Hadithi: Uchawi wa bilionea Bazoka

NYEMO CHILONGANI.
UCHAWI WA BILIONEA BAZOKA
0718069269
Sehemu ya 16

Pale alipokuwa Maganza alikuwa akitetemeka kwa hofu, ni kweli alikuwa mwanaume shupavu, aliyeweza kupambana na majambazi wengi lakini kwenye suala la kishirikina kama lile, hakika moyo wake ulikuwa na hofu tele.
Sauti iliyokuwa ikimuita hakuifahamu, ilikuwa ngeni masikioni mwake, aliisikiliza kwa umakini kabisa, ilikuwa ni ya mwanamke aliyeendelea kuita zaidi na zaidi.
Alimwangalia mke wake, alikuwa amelala pembeni, hakushtuka japokuwa sauti ile ilikuwa ikiita kwa nguvu kabisa. Akaanza kujiuliza kama lingekuwa jambo jema kuteremka kitandani na kuelekea huko ama aendelee kulala.
“Ni nani ananiita?” alijiuliza.
Hakutaka kusubiri, haraka sana akateremka na kuelekea dirishani huku mapigo yake ya moyo yakidunda kupita kawaida. Kuna wakati alitamani kuona ile ikiwa ndoto fulani ya kusisimua na muda fulani aamke na kujikuta akiwa kitandani, lakini haikuwa hivyo, kilikuwa ni kitu halisi kilichokuwa kikiendelea.
Akaelekea sebuleni, sauti ile iliendelea kuita kama kawaida. Kabla ya kuufungua mlango, akaamua kwenda dirishani na kufungua pazia, akaangalia nje. Hapakuwa na mtu yeyote yule, mbali na ile sauti iliyokuwa ikimuita, kulikuwa na ukimya mkubwa.
Akaendelea kuisikia sauti kutoka upande mwingine kabisa, ili kumuona muitaji ilikuwa ni lazima aufungue mlango na kutoka huko ndani na kuelekea nje, akaufuata mlango, akakishika kitasa.
“Unajua nani anakuita?” lilikuwa swali alilolisikia.
Ilikuwa ni sauti iliyomwambia sikioni, si sauti ya moyoni, aliisikia kana kwamba muongeaji alikuwa pembeni yake, haraka sana akageuka, hapakuwa na mtu yeyote yule. Kijasho kikazidi kumtoka, sasa akajiuliza, aufungue mlango ama auache.
“Ngoja nifuate bastola!” alisema.
Hakutaka kubaki sebuleni, haraka sana akaondoka na kurudi chumbani kwake, akaufungua mlango na kuifuata bastola yake iliyokuwa kwenye kidroo, akaichukua, akaangalia risasi, zilikuwepo kama nane hivi, sasa akarudi sebuleni, akaufungua mlango na kutoka.
Alishangaa! Alichukuwa akikiona hakikuaminika machoni mwake. Aliujua mtaa wake, alipokuwa akitoka alikuwa akikutana na nyumba za majirani nyingine na barabara ya vumbi lakini cha ajabu baada ya kuufungua mlango, macho yake yakatua kwenye majumba makubwa ya ghorofa yaliyokuwa yakiwaka taa.
Huku akiwa amesimama akishangaa, bastola ikiwa mkononi mwake na kitetemeka kupita kawaida, mara mlango wa nyumba yake ukajifunga kwa nyuma, ulipolia puu, akageuka, hakuuona mlango wala nyumba yake, sasa akawa amesimama katikati ya mji mwingine mkubwa kabisa, uliopendeza machoni mwake, tena ulikuwa kimya kabisa.
“Mungu wangu! Nipo wapi?” alijiuliza huku akishangaa.
“Maganza amka...Maganza amkaaaaa....’ alijisemea huku akijipiga vibao, akawa anajing’ata lipsi za midomo yake na hata kujifinya kwa kuhisi angeamka na kujikuta kitandani, haikuwa hivyo.
Alichokifanya ni kuanza kutembea, alikuwa akielekea mbele huku akiwa hajui ni mahali gani alipokuwa akienda. Aliangalia huku na kule, mji haukuwa na mtu yeyote yule lakini kwa jinsi alivyokuwa akizidi kutembea, kwa mbali akaanza kusikia sauti za watu waliokuwa wakiongea.
Hakujua walikuwa akina nani lakini kwa mbali akaanza kuwaona watu hao, alichokifanya ni kuongeza kasi kuwasogelea, akiwa amebakiza kama hatua kumi, hakuamini alichokuwa akikiona, migongo ya watu wale haikuwa ya kawaida, ilikuwa kama ya mijusi fulani na kwa miguuni, miguu yao ilikuwa ikifanana na ya bata, moyo wake ukapiga paaa! Watu wale wakageuka na kumwangalia.
Walikuwa na macho makubwa kama ngumi, midogo yao ilikuwa mikubwa, masikio yao yalikuwa kama ya mbuzi, vifuani walikuwa na manyoya mengi. Kwa mbali ilikuwa ni rahisi kusema walikuwa binadamu lakini alipowasogelea, alibaini hawakuwa binadamu wa kawaida, walikuwa viumbe wengine kabisa.
“Kuna mambo mengine hutakiwi kuyafuatilia,” alisema kiumbe mmoja huku akimwangalia, hapohapo Maganza akaanza kuisikia sauti ya mke wake ikimuita. Ghafla akajikuta akiwa kitandani, kwa juu kulikuwa na dripu iliyokuwa ikining’inia.
Alishtuka, hakujua alikuwa mahali gani, alimwangalia mke wake huku akiwa na mshangao mkubwa, mkewe naye alikuwa akishangaa tu, alimwangalia mume wake huku akiwa haamini kama ameyafumbua macho yake.
“Mume wangu!” alimuita.
“Mke wangu! Nipo wapi?” “Hospitali!” “Hospitali? Nafanya nini?” alimuuliza huku akiwa anajaribu kutoa sindano ya dripu iliyokuwa imepenya kwenye mshipa wake.
