sir.JAPHET
JF-Expert Member
- May 18, 2012
- 699
- 133
*Amfukuza kazi Mkurugenzi Idara ya Wanyamapori
*Maofisa wawili nao wafungashiwa virago rasmi
*Wengine wapewa onyo kali, uchunguzi unaendelea
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Khamis Kagasheki, amemtimua kazi Mkurugenzi wa Wanyamapori, Obeid Mbangwa, kutokana na tukio la kutoroshwa wanyama hai zaidi ya 100 kwenda nchini Qatar.
Mbali na Mbangwa, wengine waliotimuliwa kazi kuhusiana na tukio hilo ni Ofisa katika Ofisi ya Uwindaji wa Kitalii CITES na Utalii wa Picha mkoani Arusha, Simon Gwera pamoja na Frank Mremi, ambaye ni Ofisa katika Ofisi ya Uwindaji wa Kitalii CITES na Utalii wa Picha mkoani Arusha.
Wakati hao wakitimuliwa kazi, mfanyakazi mmoja, Bonaventura Midala ambaye ni Mkurugenzi Msaidizi, Uendelezaji Wanyamapori, ameshushwa cheo kwa sababu hakuchukua hatua zinazostahili wakati wanyama hao wanatoroshwa.
Kwa mujibu wa Waziri Kagasheki, wakati wanyama hao wanatoroshwa, Midala alikuwa Mkurugenzi Msaidizi sehemu ya kudhibiti ujangili.
Taarifa hiyo, ilitangazwa jana na Waziri Kagasheki, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa na kwamba kabla ya kufikia maamuzi hayo, ziliundwa tume huru mbili ambazo zote zilitoa mapendekezo yanayofanana. Pamoja na uamuzi huo, alisema yeyote ambaye hakuridhika anatakiwa kukata rufaa.
Ndugu waandishi wa habari, nimewaita hapa leo ili kuwaeleza juu ya hili suala la utoroshwaji wa wanyama hai kwenda nje ya nchi.
Hili ni suala ambalo Bunge lililopita la mwaka jana lililizungumzia na baada ya kulifuatilia kumekuwa na sehemu mbili muhimu.
Sehemu ya kwanza, ilikuwa inahusu watumishi wa wizara waliohusika katika utoroshaji wa wanyama, lakini sehemu ya pili ni upande wa nchi ya Qatar, ambako ndiko inasemekana wanyama ndiko walikopelekwa na pia kuna watu wengine walioko nje ya wizara, wakiwamo wafanyabiashara kama Ahmed Kamran.
Upande wa wizara, tumefanya kila jitihada kuhakikisha wale wote waliohusika katika kadhia hii tunawachukulia hatua, lakini kwa umakini mkubwa sana, kwani hatutaki kumwonea mtu, tunataka haki itendeke na sheria ichukue mkondo wake.
Uamuzi tuliochukua siyo wa kufurahisha kwa sababu hakuna anayependa fulani aachishwe kazi, lakini baada ya kulitizama suala hili kwa muda mrefu, wizara imefikia maamuzi yafuatayo na hii ni kutokana na sheria namba 8 ya utumishi wa umma ya mwaka 2002, kifungu 6 (1) ambacho kinampa mamlaka Katibu Mkuu wa Wizara kutekeleza nidhamu katika wizara.
Kutokana na hayo, wafanyakazi wafuatao wamefukuzwa kazi na tayari wameshapewa barua za kufukuzwa kazi.
Waliofukuzwa kutokana na ukiukwaji wa sheria ni Obeid F Mbangwa, huyu alikuwa Mkurugenzi wa Wanyamapori, lakini wakati wa kadhia hii, alikuwa Mkurugenzi Msaidizi, Matumizi ya Wanyamapori, alisema Waziri Kagasheki na kuongeza:
Mwingine ni Simon Charles Gwera, huyu alikuwa Ofisa, Ofisi ya Uwindaji wa Kitalii, CITES na Utalii wa Picha Arusha, ambaye naye alihusika kwa mujibu wa ushahidi pamoja na Frank Mremi wa Ofisi ya Uwindaji wa Kitalii CITES na Utalii wa Picha Arusha, alisema Waziri Kagasheki.
