Ndugu Zangu,
NIMEMSIKILIZA Rais wetu akilihutubia taifa jana jioni. Hii ni tafsiri yangu ya alichokiongea.
Kwanza kabisa nataka niseme, kuwa hotuba ile ya Rais Kikwete ni ya kihistoria. Ni moja ya hotuba muhimu sana katika historia ya nchi yetu tangu tupate uhuru. Maana, jambo lile la nne na la mwisho lililozungumzwa na Rais wa Awamu ya Nne kwenye hotuba yake, ndilo jambo lililofungua ukurasa mpya wa taifa letu baada ya miaka 50 ya uhuru. Rais
Jakaya Kikwete ameongea jambo kubwa sana usiku wa jana. Hakika, Kikwete hatabiriki na ni mtu wa rekodi. Jana ameweka rekodi nyingine.
Gwiji wa fasihi ya Kiswahili katika Tanzania na Afrika Mashariki, marehemu Shaaban Bin Robert alipata kuandika kitabu chenye kuhusu maisha yake; "Maisha Yangu Na Baada Ya Miaka 50".
Kwa hotuba ile ya Kikwete iliyobeba vision ya Kikwete kwa Tanzania kwa miaka 50 ijayo, inaweza kabisa kumweka JK katika nafasi ya kuanza kuandika kitabu juu ya kumbukumbu za maisha yake. Jinsi yeye, kama Jakaya Kikwete alivyoiona miaka yake 50 ya alikotoka na anavyoiona miaka 50 ijayo, si kwake tu, bali kwa nchi kubwa aliyojaaliwa kupata bahati ya kuiongoza. Nchi ya Tanzania.
Maana, JK kama binadamu, kuna mazuri na mabaya aliyoyafanya katika utendaji wake wa kazi maishani mwake. Na katika hili la Uona Mbali juu ya Katiba yetu, basi, kama JK atafanikiwa kuongoza juhudi hizi za Watanzania kupata Katiba iliyofanyiwa marekebisho makubwa, sina shaka yeyote, kuwa ataacha legacy kwa maana ya haiba. Katiba Mpya itakuwa moja ya jambo kubwa atakalokumbukwa nalo.
Ndio, JK atakumbukwa kama Rais aliyeongoza mabadiliko makubwa na ya kihistoria yaliyopata kufanyika katika nchi yetu. Kukumbukwa kwa kuchangia kuifanya nchi yetu kuwa mahali pema pa kuishi; kuwa nchi ya kisasa zaidi kuliko ilivyo sasa. Hofu yangu, ni kama JK ataweza kuachwa kuifanya kazi hii bila kukwamishwa na nguvu hasi za wahafidhina ndani ya chama chake, CCM.
Kwa anachotaka kufanya JK yaweza kabisa ikawa mchango wake katika kukinusuru chama chake, CCM. Kwamba CCM, kama chama, kisije kikapotea kabisa kwenye ramani ya kisiasa. Kwamba hata CCM ikija kushindwa, ibaki kuwa Chama cha Upinzani chenye nguvu na kinachoweza kurudi tena madarakani.
Maana, huko twendako, upo, uwezekano wa CCM kushindwa uchaguzi. Kwa Katiba ya sasa, siku CCM ikishindwa uchaguzi, itakuwa na maana ya chama hicho kuporomoka kama nyumba ya karata. Si hata Mzee Makamba mwenyewe alipata kutamka hadharani, kuwa Mtaji wa CCM ni Kikwete!
Na juzi hapa Mzee Makamba akatamka; kuwa hana maoni juu ya Katiba, anamsubiri JK atoe tamko. Hicho pia ni kielelezo cha mapungufu ya Katiba yetu. Na tushukuru nchi yetu haijapata bahati mbaya ya kuwa na 'mwendawazimu' pale Ikulu ya Magogoni.
Na wenye kutanguliza ubinafsi wao ndani ya CCM hawauoni ukweli, kuwa si miaka mingi kutoka sasa, Chama Cha Mapinduzi kitakuwa chama cha upinzani. Hawautambui ukweli, kuwa himaya zote duniani hujengwa na kuporomoka. Hakuna himaya iliyodumu daima. Hata Roma iliporomoka. Kwa vijana wa sasa, salamu ya " CCM Daima!" ni kielelezo cha watu waliopitwa na wakati.
