mugah di matheo
JF-Expert Member
- Jul 28, 2018
- 6,276
- 12,336
Ile kesi ya mda mrefu ilieanzishwa na Mchungaji Mtikila imepatiwa ufumbuzi na Sasa serikali ya Tanzania inatakiwa iruhusu Wagombea huru kwenye chaguzi zetu ikiwemo wa uraisi
===
Baada ya Mahakama ya Rufani mwaka 2009 kutengua uamuzi wa Mahakama Kuu uliotamka kuwa wagombea binafsi wana haki ya kushiriki uchaguzi nchini, mtetezi mkuu wa haki hiyo, mwanasiasa machachari, Christopher Mtikila hakukata tamaa.
Mwaka 2011, Mtikila alishirikiana na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kutetea wagombea binafsi katika Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu (AfCHPR).
Katika Mahakama hiyo yenye makao yake makuu Arusha, waombaji hao walitaka itoe tamko kuwa Serikali ilikiuka Ibara ya 2 na ya 13 (1) ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu (African Charter on Human and People’s Rights) kwa kufanya marekebisho ya Katiba yaliyozuia wagombea binafsi.
Pia, waliitaka itoe amri ya kuitaka Serikali ichukue hatua za kikatiba na kisheria kuhakikisha haki za binadamu zilizo chini ya Ibara ya 2 na ya 13 (1) ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu na zile za 3 na 25 za Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kisiasa na Kiraia (ICCPR) zinatekelezwa
Pia, waliiomba Mahakama hiyo iiamrishe Serikali kutoa taarifa mahakamani hapo ndani ya miezi 12 tangu siku ya hukumu kuhusu utekelezaji wa hukumu hiyo
Kwa mujibu wa Mtikila, Katiba ya Tanzania ilikiuka haki yake ya kuungana na wenzake kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi kwa kuzuia wagombea binafsi kugombea urais, ubunge na nafasi za Serikali za mitaa.
Alidai kuwa kitendo cha Serikali kuanzisha mchakato wa mabadiliko ya Katiba na hatimaye kuzuia watu binafsi kugombea urais, ubunge na Serikali za mtaa wakati kukiwa na kesi mahakamani inayosubiri kuamuliwa kuhusu suala hilo, kulikiuka misingi ya utawala bora.
Mtikila alidai kuwa kitendo cha Serikali kilikiuka haki zake chini ya Ibara ya 2, 10 na 13(1) ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu, Ibara za 22, 25 na 26 za mkataba wa ICCPR na Ibara za 1, 7, 20 na 21(1) za Tamko la Kimataifa la Haki za Binadamu.
Mchungaji Mtikila aliitaka Mahakama hiyo ya Afrika itoe tamko kuwa sheria inayozuia wagombea binafsi kugombea katika uchaguzi wa kisiasa ilikuwa inapingana na mkataba wa ICCPR.
Kabla ya kuanza kwa usikilizwaji wa kesi hiyo, Serikali iliweka mapingamizi ya awali kuhusu uhalali wa kupokewa kwa kesi ya Mtikila na mamlaka ya Mahakama hiyo ya Afrika kusikiliza shauri hilo.
Katika pingamizi la kwanza, Serikali ilidai kuwa Ibara ya 62 (2) Itifaki ya AfCHPR inaweka sharti kuwa ili Mahakama hiyo iweze kusikiliza maombi yaliyo mbele yake, mleta maombi alipaswa kutumia njia zote ndani ya nchi yake kabla ya kwenda huko.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) alidai kuwa Mtikila na LHRC hawakufanya hivyo kwa sababu uamuzi wa mwisho wa Mahakama ya Rufani ulitamka kuwa suala hilo ni la kisiasa, hivyo lilitakiwa limalizwe na Bunge. Alidai kuwa njia ya Bunge kumaliza suala hilo bado ilikuwa haijatumika.
Katika pingamizi lingine, AG alidai kulikuwa na ucheleweshwaji usio na sababu kufungua maombi katika Mahakama ya Afrika.
Pia, alidai waleta maombi walichukua muda mrefu kufungua maombi yao.
Wakati Mahakama ya Rufani ikitoa uamuzi wake Juni 17, 2010, waleta maombi walisubiri hadi Juni 2011 kufungua maombi yao.
Pingamizi lingile lililoletwa na Serikali ni kwamba Mahakama hiyo haikuwa na mamlaka ya kusikiliza shauri hilo, ikidai wakati unaodaiwa ukiukwaji huo wa haki za binadamu ukitokea, itifaki hiyo ya kuanzishwa kwa Mahakama ya AfCPHR ilikuwa haijaanza kufanya kazi.
Mwisho wa siku, Mahakama hiyo iliyatupilia mbali mapingamizi yote ya Serikali kwa kutokuwa na msingi na kuendelea kusikiliza kesi hiyo.
