HOTUBA YA MHE. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWA WANANCHI KWA MWISHO WA MWEZI WA KWANZA,
31 JANUARY 2009
Ndugu Wananchi,
Naomba nianze hotuba yangu, kama ilivyo kawaida yetu, kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuweka hai na kutupa fursa hii nyingine ya kuzungumza na taifa kwa kutumia utaratibu wetu wa kila mwisho wa mwezi.
Napenda kuelezea faraja yangu kwamba tumeuanza mwaka mpya vizuri, licha ya ajali kubwa kadhaa zilizochukua maisha ya Watanzania wenzetu wengi. Tuzidi kumuomba Mwenyezi Mungu aziweke roho za ndugu zetu hawa mahali pema peponi. Amin!
Napenda kuitumia nafasi hii kurudia wito wangu nilioutoa kwenye salamu zangu za mwaka mpya wa kuwataka wenzetu wa Jeshi la Polisi kuwa wakali na makini zaidi katika kusimamia sheria na kanuni za usalama barabarani. Na, madereva nao wazingatie ipasavyo sheria na kanuni za usalama barabarani na wakati wote watambue umuhimu wa kusalimisha roho za watu wanaowabeba kwenye magari wanayoendesha.
Ndugu Wananchi,
Nimeipokea kwa faraja kauli ya Inspekta Jenerali wa Polisi, Ndugu Saidi Mwema, kuwa wanaendelea kutengeneza mikakati na mbinu bora zaidi za kukabiliana na tatizo la ajali za barabarani. Nawatakia kila la heri.
Ndugu wananchi,
Leo ninayo mambo manne ambayo ningependa kuyazungumzia: (1) Umoja wa Afrika; (2) Hali ya Mvua; (3) Upatikanaji wa Matrekta, na (4) Uwezeshaji wa wananchi.
Umoja wa Afrika
Ndugu Wananchi
Wakati nazungumza nanyi, niko mjini Addis Ababa, Ethiopia, kuhudhuria Mkutano wa Kawaida wa 12 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika. Kama mjuavyo, katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, tumepata heshima kubwa ya kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika. Kesho au keshokutwa, panapo majaaliwa, tutakabidhi uongozi kwa kiongozi mwingine wa nchi mwanachama tutakayemchagua.
Kwa niaba yenu, sina budi kuwashukuru viongozi wenzangu wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika kwa heshima hii kubwa walioipa nchi yetu kupitia kwangu. Napata faraja kubwa kuona kuwa tumetumikia vyema Umoja wa Afrika na kuna mafanikio mbalimbali yaliyopatikana katika kipindi chetu cha uongozi. Lakini, pia yapo mambo kadhaa ambayo hatukuweza kuyamalizia ambayo tunamwachia kiongozi ajaye kuyashughulikia.
Watanzania wenzangu,
Pengine jambo la faraja kubwa kwangu wakati huu ninapomaliza kipindi changu cha uongozi ni ajenda ya msingi ya kikao chetu cha safari hii. Niliamua, na kuwaomba wenzangu, na wao wakanikubalia, kuwa katika kikao hiki tuzungumzie suala zima la kuendeleza mioundombinu barani Afrika. Nilifanya hivyo kwa kutambua kuwa umoja wa mataifa ya Afrika tunaoutaka utafanikiwa na kustawi tu pale nchi zetu zitakapokuwa zimeunganishwa kwa njia za uhakika za usafiri na usafirishaji, yaani barabara, reli na usafiri wa anga na majini. Nafurahi hiyo ndiyo ajenda yetu kuu. Nina matumaini makubwa kuwa mjadala na matokeo yake yatatufikisha mahali pazuri na kuchukua hatua muafaka za kuwezesha kutimia kwa ndoto yetu hiyo.
Hali ya Mvua
Ndugu Wananchi,
Hali ya upatikanaji wa mvua nchini inazidi kutia mashaka. Taarifa za Mikoa yenye upungufu wa mvua zinaongezeka, hasa ukanda wa kati. Hii inaashiria kwamba huenda kukawa na tatizo kubwa zaidi la upungufu wa chakula katika baadhi ya Mikoa mwaka huu.
Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika wanaendelea na tathmini ya kina ya hali ya upatikanaji wa chakula nchini ilivyo sasa. Taarifa yao itatupa sura kamili ya hali ilivyo na hatua za kuchukua kukabiliana na tatizo. Naomba wananchi msiwe na hofu, tutalikabili tatizo hili kwa ukamilifu.
