Jamani, kwani lazima?

Jamani, kwani lazima?

JAMANI KWANI LAZIMA-10

ILIPOISHIA
"Nini sasa, kwa vile nimekwambia nafanya kazi ya upelelezi?"
"Siyo hivyo, niache kwanza."
JIACHIE WEWE SASA

!Sasa nitakuachaje wakati tumekuja wote? Oke, kwa hiyo niondoke?"
"Ondoka ndiyo."

"Khaa! Unajua sikuelewi Mage!"
"Kwanza mi siitwi Mage."
"Unaitwa nani?"

"Siyo lazima kujua jina langu."
"Kumbe we mwongo!"
"Hata nikiwa mwongo we inakuhusu nini?"
Ibra alianza kuamini kwamba, Paulina hakuwa sawa kichwani, akakumbuka vile alivyoingia ndani ya daladala huku akilia.

"Lakini nakusamehe, maana hata kwenye daladala ulipokuwa ukilia nilijua kichwa chako hakiko sawasawa hata kidogo," alisema Ibra na kuchomoka zake huku akimwacha Paulina anaendelea na kilio chake.

"Huu mkosi gani mimi jamani?"
"Ina maana nitatembea na wanaume wangapi sasa?"
"Hata mwezi bado tayari wanaume watatu, mi si malaya sasa?" Paulina alijisema mwenyewe. Aliamua kesho yake arudi kwa mganga wake amsimulie kuhusu visa vyake.

***

"Sahamani babu, mimi nimerudi tena, nina shida kubwa sana," Paulia alimwambia mganga wake siku ya pili alipokwenda kwake.
"Shida gani mjukuu wangu?"
"Mimi babu nimeshatembea na wanaume watatu, mbaya zaidi wawili ni kwa siku moja."
"Enhe, kwa ajili ya mimba au starehe zako?"
"Kwa ajiili ya mimba."

"Si ndiyo vizuri, utazaa mapacha watatu."
"Siyo hivyo babu, labda nikuelezee kwanza."
"Nakusikiliza."
"Kama utakumbuka nilikuja kukwambia nimetembea na jirani yangu baba Riziki ukasema hakuwa na sifa kwa sababu shati jekundu nililinunua mimi?"'

"Nakumbuka sana tu. Ni kweli yule hakuwa na sifa."
"Enhee, sasa jana nimetembea na wanaume wawili. Nilianza na dereva wa Bajaj, alikuwa na sifa nikaenda kulala naye, tulipomaliza nikiwa na furaha kwamba tayari nimenasa kwa sababu nipo siku za hatari akaniambia yeye hana uwezo wa kumpa mimba mwanamke, aliwahi kupata ajali akaharibika nini huko sijui."
"Mh! Mwingine?"

"Nilipoachana na huyo wa Bajaj nikiwa nalia, nikampata mwingine anaitwa Ibra, naye nilimwona ana sifa zilezile ulizosema, tukaenda hotelini, nikaanguka naye, tulipomaliza akasema nisimwone vile, yeye si mweusi, amevaa maski. Yaani plastiki f'lani inamfanya mtu aonekanea na sura nyingine. Kumbe ni mweupe sana, aliivua."

"Da! Pole sana mjukuu wangu. Sasa hili eneo limekushinda, labda niiulize mizimu iniambie ni jinsi gani itakubadilishia masharti, sawa?"
"Sawa babu."

Mganga alishika vibuyu viwili, akavichezesha kwa kasi kwa muda wa kama dakika tano kisha akapandisha mashetani yake. Alipokuja kutulia akasema…
"Sasa sikia, mizimu inasema tembea na mwanaume yeyote ambaye ndugu wa mume wako."
"Mh! Babu!!"

"Naam, mizimu ndiyo imesema hivyo, mbona ni masharti rahisi sana."
"Ndiyo, lakini si ndiyo hatari kubwa ya kuvunjika kwa ndoa yangu?"