“Nilikuwa nakuamsha chumbani ukawa huamki, nilikuamsha sana lakini hukuamka, nikaamua kukuleta hospitalini,” alimwambia.
“Ulikuwa unaniamsha?” “Ndiyo! Ulilala sana, yaani kwa kawaida unaamkaga saa moja, ila mpaka saa sita nilikuwa nakuamsha na hukuwa unaamka,” alimwambia, Maganza akabaki akishangaa tu.
***
Bi. Semeni alijawa na hofu tele, mahali alipokuwa hakika kulimtisha mno, vicheko vile viliendelea kusikika na kumjaza hofu tele. Hakujua alikuwa mahali gani na kitu cha ajabu hata fisi wake hakuwa akimuona mahali hapo.
Huku akiwa anajiuliza na akitetemeka mno, ghafla akawaona watu watatu wakitoka vichakani, walikuwa ni wa kawaida tu, mikononi mwao walishika usinga na walikuwa wakitembea huku wakimfuata pale alipokuwa.
Alitamani kukimbia lakini alishindwa, miguu ilikuwa mizito kuinuka, watu wale walikuwa na tabasamu pana na walionekana kuwa na furaha tele, wakamsogelea na kumwangalia usoni.
Hakutingishika, alitamani kujitingisha lakini alishindwa kufanya hivyo, akabaki akitetemeka kwa hofu. Watu wale wakaanza kumwangalia, alikuwa akitetemeka kwa hofu tele.
“Nipo wapi? Nini kimenitokea?” aliuliza Bi. Semeni huku akiwaangalia watu hao.
“Tukuulize wewe ulikuwa unaelekea wapi!” alimwambia mwanaume mmoja.
‘Kazini!”
“Wapi?”
“Kwenye makutano yetu!” “Sasa kwa nini umekuja kwetu?” “Nimepata ajali!”
“Na mbona umebeba gogo, ulikuwa unakwenda nalo wapi?”
Bi. Semeni alishangaa, ilikuwaje mtu huyo amwambie alibeba gogo na wakati alikuwa na uhakika aliyekuwa amembeba alikuwa Bazoka. Akayapeleka macho yake kwa Bazoka na kumwangalia, alitaka kuwa na uhakika na kule alichoambiwa.
“Nimebeba gogo?” aliuliza. “Wewe hulioni hilo?” alisema mtu huyo, akamsogelea Bi. Semeni na kumpulizia dawa fulani, naye baada ya hapo, alichokuwa akikiona si Bazoka tena bali gogo kama alivyoambiwa.
“Imekuwaje?” aliuliza huku akionekana kushtuka.
“Nikuulize wewe...inakuwaje unabeba gogo na kwenda nalo sehemu! Kwani ulikuwa unakwenda nalo wapi?”
“Sikubeba gogo mimi!” “Sasa hilo nani alilibeba?” aliulizwa, akakosa jibu, akabaki akishangaa tu, alichojua ni kwamba alimbeba Bazoka, sasa ilikuwaje mpaka ionekane amelibeba gogo? Kila alichojiuliza, akakosa jibu.
Je, nini kitaendelea?
Tukutane Jumamosi.
 
NYEMO CHILONGANI.
UCHAWI WA BILIONEA BAZOKA
0718069269
Sehemu ya 17.

Bi. Semeni alihisi kuchanganyikiwa kupita kawaida, hakuamini kama kweli kile alichokuwa akikiangalia kilikuwa gogo na si mwili wa Bazoka, hakujua ni kitu gani hasa kilikuwa kimetokea.
Akalisogelea na kuliangalia vizuri, ni kweli lilikuwa gogo, sasa nini kilitokea mpaka kuwa hivyo? Alijifahamu kwamba yeye ni mchawi mkubwa, mwenye nguvu, hapakuwa na mtu aliyekuwa akimbabaisha, sasa kwa nini ionekane alibeba gogo? Ni wale watu aliokutana nao ndiyo waliokuwa na nguvu za kumbadilisha Bazoka na kuwa gogo ama Bazoka mwenyewe ndiye aliyekuwa na nguvu hizo?
“Hapana! Huyu mtupu kabisa!” alijijibu baada ya kujiuliza kama kulikuwa na uwezekano wa Bazoka kuwa na nguvu hizo.
Alimfahamu Bazoka, hakuwa mgeni na hiyo haikuwa mara ya kwanza kumuwangia, hakuwa na nguvu zozote zile, alikuwa mtupu kama ndoo isiyokuwa na maji. Kitendo cha kujiambia kwamba inawezekana alikuwa na nguvu kilikuwa ni kosa kwa kuwa kwa macho yake aliwahi kumuwangia usiku kucha.
Alikaa na hao watu, hakuweza kuondoka, uchawi wake uliharibiwa vibaya hivyo walichokifanya watu wale ni kumpa nguvu nyingine za kuweza kupaa na kuondoka naye hapo, ila sharti lilikuwa moja tu, amuache fisi wake hapo.
“Kwa sababu gani?” aliwauliza.
“Ndiyo malipo kwetu! Au unataka tukuache hapahapa?” aliuliza mwanaume mmoja huku akimwangalia.
Kuondoka mahali hapo lilikuwa jambo jema kabisa, hakutaka kubaki mahali hapo, ilikuwa ni lazima kuondoka, hiyo ndiyo ingekuwa salama yake, akakubaliana nao, akapewa nguvu, akasimama imara na ghafla akapotea na kuibukia chumbani kwake.
Alikuwa amechoka mno, akatoka chumbani harakaharaka na kuelekea bafuni. Siku hiyo alichanganyikiwa na hakuwa na gamu ya kuendelea kuloga kama siku nyingine, ilikuwa ni lazima apate kujua ni kitu gani hasa kilitokea mpaka kwa Bazoka kuonekana gogo.
Alipomaliza kuoga, haraka sana akakimbilia ukumbini, akaufuata mlango wa Bazoka na kuanza kusikiliza ndani kuhisi kama kulikuwa na kitu ama la, alichokisikia ni mwanaume huyo kukoroma, yaani alikuwa kwenye usingizi mzito mno.
