MOSCOW - Chombo huru cha habari cha Astra kimeripoti kuwa ndege za kivita za Urusi zimedondosha kwa bahati mbaya angalau mabomu 334 ndani ya Urusi na katika maeneo ya Ukraine yanayokaliwa na Urusi tangu kuanza kwa uvamizi Februari 2022. Kati ya hayo, mabomu 26 yamedondoka mwaka huu pekee.
Mhariri mkuu wa Astra, Anastasia Chumakova, amesema idadi hiyo ni makadirio ya tahadhari na imejumuisha tu matukio yaliyothibitishwa na vyanzo vya huduma za dharura, mashahidi na ushahidi wa picha.
Uchunguzi unaonyesha kuwa silaha kubwa zinazosababisha matukio hayo ni mabomu ya kuruka kwa kuelekezwa "glide bombs". Mabomu haya huwekewa kifaa maalum kinachoitwa "UMP glide kit" chenye mabawa madogo yanayofunguka baada ya kurushwa, ili bomu liweze kuelea umbali mrefu na kushambulia malengo yakiwa ndani ya anga ya Urusi, mbali na mifumo ya ulinzi wa anga ya Ukraine.
Hata hivyo, wakati mwingine mabawa hayo hushindwa kufunguka.
Ruslan Loyev kutoka kikundi cha uchunguzi "Conflict Intelligence Team" anaamini tatizo linaweza kuwa ni hitilafu katika vilipuzi vidogo vinavyoanzisha mfumo wa chemchemi unaofungua mabawa. Anasema pale kinaposhindwa, bomu hugeuka kuwa bomu la kawaida linaloanguka moja kwa moja badala ya kuruka kuelekea lengo.
Wataalamu wengine wanasema msongo wa kazi pia una mchango.
Mwandishi wa masuala ya ulinzi wa BBC, Pavel Aksyonov, amesema ndege za mabomu zinaporudi kutoka misheni moja na kutumwa mara moja kwenye nyingine bila kupata matengenezo ya kutosha, ubora hupungua na kusababisha makosa mengi.
Kiongozi wa utawala wa Kharkiv, nchini Ukraine, Oleh Syniehubov, amesema Urusi imefanya mashambulizi 473 kwa kutumia mabomu hayo katika eneo hilo tangu mwanzo wa mwaka 2026 hadi Juni 29.
Mabomu yanayodondoka kwa bahati mbaya mara nyingi hayatangazwi rasmi na mamlaka za Urusi, lakini ripoti zinaonyesha yamesababisha vifo, majeruhi na uharibifu mkubwa wa mali.
Wachambuzi wanasema kwa kuwa mabomu ya kuruka kwa kuelekezwa bado ni silaha kuu katika ghala la silaha la Urusi, basi hasara zinazotokana na kudondoka kwa bahati mbaya zitaendelea kuchukuliwa kama sehemu ya gharama ya vita.
@bbcswahili