MBUNGE wa Same Mashariki, Anne Kilango Malecela ametangaza rasmi kupiga kambi Moshi Mjini hadi mwaka 2010 ili kuhakikisha kuwa CCM inanyakua jimbo hilo, uamuzi ambao unamuingiza kwenye vita kali na mbunge wa sasa, Philemon Ndesamburo.
Katika kuonyesha kuwa Ndesamburo hana nguvu kwenye jimbo hilo, Kilango aliwaambia wanachama na viongozi wa CCM kuwa mbunge huyo kutoka Chadema ameshinda mara mbili mfululizo kutokana na matatizo ya wanaCCM wenyewe na kuwataka wajisafishe.
Kilango, ambaye amekuwa akilalamika kuwa mafisadi wanataka kuchukua jimbo lake la Same Mashariki, alitangaza mkakati huo jana wakati akihutubia katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya Kituo Kikuu cha Mabasi mjini Moshi, ikiwa dalili za wazi kwamba, CCM sasa imeanza kujipanga kufanya mashambulizi mkoani hapa ambako vyama vya upinzani vinaonekana kuwa na nguvu kubwa.
âNitapiga kambi hapa... kwanini tupate madiwani 12 na Chadema watatu halafu tushindwe ubunge,â alihoji Kilango. âNitakaa hapa mpaka nimfahamu mchawi ili nimshike mkono nimwambie Rais (Jakaya) Kikwete huyu ndiye anayetufanya tushindwe na Ndesamburo.â
Mbunge huyo aliongeza kusema:âHatuwezi kukubali kuwa na wanaCCM ambao mchana wamevaa kijani, lakini usiku wamevaa nguo nyingineâ¦nimeongea na Ndesamburo ananiambia wanaompa ubunge ni wanaCCM wenyewe⦠hili halikubalikiâ.
Alisema kuwa suala la Jimbo la Moshi Mjini kuwa chini ya upinzani tangu uchaguzi wa kwanza wa vyama vingi mwaka 1995 linampa tabu sana na hilo ndilo lililomsukuma kupiga kambi katika jimbo hilo hadi uchaguzi mkuu wa 2010.
âLeo nimebisha hodi hapa tutakuwa wote mpaka Oktoba 2010 na kama tunakosa naomba wananchi mtuambie mapema nini na ndio maana nitakuja kila siku hapa, lakini na nyinyi viongozi na wanaCCM mjitazame inakuwaje tuna madiwani 12 tukose mbunge,â alisema mbunge huyo wa Same.
Hata hivyo, alisema katika kipindi cha siku mbili tu alizokaa Moshi Mjini ameambiwa kuwa moja ya kero inayoinyima CCM ushindi ni vitendo vya unyanyasaji wanavyofanyiwa wafanyabiashara ndogondogo, maarufu kama machinga.
Kilango alifafanua kuwa hakuna mtu muhimu kama anayejitafutia riziki yake, lakini ni jambo baya kama mtu huyo anakwamishwa na kuapa kuwa kwa suala hilo la machinga, ikibidi kulifikisha kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, basi atafanya hivyo.
âSisi tuna njia zetu pale bungeni unaweza kuuliza maswali ya kawaida au maswali ya papo kwa hapo kwa Waziri Mkuu na ikibidi kumuuliza, nitamuuliza,â alisema Kilango.
Katika hali iliyodhihirisha kuwa suala hilo la machinga linagusa mioyo ya wananchi wengi wa mji wa Moshi, mara tu baada ya Kilango kulitaja, umati wa wananchi na wafuasi wa CCM ulilipuka kwa furaha.
Mbunge huyo aliamua kumsimamisha katika hadhara hiyo mwenyekiti wa wafanyabiashara ndogondogo wa Stendi Kuu ya Moshi, Vicent Asenga kuelezea kile kinachowakwaza hadi waamue kutoipa CCM kura katika vipindi vitatu mfululizo.
Asenga alisema waliingia makubaliano na Halmashauri ya Manispaa ya Moshi kwamba kama wanataka kutoa huduma ya biashara kwenye stendi hiyo, wawe na vitambulisho na sare jambo ambalo walilitekeleza kikamilifu.
Hata hivyo, mwenyekiti huyo alisema walishangaa siku moja wakivamiwa na kukamatwa na kupelekwa ofisi ya kikosi cha usalama barabarani na kutozwa faini ya kati ya Sh20,000 hadi Sh40,000 kana kwamba wao wamefanya makosa yanayohusiana na usalama barabarani.
âSisi hatuna upinzani na CCM lakini tuna upinzani na wanaotukwamisha,â alisema Asenga huku akishangiliwa na wananchi waliofurika katika mkutano huo na kuhoji kama makosa ya kufanya biashara yana uhusiano wowote na kikosi cha polisi wa usalama barabarani.
Kutokana na maelezo hayo na kuwepo wafanyabiashara wengine waliojitokeza kutaka kuzungumza, Mama Kilango aliwataka wafanyabiashara hao kuteua wawakilishi watano ambao angekutana nao jana jioni kupata picha halisi ya kero hiyo.
Suala la Machinga limekuwa kete ya kisiasa na Ndesamburo aliwahi kununua eneo kwa ajili ya kuanzisha soko la wafanyabiashara hao wadogo, lakini inadaiwa kuwa aliwekewa vizingiti na Halmashauri ya Manispaa ya Moshi, uamuzi ambao unadaiwa kuzidisha hasira ya wafanyabiashara dhidi ya CCM.
Jimbo la Moshi Mjini limekuwa likishikiliwa na upinzani tangu mwaka 1995 likianzia kwa Joseph Mtui wa NCCR (1995-2000) na Philemon Ndesamburo wa Chadema ambaye ameshikilia Jimbo hilo kwa vipindi viwili mfululizo (2000-2005 na 2005 hadi 2010).
Mwaka 1995, CCM ilimsimamisha mkuu wa Itifaki, kapteni mstaafu, Abubakar Nkya ambaye alishindwa vibaya na Mtu wa NCCR kabla ya kumsimamisha wakili Elizabeth Minde 2000 na 2005 ambaye hata hivyo hakufua dafu kwa Ndesamburo. Katika uchaguzi wa serikali za mitaa uliomalizika mwezi uliopita, CCM iliibuka na ushindi wa asimia 65 ikinyakua mitaa 39 huku CHADEMA ikichukua mitaa 21.
Maoni yangu:
Huyu mama naona anakoelekea ni kutapatapa ili ccm wamsamehe asingolewe jimboni kwake same, maana anarukia hata miti asiyoweza eti anapiga kambi moshi mjini ili 2010 ndesamburo aanguke
wadau hii imekaaje????