehemu ya mapumziko kusubiri majibu yetu.
Tulitoka hadi kwenye makochi na kukaa kusubiri majibu, muda wote tulikuwa kimya, hakuna aliyeanzisha mazungumzo. Baada ya robo saa tuliitwa kwa daktari, nilijua majibu yameishatoka.
Tuliingia kwa daktari na kukaa kimya kusubiri majibu yetu.
Baada ya kukaa kwenye viti, ndani ya chumba kukiwa kimya, daktari alikuwa akipitia karatasi ya majibu yetu. Muda ule niliutumia kumsoma anachokisoma kwa kumuangalia usoni kwake nikiamini atakachokisoma kitaonekana kwenye uso wake.
Nilimuona akisoma akiwa ametuliza macho, muda wote aliosoma karatasi ya kwanza alikuwa ametuliza macho. Aliiweka pembeni na kuchukua nyingine ambayo ndiyo iliyokuwa na jina langu. Aliisoma taratibu kama ya kwanza lakini kuna kipindi niliona kama amekodoa macho. Baadaye aliyarudisha katika hali ya kawaida.
Aliichukua karatasi ya kwanza na kuisoma upya na kuirudia yangu harakaharaka kisha alitutazama. Macho yake yalionesha kuna kitu amekiona kwenye karatasi, sikujua yangu au ya mzee Sambi.
Alikohoa kidogo na kutuita majina yetu kupitia kwenye vyeti vyetu.
Mwaija.
Abee.
Mzee Sambi.
Naam.
Majibu yenu yametoka, sasa sijui niyatoe kwa kila mmoja au kwa wote pamoja?
Kwa wote, sababu ya kuja pamoja kila mtu anataka kujua afya ya mwenzake.
Vizuri, je, mpo tayari kupokea majibu yenu?
Daktari acha mbwembwe we tupe majibu tujue tunasuka au tunanyoa,
Itaendelea katika Alkhamisi ijayo...