Aibu,fedheha na umajinuni tu ambao unaweza kukufanya kijana ukampiga babu yako au baba yako.Mzazi wa mwenzako ni mzazi wako pia.Hii inapatikana Tanzania tu kwa vijana kuwapiga wazazi wao kwa kuwa tu wamehitilafiana kimtazamo na kifkra.You can kill a thinker,but you can't kill the thought.
Kitendo kilichojitokeza siku ya Jumapili pale Blue Pearl ni ukiukwaji wa maadili ya taifa na muonekano finyu wa kundi linaloaamini limeumbwa kwa ajili ya kutawala wengine bila hata ridhaa ya wengi.
Watu hupingana kwa hoja na si kwa kupigana,Mwalimu JK Nyerere alitulea hivyo, ndiyo maana aliweza kujenga hoja bila kushika panga wala mawe na hatimaye uhuru ukapatikana.Yako wapi matunda ya Mwalimu ikiwa jumuiya ya chama chake iliyotumika kuibua vipaji vya uongozi ina dhalilika kwa vijana wake kutumika katika viashiria vya uvunjifu wa amani nchini tuhuma ambazo zina chafua jumuia hiyo na kudumaza demokrasia nchini.
Uko wapi uhuru wa kupata habari kwa mujibu wa katiba ya 1977 ibara ya 18 ikiwa uhuru huo unatumika vibaya na kuruhusu wazee wetu kunyanyaswa kwa kuwa tu wametofautiana kimtazamo na kimaono na watawala.Mwalimu alisema bila CCM madhubuti nchi itayumba,hakumaanisha kuwa ndiyo wana haki ya kutawala wengine,kauli ya Mwalimu leo inatumika vibaya na watawala kiasi cha kutumia nguvu kubwa kulazimisha matakwa yao.Walio kishika chama wamekosa umadhubuti na kutaka kuwashikia watu akili hata kama kuna ukweli unao kigharimu chama hawapendi kuusikia.
Kutokubali kukosolewa ndiko leo kumezaa hoja kudhibitiwa kwa ngumi,siasa inataka uvumilivu lakini uvumilivu wa makonde kwa wanao tofautiana kimtazamo ni anguko linalo kwenda sambamba na kauli ya marehemu Kolimba kuwa CCM imekosa dira na mwelekeo.
Kitendo kilicho fanywa na Makonda na wafuasi wake huku kikishangiliwa na kushereheshwa na M/Kiti wa bunge maalum la katiba ni ukiukwaji wa maadili ya umma na viashiria vya uvunjifu wa amani nchini.Dawa ya hoja ni hoja na si vinginevyo.
Mzee Warioba na wajumbe wa taasisi ya mfuko wa Mwalimu Nyerere ni wazee walioheshimika sana hapa nchini kutokana na utumishi wao uliotukuka,wanapoona nchi ina yumba lazima waseme hakuna sehemu sawia ya kusemea zaidi ya hadhara ili wananchi wawasikie na kama kuna hoja chama chao kimeona imekwenda vibaya wanapaswa kuijibu,na hiyo ndiyo demokrasia,kuwapiga ni anguko ambalo lisipo dhibitiwa nchi itayumba na hapo ile hoja ya bila CCM madhubuti nchi itayumba inapokuwa na mashiko.
Napenda kuwaasa Watawala kuitumia fursa ya uwepo mdogo wa amani vizuri kuliko viashiria vya uvunjifu kuachiwa vikashamiri mbele ya umma huko chombo cha dola kikiwa kimejaa ganzi na kigugumizi kisicho na mantiki zaidi ya kuonyesha uonevu wa tabaka la watawala dhidi ya watawaliwa.
Mwisho,amani haiji kwa kuinadi hadharani ilihali una watengenezea watawaliwa anguko la uvumilivu,wakichoka uvumilivu tutakuwa tumekalia kuti kavu kwa kumtaka Mungu shari maana uvumilivu una kikomo.
Makonda na wenzake wana paswa kuonywa na chombo cha dola kuchukua kusimamia sheria kwa kuwafikisha mbele ya sheria wale wote waliosababisha uvunjifu wa amani hususani katika kipindi hiki kigumu kinachotaka wananchi wapewe elimu ya uraia na kujua haki zao kabla ya kufanya maamuzi.
Nawakilisha kwa uchungu mkubwa kwa kuwa usanii siku hizi umepewa kipau mbele na media zetu kuliko uzalendo unaoonyeshwa kwa vitendo.Leo kuvinunua vyombo vya habari ni jambo la kawaida sana na kwa mantiki hii watawaliwa hawana lao kwa kuwa hata huo mhimili wa nne wa dola usio rasmi nao umeamua kufanya biashara ya maisha ya watu na rasilimali zao kwa kuwapa mafisadi coverage kubwa ya kuficha ufisadi wao na kupuuza kilio cha wengi.
Mungu Ibariki Tanzania na watu wake.