Wafuasi wa Chama cha Azimio la Umoja kinachoongozwa na Raila Odinga wameendelea na maandamano asubuhi hii kama walivyotangaza licha ya Rais wa Kenya William Ruto kusema yupo tayari kutumia Mamlaka aliyonayo kama Amiri Jeshi Mkuu kuzuia maandamano hayo.
Miongoni mwa matukio yaliyoshuhudiwa asubuhi hii ni kuchomwa kwa basi na matairi Barabarani, itakumbukwa juzi Ruto alisema amejaribu kuwaambia Odinga na Wafuasi wake wasiandamane ila wamekataa hivyo akaahidi kwamba wakilazimisha kuandamana watajua hawajui.
Akiongea akiwa eneo la Malava Kaunti ya Kakamega, Ruto alinukuliwa akisema “Nilimuita Odinga nikamuomba asitishe maandamano, wamekataa, Mimi niliwaambia ile wiki nyingine, nikaita yule Mzee wa kitendawili na nikamwambia wewe wacha hii maandamano tupeleke hii maneno yote unasema Bungeni, Wabunge waangalie kama kuna maneno ya ukweli”
“Sasa eti wamekataa hiyo ya kwenda kuongea kwa amani Bungeni, eti wanataka kurudia maandamano, eti waende wavunje mali na kuharibu biashara ya Wananchi, Mimi ndio commander-in-chief, nyinyi mtajua hamjui, waache hiyo mchezo”