Kitabu: Simba wa Tsavo

Lycaon pictus

JF-Expert Member
Jan 31, 2021
7,204
12,698


kitabu hiki kiliandikwa mwaka 1907 na JH Patterson kikiitwa The man-eaters of Tsavo. kilitafsiriwa kwa kiswahili miaka ya 1960's kikiitwa Simba wa Tsavo. Unaweza kukisoma bure ndani ya Maktaba app(by pictuss), app hiyo ipo playstore.

1630704064473.png



SURA YA I

KUFIKA KWANGU TSAVO

SIKU HIYO, ikapata adhuhuri, nikaona tunaingia Mombasa, bandari moja nyembamba yenye taabu na hatari kabisa kuiingia katika pwani ya Afrika ya mashariki. Tuliingia Mombasa tarehe 1, mwezi wa Machi, mwaka 1898.

Tuliikuta bandari imetapakaa majahazi ya Waarabu. Moyoni mwangu nalikuwa na mashaka sana, nikifikiri jinsi manahodha wa vyombo vidogo kama hivi walivyoweza kusafiri toka bandari hata bandari kama walivyokwisha zoea wenyewe bila msaada wa dira na jinsi wanavyomudu kuvuka salama katika dhoruba za mawimbi zifikazo hata bahari za mashariki katika majira fulani ya mwaka.

Merikebu yetu ilipokuwa ikienda kutia nanga, nilikumbuka moyoni visa vingi vya matendo yaliyotendwa na maharamia na wauzaji wa watumwa, ambavyo, nilipokuwa mtoto nalipendelea mno kuvisoma. Ndipo mahali papa hapa yule msafiri mkuu Vasco da Gama alipofika katika mwaka 1498. Katika njia kuu, Mombasa-ambavyo ingekuwa haki yake kuitwa barabara ya vasco da Gama-mpaka leo hivi upo mnara wa ajabu usemwao kuwa ulijengwa na baharia huyu ili uwe ukumbusho wa kufika kwake Mombasa.

Kusudi langu lililonileta huku Afrika ya Mashariki ni kushika kazi ya kuendeleza kuchimba reli inayokwenda Uganda. Kwa hiyo nilimwuliza mmoja wa mabwana Forodha anionyeshe mahali ilipokuwa afisi kuu ya reli, nami nikaambiwa kuwa afisi hiyo iko mahali kunakoitwa Kilindini, kiasi cha mwendo wa maili tatu ng’ambo ya pili ya kisiwa. Nilivyokuwa na bahati njema, nikapata troli moja inayosukumwa na waswahili wawili. Haya, nikapitishwa mbio njiani, ambayo huko nje ya mji ilipita katika sehemu kubwa iliyoshikamana miembe, mibuyu, migomba, na minazi iliyofungamana na mitambaazi yenye maua mengi ya kupendeza katika matawi yake.

Nilipokuwa nimefika Kilindini nikashika njia kwenda kwenye Afisi za reli, huko nikaambiwa kuwa maskani yangu yatakuwa bara na ya kuwa nisubiri kupata maagizo mengine zaidi baada ya siku au mbili hivi. Palikuwa na minazi mikinda mingi iliyofanya vivuli; nikapiga hema langu karibu na reli ya gari, ikawa tena nikijishughulisha kutembeatembea mjini nikinunuanunua vifaa na mahitaji yatakayonifaa huko bara nitakakokaa kwa muda mrefu.

Nalikaa mombasa kiasi cha juma zima hata tena nikaingiwa na wasiwasi wa safari yangu. Siku mojaasubuhi nikapata barua; kuisoma, nikaona ni ya kuniamuru kuondoka kwenda Tsavo, kiasi cha mwendo wa maili mia moja na thelathini na mbili hivi toka Mombasa mjini, nikashike kazi ya kuchimba reli ambayo ndiyo kwanza wakati huo iishilie hapo. Asubuhi yake mchana tukaondoka; baada ya mimi, bwana Anderson, msimamizi wa kazi, na daktari, McCullock, bwana mganga mkuu, katika gari letu maalum tulilofungiwa.

Baada mwendo wa maili ishirini, gari letu likaelekea moja kwa moja upande wa juu, tukipita ndani ya vichaka vizuri vilivyoshikamana. Kila mara tulipochungulia madirishani kutazama nyuma tunakotoka, tuliweza kuona upeo wa Mombasa na Kilindini pamoja na bahari yake ikimeremeta kwa jua kwa mbali kiasi cha upeo wa jicho. Kiasi cha kupita vilima vya Rabai tukaingia katika mbuga ya jangwa la taru, nyika yenye vichaka duni kabisa na miti mifupi mifupi ambayo wakati wa kiangazi ni kama vumbi jekundu tupu. Gari wakati wa kupita katika nyika hii vumbi hilo lilipenya ndani likatapakaa kila mahali. Katika sehemu hii wanyama hawakuonekana kwa sababu ya vichaka vingi. Ingawaje, walakini, tuliweza kuwaona wachache wao madirishani, pia tukawaona Wanyika, wenyeji wa nchi hiyo.

Mwisho wa mbuga hii yenye vumbi jekundu ni Maungu, kiasi cha mwendo wa maili themanini tokea Mombasa mjini, kwani kutoka hapo vumbi lake ni la rangi nyingine. Tokea hapo hatukuvuta hatua mara tukaingia Voi, kiasi cha mwendo wa maili mia moja kutoka Mombasa mjini, kwa kuwa hapa ni kituo kikuu ambacho tulikuwa hatujapata kufika, tukatua kidogo ili kutazama jinsi kazi ilivyokuwa ikiendelea. Katika kuendelea na safari yetu, huko mbele tuliona kuwa hali ya nchi imebadilika na ni ya kupendeza. Tokea mji uitwao Ndii, kwa mwendo mrefu reli imepita katikati ya mbuga yenye vichaka vingi vilivyopendeza mno kuliko nyika tuliyokwisha ipita. Kushotoni kwetu tuliweza kuona safu ya milima ya Ndii, nchi ya Wataita, na kwa upande wa kulia kulikingamiwa na genge la Ndungu lililozunguka kwa mbali upande wa magharibi. Hapa mwendo wetu ukawa wa taratibu kwa kuwa kila mara ilitubidi kusimama kutazama maendeleo ya kazi za kila siku zinazofanywa; vivyo hivyo kidogo kidogo hatimaye tukafika Tsavo mwisho wa safari yetu. Usiku ule nililala katika kibanda cha makuti kilichokuwa kimejengwa na wasafiri wenzangu waliotangulia. Kibanda chenyewe kilikuwa karibu kuanguka na hasa kilichakaa mno, mwisho hata mlango hakina; usiku nilipokuwa nimejinyoosha penye kirago changu naliweza kuona nyota zikiangaza kwa nje juu ya paa. Sikujua hatari gani zilizokuwa jirani nami, kama ningalijua kwamba wakati ule ule walikuwapo wanyama wawili habithi wakizungukazunguka kutafuta watakachoweza kupata wajilie, sidhani kama ningalipata usingizi katika kibanda kibovu kama hicho.

Asubuhi yake naliamka na mapema kabisa. Nilipanda juu ya kilima kidogo kilichokuwa karibu yangu, nikaona kuwa nchi yote, kwa kadiri ya upeo wa macho yangu, ni miti mitupu mifupi mifupi iliyoshikamana na miiba ya ‘subiri kidogo.’ Mahali palikuwa peupe ni sehemu ile iliyochimbwa reli tu. Mbali kwa upande wa kusini naliweza kuona pepesi za kilele chenye theluji cha mlima Kilimanjaro. Karibu ni mto Tsavo. Mto huu huenda kwa kasi kabisa nao haukauki; maji yake sikuzote yanazizima, na kwa pande hizi za Afrika ya Mashariki, mito iendayo hivi ni michache.

Nilirudi kibandani kwangu, nikatumia juhudi yangu yote kujitengenezea maskani yangu. Vitu vikafunguliwa na watumishi wangu wakanipigia hema langu mahali peupe kidogo karibu na pale kibandani nilipolala jana na si mbali na kambi ya wafanyaji kazi. Wakati huu reli ilikuwa imefika upande wa magharibi ya mto na kambi ya makuli wa Kihindi na vibarua wengine ilikuwa huko huko.
 
SURA YA II

MWANZO WA KUTOKEA NYAMAUME

KWA BAHATI mbaya raha ya kazi yetu haikuendelea kwa muda mrefu mara tukaingiliwa na mambo ya kitisho. Tuliingiliwa na nyamaume kambini, simba wawili wa ajabu, na kwa muda wa zaidi ya miezi tisa ikawa ni haika haika ya kila mara kwa wote waliohusika na kazi ya reli karibu ya Tsavo. Hayo yalianza katika mwezi wa Desemba, mwaka 1898, simba waliposimamisha kabisa kazi ya kuchimba reli kwa muda wa majuma matatu. Walipoanza kutushambulia hawakupata kumchukua yeyote katika kila usiku lakini baadaye hawakuogopa hatari yoyote. Walitumia hekima zote walizojaliwa nazo wakachagua nyakati maalum za kunyemelea watu; kwa mwendo huu walifanikiwa mno hata wafanyaji kazi wote wakaamini kuwa hao si simba hasa ila ni shetani waliojigeuza simba. Kwa hofu yao, wale makuli walinithibitishia kuwa nisijisumbue bure kujaribu kuwapiga bunduki. Walikiri kabisa kwamba ni mizimu ya masultani wawili waliokufa iliyozinduka kwa ghadhabu ikajigeuza umbo lile ili kuzuia njia ya reli isipitishwe katika nchi yao, na vile wanazuia isiendelee tena wapate kulipa kisasi.

Si muda mwingi, baadaye, kuli mmoja au wawili hivi walinipotea nikaambiwa kuwa walichukuliwa usiku katika mahema yao wakaliwa na simba. Habari yenyewe sikuitia maanani sana wakati ule. Ilivyokuwa ni kwamba wao walikuwa wafanyaji kazi hodari na kila mmoja alikuwa na pesa nyingi hivyo nikafikiri kwamba kuna baadhi ya watu katika jumla ya wale watu waliowaua wenzao kwa kijicho cha pesa zao. Lakini ilitukia siku moja asubuhi kadiri ya saa tatu au nne hivi, naligutushwa nikaambiwa kuwa jemedari wangu mmoja wa Kikalasinga jina lake Ungan Singh shujaa mwenye nguvu barabara, amechukuliwa usiku katika hema lake akaliwa na simba.

