Jaji Hamid anaondoka, anajivunia lipi?

Saint Ivuga

JF-Expert Member
Aug 21, 2008
54,363
58,386
Jaji Hamid anaondoka, anajivunia lipi?

Written by Stonetown (Kiongozi) // 15/04/2011 // Makala/Tahariri // 5 Comments

jaji-mahamudi-564x272.jpg

Kalamu ya Jabir
JAJI mkuu wa Zanzibar , Hamid Mahmoud Hamid "amestaafu" baada ya kuongoza mahakama kwa miaka 22 mfululizo na huenda alikuwa "bado anataka."
Ameondoka huku mdomo wake ukibubujika kauli ambazo hazikutarajiwa kutoka kwa kiongozi wa wadhifa wake. Hata hivyo, baadhi ya anaowaacha wanasema, "mbuyu umeng'oka."
Jaji Hamid alistaafu kwa hiari Aprili 2009; pale alipofikisha umri wa miaka 60. Rais wa Zanzibar akamwongezea miaka miwili. Sasa miaka miwili imemalizika na anaondoka huku akijikusuru.
Katika hotuba yake ya mwisho kikazi, Jaji Hamid ameshutumu na kutuhumu; ametishia kushitaki Chama cha Wanasheria Zanzibar (ZLS) kwa kile alichoita "kumchafua, kumdhalilisha, kumuonea."
Hii ilikuwa mwishoni mwa mwezi uliopita (31 Machi). Alikuwa akiapisha mahakimu na mrajis wa mahakama, mjini Zanzibar .
Jaji ameacha salamu nzito kwa wanasheria hao pamoja na MwanaHALISI ambamo safu hii ilimjadili kama kiongozi yeyote yule wa umma. Ameahidi kuwashitaki mahakamani.
Chanzo cha tuhuma za jaji ni mjadala juu ya mkataba wake wa ajira mwaka 2009 na uteuzi wa majaji wapya, Novemba mwaka jana. Mjadala ulibeba maoni na hisia za watendaji mahakamani kwa jaji ambaye pia ni mwenyekiti wa Tume ya Utumishi ya Mahakama.
Kwa upande wa wanasheria, walitishia kushitaki serikali kuhusu uamuzi wake wa kutoa ajira ya mkataba wa miaka miwili kwa jaji Hamid.
Hatua hiyo ya wanasheria iliibuka pale jaji Hamid alipopendekeza kwa rais majina ya watu watano wa kuwa majaji. Walidai hakufuata taratibu na Katiba. Miongoni mwa aliopendekeza ni mtoto wake, Fatma Hamid M. Hamid.
Hamid atakuwa amejiachia mno kwa kudai kuwa anaonewa kijicho kwa sababu amesomesha watoto wake vizuri na kuwapatia kazi. Huku ni kupayuka kwani cha muhimu ni vipi mtu anapata kazi. Utaratibu umezingatiwa?
Wazanzibari wangapi wamesomesha watoto wao lakini wakapata kazi kwa mbinde? Wengi tu. Wengi wa watoto wa wakubwa wamesoma kwa kodi za wananchi, wakiwemo waliopewa nafasi za watoto wengine walioshindwa kupenya katika uzio wa kutolea fedha.
Lipo jambo jingine. Ni wangapi watoto wao wamepenya tanuri la kupata vyeo harakaharaka? Wengine hawajapenya hadi leo. Siyo vyeo tu serikalini, bali hata fursa za kujitegemea.
Ally A. Saleh, mwandishi wa habari na mwanasheria mwenye shahada ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, hajapata kibali cha uwakili kwa mwaka wa 10 sasa.
Hivi karibuni, alisikika akisema kwa unyonge, "Ah, nimejitahidi sana kujieleza na vigezo nimetimiza. Nimeamua nifanye shughuli nyingine…."
Utaratibu wa kutoa kibali unadhibitiwa na mtu mmoja tu: Jaji Mkuu. Upande wa Tanzania Bara, utaratibu huu unatekelezwa na Kamati.
Je, jaji Hamid anapofurahia mafanikio yake ya kuhakikisha mtoto wake Fatma, anasoma na kufanikiwa kuwa jaji, anajiuliza wangapi waliomtangulia bado wanasaga lami?
Je, ni wanasheria wangapi wameondoka serikalini kwa sababu ya kukorofishwa kikazi wakati yeye akiwa kiongozi wa mahakama waliyoilalamikia?
Jaji Hamid ameondoka wakati ameshuhudia kuapishwa kwa George Kazi kuwa mrajis mpya wa mahakama kuu. George ni mwanasheria kijana aliyeonyesha uwezo. Lakini amekuta wanasheria wengi wakiwemo waliopo Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, hawajafika ngazi hiyo.
