Kujificha au kuzamia "stoway" kwenye chumba cha gurudumu za ndege "Landing Gear Bay" ni moja ya maamuzi hatari zaidi ambayo mtu anaweza kuchukua.
Takwimu zinaonyesha kuwa asilimia kubwa ya wanaojaribu hupoteza maisha kabla ya kufika safari.
Mara ndege inapopaa, hatari ya kwanza ni kupondwa na matairi yanaporudi ndani. Sehemu hiyo imetengenezwa kubana bila kuacha nafasi, hivyo mwili wa mtu unaweza kubanwa na mfumo mzito wa mitambo "Hydraulics Cylinders".
Ndege inapoendelea kupanda kufika futi 30,000 hadi 40,000, shinikizo la hewa hushuka kwa kasi na kusababisha ukosefu mkubwa wa oksijeni.
Hali hiyo humfanya mtu apoteze fahamu haraka na kupata uharibifu wa ubongo (Hupoxia) au kufa kwa kukosa hewa
Kwa wakati huo huo joto hushuka hadi nyuzi joto hasi 60 (- 60°C).
Baridi hiyo kali inafanya mwili ugande na kupata madhara mabaya yasiyoweza kupona.
Kelele kali za injini pamoja na upepo mkali pia huongeza uharibifu wa kibaiolojia mwilini kwa muda wote wa safari.
Hatari ya mwisho hutokea wakati ndege inapoanza kushuka kwenda kutua.
Milango ya sehemu ya gurudumu hufunguka ghafla ili kutoa gurudumu nje.
Mtu aliyepoteza fahamu au kudhoofika kwa baridi kali na ukosefu wa hewa ya oksijeni hushindwa kujishikilia na huanguka kutoka angani.
Kwa mujibu wa rekodi za Mamlaka ya Usafiri wa Anga ya Marekani, tangu mwaka 1947 kumekuwa na zaidi ya matukio 113 hadi 129 duniani kote ya watu kujificha kwenye chumba cha gurudumu za ndege.
Kati yao zaidi ya watu 86 hadi 100 wamepoteza maisha. Hii inamaanisha kiwango cha vifo ni takriban asilimia 76 hadi 77.
Ni watu 29 tu ndio waliorekodiwa kunusurika, na wengi wao walikuwa kwenye safari fupi ambapo ndege haikupanda hadi umbali wa juu kwenye baridi kali.
Takwimu zinaonyesha kuwa wote waliojaribu walikuwa wanaume, wengi wakiwa vijana chini ya miaka 30.
Zaidi ya asilimia 77 ya matukio yametokea katika viwanja vya ndege vya nchi zinazoendelea au zenye migogoro, hasa barani Afrika na eneo la Caribbean, ambapo vijana hao walikuwa wakijaribu kukimbilia Ulaya au Amerika ya Kaskazini kutafuta maisha bora au usalama.