Kusikia hivyo sikuwa na subira yoyote kulichungua jambo lenyewe, na kwa kweli niliamini kwamba mtu huyo alichukuliwa na simba, kwa kuwa nyayo zake zilionekana waziwazi na mburuzo wa visigino vya yule mtu aliyekamatwa vilionyesha welekeo alikoburuziwa. Zaidi ya hayo, jemadari Ungan Singh alikuwa na wenziwe aliokuwa akilala nao katika hema lake kadiri ya watu sita, na mwenziwe mmoja aliyekuwa akilala naye kitanda kimoja alishuhudia hasa kiki-kiki hiyo ikipita nje. Yeye, maskini, alieleza dhahiri jinsi simba kadiri ya saa sita ya usiku alivyojipenyeza ghafula katika hema ambalo mlango wake ulikuwa wazi akamshika koo Ungan Singh aliyekuwa amelala sawasawa na mlango wa lile hema. Wakati wa kushikwa, Ungan Singh alipiga kelele kwa kikwao: 'Choroo', yaani 'Niachilie', naye basi asikubali, akamshika simba shingoni hodari. Kwa fadhaa ya hofu iliyowaingia wenziwe, wakawa wamejikunja kimya wakisikiliza mbimbirishano nje, na baada ya muda si muda akawa amekwenda kabisa. Hapana shaka Ungan Singh alikufa baada ya pata shika, bali maskini hakuwa na kinga yoyote.

Kusikia habari hii ya kusikitisha, muda ule ule nikatoka kumwandamia yule simba, nikafuatana na Captain Haslem.

Tuliona ni heri kufuata njia ile ile aliyopita yule simba kwamba mwendo wake ulionyesha kutuatua mara nyingi kabla ya kula nyama yake. Tulipofika mahali penyewe na kuchungua sana tukaona kuwa walikuwako simba wawill yumkini walinyang'anyiana ile nyama.

Usiku ule nikapanda juu ya mti karibu ya hema la yule marehemu nikitumai kwamba wale simba watarudi tena kuja kuchukua mtu mwingine. Kule juu ya mti nalifuatwa na makuli wachache waliokuwa na hofu wakataka niwe nao kule juu; wengine wote waliobaki walijifungia kabisa mahemani mwao. Safari hii hakuna hema lililoachwa mlango wazi. Nalikuwa na bunduki yangu ya mianzi miwili, nami nikawa nimekwisha ishindilia. Baadaye nikasikia sauti ya ngurumo zao zikizidi kunisonga niliko, nikatumai kuwa sasa nitaweza kufanya lolote. Punde si punde nikasikia kimya kwa kitambo cha saa au mbili hivi, kwani ni tabia yao simba kunyepelea mawindo yao kimya kabisa. Ghafula tukasikia sauti za fadhaa katika kambi nyingine kiasi cha nusu maili umbali wake, tukajua kwamba simba amekwisha kamata mtu mwingine huko, na kwa hiyo hapo tulipokuwa hatutaona wala kusikia chochote usiku ule.

Kwenda kutazama asubuhi yake nikaona kuwa simba mmoja aliingia katika Kambi ya Mwisho wa Reli akamchukua mtu mmoja maskini aliyekuwa amelala. Kwa hiyo baada ya kupumzika kidogo usiku, nikachagua mti mzuri uliokuwa karibu na hema hilo nikapanda juu. Kwa kweli sikupendelea sana kwenda nusu maili nzima usiku mpaka huko, bali sikuogopa sana kwa kuwa mtu wangu mmoja alifuatana nami ameshika kandili inayowaka sana nyuma yangu. Naye nyuma yake aliandamiwa na mwenziwe aliyekuwa na mbuzi nitakayemfunga chini ya mti nitakaolala juu, kuwa chambo cha simba badala ya kushika mtu. Baada ya kujinega vizuri kule juu ya mti haukupita muda, mvua ikanyesha nami nikaloa chapa chapa, nikashikwa na baridi vibaya. Pamoja na hayo, nikashikilia pale pale nilipokuwa nikitumai kuwa leo nitampiga simba; ewe, mpaka kadiri ya usiku mkuu moyo ulizuka uchungu niliposikia mayowe na hoihoi za vilio zilizonijulisha kuwa wale simba wamenipiga chenga nao wamekamata mtu mwingine mahali pengine.

Wakati huu sasa, kambi nyingine za wafanyajikazi zilijitupa mbalimbali, hivyo ikawa simba wa nafasi nzuri ya kucheza kiasi cha hatua za maili nane huku. Kwa kuwa walikuwa na busara ya kuingia mbalimbali kila usiku, ilikuwa ni shida mno kuweza telea mahali. Isitoshe basi, kuwawinda mchana katika nyika iliyoshikamana kama hiyo hakika ilikuwa ni kazi ya taabu na mashaka kadhalika. Katika msitu mkubwa kama uliozunguka pande zote za Tsavo, mwinda ndiye aliyekuwa mwindwa. Ingawaje, walakini, sikukata tamaa kwamba nalitumai tu kuwa nitapata bahati ya siku moja kugundua pango lao, basi kwa tamasha hiyo, kila nilipopata nafasi ya kupumzika naliutumia wakati huo kwa kunyapianyapia msituni.

Furaha yangu ni kwamba, pamoja na wasiwasi wote huo uliotupata hapo mwanzo, simba wenyewe hawakuwa wakifanikiwa kushika mtu kila usiku, na kwa bahati palipita vichekesho vilivyojaribu kutuondolea mwako huo uliokuwa ukituhangaisha na moyo. Ilitukia siku moja usiku, Baniani mmoja mfanyaji biashara alikuwa amepanda punda wake, akashtukia amekumbwa na simba yeye pamoja na punda wake. Yule punda maskini alijeruhiwa vibaya mno; sasa basi nusura ya yule Baniani ni kwamba yule simba kucha zake zilinasa kwenye kamba iliyokuwa imefungia madebe mawili matupu ya mafuta shingoni mwa yule punda. Sasa katika kuvuta ile kamba yale madebe yakawa yanagongana gongana; simba kusikia ngo ngo ngo za madebe zikizidi kumfuata akatishika mno, na kwa hofu hiyo akaruka ndani msituni. Baniani naye akaona amepata nafasi ya kujiponya akapanda mti mmoja uliokuwa karibu yake, akalala mtini hali anatetemeka mwili mzima mpaka kulipokucha.

Baada ya mkasa huu haukupita muda, ukatokea mtu mwingine wa akida mmoja wa Kigiriki, jina lake Themistocles Pappadimitrini, aliyeponea nusura vivyo hivyo. Yeye alikuwa amelala katika hema lake akaingiliwa na simba, na kwa bahati, simba, badala ya kushika mtu, akavamia tandiko alilokuwa amelalia yule Giriki akaondoka nalo. Yule Giriki ingawa aliamka kwa fadhaa lakini alisalimika kabisa wala hakudhurika na lolote zaidi ya hofu aliyokuwa nayo.

Mkasa mwingine ni kuwa siku moja usiku makuli kumi na wanne walikuwa wamelala katika hema lao wakashtukia simba amewaingilia ndani kwa kurukia juu ya hema. Kutua kwa simba, mkono wake mmoja ulifikizia juu ya bega la kuli mmoja likavunjika vibaya mno; kwa fadhaa ya yule simba, badala ya kushika mtu akanyanyua gunia la mchele lililokuwa mle ndani akaondoka nalo, naye huko mbele alipobaini ubaradhuli wake akalitupilia mbali kwa chuki.

1630622230998.png
 
SURA YA III

HEKAHEKA KATIKA BEHEWA LA MIZIGO



WAKATI WOTE huu hema langu lilikuwa limepigwa mahali peupe kabisa pasipokuwa na boma lolote. Wakati nilipokuwa nikikaa pamoja na Daktari Rose, siku moja katikati ya usiku tuligutuka kwa kusikia kitu nje kikikungwaakungwaa katika kamba za hema letu, bali tulipotoka nje na taa hatukuona chochote. Kulipokucha asubuhi yake tukaona nyayo za simba, na kwa ishara hiyo nikaona tumenusurika kidogo tu. Kwa kuona mkasa huo nikaazimu kuhamisha maskani yangu kwenda kukaa pamoja na Daktari Brock, ambaye ndiyo kwanza afike Tsavo kuja kushika kazi ya udaktari wa nchi ile.

Tulikaa katika kibanda kimoja tulichokuwa tumekijenga upande wa mashariki ya mto karibu ya njia ya miguu iendayo Uganda, nasi tukakizungushia boma. Watumishi wetu nao walikuwa mle mle ndani ya boma na sikuzote huwashwa moto mkali usiku kucha. Kwa ajili ya kutaka baridi, mimi na mwenzangu Brock tulipendelea mno kukaa nje barazani nyakati za magharibi. Tukatumia ushupavu wetu tu hapa kujaribu kusoma au kuandika kwani hatukujua wakati gani simba atakapotuingilia mle bomani na kutuvamia. Kwa hiyo bunduki zetu tuliziweka karibu karibu sana, tukawa twaangazaangaza macho kwa wasiwasi kwa mbele kabisa ya upeo wa mwangaza wa moto. Mara moja moja asubuhi, tukaona kuwa simba walikuja karibu kabisa ya lile boma, bali bahati njema hawakudiriki kuingia ndani.

Kadhalika basi, safari hii, kambi za wafanyaji kazi zimezungushiwa maboma ya miiba; ingawaje walakini, waliweza kuruka ndani au kuvunja baadhi ya maboma na kuchukua mtu mmoja mmoja kila baada ya siku mbili tatu, na kila mara huletewa habari za uchungu kabisa kuwa mwenzetu fulani ametutoka. Hata hivyo, walakini, kwa kuwa ile Kambi Kuu ilikuwa na watu zaidi ya elfu mbili au tatu walioenea sehemu kubwa hapo Tsavo, wale makuli hawakujali sana mauti ya kitisho yanayowasibu wenzao. Nashuku kwamba kila mtu aliona kuwa, kwa kuwa wao walikuwa wengi mno, basi, mtu kupatikana ni ajali tu. Sasa basi ile Kambi Kuu ya watu ilipohamishwa mbele mambo yote yalibadilika mno. Pale naliachwa na watu kadiri ya kutosha kumaliza kazi. Pia basi kwa kuwa wale watu niliobaki nao walifanya kambi zao pamoja pamoja, simba nao kadhalika wakazidi kufanya nadhari na machachari yao yakazidi mno. Ikawa watu wakaingiliwa na hofu ile ile kama kwanza, hapo ikanibidi kutumia busara zangu zote ili kusudi kuwatuliza watu wasitoroke. Nami kwa kweli, nisingefanikiwa kuwatuliza kama nisingewaambia waache kazi zote washughulike kujenga maboma mpaka watakapokwisha zungushia kila kambi boma refu la kutosha. Katika kila boma mliwashwa moto usiku kucha; kadhalika ni wajibu wa mshika doria usiku kugonganisha madebe matupu yapatayo sita hivi yaliyokuwa yamefungwa juu ya mti maalum, kwa kuvuta kamba ndefu iliyofungia madebe hayo mtini hali ya kuwa yeye mwenyewe amejifungia ndani ya hema lake. Madebe hayo yalikuwa yakigonganishwa usiku wakati hata wakati ili kusudi kuwatisha wale simba. Lakini haikuwa dawa kitu na watu wakawa wanazidi kupungua.