Katika hukumu yake ya Julai, 2013, Mahakama ya AfCPHR ilikubaliana na hoja za Mtikila na LHRC kuwa Tanzania ilikiuka haki za raia kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi yao moja kwa moja au kupitia wawakilishi kwa kulazimisha raia kuwa wanachama wa vyama vya siasi ili wapate kibali cha kugombea urais, ubunge na Serikali za mitaa.
Mahakama hiyo ya AfCPHR ikaiamuru Tanzania kuchukua hatua za kikatiba na kisheria ‘kutibu’ ukiukwaji huo wa Katiba.
Mahakama hiyo ya Afrika ilikubali hoja kuwa mkataba wa ICCPR ulilinda haki na uhuru wa kila raia kushiriki bila kuingiliwa katika shughuli za utawala wa nchi, moja kwa moja au kupitia wawakilishi.
Kwa maoni yake, haki hiyo haikumaanishwa ifurahiwe tu na wale walio ndani ya makundi kama vyama vya siasa.
Mahakama ya AfCPHR iliona kitendo cha kuwataka watu kuwa sehemu ya vyama vya siasa au kuteuliwa na vyama vya siasa wanapotaka kuchaguliwa kilikiuka haki zao kujumuika na wengine.
Zaidi ya hapo, mahakama hiyo ya AfCPHR ilisema kwa kufanya mabadiliko ya Katiba yaliyolenga kuzuia wagombea binafsi kugombea nafasi mbalimbali za uongozi, Tanzania ilikiuka wajibu wake chini ya Ibara ya 2 ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu na pia Ibara ya 3 (2) ya mkataba huo.
Ibara hizo zinatambua kuwa kila mtu ana haki ya uhuru na kulindwa bila kubaguliwa kwa namna yoyote, ikiwamo upande wa siasa anaouamini.
Kuhusu hoja ya Mtikila kuwa Tanzania ilikiuka misingi ya utawala bora kwa kupitisha mabadiliko ya katiba yaliyofuta wagombea binafsi ili kukwepa madhara ya uamuzi wa Mahakama Kuu iliyotamka kuwa mabadiliko hayo yalikuwa kinyume cha katiba, Mahakama ya Afrika ilisema kuwa dhana ya utawala bora si dhana ya jumla na isingeweza kujibu hoja ya waleta maombi kwa sababu hawakueleza ukiukwaji wake kuhusiana na haki fulani.
Mahakama hiyo ya AfCPHR ikaielekeza Tanzania kuchukua hatua za kikatiba, kisheria na hatua nyingine zote muhimu ndani ya muda stahiki ‘kutibu’ ukiukwaji wa haki za binadamu kama ilivyoziainisha na iijulishe Mahakama hiyo hatua zilizochukuliwa.
Source: Mwananchi
===
Baada ya Mahakama ya Rufani mwaka 2009 kutengua uamuzi wa Mahakama Kuu uliotamka kuwa wagombea binafsi wana haki ya kushiriki uchaguzi nchini, mtetezi mkuu wa haki hiyo, mwanasiasa machachari, Christopher Mtikila hakukata tamaa.
Mwaka 2011, Mtikila alishirikiana na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kutetea wagombea binafsi katika Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu (AfCHPR).
Katika Mahakama hiyo yenye makao yake makuu Arusha, waombaji hao walitaka itoe tamko kuwa Serikali ilikiuka Ibara ya 2 na ya 13 (1) ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu (African Charter on Human and People’s Rights) kwa kufanya marekebisho ya Katiba yaliyozuia wagombea binafsi.
Pia, waliitaka itoe amri ya kuitaka Serikali ichukue hatua za kikatiba na kisheria kuhakikisha haki za binadamu zilizo chini ya Ibara ya 2 na ya 13 (1) ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu na zile za 3 na 25 za Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kisiasa na Kiraia (ICCPR) zinatekelezwa
Pia, waliiomba Mahakama hiyo iiamrishe Serikali kutoa taarifa mahakamani hapo ndani ya miezi 12 tangu siku ya hukumu kuhusu utekelezaji wa hukumu hiyo
Kwa mujibu wa Mtikila, Katiba ya Tanzania ilikiuka haki yake ya kuungana na wenzake kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi kwa kuzuia wagombea binafsi kugombea urais, ubunge na nafasi za Serikali za mitaa.
Alidai kuwa kitendo cha Serikali kuanzisha mchakato wa mabadiliko ya Katiba na hatimaye kuzuia watu binafsi kugombea urais, ubunge na Serikali za mtaa wakati kukiwa na kesi mahakamani inayosubiri kuamuliwa kuhusu suala hilo, kulikiuka misingi ya utawala bora.
Mtikila alidai kuwa kitendo cha Serikali kilikiuka haki zake chini ya Ibara ya 2, 10 na 13(1) ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu, Ibara za 22, 25 na 26 za mkataba wa ICCPR na Ibara za 1, 7, 20 na 21(1) za Tamko la Kimataifa la Haki za Binadamu.