Upatikanaji wa Matrekta
Ndugu wananchi,
Jambo la tatu ambalo ningependa kuliongelea ni suala zima la upatikanaji wa matrekta nchini na pembejeo muhimu za kilimo.
Mtakumbuka kwamba katika hotuba yangu ya tarehe 31 Disemba 2008, ya kuuaga mwaka 2008 na kuukaribisha mwaka 2009, nilielezea dhamira ya Serikali kuelekeza nguvu zake katika kuendeleza kilimo. Nilielezea nia yetu ya kutoa msukumo maalum katika utekelezaji wa Programu ya Kuendeleza Sekta ya Kilimo nchini, maarufu kwa jina la ASDP.
Miongoni mwa mambo ambayo tumeamua kufanya kwa ajili hiyo ni kuongeza upatikanaji wa matrekta nchini. Kwa taifa kama letu linalotegemea kilimo, hatuna budi kuongeza matumizi ya matrekta na matumizi ya wanyama-kazi kulimia badala ya kuendelea kutumia jembe la mkono.
Serikali imekuwa inachukua hatua kadhaa za kuhimiza uingizaji wa matrekta nchini. Miongoni mwa hatua hizo ni kufuta ushuru wa forodha na kodi za ongezeko la thamani kwa matrekta, plau na kadhalika kutoka nje ya nchi. Pia, baadhi ya Halmashauri za Wilaya nchini zimetumia sehemu ya pesa za ASDP kununua matrekta na kuyauza kwa vikundi vya wakulima, SACCOS, na hata mkulima mmoja mmoja.
Lakini, ukweli ni kwamba kiasi cha matrekta yanayoingizwa nchini bado ni kidogo sana. Idadi hiyo haifanani na nchi ambayo kilimo ndio uti wa mgongo wa uchumi wake, na asilimia 80 ya watu wake wanaishi vijijini wakitegemea kilimo. Hali hii haikubaliki na lazima ibadilike.
Ndugu Wananchi,
Kwa nia ya kuongezea nguvu jitihada za kuongeza upatikanaji wa matrekta nchini na pembejeo muhimu za kilimo, tumeamua kuwa mwaka huu tuahirishe ununuzi wa magari ya Serikali, isipokuwa machache sana, ambayo lazima yanunuliwe. Pia tutazuia semina, warsha, makongamano na mikutano isipokuwa pale ambapo ni lazima ifanyike.
Pesa hizo zitumike, badala yake, kununulia matrekta ili kuongeza idadi ya yale yaliyonunuliwa na Halmashauri na mengineyo yanayoletwa na sekta binafsi. Kadhalika, zisaidie kununulia pembejeo muhimu za kilimo na ufugaji.Lengo letu ni kuona wakulima wetu wengi zaidi wanatumia matrekta, hivyo kutoa fursa ya kupanua ukubwa wa mashamba yao na kuongeza tija. Pia kuona mimea na mifugo yetu inahudumiwa vizuri zaidi.
Utaratibu mzima wa usambazaji na ugavi wa matreka hayo na pembejeo utatolewa baadae na Serikali wakati wake utakapofika. Lakini, tunachotaraji ni kwamba matrekta haya yatauzwa kwa vikundi vya wakulima kupitia SACCOS au vyama vyao vya ushirika. Hii ni hatua ya mwanzo tu. Kuanzia mwakani tutatenga fungu maalum katika bajeti la kununua matrekta kwa ajili ya wakulima wetu.
Ndugu Wananchi,
Wakati tunaendelea na mpango huu wa matrekta, kama nilivyosema mwanzo, tutaendelea kuongeza kasi ya utekelezaji wa mipango ya kuleta usasa katika kilimo chetu. Kwa ajili hiyo, tayari tumejiwekea mipango kadhaa, ikiwemo ya kurahisisha upatikanaji wa mbolea, mbegu bora, na madawa ya mimea na mifugo, pamoja na kuongeza huduma za ugani, kuimarisha miundombinu ya umwagiliaji maji, na kuhakikisha masoko na bei nzuri kwa mazao ya mkulima na mfugaji.
Azma yetu ni kwamba, katika kipindi cha miaka michache ijayo, tuongeze uwekezaji zaidi kwenye kilimo na tuweke msukumo wa kipekee kwa yale mambo makubwa ya kuboresha na kuleta usasa katika kilimo chetu. Tunapenda kuona kilimo chetu kinabadilika: tunajitosheleza kwa chakula na maisha ya wakulima wetu nayo yanabadilika na kuboreka. Naamini haya yanawezekana kabisa iwapo tutafanikiwa kuyafanya haya na mengine tuliyoanza kuyafanya.
