Pole sana kwa yaliyokupata. Usikate tamaa. Kila jambo lina sababu ya kutokea. Kwa kawaida, ni vizuri mtu akaeleza sababu inayomfanya afikie uamuzi huo. Lakini ikitokea hatoi sababu, basi usiruhusu hali hiyo ikutese. Jipe moyo, ukiamini kwamba kwa namna moja au nyingine Mungu amekuepusha na jambo fulani. Mimi ninaamini kabisa, ya kwamba wakati wako unakuja na furaha yako itakamilika.
Jambo la msingi, lipokee na usiendelee kulitafakari. Kwa sababu kadri unavyoendelea kutafakari sababu zilizomfanya afikie hayo maamuzi, ndivyo unavyojiweka kwenye hatari ya kuumia zaidi. Katika maisha, kuna wakati jambo moja ni lazima liharibike ili jipya lije. Kuna watu wanatakiwa kuondoka maishani mwako, ili wengine waingie. Hayo ni mapito, yanapita, na wewe utabaki ukiwa imara, na maisha yataendelea.
Mwisho kabisa, usijiwekee mpaka au ukuta wa kihisia au kimtazamo, wenye lengo la kukuzuia usisonge mbele kimaisha au kimahusiano. Jipe nafasi nyingine, pale utakapokuwa tayari kuingia kwenye uhusiano mpya. Binafsi, ninaamini, kwamba dunia hii ina watu wema na wazuri ambao wanafahamu nini maana ya upendo na jinsi ya kuuishi. Muombe Mungu, na siku moja atakukutanisha na mmoja wao, na kamwe hutokumbuka ulikotoka. Machozi yako yatageuka kuwa furaha, na amani itatawala moyoni mwako.
Ninaamini kabisa, unastahili kuwa na furaha. Nakutakia kila la heri, Mungu akupe furaha unayostahili kuipata maisha yako yote. Yaliyopita yamepita, ni saa ya kusonga mbele.
Asante, ninaamini kwa mchango huu, na michango ya wengine, utapata kitu cha kukusaidia.