Wakati ile Kambi Kuu iliposogea mbele, kambi ya hospitali ilibaki nyuma. Ilikuwa mbali na kambi nyingine, mahali peupe hivi kiasi cha mwendo wa maili kasorobo tokea kibandani kwangu, nayo ilikuwa imezungushiwa boma madhubuti. Kinga yenyewe mwishowe ilionekana kuwa haifai kitu kuwazuia wale mahabithi, kwani wakati Fulani simba mmoja aliona mahali dhaifu katika lile boma akapenya. Katika mkasa huu dresa aliponea nusura kabisa. Aliposikia vishindo nje alifungua mlango wa hema lake. alitishika mno alipomwona nyang'au limemsimamia likimtazama. Mara hiyo alimrukia na kwa hofu yule dresa naye akarudi nyuma kwa ghafula akalikumba sanduku lililokuwa na ghasia za dawa. Kwa mshindo wa pamoja na vitakataka vilivyovunjika ndani, simba akafadhaika na papo hapo akarukia upande mwingine wa boma. Hola alikwenda kulivamia hema mlimokuwa na wagonjwa wanane wamelala, akaingia ndani. Wawili wao walijeruhiwa vibaya mno kwa kule kuwavamia kwake, bali maskini wa tatu wao, yeye alishikwa akaburuzwa mzima mzima katika boma la miiba. Wale makuli wawili majeruhi wakabaki papo hapo walipolala wamefutwa na upande mmoja wa hema uliopasuka, nasi, mimi na daktari tulipokwenda asubuhi tuliwakuta katika hali hiyo hiyo waliyokuwa nayo usiku na hema lao limewafunika. Papo hapo tukaazimia kuihamisha kambi ya hospitali karibu zaidi na ile Kambi Kuu. Pakachaguliwa mahali pengine tayari, likajengwa boma madhubuti, na wagonjwa wakahamishwa mapema kabla usiku haujaingia.

Kwa kuwa nalikwisha pata habari kuwa wale simba huenda wakatembeatembea kule kwenye kambi zilizohamwa, nikaazimia kukesha usiku kucha katika lile boma tupu kwa tumaini kwamba nitapata bahati ya kumpiga mmoja wao lakini basi, moyo ulizuka uchungu katikati ya usiku niliposikia mayowe na vilio upande ule wa hospitali mpya, zilizonijulisha dhahiri kwamba wale simba wamekwisha nipiga chenga tena mara ya pili. Asubuhi kulipokucha nikafanya haraka kwenda kule nilikosikia vilio usiku nikaona kuwa simba mmoja aliruka juu ya boma na kumchukua mchotaji maji wa hospitali. Tena nikasikia kuwa makuli wengine wote kwa nuru ya mwanga wa moto mkubwa iliwabidi watazame tu kizaazaa kilichokuwa kikipita. Ilivyotokea ni kuwa yule mchotaji maji alikuwa amelala chini, kichwa chake kilielekea katikati ya hema na miguu yake ilikaribia kugusa mwisho kabisa wa hema. Simba naye akatia kichwa chake kwa chini ya turubali akamshika miguu akamvutia nje. Ikawa yule mtu kwa ujasiri wake naye akakumbatia sanduku zito hodari ili kujizuia asichukuliwe, akakokoteka nalo hata mwisho ikambidi kuliachilia lilipokwama penye pembe ya hema. Hapo naye akapata fahamu ya kushika kamba ya hema, akajizinga nayo hodari mpaka ikakatika. Kiasi cha simba kupata kumtoa nje akamrukia kooni, na baada ya kumtupatupa huku na huku yule mtu akakata roho kabisa. Hapo tena yule simba akamwuma mdomoni kama umwonavyo paka akimshika panya, akarukaruka naye huko na huko mle bomani akitazama mahali dhaifu atakapoweza kuvunja atoke naye. Mara akapagundua, akapenya, huku anaburuza nyama yake akidondosha vipande vya nguo na nyama kama namna ya alama kuonyesha njia aliyopita katika miiba. Hivyo, mimi na Daktari Brock tuliweza kumwandamia, na kwa kiasi cha mwendo wa hatua mia huko vichakani tukakuta masalio yake.

Haya, tukaazimia tena kuhamisha kambi ya hospitali; kadhalika nayo kabla ya jua halijachwa, kazi zote zikawa zimemalizika, walakini safari hii tukaongeza imara na umadhubuti wa boma. Wagonjwa wote wakahamishwa, nami na mwenzangu Brock tukaazimia kukesha usiku ule katika behewa la mizigo lililokuwa kando limeelekea kule kulikokuwa na boma kwanza. Kwa kuwa alasiri ile ile ya tarehe 23, mwezi wa Aprili, wale simba waliwahi kuonekana mahali patatu mbalimbali katika sehemu zilizo jirani kwa hiyo tuliacha mahema mawili yamesimama vile vile mle bomani, tena tukaongezea ng'ombe kidogo kuwa chambo cha wale simba. Kiasi cha maili nne hivi kutoka Tsavo tulisikia kuwa walitaka kumkamata kuli mmoja aliyekuwa akienda peke yake barabarani. Lakini kwa bahati alipata nafasi ya mtini ali hali amezimia kabisa, naye alikaa huko alipokuja teremshwa na Mkuu wa Reli (Traffic Manager) aliyemwona kwa mbali katika gari. Baada ya hapo wale simba walijivuta mpaka karibu ya Stesheni Tsavo, na baada ya muda wa saa mbili simba mmoja alionekana na baadhi wafanyaji kazi akimnyemelea Daktari Brock wakati magharibi alipokuwa akirudi kutoka hospitali.

Kwa namna tulivyoshauriana, mimi na Daktari Brock tukatoka kibandani kwetu baada ya kwisha kula chakula cha jioni kwenda kulala kule behewani. Kwa ishara tulizoziona, tukaona tumefanya ujinga mno kuchelewa kufika kule kwenye behewa la mizigo; ikawa haidhuru, mradi tumefika salama, tukaanza kushika doria yetu yapata saa nne ya usiku. Sehemu ya chini ya mlango wa lile behewa tuliifunga na ile ya juu tukaiacha wazi kwa ajili ya kuonea: macho yetu yakawa yanaangaza kule kwenye boma lililohamwa, walakini hatukuweza kuona katika giza nene kama hilo. Baada ya muda wa saa au mbili hivi kukawa kimya kabisa na usiku ukatuelemea; punde tukasikia kijiti kinaalika nje kwa upande wetu wa kulia nasi tukajua kuwa ni ishara ya mnyama. Punde kidogo tena tukasikia mshindo mkubwa nje, tuu!! kama kwamba mtu amerukia mle ndani ya boma. Wale ng'ombe kadhalika wakafadhaika, nasi tuliweza kuwasikia wakihangaika. Kidogo tena, kukapiga kimya. Sasa nika mshauri mwenzangu kwamba nitatoka nje nilale chini nikidhani ningeweza kuona vizuri lau simba angepita upande wetu na nyama yake. Walakini, mwenzangu dakta Brock alinizuia kabisa nisitoke; nami, nalimshukuru kukubali maonyo yake kwani muda ule ule simba mmoja ingawa hatukumjua aliko, alikuwa akitunyemelea, niseme hata alikuwa karibu kabisa kuturukia.

Punde si punde nikahisi kama kwamba nimeona kitu kikitujia kwa kunyatanyata. Pia nisiamini sana kwamba huenda macho yangu yamefanya kiwi kidogo kwa sababu ya kuyakodoa sana ndani ya giza, nikamnong'oneza mwenzangu Brock kumwuliza kama naye ameona chochote na huku nikipima shabaha bunduki. Brock kwa wakati ule hakunijibu ila hatimaye tena, akaniambia kuwa naye pia aliona kitu kikipita, bali alifanya shaka kuniambia nisije nikapiga bunduki nikaambulia patupu. Kisha pakapiga kimya kabisa kiasi cha nukta au mbili, na kwa ghafla tukashtukia kiumbe akiturukia. "Hamadi simba!' kufumba na kufumbua tukapiga bunduki zetu wote sawia. Ilivyokuwa, bila ya shaka aliinama na yumkini macho yake yalifanya kiwi kwa mlipuko wa risasi, akaingia hofu kwa mishindo miwili ya bunduki ambayo mlipuko wake ulikuwa mkubwa kwa sababu ya paa la bati la lile behewa. Tungalisinzia kidogo tu sina shaka mmoja wetu angemkumba; hapo tukaona imepita nusura tu na tumeponea bahati kabisa. Asubuhi kulipokucha tukaona kuwa risasi ya Bwana Brock imejizika chini karibu kabisa na unyayo wa simba; ilimkosea padogo tu kiasi cha inchi moja au mbili. Yangu haikuonekana kabisa.

Huu ukawa mwisho wa kupambana kwangu na mmoja wa nyamaume hawa.
 
SURA YA IV

RABSHA NA WAFANYAJI KAZI


NI KWELI, kwamba kujengeka kwa Daraja ya Tsavo hakukuwa kwa raha. Nimekwisha eleza mashaka yetu yaliyokuwa yametupata juu ya simba; ilivyokuwa, hapakupita muda tangu tuondokewe na baa la simba, pakazuka baa jingine adhimu jipya la wafanyaji kazi.

