Mkutano wa pili unaojiita kama "Wa kilele wa demokrasia duniani" ulioandaliwa na serikali ya Marekani utafanyika hivi karibuni, na moja ya kumbi ndogo itakuwa barani Afrika lakini hadi sasa, ni nchi 16 tu kati ya 54 za Afrika ambazo zimethibitisha kuhudhuria. Hii imeonyesha kwa mara nyingine kuwa nchi nyingi za Afrika hazina hamu tena na "Demokrasia ya mtindo wa Kimarekani".
Katika miaka ya hivi karibuni, Marekani imekumbwa na mdororo mkubwa wa kidemokrasia, hali ambayo imeshuhudiwa na jamii ya kimataifa.
Mwaka 2021, wafuasi wa Rais wa zamani wa Marekani, Donald Trump ambao hawataki kukubali matokeo ya Uchaguzi Mkuu, walivamia kwa nguvu Bunge la Marekani, na kuwakumbusha watu juu ya udhaifu wa mfumo wa Demokrasia wa Marekani.
Katika uchaguzi wa katikati ya muhula nchini Marekani mwaka jana, mamilioni ya Wamarekani wenye asili ya Afrika na wengine waliotoka makundi ya watu wachache walinyimwa na kuwekewa vikwazo vya haki za kupiga kura, jambo ambalo lilifanya watu watilie shaka kama Marekani inafuata ahadi yake kuhusu demokrasia.
Aidha, mapambano ya sasa ya vyama viwili nchini Marekani yamezidisha mgawanyiko wa kisiasa, na vyombo vya habari na mitandao ya kijamii inakuwa mashine za uenezaji wa habari potofu za kisiasa. Kama ilivyosema taasisi ya Brookings ya Marekani, mfumo wa demokrasia wa Marekani uliowahi kujivunia unazorota kwa kasi na kuleta madhara makubwa kwa siasa, uchumi, jamii, na hata uhalali na maendeleo ya baadaye ya ubepari.
Hata hivyo, Marekani ambayo demokrasia yake ina kasoro kubwa namna hiyo inaendelea kuitetea duniani kote, na kutoa vikwazo vya upande mmoja kwa nchi nyingine kwa kutumia visingizo vya haki za binadamu na demokrasia, ambavyo vinakiuka haki za kuishi na maendeleo ya watu wa nchi hizo.
Takwimu zinaonyesha kuwa kutokana na vikwazo vya muda mrefu vilivyowekwa na Marekani, kumekuwa na msukosuko mkubwa wa kibinadamu kote nchini Sudan, na asilimia 38 ya watoto walikufa kwa utapiamlo.
Wakati huohuo, vikwazo vilivyowekwa na Marekani na nchi nyingine za Magharibi dhidi ya Zimbabwe katika miongo miwili iliyopita vimesababisha nchi hiyo kupata hasara ya kiuchumi ya zaidi ya dola bilioni 40 za kimarekani. "Demokrasia" imekuwa "silaha ya kuangamiza" mkononi mwa Marekani, ambayo hutumiwa kudhibiti nchi nyingine na kudumisha nguvu zake.
Duniani hakuna demokrasia bora zaidi, wala mtindo wa kidemokrasia unaofaa wote. Kihistoria, nchi nyingi za Afrika zilifuata demokrasia ya kimagharibi baada ya kujipatia uhuru. Hata hivyo, kwa zaidi ya nusu karne, demokrasia ya aina hiyo imeonyesha mapungufu yake makubwa barani Afrika, na moja ya dalili muhimu ni mapinduzi ya kijeshi yaliyotokea mara kwa mara na misukosuko ya kisiasa. Tatizo ni kwamba hii ni demokrasia iliyowekwa na nchi za magharibi kwa Afrika, sio chaguo la watu wa Afrika katika mchakato wa kuitafuta wenyewe.
Katika miongo kadhaa iliyopita, China imetafuta na kuendeleza demokrasia ya umma katika mchakato mzima kwa mujibu wa hali yake ya kitaifa. Ni njia ya demokrasia ambayo ni tofauti kabisa na ya kimagharibi kisiasa, kihistoria na kitamaduni.
Kwa mujibu wa matokeo ya utafiti wa maoni ya watu nje ya nchi wa "Mitindo ya demokrasia duniani" ulioandaliwa na jopo la washauri bingwa la kituo cha CGTN cha Shirika Kuu la Utangazaji la China CMG pamoja na Chuo Kikuu cha Renmin cha China, 75.4% ya watu waliohojiwa duniani wanaamini kwamba ni kutokana na kufuata mfumo wa kisiasa unaotofautiana na ule wa kimagharibi, China imepata maendeleo makubwa yanayoshangaza dunia, na kati ya wahojiwa wenye maoni hayo, wengi walitoka nchi za Afrika, na kufikia 83.1%.
Nchi nyingi za Afrika zimetambua kwamba watu wa Afrika wana haki ya kufuata mtindo wao wa kidemokrasia na kuondokana na utegemezi wao kwa Magharibi. Demokrasia ni kwa ajili ya kutatua matatizo halisi yanayowakabili watu, na kufuata ahadi na haki za kisiasa na uhuru wa watu na kutafuta maendeleo na utulivu kwa pamoja ndio demokrasia inayofaa Afrika.