Mchungaji Mtikila aliitaka Mahakama hiyo ya Afrika itoe tamko kuwa sheria inayozuia wagombea binafsi kugombea katika uchaguzi wa kisiasa ilikuwa inapingana na mkataba wa ICCPR.
Kabla ya kuanza kwa usikilizwaji wa kesi hiyo, Serikali iliweka mapingamizi ya awali kuhusu uhalali wa kupokewa kwa kesi ya Mtikila na mamlaka ya Mahakama hiyo ya Afrika kusikiliza shauri hilo.
Katika pingamizi la kwanza, Serikali ilidai kuwa Ibara ya 62 (2) Itifaki ya AfCHPR inaweka sharti kuwa ili Mahakama hiyo iweze kusikiliza maombi yaliyo mbele yake, mleta maombi alipaswa kutumia njia zote ndani ya nchi yake kabla ya kwenda huko.
Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) alidai kuwa Mtikila na LHRC hawakufanya hivyo kwa sababu uamuzi wa mwisho wa Mahakama ya Rufani ulitamka kuwa suala hilo ni la kisiasa, hivyo lilitakiwa limalizwe na Bunge. Alidai kuwa njia ya Bunge kumaliza suala hilo bado ilikuwa haijatumika.
Katika pingamizi lingine, AG alidai kulikuwa na ucheleweshwaji usio na sababu kufungua maombi katika Mahakama ya Afrika.
Pia, alidai waleta maombi walichukua muda mrefu kufungua maombi yao.
Wakati Mahakama ya Rufani ikitoa uamuzi wake Juni 17, 2010, waleta maombi walisubiri hadi Juni 2011 kufungua maombi yao.
Pingamizi lingile lililoletwa na Serikali ni kwamba Mahakama hiyo haikuwa na mamlaka ya kusikiliza shauri hilo, ikidai wakati unaodaiwa ukiukwaji huo wa haki za binadamu ukitokea, itifaki hiyo ya kuanzishwa kwa Mahakama ya AfCPHR ilikuwa haijaanza kufanya kazi.
Mwisho wa siku, Mahakama hiyo iliyatupilia mbali mapingamizi yote ya Serikali kwa kutokuwa na msingi na kuendelea kusikiliza kesi hiyo.
Katika hukumu yake ya Julai, 2013, Mahakama ya AfCPHR ilikubaliana na hoja za Mtikila na LHRC kuwa Tanzania ilikiuka haki za raia kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi yao moja kwa moja au kupitia wawakilishi kwa kulazimisha raia kuwa wanachama wa vyama vya siasi ili wapate kibali cha kugombea urais, ubunge na Serikali za mitaa.
Mahakama hiyo ya AfCPHR ikaiamuru Tanzania kuchukua hatua za kikatiba na kisheria ‘kutibu’ ukiukwaji huo wa Katiba.
Mahakama hiyo ya Afrika ilikubali hoja kuwa mkataba wa ICCPR ulilinda haki na uhuru wa kila raia kushiriki bila kuingiliwa katika shughuli za utawala wa nchi, moja kwa moja au kupitia wawakilishi.
Kwa maoni yake, haki hiyo haikumaanishwa ifurahiwe tu na wale walio ndani ya makundi kama vyama vya siasa.
Mahakama ya AfCPHR iliona kitendo cha kuwataka watu kuwa sehemu ya vyama vya siasa au kuteuliwa na vyama vya siasa wanapotaka kuchaguliwa kilikiuka haki zao kujumuika na wengine.
Zaidi ya hapo, mahakama hiyo ya AfCPHR ilisema kwa kufanya mabadiliko ya Katiba yaliyolenga kuzuia wagombea binafsi kugombea nafasi mbalimbali za uongozi, Tanzania ilikiuka wajibu wake chini ya Ibara ya 2 ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu na pia Ibara ya 3 (2) ya mkataba huo.
Ibara hizo zinatambua kuwa kila mtu ana haki ya uhuru na kulindwa bila kubaguliwa kwa namna yoyote, ikiwamo upande wa siasa anaouamini.
Kuhusu hoja ya Mtikila kuwa Tanzania ilikiuka misingi ya utawala bora kwa kupitisha mabadiliko ya katiba yaliyofuta wagombea binafsi ili kukwepa madhara ya uamuzi wa Mahakama Kuu iliyotamka kuwa mabadiliko hayo yalikuwa kinyume cha katiba, Mahakama ya Afrika ilisema kuwa dhana ya utawala bora si dhana ya jumla na isingeweza kujibu hoja ya waleta maombi kwa sababu hawakueleza ukiukwaji wake kuhusiana na haki fulani.
Mahakama hiyo ya AfCPHR ikaielekeza Tanzania kuchukua hatua za kikatiba, kisheria na hatua nyingine zote muhimu ndani ya muda stahiki ‘kutibu’ ukiukwaji wa haki za binadamu kama ilivyoziainisha na iijulishe Mahakama hiyo hatua zilizochukuliwa.
Source: Mwananchi