Baada ya kwisha kulipata jiwe la kusimamishia daraja, nikaagiza mafundi waashi Mombasa kuja kulichonga na kufanya kazi ile. Watu nilioletewa kwa kazi hiyo baadhi yao wengi walikuwa Mapatani nao ndio waliodhaniwa kuwa mafundi stadi; katika kufanya kazi kwao nikagundua kuwa wengi wao hawakuwa wakijua namna ya kuchonga mawe, ila walikuwa vibarua tu waliojitia ufundi ili wapate mshahara wa ufundi badala ya ujira wa ukibarua. Kwa kuligundua jambo hili mara nikaanzisha mtindo mpya wa kufanya kila mtu peke yake, nikapanga taratibu za mishahara ili aliye fundi wa kweli apate haki yake pengine na zaidi kama akistahili na kukata mishahara ya wale waliojitia ufundi nao ni vibarua tu. Sasa basi, kama ilivyo katika ulimwengu wetu huu, wale vibarua wadanganyifu walikuwa wengi mno kupita mafundi wa kweli, na kwa wingi wao wakajaribu kuwatisha wenzao wajilegeze ili wawe nao katika hali moja ili nami nipate kuondoa mpango huu wa kazi ya kila mtu peke yake juu ya mishahara kwa hayo sikukubali kwani naliona mtindo huo ni wa haki juu ya kufanya kazi kwa kila mmoja.

Hata siku moja nilipofika kule maweni, niliona mambo yote yanakwenda barabara bila ya upungufu, wala hapakuonyesha ishara yoyote ya udhia. Watu wote, kila mmoja alikuwa akishughulika na kazi yake, bali punde kidogo, kwa kuona wakikonyezana, nikang'amua kuwa mambo hayajatulia asawa. Nilipokabili genge la kwanza la wafanyaji kazi, jemadari wao, mtu mmoja ayari hivi, akanishtakia kuwa watu wafanyao kazi juu gengeni wamekataa kusikiliza amri yake na kwa hiyo ananitaka niende nikaonane nao mwenyewe. Papo hapo nikafahamu kuwa ile ni hila ya kunitega mimi ili nikifika katikati ya lile genge wapate kunizingira mbele na nyuma nisipate pa kutokea. Lakini hata hivyo nikapiga moyo konde, na kwamba yote yatakayonizukia haidhuru bali mradi nitakwenda nikaone yatakayokuwa. Hivyo nikaandamana na yule jemadari katika lile genge. Tulipofika kwenye genge la pili la wafanyaji kazi, nikamwona anatangulia upesi mbele, ati kunionyesha wale watu aliosema wamekataa kutii amri yake-nikashuku kwamba moyoni mwake alidhani kuwa sitaondoka mahali pale salama. Nikaandika majina yao katika kitabu changu kidogo kisha nikageuka kurudi mahali pangu. Punde ukapigwa ukelele wa kupandisha watu umori, kiasi cha watu sitini hivi, ukajibiwa na wale wenzao wa kwanza niliowapita kadiri ya mia moja hivi. Kila mtu alishika mtaimbo au nyundo, kisha wakanisonga katikati. Mimi nikasimama kimya na papo hapo mmoja wao akanijia, akanishika mikono yangu yote miwili akiwapigia kelele wenziwe kuwa 'atanyongwa na kuuawa kwa bunduki kwa sababu yangu'. Nikamkutua kwa nguvu kutoa mikono yangu nikamsukumilia mbali; bali nilipotazama nikaona hakika nimezingirwa na watu ambao kila mmoja uso wake umembadilika kwa umori wa kutaka kuniua. Lilikuwapo jitu moja ambaye alimsukumiza mwenziwe aliyekuwa naye jirani, na kwa kweli angaliniangukia. Ilivyokuwa basi, naliwahi upesi kunyaguka kando, hivyo yule mtu aliyedhamiriwa kunikumba, alijipiga penye mwamba.

Jambo hili kidogo lilileta vurugu ambayo mimi nalipata nafasi kidogo. Upesi nalirukia juu ya jiwe, na kabla hawajajiweka tayari tena nikawahi kuwakemea kwa Kihindustani. Mara wakatulia kusikiliza niliyokuwa nikitaka kuwaambia, nikawahubiria kuwa nimefahamikiwa na njama yao waliyoiunga kutaka kuniua, na kwamba hakika wanaweza kufanya hivyo wakitaka; walakini, katika kuniua kwao wengi wao wangenyongwa, kwani Serikali upesi ingegundua kweli na hivyo uongo wao wa kusingizia kuliwa na simba ungejulikana. Nikazidi kuwaambia kuwa nafahamikiwa mno kwamba ni mtu mmoja au wawili hivi waliowatia nia ya kijinga kama hiyo nikawakanya kuwa wasikubali kutiwa ujinga wa namna hiyo. Nikaendelea kuwaambia kuwa hata kama watatimiza nia yao ya kuniua, lakini atakuja Bwana mwingine kuwasimamia na je, sivyo pengine atakuwa mkali zaidi kunipita? Hapo kila mmoja akakiri moyoni mwake kuwa hakika mimi sikuwa na nia mbaya nao ila haja yangu ni kutaka haki kwa kila mmoja. Kiasi cha kuwaona kuwa wamekubali kunisikiliza hapo kidogo nikajiona katika hali ya salama, nami kwa sababu hiyo nikaendelea kuwaambia kwamba wale wasiokubali kuendelea na kazi watapewa ruhusa ya kurudi Mombasa, na ya kuwa wale watakaobaki, wakihiari kuendelea na kazi yao bila ya manung'uniko yoyote, upuuzi wao waliokwisha fanya sitautia maanani tena. Mwishowe nikawaambia kuwa kila aliyekubali kuendelea na kazi anyoshe mkono wake juu, hapo karibu wote wakainyosha mikono. Kwa wakati huo nikaona kuwa nimefaulu kuwatiisha kidogo na baada ya kuwapa ruhusa, nikashuka pale juu ya jiwe nikaendelea kutazamatazama kazi kama kwamba hapakutukia lolote nikijitia kupima jiwe hili na hili na kujaribu kutoa makosa baadhi ya kazi zilizofanywa, na baada ya kitambo cha saa moja nikarudi zangu Tsavo, salama u salimini.

Lakini baadaye nikaarifiwa kuwa matata hayajakwisha kabisa, basi nikapiga simu kwa askari polisi ya reli. Baada ya muda muda wa siku mbili tatu, askari wakafika, wakawakamata ale waliokuwa viongozi wa uasi ule wakapelekwa Mombasa, na huko wakahukumiwa na Bwana Crawford, Balozi wa Kiingereza.
 


SURA YA V

KIPINDI CHA HOFU



TANGU usiku ule tulipowasikia simba mimi na mwenzangu Brock katika behewa la mizigo, hawakurudi tena kutuudhi kwani hakika walijitenga mbali kabisa na mji wa Tsavo, mpaka baada ya Bwana Brock alipoondoka kwa safari yake ya kwenda Uganda. Kwa kitambo hicho tulichojaliwa kuwa salama, nilifikiri kwamba wakijaribu tena kuanza mashambulio yao, mtego ndicho kitu kitakachofaa mno kuwakamatia. Basi, nikaazimia kutengeneza mtego, nami nikaweza kuunda madhubuti kwa magogo ya miti, mataruma ya reli, nyuzi za simu na mnyororo mrefu mzito sana. Mtego wenyewe naliugawa sehemu mbili; sehemu moja ya kukaa wale watu na ya pili ya kuingilia simba.

Mtego wangu ulipokwisha kuwa tayari, nikaupigia hema juu ili kuzidi kuwavuta, kisha nikaujengea boma madhubuti barabara. Mlango mmoja wa nyuma ni wa kuingilia wale watu, ambao baada ya kuingia kwao wataweza kuuziba kabisa kwa kuvuta miti iliyowekwa tayari kwa kufungia, na mlango wa mbele ni wa kuingilia simba nao ukaachwa wazi. Watu niliowahi kuwaonyesha hekima hii, wote wakakataa kwanza, wakisema kuwa simba wataweza kuwakamata, bali kama yatakavyoonekana mbele, mawazo yao hayakwenda sawa. Kwa mara ya kwanza, kila usiku mwenyewe binafsi yangu nilikuwa chambo, lakini hakukutokea kitu.

Kwa kweli tulikaa miezi mingi kidogo bila ya kusumbuliwa na simba ingawa mara kwa mara tulisikia vishindo vyao katika vijiji vingine, Tangu usiku tulipokesha katika behewa la mizigo, haukupita muda mwingi, watu wawili wakachukuliwa katika kambi ya mwisho wa reli, na mwingine akakamatwa mahali kiasi cha umbali wa maili kumi hivi. Tena ashikwa watu wawili kule Engomani; mmoja aliliwa kabisa na wa pili akaumia akafa. Kama nilivyokwisha sema,si hapo Tsavo, tulikuwa shwari kabisa, na wafanyaji kazi wote walipoingia imani kuwa simba wameuhama mji, wakarudia makazi yao kama kwanza.

Mwishowe, tulifadhaishwa ghafla katika starehe yetu, llitukia usiku wa giza, kulikuwako vishindo vya kelele za hoi hoi, nasi tukajua kwamba ni wale wale adui wameanza tena kazi yao ya kukamata watu.

Katika mkasa huo, watu kadha wa kadha walilala nje kwa sababu ya kutaka upepo, wakifikiri kwamba simba wamekwenda zao kabisa nao hawatarudi tena. Usiku huo simba mmoja alionekana akijipenyeza kutaka kuingia bomani. Mara ikawa kuvurumisha mawe, magongo, vijinga vya moto upande ule alikopenyea yule simba. Hayo yote simba hayakumzuia kitu, kwani naye alijitoma katikati ya genge la watu akamnyakua mmoja akatoka naye nje katika boma la miiba. Huko nje ya boma akasaidiwa na mwenziwe aliyekuwa akingoja, nao kiasi cha hatua thelathini tokea pale bomani, wakajilia nyama yao. Ingawa jemadari alipiga risasi nyingi, simba hawakujali, wala hawakujivuta popote mpaka walipokwisha maliza kula nyama yao. Kwa kutumaini kwamba wale simba watarudi tena usiku wa pili, nilikataza yale makombo yao yasifukiwe upesi; nami, kwa tamaa hiyo, giza lilipoanza kufungamana, nikachagua mti mzuri nikapanda juu kuwavizia, Wapi, hakuna chochote kilichotokea usiku huo, ila mzee fisi, na asubuhi kulipokucha nikajua kuwa wale simba walikwenda shambulia kambi nyingine iliyokuwa mbali kidogo na Tsavo kiasi cha maili mbili. Katika shambulio hilo pia walifanikiwa kukamata mtu ambaye walimlia karibu na kambi.

