Yapo maoni ya watu mbalimbali kuwa vyakula vilivyobadiliwa vinasaba GMO ni hatari kiafya na vimetengenezwa mahususi kwa ajili ya kuua kizazi cha watu weusi.
Je ukweli upoje kuhusu jambo hili?
Je ukweli upoje kuhusu jambo hili?
- Tunachokijua
- GMO ni mmea, wanyama, au viumbe vidogo ambavyo hubadiishwa vinasaba (DNA) kwa kutumia teknolojia maalumu (uhandisi jeni) ili kuondoa sifa zake za awali na kutambulisha sifa mpya inayohitajika katika kiumbe hicho.
Kwa kawaida mchakato huo hupelekea viumbe/mimea kubadilika na kuwa na aidha umbo kubwa zaidi ya kawaida yake au kuongezeka idadi uzalishaji wake au kuwa na uwezo wa kustahimili mazingira ya uzalishaji wake.
Je, vyakula vya GMO ni hatari kiafya?
Inaelezwa kuwa Vyakula vya GMO vinachunguzwa kwa kina kabla havijauzwa kwa watu ili kuhakikisha viko salama kama vyakula vingine. Tafiti za kitaalamu zinaonesha kuwa vyakula vilivyobadilishwa vinasaba havikuathiri tofauti na vyakula vya kawaida.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) wanabainisha kuwa kwa ujumla GMO haileti ubaya wowote kwa mwanadamu. Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) lilifanya tafiti mbalimbali ili kuchunguza vyakula tofauti vilivyobadilishwa vinasaba lakini hakuna kilichobainika kuleta madhara kwenye miili ya binadamu.
Sehemu ya maelezo ya WHO yanayopatikana kwenye tovuti yao rasmi yanasema;
"Viumbe tofauti vya vyakula hivi hujumuisha jeni tofauti zilizoingizwa kwa njia tofauti. Hii ina maana kwamba usalama wake unapaswa kutathminiwa kwa msingi wa visa kwa visa na kwamba haiwezekani kutoa taarifa za jumla juu ya usalama wa vyakula vyote vya aina hii.
Vyakula vinavyopatikana kwa sasa kwenye soko la kimataifa vimepitisha tathmini za usalama na havina uwezekano wa kusababisha hatari kwa afya ya binadamu. Aidha, hakuna madhara yoyote kwa afya ya binadamu yameonekana kutokana na ulaji wa vyakula hivyo na wananchi kwa ujumla katika nchi walizoidhinishwa. Utekelezaji wa mara kwa mara wa tathmini za usalama kwa kuzingatia kanuni za Codex Alimentarius na, inapofaa, ufuatiliaji wa kutosha wa soko, unapaswa kuunda msingi wa kuhakikisha usalama wa vyakula hivi"
Aidha kuhusu matumizi ya mbegu za GMO Tanzania, JamiiForums imefanya mawasiliano na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Wizara ya Kilimo, Hudson kamoga amesema
“Msimamo wetu sisi Tanzania hatuna mbegu za GMO na hatujawahi kuruhusu mbegu hizo, kwa sababu GMO ni mbegu zinazozalishwa kwenye maabara.”
JamiiForums haijapata uthibitisho usiotia shaka kuwa mbegu na vyakula hivi vipo maalum kuondoa uhai wa watu weusi kama inavyodaiwa hivyo inachukulia suala hili kama nadharia inayopaswa kufanyia uchunguzi na utafiti mkubwa zaidi.