Uwezeshaji wa Wananchi
Ndugu Wananchi,
Jambo la nne ninalopenda kulizungumzia leo hii linahusu mabadiliko muhimu tuliyoyafanya mwaka jana kwenye sheria zinazohusu masuala ya fedha na ardhi. Mabadiliko hayo yana lengo la kuwezesha na kurahisisha utaratibu wa wananchi kupata nyumba za kuishi, kwa upande mmoja; na, upande wa pili, kuwezesha na kurahisisha taratibu za wananchi kupata mitaji na rasilimali za kuendesha shughuli zao za kiuchumi ili wapate riziki ya kuendesha maisha yao.
Mikopo ya Ukodishaji Rasilimali (Financial Leasing)
Ndugu Wananchi;
Kwa muda mrefu sasa, Watanzania wengi wamekuwa wanashindwa kushiriki kwenye shughuli za uzalishaji mali na kutoa huduma kutokana na ukosefu wa mitaji. Mfumo wetu wa sasa wa mikopo kutoka mabenki na vyombo vingine vya fedha, ambao umekuwa ukiandamana na kumtaka mkopaji kuweka dhamana ya mali yenye thamani inayolingana na mkopo anaouomba, umekuwa kikwazo kikubwa.
Kwa sababu ya kukosa dhamana, wananchi wengi wameshindwa kupata mikopo ili kutekeleza azma yao ya kuanzisha miradi na kujiongezea kipato chao.
Ndugu Wananchi,
Kwa nia ya kupunguza ukali wa tatizo hilo serikali ya awamu ya tatu iliamua kuanzisha Mpango wa Kurasimisha Raslimali na Biashara za Wanyonge Tanzania, yaani MKURABITA. Mpango huo sasa umekamilika na umeanza kutumika kuwawezesha baadhi ya wananchi wenzetu wanaoishi kwenye maeneo yasiyopimwa kupewa hati za kumiliki mali zao, na kuzitumia hati hizo kupata mikopo kutoka kwenye mabenki na taasisi nyingine za fedha. Hata hivyo, napenda kukiri kwamba Mpango huu haujaenea katika maeneo mengi nchini hivyo watu wengi bado hawajanufaika nao. Tunaendelea kuueneza na ni dhamira yetu kuongeza kasi ya utekelezaji ili watu wengi zaidi wanufaike.
Ndugu Wananchi,
Aidha, kwa nia ile ile ya kukabiliana na tatizo la upatikanaji wa mitaji, tulianzisha mpango wa mikopo ya wajasiriamali wadogo wadogo yaani shilingi bilioni moja kwa kila Mkoa ambayo sharti la dhamana kwa mkopaji halikuwepo. Mpango huu una matatizo mawili. Kwanza, pesa zenyewe ni kidogo ukilinganisha na mahitaji. Tumeazimia kuziongeza. Tatizo la pili ni kwamba mikopo hii haikukusudiwa kuwanufaisha wajasiriamali wakubwa, wa kati na wadogo, yaani wale wanaohitaji mitaji mikubwa zaidi au wanaotaka kupata zana au mitambo ya kufanyia kazi za uzalishaji mali, ambayo ni ghali. Imekusudiwa kwa wajasiriamali wadogo-wadogo (yaani micro) na siyo wadogo (small), wala wa kati (medium) au wakubwa (large).
Ndugu Wananchi;
Kwa nia ya kuwawezesha wajasiriamali wa kati na wakubwa kupata mitaji ya kupatia rasilimali za kufanyia shughuli za uzalishaji mali na huduma, Serikali ilipeleka Bungeni muswada wa sheria ya mikopo ya ukodishaji rasilimali (Financial Leasing). Sheria hiyo ilipitishwa na Bunge mnamo mwezi April 2008 na mimi kuirasimisha Julai Mosi 2008.
Kwa mujibu wa Sheria hiyo, kama mtu anataka mkopo wa kununulia trekta au lori au mashine ya kukoboa na kusagisha nafaka au zana na mitambo ya ujenzi wa barabara, na kadhalika, anaweza kupata bila kulazimika kuweka dhamana nyumba yake au mali nyinginezo alizokuwa nazo. Atapata mkopo wa zana, mitambo au kifaa anachotaka kufanyia shughuli zake na hicho kifaa chenyewe ndicho kitakachokuwa dhamana ya mkopo huo. Iwapo atashindwa kulipa deni, aliyemkopesha atamnyanganya kile kifaa na kukiuza.