Babu akiwa anajiandaa kujibu, mizimu yake ikapanda tena, safari hii ikawa mikali mpaka Paulina akataka kukimbia. Iliponyamaza, babu akamuuliza Paulina…
"Unataka mtoto?"
"Namtaka babu."
"Fuata masharti."
"Sawa babu."

Paulina aliaga na kuondoka huku akianza kuwaweka akilini ndugu wa mume wake…
"Jeijei sijui yuko wapi siku hizi?"
"Halafu Santo, yeye jana alinipigia simu sikupokea, sijui alikuwa na shida gani? Ngoja nimpigie," alisema Paulina huku akisachi namba ya Santo.
Aliiweka simu sikioni, baada ya sekunde kadhaa ikapokelewa…
"Ee, shemeji mambo?"

"Poa shem, vipi mzima wewe?"
"Mi' mzima bwana."
"Nimekumisi sana shemeji yangu, uko wapi?"
"Nipo njiani nakuja nyumbani kwako nina shida sana shemeji, jana nimekupigia simu hujapokea."
"Ni kweli shemeji, niliona simu yako lakini nikapitiwa ndiyo maana nimekupigia leo. Na mimi niko njiani naelekea nyumbani, basi tukutane kule."
"Sawa shemeji."

Paulina alimshukuru Mungu kwani alijua mwanzo hauwezi kuwa mbaya ili mradi tu akutane na shemeji yake huyo…
"Lakini sasa sijui nitaanzajeanzaje?" alijiuliza Paulina.
Waliingia nyumbani pamoja…
"Jamani shemeji langu hilo, karibu sana shemeji," Paulina alimfurahia Santo mpaka akamkumbatia na kumbusu jambo ambalo kijana huyo ambaye ni mdogo wa mumewe alilishangaa. Lakini akapata imani kwamba, ombi lake litakubaliwa maana alikuwa anataka apewe shilingi laki tatu alikuwa na shida nazo.

"Karibu ndani shemeji," alisema Paulina huku akifungua mlango.
"Asante sana shemeji."
"Karibu ukae, unakunywa nini shemeji?"
"Chochote tu. Vipi, msichana wako wa kazi yuko wapi?"
"Alikwenda kwao, mama yake mgonjwa."

"Ooo! Pole sana, uko mwenyewe sasa?"
"Ndiyo shemeji," alisema Paulina huku akimpa juisi shemeji yake, palepale akachomekea bila woga…
"Au nikunyweshe shemeji," alisema huku akimpelekea glasi kinywani…
 
JAMANI KWANI LAZIMA?! -11

ILIPOISHIA
"Ooo! Pole sana, uko mwenyewe sasa?"
"Ndiyo shemeji," alisema Paulina huku akimpa juisi shemeji yake, palepale akachomekea bila woga…
"Au nikunyweshe shemeji," alisema huku akimpelekea glasi kinywani…
ENDELEA…

Shemeji mtu huyo aliendelea kufurahia hali ile kwani alizidi kuamini kwamba mpango wake wa kuomba fedha utapita."Ninyweshe shemeji," alisema kijana huyo huku akipanua kinywa ili anyweshwe juisi na mke wa kaka yake.

Paulina alimnywesha kweli juisi kama funda mbili kisha akaweka glasi kwenye stuli na kukaa sambamba na kijana huyo kisha akamwekea mkono kwenye mabega na kumwambia…
"Shemeji Santo."
"Naam."

"Kwani wewe ni mbeya?"
"Kwa nini? Mimi si mbeya wala."
"Kweli?"

"Kweli kabisa, kwanza umbeya nitautoa wapi mimi mtoto wa kiume bwana."
"Kwa hiyo ukipewa zawadi huwezi kumwambia mtu mwingine?"
"Siwezi kusema mpaka naingia kaburini."
"Kweli?"
"Kweli kabisa."

Paulina kusikia hivyo alimvutia kwake Santo na kumlaza kwenye mapaja yake…
"Vipi tena shemeji?"
"Si umesema utatunza siri?"
"Ndiyo."