Na kumsaidia JK katika kutupitisha kwenye njia hii salama tunayoitaka sasa ni kwa Watanzania kutambua ukweli, kuwa demokrasia yetu bado changa. Tumefanya chaguzi zenye walakini mwingi, ni sehemu ya kujifunza. Na sasa tuna fursa ya kuandaa Katiba itakayotufanya tujenge misingi imara ya demokrasia yetu.
Kumsaidia JK ni kukubali ukweli kuwa Uchaguzi uliopita umeshapita. Kwamba Serikali iliyo madarakani kwa sasa ndio hiyo inayoongozwa na JK kama Rais. Hatuna Rais mwingine. Hatuna Serikali nyingine. Rais tuliye naye sasa ni Jakaya Mrisho Kikwete.
Na tuukubali ukweli pia, kuwa wakati umebadilika na kuwa wananchi wanaukubali upinzani. Na kwamba kwa sasa CHADEMA ndio chama kikuu cha upinzani kikifuatiwa na CUF. CCM, CHADEMA , CUF na wengine wana lazima ya kushirikiana katika mambo ya msingi na yenye maslahi kwa taifa letu.
Ndio, tumeumaliza mwaka jana na mjadala wa Katiba mpya. Tunaingia mwaka 2011 na mjadala wa Katiba Mpya. Hili ni jambo jema. Na lililo muhimu kabisa katika mjadala wowote uwao ni kujiuliza; nini shabaha na malengo yetu? Nionavyo, shabaha na leo letu liwe kudumisha Umoja wetu wa Kitaifa, amani na utulivu tulio nao.
Kama swali ni je, Katiba yetu ya sasa, na kwa wakati uliopo, inakidhi matakwa ya shabaha na malengo yetu kama taifa? Jibu langu ni HAPANA. Na ndio maana nimekuwa na nitaendelea kuunga mkono juhudi za kufanya marekebisho makubwa ya Katiba yetu.
Na katika hili hatuna sababu za kugombania fito ilihali nyumba tunayojenga ni moja na ni yetu sote.
Ieleweke, kuwa madai ya Watanzania kupata Katiba mpya ni madai muhimu na ya kihistoria. Tumewasikia hata wanaojidanganya, wakiandika, kuwa madai haya yanatokana na ' Njama za mabeberu!'. Hizi ni propaganda za miaka ya 70, zimepitwa na wakati.
Ni busara kutambua, kuwa wakati umebadilika. Mtanzania wa mwaka 1977 si Mtanzania wa mwaka 2010. Hoja hii ya Katiba si kama nzi anayetua na kuruka. Hoja ya Katiba kwa sasa inaongozwa na kundi kubwa la vijana wanaotaka mabadiliko. Hawa si nzi wanaotua na kuruka, ni siafu wanaokuja kwa kuongezeka idadi yao.
Na madai ya marekebisho ya Katiba si madai mapya. Si madai ya chama au kikundi kidogo cha 'wapinzani' wasioitakia mema nchi hii. Ni madai ya msingi ya Watanzania, bila kujali tofauti zao za kiitikadi, kidini, rangi na makabila.
Kama ni shauri mahakamani, basi, lilishafunguliwa. Kinachofanyika sasa ni mwendelezo wa shauri. Ndio, tunapongia mwaka 2011, madai ya Katiba mpya yatatimiza miaka 20. Yalianza tangu mwaka 1991.
Ndio, si wengi, miongoni mwa vijana wa sasa, wenye kumbukumbu ya ukweli huu. Tayari mwaka 1991 vuguvugu la kudai vyama vingi na Katiba mpya lilishaanza. Wakati huo madai makubwa yalikuwa mawili; vyama vingi na Marekebisho ya Katiba. Kuna mnaokumbuka ' KAMAKA'- Kamati ya Marekebisho ya katiba iliyondwa na wanaharakati. Hayo yalikuwa ni madai ya Watanzania ndani ya mfumo wa chama kimoja.
Marehemu Chifu Abdalah Fundikira aliongoza Kamati iliyoundwa, si na Serikali, bali wanaharakati, kuratibu mchakato wa kudai vyama vingi na Katiba mpya.