Kimsingi, ni utaratibu wa kukopa zana na vifaa vya uzalishaji mali na huduma kwa mithili ya mtu aliyekikodi. Ukimaliza kulipa deni, kifaa au zana hiyo inakuwa mali yako. Ukishindwa kulipa, zana au kifaa hicho hurudi kwa aliyekukodisha.
Ndugu wananchi,
Kiutendaji na kiutekelezaji, utaratibu huu unahusisha pande tatu, yaani muuzaji wa vifaa (supplier), taasisi ya fedha inayokopesha fedha za kununulia kifaa (lessor) na mkopaji (lessee). Mwananchi ambaye ni mkopaji huchagua zana au kifaa anachohitaji kwa ajili ya shughuli zake za uzalishaji mali au utoaji huduma.
Kisha anawasiliana na benki au taasisi ya fedha ambayo hutoa mkopo wa kununulia vifaa hivyo. Kutakuwepo na kutiliana saini mkataba wa mkopo kati ya asasi ya fedha inayokopesha na mkopaji. Baada ya hapo, mkopaji hupata vifaa na kuendelea na shughuli zake na kulipa mkopo kwa mujibu wa masharti waliyowekeana.
Zana na vifaa hivyo hubakia kuwa mali ya taasisi ya fedha iliyomkopesha mpaka pale mkopaji atakapomaliza deni lake kwa mujibu wa makubaliano. Akishindwa kulipa, zana na vifaa vyake huchukuliwa na benki au taasisi ya fedha iliyotoa mkopo. Watauza ili kufidia fedha zao walizokopesha.
Ndugu Wananchi,
Utaratibu huu unawarahisishia watu kujiendeleza kimaisha kwa gharama nafuu. Unaondoa ugumu uliopo katika kupata mikopo ya kawaida katika mabenki. Pia, Sheria hii mpya imeweka mazingira nafuu ya ulipaji wa mkopo, yaani mkopaji kulipa mkopo kulingana na mtiririko wa mapato yake (cashflow), huku akiendelea kuitumia rasilimali aliyokopa katika uzalishaji.
Ndugu wananchi,
Utaratibu huu si mgeni duniani na hata hapa nchini. Katika nchi zilizoendelea, inakadiriwa kuwa, 1/8 (moja ya nane) ya uwekezaji binafsi unagharamiwa kwa mikopo ya utaratibu huu. Kwa mfano, katika mwaka 2005, dola za Kimarekani 582 bilioni zilitumika kwa ajili hiyo. Hapa kwetu, utaratibu huo haujaenea, na pale kidogo unapotumika, haulindwi na sheria. Sheria hii sasa inaondoa kasoro hiyo.
Natambua kwamba tayari zipo baadhi ya taasisi chache ambazo zimekuwa zinatumia utaratibu huu, lakini, kama nilivyosema, isivyo rasmi na bila kulindwa na sheria. Kwa mfano, nimetaarifiwa na Benki Kuu kwamba shirika lisilo la kiserikali la SEROLEASE limekuwa likiwawezesha wanawake kupata nyenzo za kufanyia kazi kama vile majiko ya kuokea mikate, vyerehani vya kushonea, matrekta madogo, mashine za kusagisha nafaka, pikipiki, boti za uvuvi, na kadhalika. Wenyewe hubakia na kazi ya kupata mitaji yao midogo kufanyia biashara (working capital).
Ndugu Wananchi,
Nimeambiwa kuwa Mpango wa SEROLEASE umepata mafanikio mazuri. Vifaa vyenye thamani ya jumla ya shilingi bilioni 9 vimekopeshwa na ajira 20,000 zimepatikana kutokana na miradi iliyoanzishwa. Mafanikio hayo yametokana na wakopaji kuwa na nidhamu ya kurejesha mikopo yao.
Mimi naamini, kwa kutumia kigezo cha mafanikio iliyopata Shirika la SEROLEASE, taasisi nyingi za fedha, ndogo na kubwa, yakiwemo mabenki, zitashawishika kujihusisha na utaratibu huu. Hata hivyo, mafanikio ya mpango huu yatategemea jinsi Watanzania wenzetu, yaani wajasiriamali, watakavyokuwa waaminifu na kurejesha mikopo yao. Wakifanya hivyo, tutakuwa tumefanikiwa. Wasipofanya hivyo, tutakuwa tumeharibikiwa. Na, watakuwa wameniangusha kweli kweli. Juhudi zangu zote zitakuwa zimepotea bure.