"Sasa nini tena shemeji Santo, ndiyo siri yenyewe inaanzia hapa," alisema Paulina huku akiwa anatumbukiza vidole kwenye masikio ya kijana huyo.
Santo na vile ni kijana, alianza kupata joto la mwili na kujikuta na yeye akichangia kwa sehemu kwa shemeji yake huyo.

Paulina kuona hivyo akazidisha vibweka, alisimama akamlaza Santo kwenye kochi kubwa kisha akaenda kufunga mlango huku akiamini mume wake hawezi kurejea muda ule.
Alirudi kwa Santo huku akivua nguo. Santo naye hakuwa tayari kujibalaguza, alitoka kwenye sofa na kuvua nguo zake kisha akamshika shemeji yake huyo na kumwangusha chini, sasa yeye ndiyo akawa stelingi.

Paulina alilala chini akaachia uwanja na mechi ikaanzia hapo. Kwa vile ilikuwa ni wizi, Santo hakupenda kuonesha mbwembwe nyingi na pia kwa vile ni jambo ambalo hakuwahi kulifikiria katika akili zake hata siku moja, alijikuta akitangaza nia, ndipo Paulina naye akazidi kumkamata shemeji yake huyo na kumuunga mkono kwa kutangaza nia kwake, wakatangaza wote.

Haooooo! Walifika kwenye kilele cha mlima waliokuwa wakiupanda kwa raha zao!
Kwa vile ilikuwa wizi, Paulina alimtoa Santo kwenye mwili wake na kusimama, akakimbilia kuoga. Santo alivaa na kukaa kwenye sofa…

"Shemeji kama nilivyokwambia, ni mimi na wewe tu, sawa?" Paulina alimwambia Santo baada ya kurejea kutoka bafuni.
"Siwezi kusema shemeji."
"Basi nafurahi sana kusikia hivyo, lakini utunze ahadi yetu, ukisema ujue nitaachika na ukoo wenu na wangu utaniona mimi sina akili timamu. Ngoja nikupe nauli," alisema Paulina huku akisimama kwenda chumbani.

Akiwa chumbani, Paulina alisikia sauti ikimwambia…
"Yule atasema tu halafu jamii itakushangaa sana, kwanza ni shemeji yako, pili ni mtoto kwako, ni aibu nzito, labda umpe pesa ya kutakata ili atunze siri."

"Mh!" aliguna Paulina, akakubaliana na sauti aliyoisikia.
Alichota shilingi laki tano kutoka kwenye fedha zake za biashara huku akitetemeka kwani sasa dhamira ya majuto kufanya ngono na shemeji yake ilimkaa zaidi.

"Shemeji, nauli hii. Lakini nasisitiza tena shemeji usije ukamwambia mtu mwingine yeyote, hata kama ni rafiki yako kipenzi namna gani!""Shemeji siwezi, we niamini mimi," alisema Santo huku akiwa amekinga mkono kupokea kitita hicho.

Palepale aliaga, akasindikizwa hadi nje, akaondoka zake.
Njiani Santo alimshangaa mungu wake, kwamba imekuaje amekwenda kwa shemeji yake kwa shida ya fedha lakini kabla hajaisema amepewa fedha nyingi na mapenzi juu!

"Daa! Hii ngekewa sikuwahi kuifikiria. Yaani amenipa pesa bila kumwomba halafu na penzi juu! Da! Ajabu kwelikweli. Halafu inaonekana kama alikuwa ananipenda siku nyingi, sasa leo kwa kuwa yupo mwenyewe nyumbani ameamua kuvunja ukimya," alisema moyoni Santo.
***
Paulina yeye alikaa sebuleni akiwaza na kuwazua…
"Lakini aliniambia ana shida na mimi anakuja nyumbani, sasa mbona hajasema hiyo shida yenyewe? Au alitaka nimtoea hela kidogo na kwa sababu nimempa hakuwa na haja ya kusema shida yake."

