Ukweli wa Pasaka kama alivyofundisha Mungu
Kwa mujibu wa mafundisho ya Biblia, Pasaka ni mnyama ambaye wana wa Israeli waliamrishwa na Mungu wamchinje na wamle kwa kufuata utaratibu aliouelekeza Mungu na kwa lengo maalum. Maandiko yafuatayo yanathibitisha ukweli huu:
"Hapo ndipo Musa aliwaita wa Israeli, na kuwaambia, Nendeni, mkajitwalie wana kondoo kama jamaa zenu zilivyo, mkamchinje Pasaka". (Kutoka 12:21),
"Nawe umchinjie Pasaka BWANA, Mungu wako, katika kundi la kondoo na la ng'ombe, mahali atakapochagua BWANA apakalishe jina lake". (Kumbukumbu la Torati 16:2),
"Usimchinje Pasaka ndani ya malango yako yote akupayo BWANA, Mungu wako, ila mahali atakapochagua BWANA, Mungu wako, apakalishe jina lake, ndipo mtakapomchinja Pasaka jioni, katika machweo ya jua, kwa wakati kama uliotoka Misri". (Kumbukumbu la Torati 16:5-6).
Kulingana na maandiko hayo juu, tunaona hapa Biblia inafundisha wazi kuwa Pasaka ni kondoo au ng'ombe ambaye Mungu aliwaamuru wana wa Israeli wamchinje kisha wamle.
Aidha, maandiko hayo yanaonyesha wazi pia kuwa amri hiyo (ya kuchinja na kumla Pasaka) haikuwahusu watu wa mataifa mengine isipokuwa Waisraeli peke yao.