Baada ya mkasa huu, ikawa kila usiku hulala juu ya mti kwa muda zaidi ya juma moja karibu ya kila kambi walikuwa wamekamata mtu, lakini wapi, sina nilichoambulia Kwani waliendelea kuchukua mtu mmoja kila usiku katika kambi mbalimbali. Malazi haya ya kila mara kukesha usiku yalikuwa ni kazi mojawapo ya taabu na mashaka, bali ingawaje, kazi yenyewe hiyo ilinibidi niifanye kwani watu wote walinitegemea mimi kuwa kinga yao. Tabia yao huja na ngurumo za kutisha, na kiasi cha kufika hatua zile za kuingilia kambini hunyamaza kabisa wakawa wanakwenda kimya, nasi hapo hujua kwamba wamo katika hali ya kunyemelea.

Kwa yakini nalivunjika moyo kabisa kwa kutatanishwa kila usiku namna hii nami hakika naliishiwa na hekima za namna ya kufanya; ilionekana kama kwamba wale simba walikuwa 'mizimu' kweli waliojigeuza umbo lile. Kuwaandamia nyuma nyuma ni kujisumbua bure; lakini kwa kuwa kulibidi kufanywe jambo la kuwatuliza watu, nalijitahidi niwezavyo kuwanyapilia mchana mchana katika nyika iliyoshikamana na ya taabu kama hiyo kwa kitaa chote kilichotuzunguka. Kwa kweli, ningalipata kupambana nao njiani, nisingalikuwa na jambo lolote la kuweza kufanya ila nami kuwa mmojawapo kwa chakula chao. Pia basi, kwa wakati huu, nalikwisha pata mabwana wengine wasaidizi waliotoka Mombasa kuja Tsavo kwa kazi hiyo ya kukesha usiku usiku lau labda wapate bahati ya kuwapiga maayari hawa. Wapi, sote tulipambana na taabu tupu bila ya kuambulia lolote, nao simba wakawa hodari kutupiga chenga na huku wakijinyakulia mtu mmoja mmoja.

Nakumbuka mkasa mmoja, kama hivi leo, simba walipokamata mtu stesheni wakaja wakamlia karibu na kambini kwangu

Naliwasikia waziwazi wakivunja mifupa, nami tangu siku hiyo, kwa sababu ya ngurumo zao za kitisho zilizoweza kusikilikana kila mahali, masikio yangu yakawa yanavuma tu,Kwa shaka niliyokuwa nayo hakika nalijiona kuwa sina maana yoyote; ilivyokuwa ni kwamba ilikuwa kazi bure kujaribu kutoka nje, kwani hakika yule mtu alikuwa amekwisha kufa, na zaidi ya hayo giza lilikuwa nene hata mtu hawezi kuona po pote. Karibu ya bomani kwangu palikuwa na wafanyaji kazi sita katika boma lao dogo hivi, nao kadhalika kwa kusikia wale simba wakimtafuna mwenzao wakanilalamikia niwaruhusu waingie bomani mwangu. Kwa kweli naliwakubalia, bali mara nikakumbuka kuwa walikuwa na mwenzao mmoja mgonjwa kambini kwao, na katika kuwahojihoji nikaona kuwa wamemtelekeza peke yake bila ya kumjali. Papo hapo nikachukua watu wachache kuandamana nao kwenda kumchukua; kuingia hemani mwake, maskini tukamkuta mkavu wa juzi. Alikuwa amekwisha kufa kwa kihoro cha kutupwa na wenziwe.

Tokea wakati huo mambo yakaendelea kuwa mabaya zaidi. Kwa kawaida yao ilivyokuwa, simba mmoja tu ndiye aliyekuwa akiingia kukamata watu ambapo mwenziwe alikuwa akikaa nje kumngojea; lakini sasa walibadili mwendo huo wakawa wanaingia wote pamoja ndani ya maboma kila mmoja akijishikia nyama yake. Kwa mwendo wao huu wa sasa, katika juma moja la mwisho wa mwezi wa Novemba, Waswahili wawili wapagazi waliuawa; mmoja alinyakuliwa ghafla akaliwa, na wa pili alisononeka kwa muda mrefu, na Wakati wenziwe walipojikusanya kwenda kumsaidia wakamkuta amekwamishwa hodari katika miti ya boma, simba aliposhindwa kumtoa. Asubuhi yake nilipokwenda kumtazama nikamkuta bado angali hai anatweta, bali kwa kuwa aliumia mno hivyo hakudiriki kufika hospitali, akata.

Baada ya mkasa huu haukupita muda, simba wale wale wawili walifanya shambulio kali kabisa katika kambi kubwa karibu sana na stesheni Tsavo, pia karibu kabisa na nyumba ya mabati ya Mkaguzi wa reli (P.W.I.).

Siku hiyo Katika usiku wa manane, simba hao wawili walijitoma katika wafanyaji kazi. Simba kiasi cha kwisha kujinyakulia nyama yao na kuondoka nayo mara hiyo nikasikia: 'Wamemchukua, wamemchukua', nao basi hawakwenda naye mbali wakamla karibu kabisa na ile kambi. Yule bwana Mkaguzi wa Reli Bwana Dalgairns, alipiga risasi nyingi upande ule aliko wasikia simba, lakini wapi, hawakuzijali hata kidogo; walikaa hapo wakala nyama yao mpaka walipokwisha. Asubuhi yake baada ya kupatazama pale mahali, papo hapo tukaingiwa na ari ya kuwafuata wale simba kwamba Bwana Dalgairns alishuku kuwa mmoja wao yumkini alipata risasi ya mguu kwa kuona mburuzo mchangani kama wa mguu uliolemaa.

Tulipozidi kunyapilia kwa uangalifu tulishtukia tuko karibu kabisa na simba kwani tulisikia ngurumo zao za kutisha.

Tulipokuwa tukizidi kuendelea mbele kwa tahadhari na kutengatenga vichaka, tuliona mahali palipofunga giza kama mtoto wa simba; walakini tulipozidi kutafiti zaidi tukaona maskini, kumbe ni masalio ya yule mtu aliyekamatwa akaachwa na simba waliposikia harufu yetu. Walikwisha mla miguu, mkono na nusu ya kiwiliwili, na ule mburuzo kumbe ni vidole vilivyokakamaa vya mkono wa pili vilivyokuwa vikiburulika chini.

Nchi yote sasa ilikwisha jiinamia, hata siku moja (tarehe I, Desemba) niliporudi kambini kwangu niliwakuta watu wote wameacha kazi kutaka kusema nami. Kwa kweli sikuona ajabu kwa kuwa walikuwa wamepatikana na mambo ambayo yangemhofisha binadamu awaye yote. Nilipowatumia mtu kuwaita walikuja wote wakakusanyika bomani kwangu, wakanieleza kwamba hawatakubali tena kufanya kazi Tsavo. Walisema kuwa wao wametoka kwao Bara Hindi kwa mkataba na Serikali kuja kufanya kazi, bali si kuja kuwa mhanga kwa simba au 'mazimwi' kama hayo. Kiasi cha kumaliza maneno hayo, wengine wao wengi walilisimamisha gari lililokuwa lililokuwa likipita kwa kujitupia relini, kisha, wakakimbilia kujitumbukiza katika mabehewa, ati, ndio salama kupaondoka mahali pale penye hatari.

Kwa kweli baada ya haya kazi ya reli ilisimama kabisa; na muda wa majuma matatu yaliyofuatana hakuna lolote lililotendeka ila kujenga ngome za simba za wafanyaji kazi waliokuwa wamekubali kukaa. Niseme nilichekeshwa mno kwani zilijengwa juu ya lingo la matangi ya maji; juu ya mapaa na katika boriti za chuma; hasa popote pale walipoweza kwa kutaka kusalimika, ambapo wengine walitokomea mbali, wakachimba mahandaki ndani ya mahema yao na kuyaziba kwa magogo ya miti. Kila mti uliokuwa mkubwa katika kambi ulifungwa vitanda vingi juu, kiasi cha nguvu ya matawi yake yalivyoweza kuhimili, pengine hata zaidi.

Nakumbuka usiku mmoja kambi ilipoingiliwa, watu wengi walikimbilia kwenda kupanda mti mmoja, na kwa uzito wa wingi wao, mti ukawaporomosha wote waliokuwa juu kwa hofu mpaka karibu kabisa na wale simba waliokuwa wakiwa kimbia. Kwa bahati wale simba walikwisha kamata mtu mwingine, na kwa hiyo hawakushughulika kumpatiliza yeyote zaidi kwa sababu ya kula nyama yao.
 
SURA YA VI

KUNUSURIKA KWA BWANA SHAURI



KITAMBO KIDOGO kilichopita kabla ya kutawanyika kwa wafanyaji kazi, nalikuwa nimemwandikia barua Bwana Whitehead, Bwana Shauri, kumwomba aje anisaidie katika vita hii ya simba, kadhalika aje na askari wake wa kienyeji kadiri atakaoweza kuja nao. Katika majibu yake alikubali kuniletea msaada, akaniarifu kuwa nimtazamie kufika kwake tarehe 2 mwezi wa Desemba kiasi cha saa moja au mbili hivi, ambayo ni siku ya pili tangu kuondoka kwa wale makuli. Gari lililomleta lilitazamiwa kufika Tsavo kiasi cha saa kumi na mbili ya jioni, na kwa hiyo nalimtuma mtumishi wangu! mmoja kwenda stesheni akamlaki pia amsaidie kubeba mizigo yake mpaka kambini. Si muda mrefu tangu nimtume yule mtumishi, mara nikamwona huyo anakuja mbio huku anagwaya mwili mzima kwa hofu, akaniambia kuwa hakuna dalili yoyote ya gari la moshi wala mtu afanyaye kazi hapo isipokuwa simba mmoja mkubwa mno amesimama stesheni juu ya jukwaa. Maneno yake kwa kweli sikuyaamini hata kidogo, kwamba kwa wakati huu makuli wote walikuwa wakibabaika ovyo hata kama wakiona fisi, nyani, mwisho hata mbwa kichakani, mara husema ni simba tu: walakini asubuhi yake nikaona kuwa maneno yake yalikuwa kweli kwani hata babu wa stesheni pamoja na kandawala wake iliwabidi wajifungie ndani kwa kumkimbia simba huyo.

Ilivyokuwa, siku ile sikufanya haraka ya kula chakula, ikanibidi kusubiri kidogo kumngoja Bwana Whitehead, lakini hatimaye nilipoona hakuna dalili yoyote ya kutokea kwake, nikatuhumu kuwa yumkini amehairisha safari yake mpaka siku ya pili na hivyo nikajiția chakula changu peke yangu. Wakati nilipokuwa nikila nikasikia mishindo miwili ya bunduki lakini sikuijali sana kwani bunduki zilikuwa zikipigwa ovyo shafuu shafuu daima karibu karibu na kambi. Giza lilipoanza kufungamana nikatoka kwenda kuwavizia adui wetu, nami nikajitia katika tundu la chuma lililoundwa kwa mataruma ya reli nililolijenga juu ya boriti kubwa ya chuma karibu kabisa na kambi moja niliyoituhumu kuwa itavamiwa usiku ule.