“Mh! Sasa imekuwaje?” alijiuliza.
Akarudi chumbani kwake, siku hiyo hakulala, alibaki akiwa anajiuliza ni kitu gani hasa kilichokuwa kimetokea, ilipofika majira ya saa moja asubuhi, akasikia mlango wa Bazoka ukifunguliwa, na harakaharaka naye akatoka, wakakutana ukumbini, wakaangaliana.
“Shikamoo mama!” alimsalimia huku akiwa na tabasamu.
“Marahaba! Hujambo mtoto wangu!’ naye alimsalimia.
“Sijambo tu mama! Mimi nakwenda kazini!” alimwambia.
“Sawa!” aliitikia, Bazoka akatoka na kuondoka zake.
Bi. Semeni alikuwa akimsindikiza kwa macho, alimuona kwa namna alivyokuwa akiondoka, alionekana kuwa mtu mwenye furaha kupita kawaida, hilo hakutaka kuliona, kama mchawi, furaha yake ilikuwa ni kuwaona watu wakiteseka, wakihuzunika na kulia usiku kucha.
Kwa Bazoka kuwa na furaha vile, tena ndani ya nyumba yake lilionekana kuwa kosa kubwa, yaani alijiona ni kama mtu ambaye hakuwa akiifanya kazi yake vilivyo, ilikuwa ni lazima afanye kila liwezekanalo kuhakikisha mwanaume huyo anakuwa na huzuni na maisha ya hovyo kama alivyokuwa akiwafanyia wengine.
Kwa kuwa alikuwa na unguo mwingine wa chumba cha Bazoka, akauchukua na kuufuata mlango, akaufungua na kuingia ndani. Alihitaji kujua kuhusu mwanaume huyo, alikuwa na vitu gani ambavyo vilimpa shida na kujikuta akiwa amebeba gogo badala ya kumbeba yeye mwenyewe.
Akaufungua na kuingia ndani, akaanza kuangalia huku na kule, hapakuwa na kitu chochote kile, akalifungua kabati na kuangalia ndani, alichokutana nacho ni nguo tu na vitu vingine vya kawaida.
Akalitoa godoro, chini ya uvungu wa kitanda hapakuwa na kitu chochote kile. Akili yake ilimwambia inawezekana humo ndani kulikuwa na kitu hivyo akaendelea kuangalia zaidi kuona kulikuwa na nini.
“Kutakuwa na kitu humu!” alijisemea, akili yake ikamwambia tena akaangalie kwenye kabati, haraka sana akalifuata na kuangalia ndani, alikutana na nguo zilezile ila alipolifunga kabati na kugeuka nyuma, alipigwa na mshtuko baada ya kuona hakuwa tena chumbani kwa Bazoka.
“Eeh!” alishangaa.
Alikuwa katika jangwa moja kubwa, lililokuwa na mchanga mwingi kama Sahara, alibaki akiashangaa ni kwa namna gani alifika mahali pale, jua lilikuwa kali, aliangalia huku na kule, alikuwa akiweweseka, hakujua ni kwa namna gani alifika mahali pale.
Aliyafikicha macho yake, wakati mwingine alihisi kama alikuwa akiota, kile alichokuwa akikiona hakika hakukitarajia hata kidogo. Akaanza kupiga kelele kuhitaji msaada, hapakuwa na mtu aliyemsikia, alikuwa jangwani na hakujua ni kwa namna gani angeweza kutoka mahali hapo.
Huku akiwa hajui ni kitu gani alitakiwa kufanya na jua kali likimchoma, akaanza kusikia sauti za watu kutoka mbali kabisa, hakuwa akiwaona ila alikuwa na uhakika walikuwa wakija kule alipokuwa.
Aliogopa, hakujua ni kwa namna gani angeweza kutoka mahali hapo, huku akiwa ametulia tu, akawaona watu watatu wakija kule alipokuwa, walikuwa Waarabu waliokuwa juu ya ngamia zao, walivaa vilemba na walionekana kuwa na furaha tele.
Baada ya macho yao kutua kwa Bi. Semeni, wote watatu wakapigwa na mshangao, ilikuwa ni ajabu kumuona mtu mahali hapo, kwa sehemu ya jangwani kama hiyo, hawakujua alifikaje mahali hapo, na kwa jinsi alivyovaa, alikuwa kama mtu ambaye hakujiandaa kuwa hapo.
“Wewe nani?” aliuliza mwanaume mmoja, aliuliza kwa Kiarabu lakini kitu cha ajabu kabisa, Bi. Semeni aliweza kumuelewa kwa kila neno.
“Nani? Mimi?” aliuliza huku akionekana kuogopa.
“Ndiyo! Wewe! Umefikaje hapa?” aliuliza mwanaume huyo.
“Sijui! Nimejikuta tu mahali hapa, naomba mnisaidie nirudi nyumbani,” alisema, wanaume wale wakaangaliana na kuanza kucheka.
“Sasa tutakusaidiaje?” aliuliza mwingine.
“Nimejikuta nipo hapa!”
“Umefikaje? Yaani umejikuta upo hapa tu?”
“Ndiyo!”
“Ulikuwa unafanya nini mpaka umejikuta ukiwa hapa?” aliuliza mwanaume wa tatu.
Hakujibu swali hilo, akanyamaza na kuangalia chini, alijisikia aibu kubwa mno na alishindwa kujua ni kwa namna gani angeweza kulijibu swali hilo. Kuwaambia kwamba alikuwa akiloga lilikuwa jambo gumu mno, hivyo alikuwa akifikiria uongo mwingine.
“Naomba mnisaidie,” alisema bila kulijibu swali hilo.
“Unajua upo wapi hapa?”
“Hapana!”
“Upo Misri! Na ndiyo maana tunajiuliza umefikaje!” alisema mwanaume wa kwanza.
“Au ulikwenda kumloga mtu mwenye nguvu zaidi yako?” aliuliza mwanaume wa pili.