Siku hiyo mumewe aliporudi, Paulina alimpa mashamsham, mara mabusu, mara aombe denda ili jamaa ajikute akitaka mchezo…"Bwana, mi n'meshachoka. Mtu mwenyewe hushiki mimba, tunaishia starahe tuuu," alisema mumewe.

"Mwomba Mungu hachoki sweet, inawezekana siku isiyo na jina ukashangaa najaliwa kunasa."
"Mh! Mwaka gani," alihoji mumewe."Siku ikifika Mungu atanipa baby," alisema Paulina huku akizidi kumpagaisha mumewe mpaka kweli akaingia uwanjani kuanza kucheza mechi.

Lengo la Paulina lilikuwa kama atakuwa amenasa kwa Santo, basi kuwe japo na mbolea za mumewe na pia siku ikifika akawa ana mimba hata mumewe akipiga mahesabu aamini.
***
Mwezi mmoja ulikatika, Paulina hakuwa ameona ‘deizi' zake, akaanza kuhisi amenasa. Moyoni alifurahi sana kama itakuwa kweli.

Asubuhi moja ikiwa ni siku ya thelathini na tisa sasa, alimkalisha mumewe chini na kumwambia…
"Unajua sijaona kitu mwezi uliopita na zimeshapita karibu siku tisa zaidi mbele!"
"Mh! Hamna bwana, inawezekana ukawa umenasa mke wangu?"
"Sijui, labda."

"Mh! Twende hospitali wakakupime mke wangu, kama kweli mbona nitafurahi sana jamani. Sijui nitamshukuruje Mungu," alisema mwanaume huyo. Walikwenda hospitali wote huku mume akimwomba Mungu polepole moyoni.

Wakiwa wamekaa kwenye fomu kusubiri majibu, kila mmoja alikuwa na mawazo yake.
Mume mtu aliamini mkewe hana mimba ila ana matatizo tumboni ndiyo maana hakuona deizi zake lakini mke, yaani Paulina aliamini amenasa…"Paulina M…" kabla nesi hajamaliza kulitaja jina lote, Paulina na mumewe waliingia kwa daktari…
 
JAMANI KWANI LAZIMA?!-12

ILIPOISHIA
Mume mtu aliamini mkewe hana mimba ila ana matatizo tumboni ndiyo maana hakuona deizi zake lakini mke, yaani Paulina aliamini amenasa…

"Paulina M…" kabla nesi hajamaliza kulitaja jina lote, Paulina na mumewe waliingia kwa daktari…
SASA JIRUSHE MWENYEWE…
Daktari aliwakaribisha wote huku wakionesha sura tofauti, mke alikuwa akiachia tabasamu, mume aliuweka uso wake katika sura ya kupokea majibu tofauti.
"Jamani majibu yako mezani kwangu hapa, shemeji yangu unaonekana una mimba ya mwezi mmoja na wiki moja."

Paulina alianguka chini, mumewe akamfuatia, puu!
"Ala! Ni nini hii?" Aliuliza daktari lakini hakupata majibu kwani tayari watu wenyewe walikuwa hawajitambui.
Daktari alipata kibarua kigumu cha kuwaamsha wanandoa hao, walipoamka walikaa kwenye viti vyao wakiwa hoi…

"Ni nini kimewafanya mpoteze fahamu jamani?" Aliuliza dokta.
"Ni raha tu dokta," alisema mume wa Paulina huku Paulina mwenyewe akiwa anakubali kwa kutingisha kichwa tu kwamba anayosema mume wake ni ya kweli kabisa.
"Basi ndiyo hivyo jamani, mama anaonekana ni mjamzito. Kwa hiyo nawatakia kila la kheri katika kutunza mimba mpaka mtoto kuzaliwa."