Ndugu zangu,
Tunafanya yote haya kwa ajili yenu. Tunahangaika huku na kule, usiku na mchana, kutengeneza mazingira mazuri ya kuwawezesha wananchi wa Tanzania kujiendeleza kiuchumi, waongeze kipato chao ili wainue hali zao za maisha. Naona tusikubali nguvu zetu zipotee bila ya kuzaa matunda tunayoyatajia sote. Sitegemei kuwa itakuwa hivyo.
Ndugu Wananchi,
Maisha bora kwa kila Mtanzania hayatadondoka kama mvua, bali yatapatikana kwa kila mmoja wetu kufanya kazi kwa bidii na maarifa. Wajibu wa Serikali ni kutengeneza mazingira yatakayowasaidia watu wanaojituma kupata mafanikio na mapato yanayolingana na jasho lao. Ilani ya Uchaguzi ya CCM inaiagiza Serikali kuhakikisha kuwa wananchi walio wengi wanashirikishwa katika shughuli za uzalishaji mali na hivyo kuboresha hali zao za maisha. Hatua zote zinazochukuliwa na Serikali, pamoja na hii, zina lengo la kutimiza wajibu huo. Nawaomba Watanzania wenzangu na nyie mtimize wajibu wenu.
Ndugu Wananchi,
Kwa ujumla, kutungwa kwa sheria hii ya mikopo ya ukodishaji wa rasilimali (financial leasing) kutaleta manufaa makubwa kwa wajasiriamali wa Tanzania. Naomba tuitumie ipasavyo fursa hii kwa maslahi yetu.
Mabadiliko ya Mfumo na Utaratibu wa Umiliki wa Nyumba
Ndugu Wananchi;
Jambo la mwisho ambalo ningependa kulizungumzia leo linahusu mabadiliko katika mfumo na utaratibu wa upatikanaji wa mikopo na miliki ya majengo na nyumba.
Mikopo kwa ajili ya Ujenzi/Ununuzi wa Nyumba
Ndugu Wananchi;
Suala la wananchi wa Tanzania kupata nyumba bora za kuishi mijini na vijijini ni jambo tulilolipa umuhimu mkubwa Serikalini. Limesisitizwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama chetu na nililizungumzia kwenye hotuba yangu ya kuzindua Bunge letu tukufu tarehe 30 Disemba 2005.
Kwa muda mrefu, maendeleo ya makazi nchini yamekuwa yanarudishwa nyuma na kutokuwepo mfumo wa mikopo ya ujenzi au ununuzi wa nyumba na majengo. Kwa ajili hiyo, mtu analazimika kujenga au kununua nyumba kwa kutumia fedha yake mwenyewe. Uwezo wetu tunaujua wenyewe, hivyo kusababisha ujenzi kuchukua muda mrefu. Pia huwafanya baadhi ya watu wasiokuwa waaminifu kutumia njia zisizokuwa halali kujipatia hitaji hili muhimu kwa maisha ya mwanadamu.
Ndugu Wananchi,
Tuliahidi kulitafutia ufumbuzi tatizo hili la kutokuwepo utaratibu wa mikopo ya kujenga au kununua nyumba. Katika kutimiza ahadi hiyo, mwaka wa jana, 2008, tumetunga Sheria ya Upatikanaji wa Mikopo kwa ajili ya Uendelezaji Nyumba [The Mortgage Finance (Special Provisions) Act, 2008].
Sheria hii inaboresha mazingira ya upatikanaji mikopo kwa ajili ya ununuzi au ujenzi wa nyumba. Hivyo basi itasaidia wananchi kuweza kukopa kutoka kwenye mabenki na taasisi za fedha zinazotoa mikopo ya nyumba na kupata makazi bora ya kuishi. Manufaa mengine ya sheria hiyo ni kuongezeka kwa uwekezaji katika sekta za Fedha na Ujenzi, fursa za ajira nchini, na kukua kwa uchumi wa Taifa kwa jumla. Hivyo hivyo, mapato ya serikali yataongezeka kutokana na kukua kwa sekta ya Ujenzi.