Swali hilo ndilo ambalo lilimshtua kidogo Bi. Semeni, akayainua macho yake na kuwaangalia watu hao, sasa akaanza kuhisi kitu cha tofauti kabisa. Mwili wake ukaanza kumsisimka kupita kawaida, vinywele vikaanza kumsimama huku kijasho chembamba kikianza kumtoka, tena mfululizo.
“Unasema?”
“Angalia na watu wa kuwaloga, kuna siku utakuja kupoteza maisha!” alisema mwanaume wa pili, wote watatu wakatoa vicheko vikubwa, Bi. Semeni hakujua ni kitu gani kilichotokea lakini alimuona ngamia mmoja kwa kutumia mguu wake wenye kwato akiuinua kidogo, akauchota mchanga na kummwagia usoni, mchanga ukampiga, akayafumba macho yake kujizuia, alipoyafumbua, akajikuta akiwa chumbani kwa Bazoka.
“Mamaaaaaa....nakufaaaaa...” alipiga ukunga, haraka sana huku akionekana kuchanganyikiwa, akatoka ndani ya chumba kile, akaufungua mlango, alikuwa akitetemeka, hofu nzito iliutawala moyo wake, hakuamini kile kilichokuwa kimetokea kilimtokea.
Akakimbilia chumbani kwake, alikuwa akitetemeka kwa hofu, yaani mchawi nguli kama yeye, aliyebobea kwenye mambo ya uchawi, leo alikuwa na hofu, moyo wake ulikuwa ukiogopa kupita kawaida.
Akapanda kitandani na kukaa kwenye pembe, akajikunyata kwa kukunja miguu yake na kuanza kulia huku mapigo yake ya moyo yakidunda kwa nguvu.
“Mama nakufaaaa...mama nakufaaa...” alisema mfulilizo huku akilia.
***
Maganza hakuamini alichokuwa amekisikia kutoka kwa mkewe, alimwangalia kwa mtazamo wa kutaka kusikia tena na tena kile alichomwambia. Alisema kuwa alilala mpaka saa sita, haikuw akawaida yake lakini suala la kulala na kile kilichotokea vilikuwa vitu viwili tofauti kabisa.
Alikumbuka vilivyo alikuwa kwenye mji wa ajabu, mzuri kwa macho lakini kulikuwa na viumbe wa ajabu, waliokuwa na muonekano wa kutisha mno, waliwambia kulikuwa na mambo mengine hakutakiwa kabisa kuyafuatalia.
Alijiuliza mambo gani hayo? Kulikuwa na mambo mengi mno lakini mengine hakutakiwa kuyafuatilia hata kidogo. Kipindi hicho hakuw ana jambo jingine la kufuatilia zaidi la suala la mtoto Yusufu ambaye alitekwa na hakujua alikuwa mahali gani.
“Ni kuhusu yule mtoto?” alijiuliza.
“Unasemaje?” aliuliza mkewe, alimsikia mumewe akiwa ameongea jambo fulani.
“Hebu twende nyumbani!” alimwambia.
“Lakini unaumwa!”
“Hapana! Siumwi,’ alisema Maganza huku akitoa sindano ya dripu iliyokuwa kwenye mshipa wake.
Hakutaka kubaki hospitalini hapo, ilikuwa ni lazima kuondoka na kurudi nyumbani kwake. Alishangaa kuona moyo wake ukiwa na hamu kubwa ya kutaka kufahamu zaidi kuhusu mtoto Yusufu, ilikuwa ni lazima aujue ukweli wa kile kilichokuwa kimetokea.
Daktari alijaribu kumzuia lakini alishindwa, ilikuwa ni lazima kuondoka na kwenda kumaliza kazi aliyokuwa ameianza. Mkewe alikuwa akimshangaa njia nzima, mumewe alionekana kuchanganyikiwa, alionekana kuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea, ila hakutaka kumwambia.
Alijaribu kumuuliza maswali mengi lakini hakujibu zaidi ya kung’ang’ania warudi nyumbani kwanza, wakafanya hivyo. Walipofika, akaingia bafuni, akaanza kuoga na kuendelea kufikiria kilichokuwa kimetokea.
Hakika kilimtisha mno, wakati mwingine alihisi kama alikuwa akiota lakini cha ajabu mambo yalikuwa yakitokea kabisa kwenye ulimwengu halisi. Akiwa humo, akasikia simu yake ikiita, akamwambia mkewe aipokee.
“Ipokee tu! Ni nani?” alimuuliza.
“Kamanda Kizota!” alijibu.
Haraka sana akatoka na kuifuata simu aliyokuwanayo mkewe, akaichukua na kuipokea, alichokisikia ni sauti ya kamanda wake, Kizota akimwambia kulikuwa na jambo kubwa limetokea ofisini hivyo alitakiwa kwenda haraka sana.
“Jambo gani?”
“Juu ya uchunguzi uliokuwa unaufanya!”
“Wa mtoto albino?”
“Ndiyo!”
“Imekuwaje?”
“Njoo haraka ofisini,” alisema kamanda huyo na kukata simu. Maganza akaanza kuvaa harakaharaka ili awahi huko kazini kuona ni kitu gani hasa kilikuwa kimetokea.

Je, nini kitaendelea?
 
YEMO CHILONGANI
UCHAWI WA BILIONEA BAZOKA
0718069269

SEHEMU YA 18.

Maganza hakutaka kusubiri, haraka sana akaondoka kuelekea kazini kwake kwani kwa jinsi alivyoambiwa na kamanda wake, Masumbuko, alijua kabisa kulikuwa na kitu.
Akiwa ndani ya gari lake, mawazo yake juu ya kile kilichotokea hayakukoma, bado alikuwa akikumbuka na hakujua ni kitu gani hasa kilisababisha kuwepo kwa miujiza ile.
Mara ya kwanza alihisi labda kwa sababu alifuatilia suala la Yusufu lakini baadaye akahisi halikuwa hilo, alipewa onyo la kufuatilia juu ya jambo jingine, ama ambalo lingetokea baada ya hapo.
