bibikuku
JF-Expert Member
- Feb 16, 2011
- 832
- 495
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumatano, Aprili 6, 2011, ameungana na mamia ya waombolezaji katika kumzika Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Mamlaka ya Reli Tanzania (TRAWU) Bwana Sylvester Raphael Rwegasira yaliyofanyika kwenye makaburi ya Kinondoni, Dar es Salaam.
Rwegasira aliyekuwa na umri wa miaka 52 alifariki dunia ghafla asubuhi ya Jumatatu wiki hii kwenye Hospitali ya Dar Group alikokuwa amekimbiziwa kutokana na matatizo ya ugonjwa wa moyo.
Pamoja na Rais Kikwete kwenye mazishi hayo walikuwa ni viongozi wa Serikali kutoka Wizara za Uchukuzi, na Kazi na Ajira na viongozi wa vyama vya wafanyakazi nchini.
Miongoni mwa viongozi waliohudhuria mazishi hayo ni pamoja na Waziri wa Kazi na Ajira, Mheshimiwa Gaudencia Kabaka, Katibu Mkuu wa Wizara ya Kazi na Ajira, Bwana Erick Shitindi na Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Bwana Omari Chambo.
Viongozi wa vyama vya wafanyakazi wameongozwa na Mwenyekiti wa Taifa wa TRAWU, Bwana Bakari Kiswala na Mwenyekiti wa Taifa wa Muungano wa Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Bwana Omari Ayubu.
Akizungumza kwa ufupi sana katika mazishi hayo baada ya kuwa ameombwa na Bwana Kiswala, Mheshimiwa Rais Kikwete ametoa pole kwa familia ya marehemu, kwa watumishi wenzake katika sekta ya usafirishaji wa reli na kwa TUCTA akisema kuwa marehemu alikuwa mtetezi wa kweli kweli wa wafanyakazi nchini.
Poleni nyote kwa msiba huu mkubwa. Napenda kuwahakikishieni kuwa msiba wenu ni msiba wetu pia, amesema Rais Kikwete na kuongeza:
Najua fika kuwa huu ni wakati mgumu kwa familia, lakini vile vile ni wakati wa subira na uvumilivu kwa sababu kila binadamu lazima apitie katika njia hiyo. Kama kuna jambo ambalo kila mmoja wetu ana uhakika nalo basi ni kufikiwa na mauti.
Wakati msiba huo ulipotokea Rais Kikwete alituma salamu za rambirambi kwa familia ya Marehemu Rwegasira kupitia kwa Waziri wa Uchukuzi, Mheshimiwa Omar Nundu ambako alimwelezea marehemu kama kiongozi shupavu na mtetezi asiyeyumba wa haki za wafanyakazi.
Rais Kikwete alikuwa amepanga kukutana na kuzungumza na viongozi wa vyama vya wafanyakazi nchini kuhusu masuala mbalimbali kuhusiana na haki za wafanyakazi leo, Jumatano, Aprili 6, lakini Rais aliahirisha kikao hicho kufuatia msiba huo. Kikao hicho kitafanyika baadaye.
Mwisho.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
06 Aprili, 2011