Kosa kuu la Kikwete, Lowassa na Rostam
Ansbert Ngurumo
LIPO kosa moja kubwa sana la wanamtandao wa Rais Jakaya Kikwete. Kwa miaka mingi, wamejaribu kuungoa muhimili wa nne wa dola - vyombo vya habari. Kwa kiasi fulani wamefanikiwa kuulegeza.
Mbinu kubwa waliyotumia ni kuwakumbatia (baadhi ya) wahariri. Wakawatumia, nao wakatumika; wengine wakafukuzwa hata kazi kwenye kampuni walizokuwamo, wakapewa kazi nyingine na wale wale waliowafukuzisha.
Wamewagawa wanahabari na kuwapa lebo za bei zao katika jamii, hata pale ambapo hawakuwalipa chochote. Taratibu, kwa makusudi au bila kujua, mtandao ulioongozwa na Kikwete, Edward Lowassa na Rostam Aziz umejikuta unaumba kizazi kipya cha mafisadi miongoni mwa wahariri.
Heri wangekuwa wameshirikiana na kizazi cha wazee, kinachostaafu kazi muda mfupi ujao. Ukubwa wa dhambi unatokana na ukweli kwamba wengi miongoni mwa kizazi hiki ni vijana, ambao kama Mungu amewajalia uzima, wataendelea kuongoza vyombo vya habari. Tutaweza kuwaongoa na kuwabatiza? Au wao ndio watakaotuongoa sisi?
Je, wale waliowaharibu wahariri hawa, watafika mahali watambue kosa lao, wajute na kutubu na kuongoka pamoja jeshi lao? Au ndiyo tukubali kwamba maangamizi ya taifa yamejikita katika kizazi hiki? Kwa nini kizazi chetu kijiruhusu kuwa cha laana kwa mingi ijayo?
Kuna usemi wa wahenga kwamba ukitaka kumuua mbwa, ua pua yake. Kina Rostam walijua kwamba pua ya uandishi ni wahariri. Walidhamiria kuua pua za waandishi kwa nia mbili. Kwanza, wawasaidie kuingia madarakani bila kuwahoji, wailegeze jamii iwashabikie, iwaunge mkono. Hilo walifanikiwa.
Pili, walitaka waandishi wawasaidie kutawala. Wawasindikize katika kuandika na kuridhia mikataba mibovu. Wawe washirika katika kuchuma na kugawana kasungura miongoni mwao, ikiwezekana wawarushie makombo (maana wahenga husema mbwa wa mfalme ni mfalme wa mbwa wengine).
Hili la pili lilifanikiwa kidogo, baadaye likashindikana kwa sababu jamii iliamka mapema kuliko wao walivyodhani. Ufisadi ukawa hoja kuu ya wananchi baada ya kuona mafisadi ndio wanaotawala!
Ingawa hawakuwa wameweza kuwakamata wahariri wote, kazi iliyofanywa na hao waliowekwa sawa, ilikuwa na kishindo kikubwa kilichoitikisa nchi katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, na kimeacha sumu kali katika fani ya uandishi wa habari. Matokeo yake, waandishi hawaaminiani, na hadi sasa wanatafunana wao kwa wao kama samaki. Kikwete na kundi lake, hawawezi kukwepa dhambi hii.
Na ndiyo maana, hata serikali ilitaka kuwatumia hawa hawa kupitisha muswada (ambao yenyewe iliuita) wa uhuru wa habari mapema mwaka jana. Wadau wa habari waliuchunguza na kukuta umeficha hila nyingi za serikali na wapambe wao. Wakaukataa kwa kuwa muswada ulikuwa unalenga kuwakabidhi maadui wa uhuru mamlaka ya kuteka uhuru huo.
Ulikuwa utumwa mpya katika lugha tamu tamu. Wakubwa walikurupuka kutunga sheria mpya haraka haraka kulinda siri zao, kuwadhibiti waandishi wakorofi.
Mgawanyiko huu miongoni mwa wanahabari umeendelea kuwapo, hata baada ya wanahabari kushikamana na kuunda Jukwaa la Wahariri, Mei, 2007. Lakini mgawanyiko wa wahariri (wa jinsi hii) unalisaidiaje taifa?
Kwa kukumbushana tu, katika kuzindua Jukwaa la Wahariri, wanahabari hao walijipa malengo kadhaa, yakiwamo yafuatayo; Kwanza, walidhamiria kukilea chombo hicho ili kikue na kutekeleza madhumuni ya kuanzishwa kwake.
Pili, walisisitiza kwamba jukwaa hilo si chombo cha kupambana na serikali na wala si cha kumkomoa mtu yeyote katika jamii, bali ni chombo chenye kazi ya kuwahabarisha, kuwaelimisha na kuwaburudisha wananchi, bila kusahau wajibu wa kuikosoa serikali na jamii pale zinapoteleza.