Hata wakati huo Mzee Mwinyi, kama Rais, aliweka ' mkwara', kuwa madai hayo yasiendeshwe na watu au makundi ya watu bila kibali cha Serikali. Presha ya madai ilipoongezeka, tunakumbuka, kuwa Mzee Mwinyi aliweza kusoma alama za nyakati. Aliongea pale Chuo Kikuu Mlimani na kuweka bayana dhamira ya Serikali ya kuunda ' Tume ya Nyalali' . Tume hiyo ilizunguka nchi nzima kuwauliza Watanzania kama wanataka kuendelea na Chama kimoja au Vyama vingi.
Itakumbukwa, Chifu Fundikira alipata kutamka; kuwa huko ni kupoteza muda na fedha za wananchi. Itakumbukwa pia, Mabere Marando alikuwa Katibu wa Kamati ile ya wanaharakati ya kuratibu mchakato wa madai ya kuwepo na vyama vingi na marekebisho ya Katiba. Marando alipata kutamka na kunukuliwa na Daily News, April, 12, 1991; " We have a bad political system because our Constitution embraces political discrimination. What we want is that all of us should shout out that our Constitution is bad." ( Mabere Marando, Daily News, April 12, 1991)
Ndio, Marando aliyasema hayo katika Semina ya kwanza ya Kamati ya kuratibu mchakato wa madai ya vyama vingi na Katiba mpya iliyoongozwa na Chifu Fundikira. Semina hiyo iliudhuriwa na watu wapatao 800 kwa mujibu wa taarifa ya Daily News la April 12, 1991.
Na akina Chifu Fundikira waliandamwa sana. Kwa mujibu wa Daily News la April 26, 1991, Mbunge wa Shinyanga, Ndugu Paulo Makolo alimshambulia Fundikira kwa kusema kuwa , katika hilo la kuwa na vyama vingi na katiba mpya , Chifu Fundikira hawasilishi mawazo ya Wasukuma na Wanyamwezi wenzake; " This is not a Wanyamwezi and Wasukuma movement. It is the selfish interests of Fundikira and his ten colleagues. Our people are not after parties. They want food, water, education and health care." ( Paulo Makolo, MP, Shinyanga, Daily News, April 26, 1991). Mwenyezi Mungu umrehemu Chifu Abdalah Fundikira.
Maggid
Iringa,
Januari Mosi, 2011
http://mjengwa.blogspot.com
NIMEMSIKILIZA Rais wetu akilihutubia taifa jana jioni. Hii ni tafsiri yangu ya alichokiongea.
Kwanza kabisa nataka niseme, kuwa hotuba ile ya Rais Kikwete ni ya kihistoria. Ni moja ya hotuba muhimu sana katika historia ya nchi yetu tangu tupate uhuru. Maana, jambo lile la nne na la mwisho lililozungumzwa na Rais wa Awamu ya Nne kwenye hotuba yake, ndilo jambo lililofungua ukurasa mpya wa taifa letu baada ya miaka 50 ya uhuru. Rais
Jakaya Kikwete ameongea jambo kubwa sana usiku wa jana. Hakika, Kikwete hatabiriki na ni mtu wa rekodi. Jana ameweka rekodi nyingine.
Gwiji wa fasihi ya Kiswahili katika Tanzania na Afrika Mashariki, marehemu Shaaban Bin Robert alipata kuandika kitabu chenye kuhusu maisha yake; "Maisha Yangu Na Baada Ya Miaka 50".
Kwa hotuba ile ya Kikwete iliyobeba vision ya Kikwete kwa Tanzania kwa miaka 50 ijayo, inaweza kabisa kumweka JK katika nafasi ya kuanza kuandika kitabu juu ya kumbukumbu za maisha yake. Jinsi yeye, kama Jakaya Kikwete alivyoiona miaka yake 50 ya alikotoka na anavyoiona miaka 50 ijayo, si kwake tu, bali kwa nchi kubwa aliyojaaliwa kupata bahati ya kuiongoza. Nchi ya Tanzania.
Maana, JK kama binadamu, kuna mazuri na mabaya aliyoyafanya katika utendaji wake wa kazi maishani mwake. Na katika hili la Uona Mbali juu ya Katiba yetu, basi, kama JK atafanikiwa kuongoza juhudi hizi za Watanzania kupata Katiba iliyofanyiwa marekebisho makubwa, sina shaka yeyote, kuwa ataacha legacy kwa maana ya haiba. Katiba Mpya itakuwa moja ya jambo kubwa atakalokumbukwa nalo.
