SAA 24, tangu tiketi za mchezo wa Simba na Wydad Casablanca sambamba na ule wa Raja Casablanca na Al Ahly ziwekwe sokoni, tiketi hizo zimeuzwa zote huku mashabiki wakitakiwa kulipa Sh 160,000 ili kumwona Jean Baleke akiwa uwanjani.
Michezo hiyo ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa inatarajiwa kupigwa wikiendi hii na mwakilishi wa Tanzania, Simba itakuwa kwenye Uwanja wa Mohammed IV, Ijumaa Aprili 28, kuivaa Wydad huku Raja ikivaana na Al Ahly Aprili 29, kwenye uwanja huo huo.
Kiingilio cha chini cha mchezo kati ya Wydad na Simba ambayo ina mastaa wakubwa, Clatous Chama na Jean Baleke wenye mabao manne kila mmoja kwenye michuano hiyo, ni Dirham 30, sawa na Sh6,000 za Kitanzania, huku kiingilio cha juu ni Dirham 700 (Sh160,000).
Moja ya silaha kubwa za Raja na Wydad ni mashabiki wao wanaojitokeza kwa wingi hususan kwenye mechi muhimu kama hizo na hushangilia kwa nguvu zote kuanzia mwanzo hadi mwisho wa mchezo bila kujali matokeo.