Huku akiwa na mawazo hayo, mara akafika ofisini kwake, haraka sana akateremka na kuelekea ndani ambapo akapitiliza mpaka kwa mkuu wake wa kazi na kukaa kwenye kiti.
Macho yake yalikuwa yakimwangalia mwanaume huyo aliyekuwa nyuma ya meza, hakuzungumza kitu kwanza zaidi ya kusalimiana tu. Kwa jinsi alivyomwangalia Maganza siku hiyo alionekana kutokuwa sawa kabisa.
Alimjua, alipokuwa kwenye hali ya kawaida, alilijua hilo na hata alipokuwa kwenye hali tofauti kama aliyokuwanayo, napo alijua. Alihitaji kufahamu ni kitu gani hasa kilichokuwa kimetokea, hivyo akamuuliza.
“Hakuna kitu!” alimjibu huku akimwangalia.
“Hapana Maganza, unajua nakufahamu sana, hebu niambie kuna nini!” alimwambia.
Maganza akabaki kimya kwa sekunde kadhaa, kichwa chake kilijipa nafasi ya kujiuliza kama lingekuwa jambo sahihi kumwambia kile kilichotokea ama la.
“Mauzauza tu!” alimwambia.
“Mauzauza gani tena?” aliulizwa.
Akaanza kumuhadithia kila kitu kilichokuwa kimetokea. Kamanda Masumbuko alibaki kimya akimsikiliza kijana wake, kwa jinsi alivyosimulia, alijua dhahiri aliogopa japokuwa alikuwa kamanda aliyekuwa akimtumainia sana.
Alipomaliza, Masumbuko akashusha pumzi ndefu.
“Pole sana! Ila nahisi ni kwa sababu umechoka sana,” alimwambia.
“Kuchoka ndiyo yatokee hayo?”
“Inawezekana pia. Unajua kwa jinsi unavyohangaika, hutulii nao ubongo unachoka sana na mwisho wa siku unajikuta ukianza kukuletea mambo ya ajabu ajabu,” alimwambia huku akitoa tabasamu la mbali.
“Lakini niliyaona mauzauza, halafu nikashtuka na kujikuta hospitalini!” alimwambia.
“Najua! Ubongo ukichoka kuna mambo mengi sana yanaweza kutokea. Jipe moyo na jua hakuna lolote lile,” alimwambia.
“Sawa. Aya naomba uniambie kuhusu uliloniambia,” alimwambia.
“Ile maiti ya yule mtoto imepatikana!”
“Huyu albino/’
“Ndiyo! Imepatikana huko msituni, ilitupwa! Cha ajabu kabisa hakuna kiungo chochote kilichochukuliwa,” alimwambia.
“Yaani umesemaje?”
Akarudia tena, kama alivyoshangaa bosi wake hata naye alishangaa pia. Ilikuwa ni vigumu kwa mtoto mwenye ulemavu wa ngozi kutekwa na kupelekwa sehemu halafu mwili ukutwe bila kunyofolewa kiungo chochote kile.
Lilikuwa ni jambo lisilowezekana na hapo ndipo wakaanza kuhisi inawezekana muuaji aliamua kufanya mambo hayo kwa sababu zake binafsi lakini si kuchukua kiungo chochote cha mtoto huyo.
“Wazazi wake wamepewa taarif?” aliuliza.
“Ndiyo! Mwili ulichukuliwa na kupelekwa mochwari1’ alijibiwa.
“Sawa. Nataka kwenda mahali ulipokutwa mwili huo,” alisema.
“Haina shida.”
Akachukuliwa polisi mmoja na kuanza kumsindikiza huko mwili ulipokuwa umeokotwa. Njiani walikuwa wakizungumza mengi lakini suala kubwa lililokitawala kichwa chake kilikuwa ni yale mauzauza yaliyokuwa yametokea.
Aliogopa kwa kiasi fulani lakini hilo halikumfanya kurudi nyuma na kuacha kile alichokuwa akikifuatilia, ilikuwa ni lazima aendelee nacho kwani alijua tu kwamba mwisho wa siku angeweza kumfahamu mtu aliyefanya mauai hayo yote.
Hawakuchukua muda mrefu wakafika mpaka ndani ya msitu wa Pande na kuteremka, wakaanza kuelekea huko mwili ulipokuwa umeokotwa. Walipofika, wakaanza kuangalia eneo hilo.
Maganza alikuwa makini kabisa, hakuyatuliza macho yake, alikuwa akiangalia huku na kule, alihitaji kujua ni kwa namna gani mtu aliyekuwa amemteka mtoto huyo aliingia msituni humo na cha ajabu kabisa hakuufanya kitu chochote.
“Labda watu walitokea na kumfukuza!” alijisemea.
“Hapana! Kama ingekuwa hivyo mwili ungepatikana tangu siku ya kwanza,” alijijibu.
“Au alikuwa na kisasi na wazazi wa mtoto huyu?” alijiuliza swai jingine.
“Hapana! Kama ni hivyo wazazi wangeniweka wazi, tena kwenye suala zito kama la kutekwa kwa mtoto wao wasingenificha chochote kile,” alijijibu kwa mara nyingine.
Kwa kifupi kila alichokuwa akijiuliza mahali hapo alikuwa na majibu yake ambayo yaliyafanya maswali yake kutokuwa na nguvu kabisa. Alikaa na kupeleleza mahali pale kama nusu saa na alipomaliza, akamchukua polisi mwenzake na kuondoka naye mahali hapo.
“Unahisi muuaji atakuwa nani?” aliuliza mwenzake.
“Bado ni vigumu sana kufahamu!”
“Ugumu hasa upo wapi?”
“Hakuna shahidi aliyemuona! Yaani hapa ningepata hata shahidi mmoja aliyeona gari, ningekuwa na uhakika wa kumpata muuaji,” alimwambia.
“Kwa sababu gani?”
“Basi tu! Uchunguzi wangu kwenye hili, kulifahamu gari lake ni muhimu sana,” alisema.