"Tunashukuru sana dokta," alisema mume wa Paulina huku wakisimama.
Siku hiyo wawiili hao waliondoka hospitalini hapo kwa kushikana mkono kwa furaha. Ndoto iliyopuuzwa na mume ilionekana kutimia…

"Ama kweli Mungu ni mkubwa jamani! Loo! Leo hii kweli mke wangu umenasa! Hata siamini."
"Hata mimi mume wangu siamini, hapa namwomba Mungu anipe uzima hadi siku ya kujifungua itakapofika. Mungu ni mwema sana jamani!"

***
Maisha ya Paulina nyumbani kwake yalikuwa ya kudeka sana. Mumewe alihakikisha anapata kila kitu alichotaka ili tu aweze kumlea mtoto wake aliye tumboni…
"Baby, leo ukirudi niletee mihogo mibichi jamani, nimeimisije!"
"Usipata tabu mke wangu, nitakueletea ya kutosha."
"Nitashukuru sana halafu ukipata nafasi ingia supermarket ninunulie soseji."
"Umepata."

***
Ulikuwa mwezi wa tatu wa ujauzito, siku hiyo shemeji wa Paulina, yaani Santo alikuwa hana kitu mfukoni, aliamua kumpigia simu Paulina…
"Mimi sina kitu halafu yeye anajifanya amenikaushia, ala! Kama vipi mimi nitamwanika hadharani kwamba alinipa penzi," alisema moyoni Santo huku akiiweka simu sikioni.
Paulina alipoiona simu ya shemeji yake, moyo ulilipuka kwa wasiwasi…

"Mh! Anasemaje huyu naye jamani? Mbona kama ana lake jambo?" Alisema huku akiipokea simu hiyo…
"Shemeji mambo?"
"Poa shemeji, niambie," alijibu Paulina.
"Niko poa, ila nina shida na hela shemeji."
"Kama shilingi ngapi?"
"Kama laki moja."
"Nakurushia sasa hivi kwenye simu."
"Sawa."

Paulina alituma mtu kwenye kibanda cha simu akarushiwa yeye shilingi laki moja kisha na yeye akamrushia Santo.
Santo alifurahi sana na ikawa ndiyo kitega uchumi chake. Kila alipohisi kuishiwa mfukoni alimpigia simu Paulina na kumwambia. Siku moja Paulina akamwambia…
"Shemeji mimi sina hela sasa hivi, nina mambo mengi sana, juzi tu nimetoka kukupa pesa, leo tena unataka aaa!"

Santo alikasirika sana, akamjibu….
"Ahaaa! Umechoka kuwa na heshima siyo?"
"Heshima gani?"

"Heshima gani! Kwani hujui mimi na wewe tulifanya nini siku ile hapo nyumbani kwako?"
"Una ushahidi?"

"Kwa hiyo suala ni ushahidi siyo?"
"Ndiyo, nitasema unanisingizia. Umetumwa."
Santo akakata simu.
Kumbe siku ile ya tukio, Santo kwa kutumia kamera ya simu yake alimpiga picha shemeji yake akiwa anavaa khanga na kutoka mbio kwenda bafuni baada ya tendo hivyo baada ya kukata simu alimtafuta kwenye BBM akamtumia.

Paulina wakati huo naye alikuwa akiperuzi kwenye mtandao huo pale picha yake ilipoingia kwa kutumwa na Santo…

"Mh! Huyu si mimi, nani katuma? Ha! Huyu mwanaharamu yaani anaanza kuni…" Paulina hakumaliza maelezo yake mwenyewe, palepale alimwendea hewani Santo…
"Shem ndiyo nini hivi? Ina maana siku ile kumbe ulinipiga picha siyo?"
"Si ulisema sina usdhahidi, sasa nimetaka kukuhakishia ninao. Unasemaje?"
Paulina alikata simu, akaenda chumbani haraka na kuchukua shilingi laki moja akamtumia Santo bila kumwambia kitu chochote kingine.