Kiasi cha kwisha kujiweka vizuri nalishtuka kusikia simba wakinguruma na kuvuta mori, wakitafunatafuna mifupa kiasi cha hatua sabini toka mahali nilipokuwa. Sikuweza kujua ni kitu gani wanachokula kwa sababu sikusikia vishindo vyovyote kambini. Mwishowe nikafikiri kuwa yumkini wamemkamata mtu maskini aliyekuwa akijiendea na njia zake. Baada ya muda kidogo naliweza kuona macho yao yakimereteka katika giza, nami nikajitahidi kulenga shabaha bunduki yangu nikapiga; wapi, hawakujali lolote ila walijivuta kando pamoja na nyama yao wakarudi nyuma ndani ya vichaka ambako sikuweza kuwaona tena. Huko walistarehe wakala nyama yao hata wakamaliza kabisa.

Nikirudia nyuma, kulipokucha, baada ya kuhakikisha yote yaliyopita usiku nalitoka pale tunduni pangu nikaelemea upande ule niliowasikia usiku. Njiani, maskini, nimwone nani, ni mgeni wangu Bwana Whitehead ambaye hakutokea usiku wa jana, taabani kabisa; kwa kweli alikuwa amevurugika mno.

Kumwona tu nikashangaa, nikamwuliza: 'Je, baba, watokea wapi? Mbona hukutokea wakati wa chakula jana usiku?"

Akanijibu: 'Nakusifu kwa ukarimu wako: ama wajua mno kumkaribisha mtu vilivyo.' Nikamwuliza: 'Je, bwana, kulikoni?’ akanijibu: 'Ni yule nduli wako mtoa roho za watu, alitaka kuniua jana usiku.’

Nikamjibu katika hali ya kustaajabu: 'Nenda wee, waota nini?

Hakunijibu tena ila alinigeukia nyuma akanionyesha mgongoni, akasema: 'Na hii siyo ndoto yenyewe?’

Nguo yake iliraruliwa kwa kucha toka ukosini mpaka na mwilini alipigwa makucha manne barabara. Bila kuendelea kusemezana zaidi nikamchukua mpaka hemani kwangu, nikamwosha na kumfunga dawa majeraha yake sasa, nilipomwona kidogo ametulia, nikaanza kumweleza mkasa wote nilioupata usiku na niliousikia.

1630881490656.png


Ilitukia kuwa gari lililomleta lilichelewa sana, hivyo, alipofika Tsavo ilikuwa usiku sana, na njia ya kujia kwangu alipitia majanini. Katika safari yake aliandamana na askari wake mmoja jina lake Abdallah, sajini katika askari wake aliyekuwa nyuma yake amechukua taa inayowaka njia nzima walikuwa salama ila walipofika nusu ya njia mahali palipofunga giza hivi ndipo akatokea simba mmoja akawarukia, akamtupilia mbali chini Bwana Whitehead kama kitaka akamrarua kama nilivyomwona. Kwa bahati njema alikuwa na bunduki yake naye papo hapo akaiwasha moto. Umeme na kile kishindo cha bunduki, yumkini ndicho kilichomrusha akili yule simba kwa kitambo kidogo hata Bwana Whitehead akapata nafasi ya kujizoazoa: lakini mara hiyo hiyo akarudi tena na safari hii akaangukia kwa Abdallah akamkumba moja kwa moja. Abdallah, maskini hakudiriki kusema lo lote ila: 'Eh. Bwana, Simba!' Abdallah alipokuwa akiburuzwa na simba gengeni, Bwana Whitehead alipiga tena bunduki, lakini hana alichoambua, na yule simba naye akazidi kutokomea na nyama yake ndani kabisa ambako hakuweza tena kumwona.

Nikachukulia fahamu kuwa kumbe ni askari wa Bwana Whitehead ndiye niliyemsikia usiku akitafunwa na simba. Yeye Bwana Whitehead mwenyewe aliponea nusura; vijeraha vyake havikuingia ndani sana na kwa hiyo havikumwuguza sana.

Siku hiyo hiyo, tarehe 3 mwezi wa Desemba, watu wa kuja kuwinda simba wakaongezeka. Bwana Farquhar, bwana askari, alifika kutoka Mombasa pamoja na kikosi cha askari kadiri ya ishirini kuja kupigana na baa hili la simba, ambao sifa yao imeenea mbali kila mahali. Watu wakajipanga tahadhari kabisa ikawa askari wa Bwana Farquhar anywa juu ya miti karibu ya kila kambi. Kadhalika, kwa wakati huu mabwana wengine wengi wa serikali walichukua livu zao kuja kushirikiana nasi, na kila mmoja wao alijiweka vizuri mtini, ila Bwana Whitehead, pamoja katika tundu langu la chuma pale juu ya jukwaa la chuma. Zaidi ya hayo, baada ya kusemezana sana, ule mtego wangu wa simba niliokuwa nimeutengeneza ukadhibitishwa ukawa tayari kutumika, wakatiwa askari wawili sehemu ya salama kuwa chambo.

Mpaka wakati wa magharibi, matengenezo yetu yote yakawa tayari na kila mmoja akakaa mahali pake alipochaguliwa. Tukakaa kimya mpaka kadiri ya saa tatu ya usiku. Dhana yangu ikasibu kuwa simba mmoja amekwisha ingia mtegoni kwa kusikia mtego ukifyatuka. Hakika ilikuwa kweli lakini matokeo yake yalikuwa hayana maana.

Ilivyokuwa ni kwamba wale askari waliokuwa chambo, upande wao kulikuwa na taa ikiwaka, nao, kila mmoja alikuwa na bunduki na baruti ya kutosha. Kadhalika walikwisha pewa amri ya kupiga mara simba akiingia mtegoni. Haya basi, badala ya kupiga kama walivyokwisha agizwa ajabu, wote walishikwa na hofu simba alipoingia na kujipiga piga ovyo na mataruma ya kule kwake, akili zikawapotea, wakawa hawana hata fahamu ya kufyatua bunduki zao. Bwana Farquhar aliyekuwa karibu nao akawakemea. Walipopata fahamu za kupiga, walijipigia ovyo tu popote walipoelekeza bunduki zao.

Mimi na Bwana Whitehead tulikuwa sawasawa na upande ule ambao wangepigia bunduki zao na hivyo risasi zao zilikuwa zikituvumia zikipita. Walipiga zaidi ya risasi ishirini na mwishowe walifyatua taruma moja kwa kulipiga risasi, na hapo wakampatia simba nafasi ya kuokoka, akatoka.

Naliona ajabu, mpaka sasa naona ajabu jinsi walivyoshindwa kumwua mara zote hizo, kwani wangaliweza kabisa kugandamizia midomo ya bunduki zao mwilini mwa simba. Ilisikitisha kuona kifo cha simba kilichokuwa dhahiri namna hiyo, kuwa amesalimika kwa hofu ya wale askari.

Vivyo hatukukata tamaa, na asubuhi kulipokucha tukaanza kuwafuata porini. Mwendo wetu wa mchana kutwa ulikuwa wa kutambaa tu katika vichaka vya miiba, na ingawa mara tulisikia ngurumo zao, lakini hatukuwahi kupambana nao.Sote hakuna aliyepata kuona lolote isipokuwa Bwana Farquhar, yeye aliwahi kumwona mmoja alipokuwa akiruka kichakani.

Tuliendelea na kazi hiyo ya kuwinda kwa muda wa siku mbili, nasi, zaidi ya uchovu hatuna tulichoambua; kwa wakati huu ikawa Bwana Farquhar pamoja na watu wake iliwabidi warudi kwao Mombasa. Bwana Whitehead naye akarudi mjini kwake, nami nikabaki katika hali yangu ya upweke na nyamaume wangu.
 
SURA YA VII

KIFO CHA NYAMAUME WA KWANZA



BAADA YA siku au mbili hivi tangu kuondokewa na wageni wangu, siku hiyo, tarehe 9 mwezi wa Desemba, kiasi cha kutoka bomani kwangu, nikamwona mtu mmoja akinikimbilia kwa fadhaa huku akipiga kelele: 'Simba, simba', na vile akikimbia anatazamatazama nyuma mara kwa mara, Nilipokuwa nikimhoji, nikafahamu kuwa simba walitaka kumkamata mtu huyo kwenye kambi iliyokuwa karibu na mto, na walipomkosa wakamkamata punda mmoja wakamwua, nao kwa wakati huo wakawa wameshughulika na karamu yao, wala si mbali na hapo kambini. Hapo nikaona nimepata bahati.

Nikakimbilia nyumbani upesi kwenda kuchukua bunduki moja kubwa niliyoachiwa na Bwana Farquhar. Niliporudi nikaandamana na yule mtu kuwafuatia wale simba, ambao kwa wakati huo, naliamini kabisa kuwa wameshughulika kula nyama yao.

Naliwatambalia vizuri sana hata naliweza kumwona mmoja wao kidogokidogo katika vichaka, bali kwa bahati mbaya yule kiongozi wangu alivunja mti mkavu ukalika. Yule simba akasikia mwaliko huo naye akavuta mori, bali mara akajitia vichakani ndani kabisa. Kwa kuona kuwa amenikimbia tena, nikarudi kambini kwa haraka, nikawaita wafanyaji kazi waliokuwapo, nikawaambia wachukue mitaimbo, madebe na vitu vingine vyenye kelele watakavyoweza kupata. Nikafanya haraka kuwapanga kwa mduara kukizingira kile kichaka, kisha nikamwagiza yule msimamizi wao waanze kupiga ghasia zile zote kwa umoja, naye alipoanza kuwaamrisha wenziwe, mimi nikapata nafasi kuzungukia upande wa pili. Kisha nikapenyapenya peke yangu na mara nikagundua mahali pazuri palipoelekea kwamba yule simba ataweza kupita atakaporudi kwa sababu palikuwa katikati ya njia yao iliyoelekea sawa na mahali pale alipojificha. Nikajilaza chini nyuma kichuguu tayari kwa lolote litakalozuka. Punde si punde makuli nao wakawa wameanza vishindo vyao, na mara hiyo likazuka simba kubwa likapita mahali peupe hivi. Si furaha hiyo niliyokuwa nayo. Tangu tuanze kuhangaika kuwasaka simba, hii ilikuwa mara yangu ya kwanza kuona mmoja kwa nafasi kama hiyo, na kwa kweli furaha niliyokuwa nayo haikuwa na kifani.