Walipotoka hapo wakaelekea nyumbani kwa akina Yusufu ambapo huko wakazungumza na wazazi wake, walichomwambia ni kwamba hawakuwa wakifahamu lolote lile na kwa sababu mwili wa mtoto wao ulipatikana, hawakuwa na jinsi, ilikuwa ni lazima kuuzika kwa heshima zote.
Moyo wa Maganza uliuma mno, aliuona mzigo wa mauaji hayo ukiwa kichwani mwake, ilikuwa ni lazima kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha anafanikiwa kumpata muuaji huyo kwani wazazi wa marehemu walitia huruma na walionekana kutokuwa na tumaini lolote lile zaidi yake tu.
Akarudi ofisini, bado kichwa chake kilikuwa na mambo mengi mno, hakujua ni kwa namna gani angeweza kumpata muuaji huyo lakini yeye kama mpelelezi aliyekuwa hatari basi ilikuwa ni lazima kuhakikisha anampata mtu huyo.
***
Bi. Semeni aliendelea kupiga kelele za kudai alikuwa akifa, kwa mambo yote aliyowahi kuyafanya, kwa kipindi hicho yalionekana kuwa hatari, nusu ya kuchukua roho yake.
Alikuwa akilia kama mtoto chumbani mule tena akiwa kitandani mwake, moyo wake ulikuwa na hofu tele na alijua muda wowote ule watu wale wangekuja na kudai roho yake, walimwambia aache kuloga watu waliokuwa na nguvu zaidi yake, hapo kidogo kulimchanganya.
Huku akiwa anapiga kelele za hofu, mara akasikia mlango ukigongwa, akashtuka, ilikuwa ni usiku sana, sasa kama kulikuwa na mtu aliyekuwa akigonga mlango huo, bila shaka alikuwa Bazoka na si mtu mwingine, akanyamaza na kuanza kusikilizia.
“Mama! Mama kuna nini?” aliisikia sauti kutoka mlangoni, ilikuwa ni ya Bazoka.
Moyo wake ukapiga paa! Hakuamini kama mwanaume huyo angefika mlangoni na kumuuliza swali kama hilo, aliamini wanaume wale waliosema hakutakiwa kuwaloga watu waliokuwa na nguvu zaidi yake, walimaanisha Bazoka, lakini ilikuwaje awe yeye na wakati mara ya kwanza alimwangalia na hakuwa na uchawi wowote ule.
Akaufuata mlango na kuufungua, macho yake yakatua kwa Bazoka aliyekuwa akishangaa kwa kile kilichokuwa kikiendelea, zilisikika kelele kubwa akiwa chumbani kwake na alitaka kujua kulikuwa na nini.
“Mama kuna nini?” aliuliza Bazoka huku akimwangalia mwanamke huyo.
“Hakuna kitu!”
“Umepiga kelele mpaka umenishtua! Nilidhani kuna wezi,” alisema Bazoka.
“Hapana! Ni ndoto mbaya!” alimwambia.
“Pole sana! Inabidi usome dua,” alimwambia.
Kwa jinsi alivyoonekana tu usoni mwake, Bazoka hakuonekana kufahamu lolote lile, yaani alionekana kuwa mgeni wa kila kitu kilichokuwa kimetokea, ikambidi Bi. Semeni afunge mlango na kutulia chumbani kwake.
Sasa akawa anajiuliza ni kitu gani alitakiwa kufanya, je, ni kweli Bazoka alikuwa mchawi ama alikuwa akiweweseka yeye tu? Alianza kujiwa na mambo hayo ya mauzauza baada ya mwanaume huyo kuhamia humo ndani, je, aendelee kuishi naye ama amfukuze?
“Bora nimfukuze, na kodi yake namrudishia! Siwezi kuishi na mchawi,” alisema, yaani alijisahau kabisa kwamba hata yeye alikuwa mchawi.
Usiku huo hakulala, alikuwa akijifikiria mambo mengi lakini kubwa zaidi lilikuwa ni hofu, alihisi endapo angelala asingefanikiwa kuyafumbua macho yake milele. Asubuhi ilipofika baada ya kukesha kama popo, aliposikia mlango wa Bazoka unafunguliwa tu, haraka haraka akawahi.
“Naomba tuongee!” alimwambia, Bazoka hakuwa na shida, akasimama.
“Niambie mama!” alimwambia.
“Nataka uhame hii nyumba,” alimwambia.
Bazoka alishtuka, hakuamini alichokisikia, ilikuwaje ahame nyumba na wakati ndiyo kwanza alihamia nyumbani hapo? Ni kama hakusikia alichoambiwa, akamuuliza tena na tena, mwanamke huyo alimwambia vilevile kwamba ni lazima ahame nyumba hiyo.
“Sasa nitahamia wapi mama?” alimuuliza.
“Popote pale!”
“Mama! Kwani kuna nini kimetokea?”
“Nimesema uhame niishi kwa amani!”
“Jamani! Kwani mimi nimefanyaje mama?” alimuuliza.
“Sitaki maswali, ninataka uhame, tena leo hii hii, na hela yako nakupa,” alisema mwanamke huyo, hapohapo akaingia chumbani kwake, akachukua pesa na kumpa Bazoka, tena ikiwa ni kodi nzima.
Bazoka alibaki amepigwa na butwaa tu, hakuamini alichokuwa akikina muda huo, kwa Bi. Semeni kumtaka kuhama ndani ya nyumba hiyo hakika kulimshangaza kupita kawaida. Akajiuliza mswali mengi ambayo yota hayo hakuwa na majibu nayo.
Mwanake huyo ndiye alikuwa mwenye nyumba, hakutakiwa kumgomea hata kidogo, kama alivyoambiwa ahame basi ilikuwa ni lazima afanye hivyo, hivyo alichokifanya ni kuwasiliana na dereva wa gari, baada ya hapo, akamtafuta Frank na kumueleza kilichokuwa kimetokea.