Tatu, waliazimia kukifanya chombo hicho kuwa mstari wa mbele katika kuisaidia serikali kuleta maendeleo ya Watanzania. Hivyo, walijipa jukumu la kukutana na kujadiliana kuhusu masuala mbalimbali yenye maslahi kwa Watanzania, kuhoji utendaji wa viongozi na mchango wao katika maendeleo ya nchi na maslahi ya wananchi.
Nne, walisisitiza kwamba chombo hicho kingekuwa kiunganishi na sauti ya pamoja ya wahariri kwa niaba ya wananchi; ili jukwaa hilo liwe kwa manufaa ya wakulima, wafanyakazi, wafanyabiashara, wajasiriamali na makundi mengine katika jamii.
Mara tu baada ya uzinduzi huo, wahariri hao walionywa mwanzoni kabisa juu ya utendaji wao. Aliyewaonya ni mwandishi mkongwe, Ndimara Tegambwage, ambaye huandika safu ya SITAKI katika gazeti hili.
Aliandika hivi: Sitaki wahariri wakuu wa vyombo vya habari nchini waunde umoja utakaokufa haraka; kwa kishindo kikubwa na kwa aibu tupu. Kwani hadi sasa baadhi ya wahariri wamekuwa wakiishi kama wapigania uhuru; wengine kama marafiki wakuu wa watawala; wengine kama watawala wenyewe na wengine kama mbifemuki vyovyote itakavyokuwa.
Baada ya kuchambua kwa kina maana na lengo la jukwaa hilo, mwandishi huyo alihoji mambo kadhaa, akasema: Je, umoja huu una ubavu wa kuvunja kambi zilizotokana na ama utashi wa wahariri binafsi, shuruti za kimaisha, urafiki na watawala au mlegezo wa maisha utokanao na rushwa na ufisadi kadha wa kadhaa?
Kwamba huu si umoja wa kurahisisha mahusiano kati ya baadhi ya viongozi wachache na wahariri ambao ni baunsa wa langoni kwa shabaha ya kuendeleza usiri wa fikra na matendo ya serikali?
Kwani wahariri wakiamua habari ichapwe itachapwa, wakikataa itadoda na kutoweka. Uamuzi wao unadhihirisha uwezo mkubwa unaopaswa kukabidhiwa kwa watu makini.
Je, umoja umekuja bila kushawishiwa kuwa daraja au bomba la kupitishia bahasha za kupoza nyoyo na kalamu? Na katika kambi zilizopo, kila moja ikijiita bora, suala la bahasha haliwezi kuvuruga umoja huu katika uchanga wake?
Yote haya yanasemwa kutokana na mazingira ya uandishi na waandishi, hasa wahariri, yaliyojitokeza tangu 2005 ambako waandishi na wahariri walishindana kuremba wagombea urais na viti vingine, ili baadaye wafikiriwe kuingia utukufu wa kisiasa; si kwamba wagombee nafasi hizo na kuingia katika siasa au kuwa karibu na wanasiasa, bali wateuliwe kufanya kazi Ikulu, au wawe wakuu wa mikoa, wilaya au nafasi nyingine! Hivi sasa, kwa wengi, ni masimulizi ya matumaini yaliyopotea.
Kama Ndimara angeamua kutaja majina ya wahariri, vyombo vyao na makundi yao katika hiki anachokieleza hapa, angefanya hivyo kirahisi. Anawajua wahariri wetu. Anaona kazi zao. Anajua uhusiano wao na waajiri wao na rafiki zao wa kisiasa. Anajua vishawishi vinavyowazonga, na anajua msukumo na msimamo wa baadhi yao.
Anawajua wanaoendekeza njaa, na ambao wameugeuza uandishi kuwa ukarani. Anawajua pia walio tayari kufa njaa, ili dhamira kuu ya kazi yao itimie. Anawajua waandishi wanaojiona kuwa sehemu ya serikali, na wengine walio upande wa wananchi.
Na katika vita hii ya sasa dhidi ya ufisadi, wahariri hawajashinda vita ya mafisadi kuwagawa katika makundi. Kundi moja linawatetea mafisadi, jingine linawamulika mafisadi.
Na kama wahariri wasingekuwa wamegawanyika hivi, Watanzania wangekuwa wameshashinda vita dhidi ya ufisadi tangu zamani. Lakini mafisadi walijua hilo hata kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2005. Walijua nguvu ya wahariri, na walijua udhaifu wao. Na baadhi yao walijua hata bei zao!
Nguvu hizo, udhaifu huo na bei hizo, ndizo zimekuwa kinga madhubuti za mafisadi kwa miaka mitatu sasa. Hata wakibanwa vipi, wana mahali pa kutokea kuzungumzia, kupotosha mjadala au hata kujisafisha.
Na makundi haya yote yamo katika jukwaa la wahariri. Yanahujumiana na kudhalilishana. Na katika kufanya hivyo, yanawachanganya wananchi.