Ndio, JK atakumbukwa kama Rais aliyeongoza mabadiliko makubwa na ya kihistoria yaliyopata kufanyika katika nchi yetu. Kukumbukwa kwa kuchangia kuifanya nchi yetu kuwa mahali pema pa kuishi; kuwa nchi ya kisasa zaidi kuliko ilivyo sasa. Hofu yangu, ni kama JK ataweza kuachwa kuifanya kazi hii bila kukwamishwa na nguvu hasi za wahafidhina ndani ya chama chake, CCM.
Kwa anachotaka kufanya JK yaweza kabisa ikawa mchango wake katika kukinusuru chama chake, CCM. Kwamba CCM, kama chama, kisije kikapotea kabisa kwenye ramani ya kisiasa. Kwamba hata CCM ikija kushindwa, ibaki kuwa Chama cha Upinzani chenye nguvu na kinachoweza kurudi tena madarakani.
Maana, huko twendako, upo, uwezekano wa CCM kushindwa uchaguzi. Kwa Katiba ya sasa, siku CCM ikishindwa uchaguzi, itakuwa na maana ya chama hicho kuporomoka kama nyumba ya karata. Si hata Mzee Makamba mwenyewe alipata kutamka hadharani, kuwa Mtaji wa CCM ni Kikwete!
Na juzi hapa Mzee Makamba akatamka; kuwa hana maoni juu ya Katiba, anamsubiri JK atoe tamko. Hicho pia ni kielelezo cha mapungufu ya Katiba yetu. Na tushukuru nchi yetu haijapata bahati mbaya ya kuwa na 'mwendawazimu' pale Ikulu ya Magogoni.
Na wenye kutanguliza ubinafsi wao ndani ya CCM hawauoni ukweli, kuwa si miaka mingi kutoka sasa, Chama Cha Mapinduzi kitakuwa chama cha upinzani. Hawautambui ukweli, kuwa himaya zote duniani hujengwa na kuporomoka. Hakuna himaya iliyodumu daima. Hata Roma iliporomoka. Kwa vijana wa sasa, salamu ya " CCM Daima!" ni kielelezo cha watu waliopitwa na wakati.
Na kumsaidia JK katika kutupitisha kwenye njia hii salama tunayoitaka sasa ni kwa Watanzania kutambua ukweli, kuwa demokrasia yetu bado changa. Tumefanya chaguzi zenye walakini mwingi, ni sehemu ya kujifunza. Na sasa tuna fursa ya kuandaa Katiba itakayotufanya tujenge misingi imara ya demokrasia yetu.
Kumsaidia JK ni kukubali ukweli kuwa Uchaguzi uliopita umeshapita. Kwamba Serikali iliyo madarakani kwa sasa ndio hiyo inayoongozwa na JK kama Rais. Hatuna Rais mwingine. Hatuna Serikali nyingine. Rais tuliye naye sasa ni Jakaya Mrisho Kikwete.
Na tuukubali ukweli pia, kuwa wakati umebadilika na kuwa wananchi wanaukubali upinzani. Na kwamba kwa sasa CHADEMA ndio chama kikuu cha upinzani kikifuatiwa na CUF. CCM, CHADEMA , CUF na wengine wana lazima ya kushirikiana katika mambo ya msingi na yenye maslahi kwa taifa letu.
Ndio, tumeumaliza mwaka jana na mjadala wa Katiba mpya. Tunaingia mwaka 2011 na mjadala wa Katiba Mpya. Hili ni jambo jema. Na lililo muhimu kabisa katika mjadala wowote uwao ni kujiuliza; nini shabaha na malengo yetu? Nionavyo, shabaha na leo letu liwe kudumisha Umoja wetu wa Kitaifa, amani na utulivu tulio nao.
Kama swali ni je, Katiba yetu ya sasa, na kwa wakati uliopo, inakidhi matakwa ya shabaha na malengo yetu kama taifa? Jibu langu ni HAPANA. Na ndio maana nimekuwa na nitaendelea kuunga mkono juhudi za kufanya marekebisho makubwa ya Katiba yetu.
Na katika hili hatuna sababu za kugombania fito ilihali nyumba tunayojenga ni moja na ni yetu sote.