Jaji Hamid anasemaje kuhusu mwanasheria kama Yesaya Kayange ambaye pamoja na kukaimu nafasi hiyo tangu tarehe 3 Januari 2005 amekwepwa na badala yake kuteuliwa mwanasheria aliyekuja baadaye.
Ni katika hafla hiyohiyo, aliapishwa Juma Silima kuwa Mwenyekiti wa Mahakama ya Ardhi na Ali Ameir kuwa naibu mrajis kwa upande wa Pemba . Hawa wote hawajawa majaji. Jaji mkuu ndiye mpendekezaji wa nani awe hakimu au jaji.
Lakini ni yeye anayelaumiwa kupendekeza jina la Rabia Hussein kuwa jaji ilhali upo ushahidi kwamba jina lake halikuwahi kujadiliwa na Tume ya Utumishi ya Mahakama ambayo yeye ni mwenyekiti.
Wapo waliosema kwamba uteuzi huu wa dakika za mwisho ulikuwa wa kufunika kombe ili mwanaharamu apite. Dunia ya leo inahitaji msemo mpya, "Funua kombe mwanahalali asimame."
Hizi ni hoja jadiliki ambazo zinamgusa jaji mkuu anayeondoka ofisini. Ni hoja zilizoibuka pale alipostaafu kwa hiari, Aprili 2009 akiwa bado na miaka mitano ya kutumika hadi umri wa kustaafu kisheria (65).
Hatua yake hii ilivuta mjadala: Nini maana ya mtumishi kustaafu kwa hiari halafu akataka ajira ya mkataba? Itakuwa kutafuta madaraka au mapato; au yote mawili?
Aidha, mkataba wake haukujadiliwa na Tume ya Utumishi, angalau mpaka taarifa zilipokuwa zinachapishwa. Ilikuwa kama hadithi ya mtu kununua soji kabla ya kujua ukubwa wa farasi atakayevalishwa.
Kifungu cha 94 cha Katiba ya Zanzibar kinashurutisha jambo hilo kufanywa kwa mashauriano na Tume ya Utumishi ya Mahakama ambayo ndiyo itataja kazi atakazopaswa kuzifanya jaji mkuu anayeajiriwa kwa mkataba, pamoja na kupanga viwango vya marupurupu yake.
Wakati ule, jaji Hamid aliulizwa swali hili na majibu yake yakawa mafupi, "Najua nimeongezewa muda tu, basi. Nimepewa mkataba wa miaka miwili. Hicho ndicho ninachokijua."
Kwa mujibu wa katiba, jaji akishastaafu, iwe kwa hiari au kwa lazima kisheria, anakuwa amekoma kuwa jaji na kwa hivyo, amepoteza kiapo cha awali cha uaminifu alichokula.
Jaji Dk. Steven Bwana, katika kitabu chake kiitwacho "Haki, Amani na Maendeleo: Nafasi na wajibu wa mahakama Tanzania ," anasema majaji wanaostaafu na kupewa mikataba si majaji kwa mujibu wa katiba.
Jambo zuri ambalo jaji Hamid angefanya siku alipoaga, ilikuwa ni kueleza anaiachaje mahakama aliyoiongoza kwa miaka 22. Hakufanya hivyo. Kilichomsukuma badala yake, kujikita katika kauli za majigambo, mashambulizi na vitisho anakijua zaidi yeye mwenyewe.
Kisiwani Pemba, hadi jaji anastaafu kwa mara ya pili, hakuna jaji mkazi. Hii maana yake ni kwamba rufaa yoyote iliyotokana na maamuzi ya mahakama za mkoa wa Pemba , hulazimika kusikilizwa Unguja au apangiwe jaji wa kuzisikiliza kutokea Unguja.
Jaji Hamid alipoingia mwaka 1989, alikuta Pemba kuna jaji Abubakar Mukri akisikiliza kesi za mahakama kuu.
Huyu alikuwa wakili na baada ya mapinduzi ya 1964 akateuliwa kuwa jaji na kupangiwa kufanya kazi mahakama kuu Pemba . Bali tangu alipofariki dunia, karibu miaka 20 sasa, hakuteuliwa mwingine.
Chini ya utawala wa jaji Hamid, wanasheria wanalalamika kukosa ripoti za maamuzi ya kesi mbalimbali, za ndani na nje ya nchi ambazo hutumika kufanyia rejea. Kihistoria, Zanzibar ilikuwa maarufu kwa ripoti hizi.
Malalamiko mengine ni ya kesi kuchukua muda mrefu kabla ya kupangiwa jaji wa kusikiliza, bali zikiwepo nyingine zilizopangiwa jaji haraka isivyo kawaida. Mpangaji ni jaji mkuu.
Ukweli ni kwamba mahakama Zanzibar inasubiri mabadiliko katika kila nyanja: miundombinu, watendaji, ujuzi, maslahi na utendaji uliotukuka wa kushawishi wananchi kuiamini.
Kwa kuwa angalau mahakama bado zipo, itakuwa vema naye akizitumia kudai haki. Aende tu
source: mzalendo.net
 
