Mzee Mwanakijiji
Platinum Member
- Mar 10, 2006
- 33,476
- 39,995
Habari kwamba mitambo ya kufulia umeme ya Dowans imeshauzwa kwa kampuni ya kigeni wakati sakata lao na Serikali ya Tanzania halijaisha ni habari za kukera, kuuddhi na zenye kukejeli uwezo wa Watanzania kusimamia maslahi yao. Kwa muda mrefu sasa tangu sataka la Richmond tumeweza kudokeza na kuonesha jinsi gani kampuni ya Dowans iliingia nchini kiulaghai na kufanikiwa kuchotewa mabilioni ya fedha za walipa kodi wa nchi yetu.
Siyo hivyo hivyo tu tumeshuhudia katika muda huu wote ni jinsi gani Rais Kikwete na serikali yake wamekuwa dhaifu kama mbwa mbele ya chatu inapokuja kampuni ya Dowans kwa sababu ambazo sote tunazijua kuu ni kuwa mmiliki wa Dowans ni rafiki wa karibu wa Meneja wa kampeni ya Urais ya Kikwete 2005 Brig. General Al-Adawi wa UAE na alikuwa mfadhili wa mamilioni ya fedha wa kampeni hiyo.
Tulionesha huko nyuma jinsi gani kampuni hii ya Dowans iliingizwa kinyemela na kupewa urithi wa mkataba tata wa Richmond ambayo kesi yake sasa imehamishiwa Dubai, UAE!! na jinsi gani serikali ilikuwa na kila haki ya kisheria kuichukua mitambo hiyo na kuitaifisha kama tu ingekuwa na ujasiri wa kuongoza.
Matokeo yake kama watoto waliodekezwa serikali yetu ikaendelea kuremburiana machona Dowans hadi imefika mahali kuwa mitambo hiyo imeweza kuuzwa huku Waziri Ngeleja, Waziri Mkuu PInda, na Rais Kikwete wakiangalia wasijue la kufanya. Haya yote yamefanyika kwa sababu ya kiburi cha watu wachache, kiburi ambacho bila ya shaka kitaendelea kuligharimu taifa letu zaidi katika sekta hii ya nishati ya umeme.
Hii imetuacha wapi?
mitambo ya Dowans imeshauzwa kwa kampuni ambayo haitajwi (natabiri kuwa tutalazimika kununua umeme kutoka kwa kampuni hiyo mpya pindi wakianza mgao tena - muda si mrefu ujao); matokeo yake:
a. Hata kama tukitaka kuikamata mitambo hiyo sasa hivi hatuwezi kwani siyo ya Dowans tena
b. Kama tukitaka umeme tunaweza sasa kununua kwani tutakuwa tunanunua kutoka kwa kampuni nyingine na siyo Dowans.
c. Fedha ambazo tumeshawalipa kwa kusafirisha mitambo.. Bil. 40 ndio zimeshaliwa na siyo Kikwete wala Ngeleja watakaozipigania zirudi.
d. Kampuni ya Dowans itaanza mchakato muda si mrefu wa kufilisiwa na kutokomea nchini kama ilivyo kawaida ya kampuni za kitapeli.
e. CCM wataomba kura tena wakiahidi kutatua tatizo la nishati na watanzania kama waliorogwa watawapa tena!!
Kuna kila dalili kuwa Watanzania ni watu wa ajabu zaidi duniani kwani hawahusishi matatizo yao ya maisha ya kila siku na uongozi wa kisiasa uliopo madarakani. Wengi wao wanaamini yote yametokea kwa "mapenzi ya Mungu" na kwa "bahati mbaya" na hukesha wakiombea kuwa hali ije kugeuka kuwa nzuri.