Wakati hao wakichukuliwa hatua hiyo, alisema maofisa wawili wa wanyamapori daraja la pili, wamepewa onyo kali la maandishi kwa kuwa walitekeleza maagizo haramu ya wakubwa wao wa kazi.
Aliwataja maofisa hao kuwa ni Martha Msemo, ambaye ni Ofisa Leseni, Ofisi ya Uwindaji wa Kitalii, CITES na Utalii wa Picha Arusha na Anthonia Anthony, ambaye ni Ofisa Leseni, Ofisi ya Uwindaji wa Kitalii, CITES na Utalii wa Picha jijini Dar es Salaam.
Mwingine aliyepewa onyo kali la maandishi ni Silvanus Okudo, ambaye ni Mkuu wa Kituo cha Uwindaji wa Kitalii, CITES na Utalii wa Picha Arusha. Alisema Okudo amechukuliwa hatua hiyo kwa kuwa alishindwa kufuatilia na kupata maelekezo ya Mkurugenzi wa Wanyamapori kuhusu mtumishi wake aliyekiuka sheria katika utoaji wa vibali.
Alisema Okudo, alishindwa kupeleka kwa Katibu Mkuu, taarifa kuhusu mtumishi huyo ili achukuliwe hatua za kinidhamu.
Sambamba na hao, Waziri Kagasheki alisema maofisa wawili ambao ni Mohamed Madehele wa Ofisi ya Matumizi Endelevu ya Wanyamapori na Mariam Nyallu wa Kituo cha Uwindaji wa Kitalii, CITES na Utalii wa Picha Arusha, wanaendelea kuchunguzwa.
Akizungumzia Serikali ya Qatar ambayo ndege yake ilitumika kusafirisha wanyama hao kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro, alisema Serikali ya nchi hiyo haitaki kutoa ushirikiano wowote, licha ya kuombwa kufanya hivyo.
Kutokana na hali hiyo, alisema Serikali ya Tanzania haijakata tamaa na kwamba imeunda timu ya watu mbalimbali, wakiwamo kutoka Idara ya Usalama wa Taifa, Ofisi ya Mwendesha Mashitaka Mkuu (DPP), Wizara ya Katiba na Sheria kwa ajili ya kushughulikia jambo hilo.
Baada ya Serikali ya Qatar kukaa kimya, tulilazimika kuandika barua makao makuu CITES kule Geneva, Uswiss kisha Qatar wakatuandikia barua, kwamba wamepata barua kutoka Geneva.
Lakini hatujakata tamaa, tutakwenda Qatar, tutawahoji mapailoti wa hiyo ndege pamoja na kuangalia vibali vya kuwachukua hao wanyama ili kujua vilipatikanaje.
Kuhusu huyu mfanyabiashara Ahmed Kamran, ambaye alihusika katika suala hili, yeye ushahidi upo na wakati wowote atafikishwa mahakamani, alisema.
Novemba 24 mwaka juzi, wanyama hai 116, wakiwamo twiga wanne na ndege 16, walitoroshwa nchini kwa kupakiwa kwenye ndege ya Shirika la Ndege la Qatar kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) na kupelekwa nchini Qatar kinyume cha sheria.
Baada ya tukio hilo, aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Ezekiel Maige, alimsimamisha kazi Mkurugenzi wa Wanyamapori, Obeid Mbangwa, ili kupisha uchunguzi wa tukio hilo.
Wakati Maige anatoa uamuzi huo katika Bunge la Bajeti, Mbangwa alikuwapo bungeni na baada ya kusikia hivyo, alitoroka bungeni akipitia mlango wa nyuma ili kuwakwepa waandishi wa habari pamoja na wapiga picha waliokuwa wakimfuatilia.
Hata hivyo, wapiga picha ambao walikuwa wamejipanga katika milango yote ya kuingia katika ukumbi wa Bunge, walifanikiwa kumpiga picha, ingawa yeye na wapambe wake hawakutaka apigwe picha.
Kutokana na uzito wa suala hilo la kusafirisha wanyama hai, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, alisema Serikali imesitisha utoaji wa vibali vya kusafirisha wanyama hai kwenda nje ya nchi, hadi itakapotangazwa tena.
SAAAFI SAANA KAGASHEKI UMEANZA VIZURI MALIZA VIZUURI KILA LAHERRI TUKO NYUMA YAKO!!