Akawa anakwenda taratibu taratibu huku akitua kutazama huko na huko. Mimi nalikuwa nimejiziba kidogo tu na lau kama asingefadhaika kwa ghasia za vishindo nyuma yake sina shaka angeniona. Kwa kuwa hakuwa na habari za kuwapo kwangu karibu, sikufanya haraka, nikamwacha asogee kiasi cha hatua kumi na tano ili niweze kumlenga shabaha vizuri kwa bunduki. Kitambo cha kujinega nifanye hivyo, akaniona, akashangaa mno kwa vile alivyoniona ghafla, naye akasita, akajirusha kinyume akaanguka kitakotako akavuta mori kwa ghadhabu. Kwa vile kichwa chake kilivyokaa sawasawa na shabaha ya bunduki yangu nikashukuru kuwa leo lazima nitampiga; bali wapi, silaha usiyoizoea usiiamini. Nilipofyatua ule mtambo wa bunduki, wapi, nikasikia pufy, ishara ya kunijulisha kuwa bunduki haikufyatuka na hapo nikawa nimeingiwa na hofu. Bahati yangu ni kuwa yule simba alifadhaika mno kwa ghasia na vishindo vya wale makuli, hata ikawa badala ya kunirukia akazidi kujitia ndani vichakani. Kwa wakati huu nami fahamu zikanijia na kiasi cha kuruka kwake nikamwachia nao mwanzi wa pili.

Ngurumo yake ya mori ilinijulisha kuwa risasi hii ya pili ilimpata mahali; bali pamoja na hayo pia alinusurika akakimbia kabisa, nami ingawa nalimwandamia kwa kufuata nyayo zake kitambo kidogo bali mwishowe alinipotea katika magenge ya mwamba.

Kwa ghadhabu za kumkosa yule simba, nikatukana mwenye bunduki, fundi, hata na bunduki yenyewe barabara. Ikawa Wahindi wote wakazidi kuthibitisha kuwa wale simba hakika walikuwa mizimu wasioweza kuuawa kwa silaha yote. Kwa kweli, walidhihirisha kuwa ni mizimu.

Haya basi, baada ya mkosi huu, hakika hatukuwa na la kufanya ila kurudi kambini, walakini, kabla ya kurudi nikaona heri niende nikamtupie jicho yule punda aliyeuawa naye nikamkuta ameliwa upande tu, upande wamemwacha. Sasa basi, nikaona bila ya shaka simba mmojawapo ataurudia ule mzoga wa punda usiku. Kwa dhana hii, kwa sababu hapakuwa na mti wowote karibu yake, nikajengewa ulingo! kiasi cha futi kumi toka pale ulipokuwa ule mzoga. Kimo chake ulipata futi kumi na mbili nao ulitiwa nguzo nne zilizoelekeana na katikati pakawekwa ubao wa kukalia Zaidi ya hayo, kwa kuwa usiku haukuwa wa mbalamwezi, ule mzoga nikaufunga hodari kwa nyuzi za chuma penye suma la mti na mapema ili kusudi simba wasiweze kuuburuza kabla sijadiriki kuwapiga bunduki.

Jua lilipokucha nikapanda ulingoni pangu, na kwa kuwa mpagazi wangu wa bunduki alikuwa mgonjwa wa kifua, basi nikapanda peke yangu. Nilifikiri juu ya kukohoa kwake, nikachelea atakohoa hivyo ikawa yote yatuharibikie.

Giza likafungamana na kukawa kimya ajabu. nikashtuliwa na mwaliko wa kijiti, nami nilipotega masikio yangu kwa makini, nikasikia namna ya mnyama mkubwa akipita katika vichaka. Moyoni mwangu nikatuhumu: nyamaume nini, bila ya shaka kwa kuwa ni usiku nitapata bahati ya kumpiga mmoja wao'. Kidogo tena pakapiga kimya; mimi pale nilipokuwa nalikuwa kama sanamu ya udongo kwa namna nilivyojituliza, kila mshipa wanigonga kwa hofu. Si muda mara hofu yote ile juu ya simba ikanitoka, kukaakaa kidogo mara nikasikia mguno mnene - hakika ni ishara ya njaa - ukitokea vichakani, na papo hapo nikasikia chakarakara ya vijiti kwa vile alivyokuwa akija. Punde si punde nikasikia kimya tena na ngurumo ya ghadhabu, nikajua bila ya shaka amenigundua pale juu nilipokuwa, nami nikajuta mno kwa kufikiri ajali ile iliyonikabili wakati ule.

Naam; muda si muda mambo yakabadilika ajabu. Mwinda akawa mwindwa; ilivyokuwa ni kwamba yule simba badala ya kwenda zake au kufuata ule mzoga wa punda aliowekewa, akaanza kuninyemelea kimang'amung'amu. Kwa muda wa saa mbili nzima akawa akijipitishapitisha karibu na pale ulingoni pangu. Kwa kweli kila dakika nalikuwa nikitazamia kuwa yumkini ataupiga kumbo ulingo wangu. Hapo juu nilipokuwa nikawa nawaza: je, kama nguzo moja ikitetereka ikavunjika, au kama yule simba atajipinda aruke kule juu niliko, mambo haya yatakuwaje-mawazo hayo yakanitia unyonge. Mara nikasikia kitu kikitambaa nami papo hapo nikajijutia nafsi yangu kwa kukaa mahali pale pa hatari.

Baada ya muda kidogo nikamsikia simba akininyemelea taratibu. Sikuweza kumwona vizuri bali kiasi nilichomwonea kilitosha nikabahatisha kumlenga shabaha nikafyatua bunduki, Ndipo nikasikia ngurumo moja kwa moja kadhalika nikaweza kumwona akijitupa huko na huko. Baada ya hapo sikuweza kumwona tena kwamba kule kurukaruka kwake kumemwezesha atokomee ndani vichakani.

Hatimaye nikasikia ngurumo za nguvu kabisa, ambazo zilififia kidogokidogo hata mwisho zikanyamaza kabisa; moyoni nikashuku kuwa bila ya shaka nimempata nduli mmoja na ya kua usafii wake umekoma.

Kitambo cha kwisha kupiga bunduki, nikasikia sauti kadha wa kadha za watu kambini wakiniuliza kama nimesalimika. Nikawajibu kuwa nimesalimika wala sina shaka ya kuwa simba mmoja nimemwua: ambapo kiasi cha kusikia kwao kufa kwa simba huyo, ajabu, watu walirukaruka kwa mayowe ya furaha, na ingawa ni usiku bali hawakujali. Punde nikaona watu wanatoka kambini mwao; hakuna aliyebaki kambini kwa furaha. Wakaja wakanizunguka pale ulingoni pangu, nikastaajabu kuwaona wanajitupa chini mbele yangu wakinisifu: "Astahili salama, astahili salama.

1630947163866.png


Usiku ule naliwakataza kabisa wasijaribu kumtafuta yule simba kwamba huenda mwenziwe akawa karibu; na pamoja na hayo, pengine angali hai hata ataweza kumrukia mmoja wetu akafa naye pamoja. Ikawa wote tukarudi kambini salama u salimini na furaha yetu, ambako usiku kucha watu walikesha kwa ghasia; Waswahili na watu wengine wa kibara wanaifurahia siku hiyo kwa kucheza ngoma za kikwao.

Kabla ya kupambazuka sawasawa nikashika njia kwenda kule ulingoni kwangu kwamba sikukubali moyoni kuwa hata kama yule simba atakuwa hakufa bali hataweza kunipotea kabisa.

Nikafuata mchuruziko wa damu, na baada ya hatua chache, kutupa jicho penye kichaka kilichozunguka nikashtuka kumwona simba mkubwa amenikabili mbele yangu kama kwamba yu hai amejikunja tayari kunirukia. Nilipozidi kutazama nikasadikisha moyoni kuwa amekwisha kufa hapo tena wale watu nilioandamana nao wakamzunguka, wakacheka kwa furaha wakipiga kelele kama watoto wadogo. Baada ya kwisha shukrani zao, nikamwangalia yule simba vizuri, nikaona kuwa risasi mbili zilitosha kumwua-moja ilimwingia kwa nyuma ya bega la kushoto, yadhihirisha kuwa imemwingia mpaka moyoni na ya pili imemwingia katika mguu wa nyuma. Simba mwenyewe hakika ni mkubwa sana; urefu wake tokea puani hata mkiani ni futi tisa na inchi nane.
 
SURA YA VIII

KIFO CHA NYAMAUME WA PILI



ISIDHANIWE KWAMBA kwa sababu ya kufa kwa simba huyu, matata na taabu ya Tsavo ndio mwisho; la, ingawa mwenziwe alitulia kidogo tu naye mara siku moja akampigia hodi bwana Mkaguzi wa Reli nyumbani kwake akamfanyia vituko vingi barazani. Yule bwana Mkaguzi kusikia ghasia nyingi barazani kwake alidhani ni kuli mmoja aliyekuwa amelewa sana na kwa hiyo akamkemea kwa ghadhabu: 'Ondoka weel'; bahati yake ni kwamba hakutoka nje wala hakufungua mlango. Yule simba kwa hasira za kumkosa mtu akakamata mbuzi wawili wa yule Mkaguzi wa Reli akawala papo hapo.

Nilipopata habari za mkasa huu, siku ya pili nikaazimia kukesha pale karibu ya nyumba ya yule Mkaguzi wa Reli. Kwa bahati palikuwa na kibanda cha mabati karibu yake kilichokuwa na tundu pana ya kutosha kupenyezea mdomo wa bunduki; nje nikafunga mabeberu matatu ya mbuzi katika taruma moja la reli lililokuwa na uzito wa ratili 250, yaani chambo cha simba.

Usiku kucha hakutokea, mpaka karibu ya alfajiri, akatokea, akamvamia mbuzi mmoja akaondoka naye, na papo hapo akawa anawaburuza wale wengine wazima pamoja na lile taruma la reli. Nikapiga risasi nyingi sana upande ule aliokuwako, lakini kwa kuwa ni usiku wa giza hata mtu hawezi kuona chochote hivyo sina nilichoambulia ila kumpiga mbuzi mmoja katika wale aliowachukua kwa kuwaburuza. Nalitamani sana kuwa na tochi kwa mambo ya namna hii.