Frank alishangaa sana, hakuamini alichoambiwa kuhusu Bi. Semeni, ilikuwaje mwanamke huyo amwambie ahame? Kwa sababu gani? Kulikuwa na suala la kupiga kelele usiku, nalo lilisababishwa na nini?
“Ama wewe mchawi?” aliuliza Frank kimasihara.
“Mimi na uchawi wapi na wapi? Yaani amenishangaza mno!” alimwambia.
“Kwa hiyo?”
“Inabidi nihame tu! Kanisaidie kuhamisha vyombo!” alimwambia Frank.
“Mimi nikakusaidie kuhamisha vyombo?”
“Sasa unaogopa nini?”
“Haiwezekani kaka! Wewe utahamisha na dereva!” alimwambia, Frank mwenyewe alimuogopa Bi. Semeni kupita kawaida.
Baada ya dakika kadhaa Bazoka akapigiwa simu na dereva na kuambiwa tayari alifika mahali hapo hivyo alitakiwa kwenda kusaidiana naye kutoa vyombo, haikuwa tatizo, akaenda na kufanya hivyo.
Majirani walikuwa wakimwangalia tu, wao wenyewe walilitegemea lile lililokuwa likitokea, hapakuwa na mpangaji aliyeishi sana ndani ya nyumba hiyo, hivyo walihisi hata Bazoka naye yalimshinda na hivyo kuamua kuhama.
“Hii nyumba jamaa aliichukulia kawaida sana, hii nyumba ni hatari zaidi ya kuzimu, kijana aliambiwa weeee, hakusikia, sasa leo amejionea,” jamaa mmoja aliwaambia wenzake.

Je, nini kitaendelea?
 
NYEMO CHILONGANI
UCHAWI WA BILIONEA BAZOKA
0718069269
SEHEMU YA 19.

Watu wote waliamini Bazoka ndiye aliyekuwa amepata tatizo kama wapangaji wengine na hivyo aliondoka nyumbani hapo akimuogopa mwanamke huyo aliyekuwa mchawi kupindukia.
Wengi waliongea kwa kejeli, walikumbushana namna walivyomwambia Bazoka kuhusu nyumba hiyo, jinsi Bi. Semeni alivyokuwa mchawi, alivyopenda kutesa watu, kuwalaza baharini na hata kuwalimisha lakini cha ajabu, kijana huyo hakusikia, akaamua kuingia ndani ya nyumba hiyo.
Kilichompata, leo hii alikuwa akihama nyumba hiyo, aliamua kukimbia bila kuaga, watu wote waliamini yeye ndiye aliyemkimbia mwanamke huyo lakini baada ya kuambiwa na Frank kwamba ni Bi. Semeni ndiye aliyemfukuza Bazoka, hakika kila mmoja alibaki na mshangao.
Kilikuwa ni kitu kisichowezekana hata kidogo, Bi. Semeni hakuwa na mpinzani mtaa mzima, aliogopwa na kila mtu, sasa ilikuwaje leo aje kijana, tena alionekana kuwa sharobaro halafu afukuzwe na mwanamke huyo? Labda kama kulikuwa na tatizo jingine.
“Labda alikuwa mchafu...” alisema jamaa mwingine.
“Mh! Kijana alikuwa msafi sana yule,” alisema mwanaume mwingine.
“Au alikuwa mbeya!”
“Kwani alizoeana na watu wengine?”
“Sasa kwa nini afukuzwe?”
“Au naye mchawi?”
“Weeee....hata kama angekuwa mchawi, hawezi kufua dafu kwa Bi. Semeni! Hivi mnamjua mwanamke yule kweli ama mnamsikia tu? Kuna siku mtoto alimpiga na mpira bahari mbaya, akasonya tu, mtoto aliugua wiki nzima...sasa wewe unachezaje na mtu huyo!” alisema jamaa wa kwanza.
Kwao, Bi. Semeni alikuwa tishio, aliogopwa na kila mtu aliyekuwa akiishi hapo Magomeni. Stori kuhusu Bazoka kuhama nyumba hiyo zilikuwa zikiendelea kusikika, na kila mtu aliposikia kwamba ni mwanamke huyo ndiye aliyeamua kumfukuza, hakika walishangaa.
Bazoka aliamua kutafuta nyumba nyingine na kwenda kuishi huko, hakutaka kurudi nyumbani mpaka pale ambapo angehakikisha anammaliza Bi. Semeni, alikuwa na hasira naye kwa kuwa alisikia mara kadhaa alikuwa mchawi, sasa alitaka kummaliza kwa kuwa aliamini kwa kufanya hivyo angewafanya hata watu wengine wawe na amani.
Alichukua ramani ya nyumba nzima, alijua ratiba ya mwanamke huyo, alitaka kummaliza kwa gharama yoyote ile. Alijaribu kujiuliza ni kwa kitu gani alitakiwa kummaliza nacho na jambo pekee alilotaka kutumia kama silaha yake kubwa ni kumchoma visu kadhaa.
Hakuwa na huruma, roho yake ilibadilika, pesa zilimbadilisha kila kitu na ilikuwa ni lazima afanye kila liwezekanalo kuhakikisha ule utajiri aliokuwanao unaendelea kuwepo maishani mwake.
Alichokitaka ni kuwasahaulisha watu, hakutaka kuwasiliana na Frank japokuwa alimtumia ujumbe kwa njia ya simu kwamba mkewe, Sarah alijifungua salama kabisa, alichokuwa akikihitaji ni kuwaondoa watu mawazo kuhusu yeye, wakati wakiwa wamesahau hapo ndipo angekwenda na kummaliza mwanamke huyo.
Ilikuwa ni lazima kupitia njia ya kule nyuma, aingie ndani na kummaliza mwanamke huyo. Siku hiyo ilikuwa ni Jumamosi na kwa kawaida mwanamke huyo alikuwa akishinda nyumbani tu.
Akanunua kisu na kukinoa, kilikuwa ni silaha yake aliyokuwa akiitegemea kwa lengo la kwenda kummaliza mwanamke huyo, alipohakikisha kipo sawa na tayari ilikuwa imepita wiki moja tangu aondoke nyumbani kwa Bi. Semeni, majira ya saa mbili akarudi nyumbani hapo.