"Hapo sawa, asante sana," alisema Santo kwa meseji, Paulina hakujibu kitu chochote.
Alianza kubaini ugumu wa kitendo alichokifanya cha kulala na shemeji yake huyo. Alihisi kuna mazito zaidi yanakuja mbele…

"Sijui dawa yake ni nini? Ila nikisema nimwache iko siku ataweza hata kusema mtoto ni wake. Halafu siku akimwaga mboga, kaka'ke ataamini na atajua hata mimba ni yake kwa vile sisi kama sisi tumekaa muda mrefu sijawahi kushika mimba.

"Yule dawa yake ni kumfanyia mpango wa kumtoa uhai, kama kweli naipenda ndoa yangu na kama kweli napenda mtoto wangu," alisema moyoni Paulina na kusonya msonyo mkubwa sana, akatoka kitandani na kwenda sebuleni huku akisema kwa sauti ya juu…
"Hakuna njia nyingine lazima nimuue tu."

"Umuue nani mke wangu? Mbona sikuelewi au umechanganyikiwa?" Mumewe alimuuliza wakati akiingia mlango mkubwa kutokea kazini na kukutana na maneno ya kuua ya mkewe.
 
JAMANI KWANI LAZIMA?!-13
ILIPOISHIA
"Hakuna njia nyingine lazima nimuue tu."
"Umuue nani mke wangu? Mbona sikuelewi au umechanganyikiwa?" mumewe alimuuliza wakati akiingia mlango mkubwa kutokea kazini na kukutana na maneno ya kuua ya mkewe.
JIENDELEZE KIVYAKO…

"Ah! Si hawa mende."
"Mende mende au mende watu?"
"Mende mende mume wangu."
"Wamefanyaje? Mbona wapo kila siku tu."
"Wanaongezeka kwa kasi mume wangu. Hata jana si nilikwambia kwamba siku hizi mende ni wengi ndani."

"Oke, sawa. Nitanunua dawa baadaye, pole sana mke wangu."
"Asante mume wangu," alijibu Paulina huku macho yake yakiwa yanaangaza angaza sehemu mbalimbali za sebule kwa ajili ya kujibalaguza.

***
Mimba ilizidi kuwa kubwa, sasa ilikamata mwezi wa tano, kubwa kabisa na baadhi ya watu walishangaa kwani walijua Paulina hawezi kuzaa tena kwa jinsi alivyokuwa akihangaika kusaka mimba.
Siku moja baba Riziki alikutana na Paulina akiwa anatoka kliniki…
"Nilikuwa nakutafuta sana jirani," alisema baba Riziki…
"Nipo mbona!"

"Sawa upo, lakini nataka kukwambia kutoka moyoni kwamba hiyo mimba uliyonayo ni yangu."
"He! Una uhakika gani?"
"Nina uhakika, ulinipigia simu ukasema una matatizo ya kupata mimba, nikakupa namba ya dokta, lakini anasema hukuwahi kwenda hata siku moja na ulikutana kimwili na mimi. Wakati tunakutana uliniambia ndiyo kwanza unazini nje ya ndoa, hujawahi. Kwa hiyo si mimba yangu hiyo kweli?"
"Si yako."

"Ya nani?"
"Kwani si nina mume?"
"Hata kama. Huyo mume ndiyo unasema hawezi kukupa mimba, mimi ninavyojua mimba yangu."
"Sasa baba Riziki kama mimba ni yako, unataka kusemaje?"

"Nataka utambue hivyo, mtoto akizaliwa iko siku nitamtaka mimi baba mtu."
"Utamtakaje wakati unajua wazi kwamba mimi ni mke wa mtu na wewe ni mume wa mtu?"
"Mimi mke wangu hana neno, nikimwambia umezaa na mimi wala hana shida."
Paulina alihisi wingu zito mbele ya safari yake ya ndoa na mume wake…
"Mimba si yako," alisema Paulina huku akiondoka.

"Yangu, we ngoja tu siku ifike tutajua kila kitu," baba Riziki naye alisema huku akiondoka zake.
Mbele kidogo, Paulina aligeuka kumwangalia baba Riziki, alimkasirikia kiasi cha kutamani kama angekuwa jirani yake amng'ate meno mpaka damu chapachapa.

