JK, kama huwezi kuyazungumza mambo ambayo Watanzania wengi wanataka uyazungumze ni bora kuachana na hizo blah blah zako za kila mwisho wa mwezi zisizo na kichwa wala miguu.
Baada ya kimya kirefu, Rais asema…
Ba Mdogo
Tanzania Daima~Sauti ya Watu
NIMESHANGAZWA na utetezi alioutoa Rais Jakaya Kikwete kwamba alishindwa kuzungumza (au kuwaambia) wananchi wake kwa muda wa miezi mitatu kutokana na kubanwa na muda.
Mwenyewe amesema katika hotuba yake ya mwisho wa mwezi uliopita kuwa alishindwa kuzungumza na wananchi kwa sababu kila ilipofika mwisho wa mwezi, wakati alip[opaswa kutoa hotuba hizo, alikuwa nje ya nchi.
Lakini huko nyuma, tulishazoeshwa na mtangulizi wake, ambaye ndiye aliyeasisi mpango wa kuzungumza na wananchi kila mwisho wa mwezi, anapojiona kuwa hatokuwapo nchini, alirekodi hotuba yake na kuiacha ili itangazwe siku muafaka.
Rais Kikwete anasema ameshindwa kufanya hivyo kwa sababu amepata maoni kutoka kwa baadhi ya watu kuwa hawaufurahii utaratibu huo.
Hawaufurahii kwa sababu wanamuona leo akizungumza nao, lakini wakati huo huo wanamsikia akizungumza akiwa nje ya nchi katika shughuli nyingine.
Hili linaleta maana yoyote? Najiuliza hivi kwa sababu katika hayo mazungumzo yake, sidhani kama watu wanamuangalia yeye zaidi ya ujumbe anaoutoa.
Kama imebainika kuwa watu wanavutwa zaidi na mzungumzaji kuliko ujumbe wake, hiyo ni dalili ya wazi kuwa hakuna ujumbe wa nguvu unaotolewa na hicho kinachozungumzwa na mzungumzaji.
Je, tuliishiwa na habari muhimu kiasi hicho katika kipindi hiki chote? Aliyoyazungumza Rais ni muhimu, lakini hivi umuhimu wake unalingana na aliyoacha/kukwepa kuyazungumza?
Nilitarajia kuwa baada ya kimya cha muda mrefu, Rais angeibuka na mambo ambayo kwa hakika yamelitikisa taifa kama yeye mwenye alivyoeleza kwenye hotuba yake. Inashangaza kwamba wakati anajua kuwa kuna mambo yaliyolitikisa taifa, anaamua kuzungumza mambo mengine ambayo umuhimu wake hauwezi kulinganishwa na kutikisika kwa taifa.
Lakini labda ninaweza kuwa ninalaumu kitu nisichokifahamu kwa undani kwa sababu inawezekana kwa vipimo vyake, aliyoyazungumza ndiyo ambayo Rais anayoyaona kuwa mambo mazito kwa taifa kwa kipindi chote ambacho alikaa bila kuzungumza na wananchi.
Kama ndivyo, mimi naomba nitofautiane naye. Hii ni kwa sababu mengi ya aliyoyasema, yanayohusisha zaidi ziara zake nje ya nchi (ambayo ndiyo sababu iliyomfanya ashindwe kuzungumza na wananchi wake), yaliripotiwa kwa mapana na vyombo vya habari. Nakumbuka katika baadhi ya ziara hizi, ujumbe wa Rais ulihusisha pia waandishi wa habari.
Pia, huko alikokwenda, kutokana na wadhifa wake kama Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU), alivutia waandishi wa habari wa kimataifa na ambao walisaidia kupeperusha ujumbe wa kilichojiri kila alipo.
Mengi ya mambo hayo, hayakuwa na utata wowote, hasa yanapohusishwa na Tanzania na mustakabali wa wananchi wa Tanzania kulingana na matatizo yanayowakabili hivi sasa.
Kwa upande mwingine, yapo masuala kadhaa hapa nyumbani, ambayo yana utata na yanahitaji ufafanuzi wa kina na wengi waliposikia kuwa Rais hatimaye amepata nafasi ya kuzungumza na wananchi wake, atatoa ufafanuzi kuhusiana na masuala hayo.
Kuna suala zima la mgogoro wa kisiasa Zanzibar. Hadi dakika za mwisho, hatua iliyokuwa imefikiwa kwenye mazungumzo hayo, ilionyesha kuwa yamekwama na ilielekea kuwa mtu mwenye nafasi kubwa ya kuyakwamua ni yeye, ambaye ndiye aliyeyaanzisha. Lakini kwake hili halikuonekana kuwa muhimu.
Kuna suala la uchunguzi wa wizi wa mabilioni ya fedha za umma kupitia akaunti ya malipo ya madeni ya nje (EPA) ya Benki Kuu (BoT). Nalo hakuliona kuwa lina umuhimu wa kuzungumzwa? Miezi sita aliyopitoa kwa timu ya kuchunguza wizi huo imeshapita.
Kwa kuwa wanaofanya uchunguzi huo wanaonekana kuamua kutowaeleza wenye fedha wamefikia wapi katika uchunguzi wao, ilikuwa vema kwa mtumishi huyu wa Watanzania awaeleze mabosi wake kuhusiana na hilo.