NADHANI HAPA HAKUNA MFUMO KRISTO , Na huu ni mfano bora tu unaoonyesha kuwa viongozi wengi wa Tanzania wanaweka maslahi yao mbele kwanza na watoto wao na wala sio maslahi ya dini kama wengi wao walichokuwa wanadai siku za karibuni, huu ni mfano mzuri nasa tu
 
That is simply a 'million dollar question to ask even in the case of Yussuf Makamba as he is now going home after serving CCM for awhile as the Secretary General.
 
Sioni kama kuna kosa lolote la jaji kumpendekeza mwanawe iwapo ana qualifications na experience kiwango kinachotakiwa.
she's after all a citizen like the rest, ila ikiwa kakiuka vipengele vya sheria ili kufanikisha hilo then the whole system ambayo imetoa nafasi kwa viongozi kuabuse power should be condemned rather than an individual who may very well be acting within his right. kumsimanga individual badala ya kutaka mabadiliko kwenye vipengele vya sheria may seem pretty petty and personal.
 
Sioni kama kuna kosa lolote la jaji kumpendekeza mwanawe iwapo ana qualifications na experience kiwango kinachotakiwa.
she's after all a citizen like the rest, ila ikiwa kakiuka vipengele vya sheria ili kufanikisha hilo then the whole system ambayo imetoa nafasi kwa viongozi kuabuse power should be condemned rather than an individual who may very well be acting within his right. kumsimanga individual badala ya kutaka mabadiliko kwenye vipengele vya sheria may seem pretty petty and personal.

you cant be serious dude!! huh!
 
Sioni kama kuna kosa lolote la jaji kumpendekeza mwanawe iwapo ana qualifications na experience kiwango kinachotakiwa.
she's after all a citizen like the rest, ila ikiwa kakiuka vipengele vya sheria ili kufanikisha hilo then the whole system ambayo imetoa nafasi kwa viongozi kuabuse power should be condemned rather than an individual who may very well be acting within his right. kumsimanga individual badala ya kutaka mabadiliko kwenye vipengele vya sheria may seem pretty petty and personal.

Umesoma article nzima au ume scan tu.
 
Back
Top Bottom