[h=1]MAMA YANGU ADUI YANGU - 46-[/h]
ILIPOISHIA:
Baada ya muda nililiona gari la mzee Sambi likisimama mbele yetu. Nilishtuka mpaka mapigo ya moyo yakanienda mbio. Baada ya gari kusimama alishuka mzee Sambi na kuja kwenye gari letu.
Alipofika alitoa miwani yake na kusema kwa kushtuka:
"Ni wewe Mwaija?"
"Ndiye miye, ulidhani nitakufa?"
"Sivyo Mwaija ni historia ndefu."
"Ya kunitaka kuniua na kunidhuruma mali yangu?"
"Mwaija naomba tukae pembeni tuzungumze."
"Katu sitazungumza na wewe muuaji," nilimjibu kwa hasira.
"Usiniite hivyo Mwaija nipe nafasi unisikilize."
"Ili?"
"Utajua sababu ya mimi kuondoka ghafla."
"Nikijua itanisaidia nini, nilikufuata kukuliza?"
SASA ENDELEA...
"Ha! Mwaija umeolewa?" mzee Sambi alishtuka baada ya kuiona pete ya ndoa kutokana na kurusha mikono yangu wakati nilipokuwa nikiongea.
"Ulifikiri siolewi?" nilimjibu kwa nyodo.
"Na huyo mtoto ni wako?" alizidi kushtuka kila dakika.
"Ndiyo, uliambiwa mi ni mgumba?" nilimjibu kwa nyodo.
"Mwaija angekuwa wangu huyo, mama yako anahusika kwa kiasi kikubwa kuvuruga uhusiano wetu."
"Aliyetaka kuniua ni mama yangu au mkeo?"
Muda wote dereva wa teksi alikuwa akitushangaa kwa jinsi tulivyokuwa tukitupiana maneno.
"Huwezi kunielewa naomba basi uje kwenye gari langu tuzungumze."
"Mlinikosa kuniua hamtanipata tena, ulimtuma mkeo aniue ili mchukue nyumba. Sawa, mmechukua vyote hivyo, lakini sijawafuata kuwaulizia kitu chochote."
"Mwaija nyumba bado ni yako."
"Usinichefue, kukusikiliza usinifanye mjinga, uliniambia nini kuhusu mkeo na matokeo yake kimetokea nini? Kwa taarifa yako najua kila kitu katika ile nyumba."
Nilimweleza yote tangu siku nilipokwenda na kumkuta na mkewe wakiwaonesha wapangaji nyumba. Nilimuona akishangaa kama kaona meli barabarani.
"Basi naomba tuzungumze Mwaija ili unielewe nipo radhi kukupa chochote ili tuondoe tofauti zetu."
"Naomba hayo tuachane nayo, endelea na maisha yako na mkeo mchawi. Acheni kuwaroga watoto wa watu kwani mnawaharibia mambo yao."
"Mwaija maneno gani hayo?"
"Tuachane na hayo, naomba uendelee na safari yako."
"Sasa?"
"Kuhusu nini?"
"Nipe hata dakika tano."
"Nimeitwa nyumbani mama anaumwa naomba uniache niwahi."
"Naomba namba yako ya simu."
"Siwezi kukupa, mume wangu ana wivu sana."
"Sasa ita.."
"Dereva hebu tuwahi safari yetu."
Dereva aliondoa gari na kumuacha mzee Sambi akiwa amesimama barabarani. Dereva hakuniuliza mpaka tulipofika kwenye kona ya Maguruwe.
"Dada vipi?"
"Achana naye," nilimijibu kwa mkato.
Nilijikuta nikiwa mtu mwenye hasira baada ya kuachana na mzee Sambi mpaka machozi yalinitoka huku kifua kikinijaa kwa hasira. Nilifika nyumbani na kumlipa dereva kisha niliingia ndani.
Nilipokelewa na mama na ndugu zangu pamoja na mama Amina.
"Karibu mama yangu," mama Amina alinitania kutokana na kumwita mwanangu jina lake kama shukurani kwake kwa kuwa sehemu ya kupatikana kwa mwanangu.
"Asante, shikamoo."
"Marahaba mama yangu."
"Shikamoo mama," nilimgeukia mama.
"Marahaba, za nyumbani?"
Mama yangu aliitikia kwa unyonge, hali ile ilizidi kuniumiza moyoni.
"Nzuri mama, shikamooni dada zangu."
"Marahaba mama Husna," waliitika wote.
Nilikwenda kukaa pembeni ya mama na kumpa mjukuu wake, alimpokea na hapohapo nikagundua mama alikuwa akitokwa na machozi.
Baada ya kuketi mama Amina alifungua kikao kile cha kifamilia.
"Jamani nina imani mtashangaa kuuona uwepo wangu hapa kwenu kwa muda huu," alianza kuzungumza mama Amina.
"Walaa," tulijikuta tukijibu kwa pamoja.
"Basi leo sikuja kama mlivyonizoea, kuna jambo zito limenileta ambalo nina imani hamlijui lakini mama yenu anataka mlijue kabla mauti hayajamchukua.
"Nina imani hivi karibuni mmeona mabadiliko ya hali ya mama yenu?"
"Ni kweli," tulijibu kwa pamoja.
"Nina imani hali hii imewashtua sana na kukosa jibu, ni kweli?"
"Kweli," dada alijibu.
"Nina imani mi si msemaji ila mzungumzaji mkubwa ni mama yenu ataeleza kinachomtesa moyoni mwake."
"Hakuna tatizo," dada mkubwa alijibu.
"Kabla sijamkaribisha mama yenu naomba kuwauliza."
"Uliza tu," tulimkubalia.
"Je, mnampenda mama yenu?"
"Zaidi ya sana."
"Kama amewakosea mpo tayari kumsamehe?"
"Leo mpaka kesho kiama," tulijibu wote kwa vile tulikuwa tukimpenda sana mama yetu.
Nini kiliendelea? Usikose kusoma Alkhamisi ijayo.