Umiliki wa Sehemu za Majengo (Unit Titles)
Ndugu Wananchi,
Sheria nyingine tuliyoipitisha Bungeni mwaka jana, itakayosaidia Watanzania kumiliki nyumba, ni ile ya Unit Titles Act, 2008. Kwa mujibu wa sheria hiyo, watu wanaoishi au wenye ofisi katika jengo la ghorofa lenye fleti au ofisi kadhaa wanaweza kununua na kupata hati za kumiliki fleti wanazoishi ama ofisi wanamofanyia kazi.
Hivi sasa, jambo hilo haliwezekani kwa vile hati ya kiwanja ni moja tu, yaani ya yule mwenye ghorofa. Kwa mujibu wa sheria hii mpya, sasa unaweza kununua na kupewa hati ya kumiliki fleti uliyonunua. Tena hati hiyo unaweza kuitumia kama dhamana kukopea katika mabenki. Aidha unaweza kuuza fleti yako kwa mtu yeyote, na hati ikabadilishwa mmiliki na kuwa ya yule mnunuzi mpya.
Ndugu Wananchi,
Kuwepo kwa ile sheria ya mikopo ya uendelezaji wa majengo kutatoa fursa kwa watu kupata mikopo ya kununua fleti katika maghorofa wanayoishi sasa au hata mengine yatakayojengwa. Aidha Sheria hizi mbili, zitasaidia kuchochea ujenzi wa majengo ya ghorofa kwa ajili ya kuuza fleti zilizomo. Kwa kufanya hivyo, sheria hizi zitasaidia Watanzania kupata makazi bora ya kuishi. Nawaomba Watanzania tuzitumie fursa zitakazotolewa na sheria hizi mbili kuinua hali zetu za maisha.
Kutengeneza Kanuni
Ndugu Wananchi,
Kwa mujibu wa sheria za nchi yetu, ili Sheria hizi tatu, yaani Sheria ya Mikopo ya Ukodishaji Rasilimali (Financial Leasing Act, 200, Sheria ya Umiliki wa Sehemu za Majengo (Unit Titles Act, 200 na Sheria ya Mikopo ya Uendelezaji wa Nyumba [The Mortgage Finance (Special Provisions) Act, 2008] ziweze kutumika, ni lazima zitengenezwe Kanuni (Regulations) zitakazofafanua jinsi Sheria hizi zitakavyotumika, kifungu kwa kifungu. Kanuni hizo hutengenezwa na Wizara husika na kutolewa kwa amri ya Waziri anayehusika. Kwa kawaida, amri hiyo hutangazwa katika Gazeti la Serikali.
Kazi ya utengenezaji wa kanuni za Sheria hizi tatu imekuwa inaendelea. Naambiwa inakaribia kukamilika. Nimewasisitiza Mawaziri wahusika na masuala ya ardhi na fedha kuongeza kasi ya kukamilisha kanuni hizo ili watu waanze kunufaika nazo. Hakika tuko nyuma sana ya wakati.
Kadhalika nimewataka waanze kazi ya kuelimisha umma kuhusu sheria hizo ili wananchi wazielewe na kuzitumia kuinua hali yao ya maisha. Wakati huo huo, nimemtaka Waziri wa Fedha na Uchumi ashirikiane na Gavana wa Benki Kuu kuyatayarisha mabenki na asasi za fedha nchini kuanza kujiandaa kutoa mikopo. Nisingependa kuona tunachelewa baada ya Kanuni kutoka.
Hitimisho
Ndugu Wananchi,
Leo nimeongelea jitihada za Serikali kutengeneza fursa kwa wananchi kujiendeleza kiuchumi. Mwishowe ni jukumu la wananchi kuzitumia fursa hizi. Tujiandae na kujipanga kutumia fursa zitakazotokana na mabadiliko haya. Tutaendelea kuelimishana na kuelekezana namna ya kuzitumia fursa hizi. Napenda kuwahakikishia kwamba Serikali itaendelea kuhangaika kwa ajili yenu kubuni mbinu na mikakati ya kuhakikisha kuwa tunajenga uchumi wa kisasa ambao unawashirikisha wananchi walio wengi, kama ambavyo Ilani ya Uchaguzi ya CCM inavyotuelekeza.
Mwisho kabisa, naomba niwashukuru tena kwa kuendelea kuiunga mkono Serikali katika jitihada zake za kuwaletea maendeleo. Nawaomba tuendelee kushirikiana na kusaidiana. Aidha, tuendelee kuipenda na kuitumikia nchi yetu kwa moyo wetu wote.
Mungu Ibariki Afrika
Mungu Ibariki Tanzania
Asanteni kwa kunisikiliza!