Ieleweke, kuwa madai ya Watanzania kupata Katiba mpya ni madai muhimu na ya kihistoria. Tumewasikia hata wanaojidanganya, wakiandika, kuwa madai haya yanatokana na ' Njama za mabeberu!'. Hizi ni propaganda za miaka ya 70, zimepitwa na wakati.
Ni busara kutambua, kuwa wakati umebadilika. Mtanzania wa mwaka 1977 si Mtanzania wa mwaka 2010. Hoja hii ya Katiba si kama nzi anayetua na kuruka. Hoja ya Katiba kwa sasa inaongozwa na kundi kubwa la vijana wanaotaka mabadiliko. Hawa si nzi wanaotua na kuruka, ni siafu wanaokuja kwa kuongezeka idadi yao.
Na madai ya marekebisho ya Katiba si madai mapya. Si madai ya chama au kikundi kidogo cha 'wapinzani' wasioitakia mema nchi hii. Ni madai ya msingi ya Watanzania, bila kujali tofauti zao za kiitikadi, kidini, rangi na makabila.
Kama ni shauri mahakamani, basi, lilishafunguliwa. Kinachofanyika sasa ni mwendelezo wa shauri. Ndio, tunapongia mwaka 2011, madai ya Katiba mpya yatatimiza miaka 20. Yalianza tangu mwaka 1991.
Ndio, si wengi, miongoni mwa vijana wa sasa, wenye kumbukumbu ya ukweli huu. Tayari mwaka 1991 vuguvugu la kudai vyama vingi na Katiba mpya lilishaanza. Wakati huo madai makubwa yalikuwa mawili; vyama vingi na Marekebisho ya Katiba. Kuna mnaokumbuka ' KAMAKA'- Kamati ya Marekebisho ya katiba iliyondwa na wanaharakati. Hayo yalikuwa ni madai ya Watanzania ndani ya mfumo wa chama kimoja.
Marehemu Chifu Abdalah Fundikira aliongoza Kamati iliyoundwa, si na Serikali, bali wanaharakati, kuratibu mchakato wa kudai vyama vingi na Katiba mpya.
Hata wakati huo Mzee Mwinyi, kama Rais, aliweka ' mkwara', kuwa madai hayo yasiendeshwe na watu au makundi ya watu bila kibali cha Serikali. Presha ya madai ilipoongezeka, tunakumbuka, kuwa Mzee Mwinyi aliweza kusoma alama za nyakati. Aliongea pale Chuo Kikuu Mlimani na kuweka bayana dhamira ya Serikali ya kuunda ' Tume ya Nyalali' . Tume hiyo ilizunguka nchi nzima kuwauliza Watanzania kama wanataka kuendelea na Chama kimoja au Vyama vingi.
Itakumbukwa, Chifu Fundikira alipata kutamka; kuwa huko ni kupoteza muda na fedha za wananchi. Itakumbukwa pia, Mabere Marando alikuwa Katibu wa Kamati ile ya wanaharakati ya kuratibu mchakato wa madai ya kuwepo na vyama vingi na marekebisho ya Katiba. Marando alipata kutamka na kunukuliwa na Daily News, April, 12, 1991; " We have a bad political system because our Constitution embraces political discrimination. What we want is that all of us should shout out that our Constitution is bad." ( Mabere Marando, Daily News, April 12, 1991)
Ndio, Marando aliyasema hayo katika Semina ya kwanza ya Kamati ya kuratibu mchakato wa madai ya vyama vingi na Katiba mpya iliyoongozwa na Chifu Fundikira. Semina hiyo iliudhuriwa na watu wapatao 800 kwa mujibu wa taarifa ya Daily News la April 12, 1991.
Na akina Chifu Fundikira waliandamwa sana. Kwa mujibu wa Daily News la April 26, 1991, Mbunge wa Shinyanga, Ndugu Paulo Makolo alimshambulia Fundikira kwa kusema kuwa , katika hilo la kuwa na vyama vingi na katiba mpya , Chifu Fundikira hawasilishi mawazo ya Wasukuma na Wanyamwezi wenzake; " This is not a Wanyamwezi and Wasukuma movement. It is the selfish interests of Fundikira and his ten colleagues. Our people are not after parties. They want food, water, education and health care." ( Paulo Makolo, MP, Shinyanga, Daily News, April 26, 1991). Mwenyezi Mungu umrehemu Chifu Abdalah Fundikira.
Maggid
Iringa,
Januari Mosi, 2011
http://mjengwa.blogspot.com