Asubuhi ya pili nikatoka kumwandamia pamoja na watu wengi kambini. Haikutupata taabu ya kumtafuta sana kwakuwa tulijua kuandama ile miburuzo ya mbuzi na lile reli, na baada ya mwendo wa nusu au robo maili tukamwona mahali amestarehe na karamu yake. Hapo amezibwazibwa kidogo na vichaka, naye aliposikia harufu yetu akaanza kuvuta mori kwa ghadhabu; hatimaye tulipomsonga mno akaruka kwa ghafla sana akaingia vichakani, hapo ikawa watu wote wakakimbilia kupanda mitini isipokuwa msaidizi wangu Bwana Winkler, yeye alisimama pamoja nami kiume tangu mwanzo hata mwisho.

Yule simba katika kuruka kwake, hakuwa amenuia uovu kwa wakati ule na tulipokuwa tukimtupia mawe upande ule tulikomwonea mwisho, kwa sababu ya kimya tukakisi kuwa bila ya shaka alikwenda zake kimya kimya. Kwa hiyo tukazidi kuendelea na tulipofika mahali alipokuwa akila karamu yake tukahakikisha kuwa kweli amekwenda zake hali ameacha mbuzi wawili bila ya kuwafanya lolote.

Tulidhani bila ya shaka atarudi tena kuja kumaliza nyama, yake, nikajenga dunguma dhubuti kabisa kiasi cha hatua chache tokea pale palipokuwa na ile mizoga ya mbuzi, nikakaa mahali pangu kabla giza halijafungamana. Safari hii nikamchukua mpagazi wangu wa bunduki, Mahina, anisaidie kukesha kidogo maana nalikuwa nimechoka vibaya mno kwa kulemelewa na usingizi wa siku nyingi bila ya kufumba jicho.

Nalikuwa nimestarehe katika usingizi mara nikaona mkono wangu ukitomaswa nami kwa kugutuka taratibu nikamwona Mahina akinionyesha ule upande ilikokuwa ile mizoga ya mbuzi. Hana alilokuwa akininong'oneza ila kusema 'Simba'. Nikakumbatia bunduki yangu ya mianzi miwili niliyokwisha ishindilia marisasi tayari. Baada ya muda nikachekelea moyoni kwa kumwona simba akipita pale pale niliposhuku kuwa atapita tena karibu yetu kidogo. Sikuchelewa, nikamwachia nayo mianzi yote miwili sawia begani mwake, na katika kurukaruka kwake nikamwona akijipiga mikambi huku na huku. Upesi nikakimbilia kutia risasi nyingine, bali kabla ya kushindilia akanitoka machoni akaingia vichakani, hapo tena ikawa ni kujipigia ovyo shafuu shafuu. Sikuwa na wasiwasi sana kwani nina hakika ya kumwona asubuhi yake nami mara kulipokucha nikashika njia kwenda kumfuata. Ingawa nalichukua mwendo mrefu bali sikupata taabu ya kumwandamia kwa mchuruziko wa damu yake, na kwa kuwa mwendo wake ulikuwa wa kusitasita hapa na hapa nikawa na hakika kabisa kuwa ameumia vibaya.

Hatimaye nikahakikisha moyoni kuwa sina nilichopata kwani baada ya hatua chache baada ya hapo ile michirizi ya damu ikanipotea ardhi ikawa ya mwamba mtupu, hivyo nikashindwa kabisa kufuata nyayo zake.

Tulikaa shwari pasi na taabu yo yote ya adui wetu kwa muda wa siku kumi, nasi tukashuku kuwa bila ya shika amekwisha kufa kwa sababu ya kujeruhiwa kwake. Lakini usiku wa tarehe 27, mwezi wa Desemba, naliamshwa kwa Fadhaa ya kelele za watu wangu wa troli waliokuwa wamelala juu ya mti nje karibu na boma langu, kuwa simba mmoja alikuwa akijitahidi kutaka kuwakamata.

Mwezi ulizibwa kabisa na mawingu na pia ilikuwa shida mtu kuweza kuona chochote ila kilicho karibu yake; nikaona sina la kufanya ila kujipigia bunduki ovyo kiasi cha kumtisha yule simba awape nafasi. Kwa kweli hekima hizo zilifaa kwa kuwa wale hawakusumbuliwa tena usiku ule: lakini yule simba alionyesha dhamiri yake kwani asubuhi kulipokucha tu tukaona kuwa alijaribu kumwendea kila mtu hemani kwake na hapo penye shina la mti palitapakaa nyayo zake.

Jioni ya pili nikapanda juu ya mti ule ule kwa kutumaini kuwa atajaribu tena kuja kutafuta mawindo yake. ulinichwia vibaya mno, kwa kuwa wakati nilipokuwa nikipanda ule mti ilikuwa karibu kabisa kumgusa nyoka mkubwa sana aliyekua amejizingirisha katika tawi moja la mti, hakika nalishuka mbio mbio, lakini mtu mmoja akamchokora kwa mti mrefu akaondoka.

Bahati njema usiku ule haukuwa na mawingu, na mwezi nao ukang'aa na kuangaza kila kitu kama mchana. Nalikaa macho mpaka saa 8 ya usiku ndipo nilipomwamsha Mahina kushika zamu yake nami nipate kulala. Nalilala kwa muda wa saa nzima kisha nikagutuka ghafla na kushuku kuwa kuna hatari fulani. Pamoja na kugutuka kwangu, Mahina alikuwa macho wakati wote wala hakuona kitu chochote; nami ingawa nalitazama sana huko na huko, pia sikuweza kuona chochote. Nalikuwa nikitaka kulala tena hali nina mashaka moyoni, mara nikasikia kama kitu fulani kinapita kwa chini katika vichaka. Nilipo pakodolea macho sana pale mahali kwa dakika mbili hivi, nikaona ni kweli. Alikuwa nyamaume akitunyemelea taratibu kabisa.

Kule kuja kwake kulidhihirisha kuwa hakika ni mwindaji hodari wa watu: hivyo nami sikutaka kumfanyia haraka. Nikamwacha akaja mpaka alipokuwa karibu kabisa kiasi cha hatua ishirini hivi- nikamwachia nayo risasi ya kifua. Naliisikia ile risasi ikimwingia kifuani bali kumbe haikuwa na marisau ya nguvu kuangusha kitu, kwamba kiasi hicho hicho kageuka kurudi zake kwa hatua ndefu mno.

Kabla hajanitoka machoni nikadiriki kumpiga risasi nyingine tatu, na sababu ya ngurumo wake nikachukulia fahamu kuwa risasi mojawapo katika hizi imempata. Tukawa na wasiwasi kutakucha lini na kiasi cha kuanza kupambazuka tukatoka kwenda kumtafuta. Nikamchukua mtu mmoja wa kunisaidia ili nipate nafasi ya kupeleleza kwa makini, na Mahina akawa karibu yangu amechukua bunduki moja ndogo.

Michuruziko ya damu iltapakaa sana, kwahiyo hatukupata taabu ya kumwandamia sana; na basi, hatukwenda zaidi ya robo maili katika vichaka mara mbele yetu tukasikia ngurumo ya ukali. Nilipotupa jicho kwa makini nikamwona nyamaume amesimama anatazama upande ule tunaotokea, meno yake nje tayari kwa shambulio. Sikusubiri, nikamlenga shabaha na kumwachia risasi. Mara hiyo naye hakungoja akaturukia, hapo tena nikamwachia risasi ya pili ikamwangusha; punde baada ya nukta akajizoazoa kunifuata. Risasi ya tatu haikumpata, kwahiyo nikanyoosha mkono nichukue ile bunduki ndo nimmalize nayo. Kumbe Mahina amekwisha ona vimoto hakuweza kusubiri ila kukimbilia mtini pamoja na ile bunduki.

Nikaona tena hapana kinga ila nami kuwaandama wenzangu tukajiponye kule juu ya mti: kwa bahati, kama si risasi iliyomvunja mguu wake wa nyuma hakika angalinika mata. Hata hivyo, si muda mrefu uliopita tangu nipande juu ya mti mara naye akafika pale shinani.

Sasa basi, alipoona amekwisha nikosa akaanza kurudi vichakani, lakini nami kwa wakati huu ile bunduki nikawa nayo, na risasi ya kwanza niliyompiga ikawa ndiyo mauti yake. Kwa ujinga wa kumwona kuwa amelala kimya nikadhani kwamba amekwisha kufa kabisa kumbe vile angali akitweta; nikashuka mbio mbio mtini kumfuata, loo! akajizoa mara yake ya mwisho kunirukia. Wapi, nikammaliza kwa risasi mbili, moja ya kifua na ya pili kichwani, kabisa akaanguka kando kiasi cha hatua tano penye tawi la mti lililoanguka akafa kiume huku akitafuna lile tawi kwa hasira.

Ikawa watu wote kambini waliosikia vishindo vya bunduka walifika, na kwa mfundo waliokuwa nao kwa yule simba kwa kuwaua wenzao kadha wa kadha wakataka kumkatakata vipande vipande, bali nikajitahidi mno kuwazuia. Hatimaye wakamchukua mpaka bomani kwangu ambako si mbali pale tulipokuwa. Tulipomtazama tukaona risasi hazipungui sita zimemwingia mwilini, na mgongoni kuna alama zamarisau yale niliyompiga nayo kwanza nilipokuwa juu ya lile dungu kiasi cha siku kumi hivi zilizopita.

Habari zikavuma kila mahali kuwa yule nduli wa pili naye amekufa. Wenyeji wa nchi wakaja pande zote pwani na haraka kuja jionea wenyewe vioja hivyo pamoja na kumjua huyo 'mwua nduli', kwa namna walivyoniita.

Makuli hodari wote wa kazi waliotoroka wakarudi tena Tsavo kurudia kazi na hatukusumbuliwa tena na nduli hawa watoa roho za watu. Shani gani hiyo niliyoona kwa mabadiliko juu ya juhudi za kazi za wafanyaji kazi wangu baada ya kuwaua wale simba wawili! Badala ya kutaka kuniua tena kama walivyotaka kufanya mara ya kwanza, wakawa na shukrani kwangu wakanipa sinia moja kubwa ya fedha, pamoja na utenzi ulioandikwa kwa Kihindustani unaoeleza taabu na mashaka yetu yote yaliyotusibu na namna nilivyojitahidi kuwaokoa.

Simba hao wawili walikula makuli wa Kihindi wasiopungua ishirini na nane na wenyeji kadha wa kadha ambao idadi yao haikuweza kuhesabika.
 
Back
Top Bottom