Kwa mfano mmoja wa hivi karibuni, yeyote aliyesoma habari za juzi katika magazeti kadhaa yanayoegemea kwa CCM na serikali, yakieleza jinsi wananchi wa Tarime walivyofanya fujo Alhamisi jioni na kuwatimua baadhi ya viongozi kwenye mazishi ya aliyekuwa Mbunge wa Tarime, Chacha Wangwe; halafu akasoma gazeti hili likieleza habari tofauti, jinsi viongozi hao hao walivyopokewa kwa heshima zote na kusindikizwa hadi walipopaswa kwenda; na baadaye akasoma habari ikimnukuu msemaji wa familia ya Wangwe, kwamba familia inasikitishwa na kushangazwa na uandishi chonganishi zilizotungwa kwa lengo la kisiasa; atabaki anawashangaa wahariri.
Lakini baadaye imedhihirika kwamba kuna kundi lilipewa pesa lifanye fujo msibani kwa maslahi ya kisiasa, lakini bahati nzuri lilifahamika na kudhibitiwa, huku waandishi waliohusishwa walishaandika habari yenye tukio ambalo halikutokea!
Tutaidhalilisha taaluma kiasi gani kabla ya kushituka na kusema inatosha? Je, msomaji wa kawaida asiyejua makundi hayo ya wahariri, na mbinu zinazotumika kuwagawa, ataamini habari ipi na kupuuza ipi? Ni lini taifa litaondokana na kizazi hiki cha ufisadi uliojikita ndani ya mfumo unaotafuna hata taaluma za watu?
Ninavyoamini mimi, wanahabari hawana kosa kuwa na itikadi au kuwa wanachama kwa hiari. Kosa ni kujifanya hawana itikadi, huku wakifanya kazi za kueneza itikadi za vyama ambavyo wanadai hawaviungi mkono. Yawezekana kuna mawili; ama hawajui maana ya itikadi, au hawajui umuhimu wa kuwa na itikadi. Lakini kwa mujibu wa matendo yao, nao wana itikadi.
Bado nawatafuta wanahabari wasio na itikadi. Sijawaona. Labda wapo! Lakini wale ninaowajua, wanaochomoza sana katika maandishi yao, ni waandishi wenye itikadi - ama za kuambukizwa au zinazotokana na imani zao wenyewe.
Wale wenye itikadi za kuambukizwa, hawana msimamo. Ni vipepeo. Ni vinyonga. Hawaaminiki. Wanabadilikabadilika kulingana na urafiki au ugomvi walionao kwa wenye itikadi. Na katika siasa za Tanzania, hili ndilo kundi la wanamtandao, na ndilo limekuwa linashutumiwa kwa kuufanya uandishi wa habari kuwa ukarani.
Na imedhihirika kwamba hata ndani ya CCM, waandishi wenye kufuata itikadi thabiti ya CCM, hawana kiherehere, hawajipendekezi, hawatumiwi. Na hawasikiki sana hadi wakati wa uchaguzi. Wenye itikadi za kuambukizwa, ndio wanaosikika sana; ndio wanaotumiwa na wakubwa. Ndio wanaotuhumiwa kufanya ukarani!
Na baadhi yao ni wasomi ambao wangepaswa kutusaidia kuukomboa uandishi kutoka kwenye utumwa huu. Wenye itikadi zitokanazo na imani binafsi katika masuala kadhaa, wamejipambanua kama watu wenye msimamo. Hawatazami sura, cheo au uwezo wa kifedha wa mtu yeyote. Hawatafuti urafiki au maslahi binafsi bali wanaangalia picha pana zaidi; mustakabali wa jamii nzima.
Naamini kwamba kila mmoja wetu yumo katika mojawapo ya makundi haya. Ni lipi litaivusha Tanzania kuelekea huko tuendako, tunakotamani kuwarithisha watoto wetu? Katika mgawanyiko wetu, wananchi wanatuona. Upande mmoja kuna wanahabari wapambanaji dhidi ya ufisadi; upande mwingine kuna marafiki wa mafisadi, watetezi na mashabiki wao, wanaotumika kudhoofisha vita dhidi ya ufisadi.
Inasikitisha inaposemekana kuwa walio nyuma ya ukarani huu ni wale wale waliokuwa wanahusishwa na ufisadi mkubwa katika miaka mitatu iliyopita; wale wale waliowatumia waandishi kuwachafua na kuwadhoofisha washindani wenzao kabla ya uchaguzi mkuu mwaka 2005; na wale ambao katika siku za hivi karibuni wamekuwa wakitapatapa kujisafisha na uchafu wa tuhuma za ufisadi.
Wanasiasa na wafanye watakavyo; maana ni wanasiasa. Lakini je, hawawezi kufanikisha njama zao bila kutumia waandishi? Iwe itakavyokuwa, huu umeshakuwa ugonjwa wetu; na waliotuambukiza ugonjwa huu tunawajua. Na hili ndilo kosa kubwa ambalo kizazi hiki hakitawasamehe iwapo hawatatubu na kuacha!
+447853850425
ansbertn@yahoo.com
Utakapojua Hujui Ndipo Utakapojua