***
Baada ya kufika nyumbani kwake, Paulina aliweka simu kwenye chaja lakini kabla hajaiachaji, meseji iliingia…

"Shemeji mi nina shida ya shilingi milioni moja, inakuaje sasa?"
Ujumbe huo ulitoka kwa mdogo wa mume wake, Santo ambaye kihalisia ndiye mwenye mimba ile.
"Mh! Ameanza huyu. Hivi hii tabu itakuwa mpaka lini? Shilingi milioni moja kwa usawa huu, itapatikana wapi?" alijiuliza Paulina huku hasira zikianza kupanda…

"Mimi sina milioni moja shemeji, nisamahe sana," alijibu.
"Kama huna ndiyo unitafutie sasa."
"Khaa! Hivi huyu Santo ana akili kweli? Yaani mimi nihangaike kumtafutia pesa yeye kweli. Haiwezekani."
Paulina hakumjibu kitu Santo. Naye Santo alipoona ukimya kwa muda mrefu akamtumia ile picha yake akiwa anavaa kanga siku walipokutana kimwili sebuleni…

"Una maana gani kunitumia picha hii shemeji? Si ulishanitumia!"
"We unajua nina maana gani!"

"Mh!" Aliguna Paulina, akakaa kwenye kochi na simu yake mkononi. Mpaka hapo, Santo alikuwa hajui kama shemeji yake ni mjamzito.

Paulina alichekecha sana, kwa kutumia akili zake timamu akabaini kwamba, uzembe wowote ule, anaweza kuharibu ndoa yake bila sababu. Alikuwa na akiba benki ya shilingi milioni kumi na mbili, akaazimia akachukue hiyo shilingi milioni moja ampe Santo.
Lakini hakutaka kumpa kwa kumrushia kwa simu, alimwambia wakutane mahali wazungumze kwanza kisha ndiyo ampe pesa hizo.

"Tukutane pale baa ya Kwazulu Natal shemeji nikupe hizo pesa," alisema Paulina.
"Pale kwenye njia ya kwenda bondeni?"
"Ndiyo."
"Saa ngapi?"

"Mi ndiyo najiandaa kwenda ATM kisha nakwenda pale."
"Sawa."
Santo alijiandaa, akatoka kwenda hotelini hapo akiwa na furaha. Aliyetangulia kufika ni yeye, akaagiza soda na kuanza kunywa.

Nusu saa mbele, shemeji yake Paulina alitokea akiwa amekunja sura hakuna mfano lakini alipomuona Santo alijifanya kuchangamsha sura ili asimjue.
"Ha! Shemeji, una kibendi?" (kibendi ni mimba).

"Kumbe ulikuwa hujui?" alisema Paulina huku akianza kujilaumu kwa kujitokeza na mimba kwa Santo maana ataweza kuhisi ni yake kwa vile anajua ameishi na kaka yake kwa muda mrefu bila mimba na anajua amekuwa akihangaikia kwa udi na uvumba kuitafuta.
"Nilikuwa sijui shemeji. Ni yangu nini?"
"Mmmh! Umeanza shemeji, ya kaka yako hii. Acha mambo yako."
"Oke, nilitaka kujua tu."

Paulina alikaa vizuri, akaanza kwa kusema…
"Shemeji tusipoteze muda sana. Lengo la kukutana nataka kukwambia kwamba, ifike mahali nichungie heshima yangu katika familia. Unajua kabisa ndugu au kaka yako akijua umelala na mimi nini kitafuatia. Sasa sijui lengo lako niachike au?"

"Siyo lengo langu shemeji, ila unajua wakati mwingine nakutisha tu ili unisaidie maana hali yangu mbaya, nina uhitaji mkubwa sana shemeji, usinione hivi."
"Kwa hiyo hali hii ya wewe kunitisha itakwenda mpaka mwaka gani?"

ITAENDELEA SAA MBILI HAPA HAPA USIKOSE
 
Back
Top Bottom