Alipotoa hadidu za rejea kwa timu hiyo, alisisitiza kuwa kurejeshwa kwa fedha ni suala muhimu na lipewe kipaumbele. Tuliambiwa kuwa takriban sh bilini 60 zimerudi lakini BoT wanasema fedha hizo hazijapelekwa kwao. Hakuna taarifa zozote fedha hizi zimekwenda wapi. Au zimewekwa kwenye akaunti ya mtu binafsi? (Tulishaambiwa kuwa si fedha za serikali.).
Kuna suala zima la kupanda kwa gharama za maisha kunakotokana na kupanda kwa bei za mafuta na nafaka duniani. Tanzania imeathirika kama zilivyoathirika nchi nyingine. Si ajabu iwapo suala la kupanda kwa bei za bidhaa hizi, likaathiri bajeti zinazoendelea kupitishwa.
Kwa nini Rais hakuona umuhimu wa kulizungumzia hili? Au hana cha kuzungumza kuhusu hilo? Tunaamini kuwa kama nchi tunapaswa kuwa na mikakati yetu ya kukabiliana na hali hiyo. Hatuwezi kuwaambia wananchi waongeze uzalishaji tu ikawa ndio dawa ya tatizo hilo.
Hata wananchi wakilima na kuongeza uzalishaji, serikali nayo inafanya nini kukabiliana na hali hiyo? Ina mchango gani katika harakati za wakulima kuongeza uzalishaji?
Rais alishapokea ripoti ya tume aliyoituma kuchunguza mikataba ya sheria za madini. Nilitarajia kuwa huu ulikuwa wakati muafaka wa kutoa ufafanuzi kuhusu kilichoelezwa kwenye ripoti hiyo na kueleza serikali imeyachukuliaje mapndekezo yaliyotolewa.
Hata kama kazi hiyo haijakamilika, ingetosha tu kubainisha msimamo wa jumla wa serikali kuhusiana na ripoti hiyo. Je, imekidhi haja? Ina msaada wowote wa kuikomboa nchi kutoka kwenye matatizo ambayo yalisababisha timu hiyo iundwe? Lakini hatujaambiwa hayo.
Rais amekiri katika hotuba yake kuwa kumetokea mambo ambayo yameitikisa nchi. Lakini hayo aliyoyazungumza ndiyo yaliyoitikisa nchi kweli?
Kwa upande mwingine, hivi ni lazima aongee kila mwisho wa mwezi? Katika utaratibu wa kukabiliana na matatizo, mikakati inatakiwa kulikabili tatizo pale linapojitokeza.
Ni vema kuwa amejiwekea utaratibu wa kuzungumza kila mwisho wa mwezi. Lakini ingekuwa vema akafahamu kuwa utaratibu huu si msahafu kwamba hauwezi kubadilika. Ingekuwa vema na msaada mkubwa kwa Watanzania kila linapotolea jambo kubwa, rais akachukua muda kuzungumza na wananchi wake.
Ingekuwa busara kila linapotokea jambo linalolitikisa taifa, Mkuu wa Nchi akajipa muda kuzungumza na watu wake. Haisadii kuliacha taifa linatikisika, lipo kwenye majonzi, halafu mkuu wa nchi anakwenda nje.
Kwa kuwa utaratibu wa kuzungumza na wananchi umewekwa naye, ni dhahiri kuwa anaweza kuubadilisha. Na mimi napendekeza aubadilishe ili kumwezesha kuzungumza na wananchi wakati wowote inapolazimu kufanya hivyo.
Anaweza kuendelea na utaratibu wa kuzungumza na wananchi kila mwisho wa mwezi. Lakini pale anapoona kuwa kuna jambo muhimu la kulizungumza, na ratiba zake zinambana kiasi kwamba hatopata muda mwishoni mwa mwezi kuzungumzia hilo, ni vema akatafuta wakati mwingine wowote kuzungumza na wananchi kuhusu jambo hilo, si lazima iwe mwisho wa mwezi.
Ikumbukwe kuwa mawasiliano ni moja na nyenzo muhimu ya maendeleo. Kusikokuwa na mawasiliano inakuwa vigumu sana kuwaunganisha watu katika jambo lolote linalofanyika. Iwapo Rais atakatiza mawasiliano na wananchi wake kama hivi, asishangae wananchi watakapomuona kuwa amebadilika.
Hata kwa utaratibu wa kurekodi hotuba zake, iwapo jambo litakalokuwa linazungumza ni la muhimu, hao wanaolaumu kuwa hawapendi kumsikia katika hotuba za kurekodiwa, watafuta usemi wao.
Wananchi hivi sasa wanalazimika kuishi katika dunia ya uvumi. Kuna uvumi mwingi kuhusiana na mambo makubwa yanayolikabili taifa na ndhani haya ndiyo yanayosababisha mtikisiko ambao hata rais ameuona.
Ukweli huondoa uvumi. Ni wakati sasa rais akajenga mazoea ya kutoa ufafanuzi wa masuala haya kabla uvumi haujaanza kusambaa.
Kuna haja gani ya kuendelea kuficha mambo ambayo nusu yake yanajulikana na wananchi hata wa kawaida? Kwa kuwa hakuna anayejitokeza kusema ukweli ulivyo, wananchi wanaanza kutunga yao ili kujazia maswali ambayo hayana majibu katika taarifa wanazozipata.
Katika mazingira kama haya, mchawi ni yule anayeficha taarifa.