Hakutaka kupitia mlango wa mbele, ilikuwa ni lazima kuruka ukuta na kuingia ndani kupitia nyumba. Huko hapakuwa na mtu, japokuwa kulikuwa na uwazi fulani lakini watu waliogopa hata kuisogelea, walimuogopa mwanamke huyo na watu wengi hasa vijana waliokuwa wakitaka kuweka kijiwe kuegemea ukuta wa nyumba hiyo, walichokuwa wakikiona kilikuwa ni mauzauza tu, hivyo hawakuwa wakikaa karibu nayo kabisa.
Hilo lilimpa urahisi sana Bazoka wa kufanya kile alichotaka kufanya, akausogelea ukuta, akaupanda na kuteremkia kwa ndani huku akijitahidi kusisikike sauti yoyote ile.
Mazingira ya hapo uani hayakuwa mazuri kabisa, machafu kwa kuwa Bi. Semeni hakuwa na muda wa kufanya usafi hata kidogo. Aliangalia huku na kule, kulikuwa na mwanga hafifu hivyo akaanza kuusogelea mlango wa kuingia ukumbini, akakishika kitasa na kujaribu kuufungua.
Mlango ukafunguka. Bi. Semeni hakuwa na kawaida ya kufunga milango yake, alikuwa akijiamini kwamba hapakuwa na mwizi yeyote aliyethubutu kuingia na kumuibia, hivyo alikuwa akiiacha bila kuifunga na funguo.
Bazoka akaingia mpaka ukumbini, alisimama huku akiwa ameyategesha masikio yake kusikiliza sauti ya mwanamke huyo, alihitaji kujua alikuwa chumba kipi.
“Nitaua mtu...nimesema nitaua mtu..” aliisikia sauti ya mwanamke huyo kutoka chumbani kwake.
Ndiyo ilikuwa kawaida yake, kila alipokuwa peke yake, kitu alichokuwa akipenda kuongea ni kumwaga damu tu, alikuwa mchawi kupindukia, yaani kuua kwake ilikuwa starehe yake kupita kitu chochote kile.
“Koh koh koh...” alikohoa Bazoka.
Alifanya hivyo makusudi, alitaka mwanamke huyo asikie kikohozi hicho ili ajiulize alikuwa nani. Na kweli ikawa hivyo, baada ya Bi. Semeni kusikia kikohozi hicho, kwanza akanyamaza, akaanza kusikiliza vizuri.
Ni kweli alisikia mtu akiwa anakohoa, hakujua alikuwa nani, hakuamini kama kulikuwa na mtu ambaye angediriki kuingia ndani ya nyumba yake, kila mtu aliyahofu yale ambayo yangemkuta baada ya kufanya hivyo.
Aliponyamaza, napo kukawa kimya, akahisi inawezekana alisikia vibaya hivyo kuendelea kuongea maneno yake ya vitisho. Huku akiendelea, akasikia tena kikohozi, sasa wakati huu akawa na uhakika kwamba mtu aliyekuwa amekohoa alikuwa ndani ya nyumba yake.
Kwanza akaogopa! Sababu iliyomfanya kuogopa ilikuwa moja tu, ilikuwaje mtu kuingia ndani ya nyumba yake bila kuogopa chochote kile? Je, alikuwa akijiamini? Na kama alifika humo na kujikoholesha, kwa nini alifanya hivyo?
Sasa kilichotokea akaanza kuogopa yeye, akahisi kabisa kulikuwa na kitu. Akaanza kujiuliza kama lingekuwa suala jepesi kuufuata mlango na kuufungua kuona kilichokuwa kikiendelea ama atulie chumbani.
“Wewe ni nani?” aliuliza kwa sauti, tena ile iliyojaa hofu.
“Hahaha!” alisikia kicheko tu.
“Wewe nani?” aliuliza, mara hii kwa ukali kidogo.
Hakujibiwa zaidi ya kuona mlango wa chumbani kwake ukianza kufunguliwa, alisimama wima karibu na kitanda chake, mtu aliyekuwa akiufungua alikuwa Bazoka ambaye alichungulia na kumuona mahali alipokuwa amesimama.
Bi. Semeni alimuona mtu akiwa amechungulia kidogo tena kwa haraka sana, halafu akarudi, hapohapo akauona mkono tu wa Bazoka ukiifuata swichi ya ndani kwake humo ambayo ilikuwa karibu na mlango, akaizima.
“Wewe nani?” aliuliza tena mwanamke huyo, hofu ilimtawala mno.
Bazoka akaingia ndani, hakuonekana usoni mwake japokuwa mwanamke huyo alikuwa akimuona, haraka sana akasogelewa pale alipokuwa amesimama.
“Wewe nani?” aliuliza mwanamke huyo, haraka sana Bazoka akakitoa kisu chake kwa lengo la kumchoma mwanamke huyo.
Hata kabla hajamchoma, ni ghafla sana akaanza kusikia upepo mkali ukivuma, kama kulikuwa na miti mingi mahali hapo, huku akijiuliza ni kwa namna gani ghafla kukiwa na upepo mkali namna hiyo, akajikuta akiwa amesimama katikati ya pori kubwa.
Alishtuka, aliangalia huku na kule, alikuwa porini, kisu chake kilikuwa mkononi na hakujua Bi. Semeni alikuwa mahali gani. Upepo ule uliendelea kuvuma mfululizo, ulimchanganya, huku akiwa hajui afanye nini, akaanza kusikia sauti za wanyama, hasa fisi wakilia.
“Mhh!” aliguna.
Akaanza kusikia vishindo kutoka mbele yake, ni kama kulikuwa na mtu aliyekuwa akija kule alipokuwa. Alisimama imara, alitaka kuona ni nani ambaye angefika mbele yake, alikuwa akitetemeka, hapo akagundua kuwa Bi. Semeni hakuwa mtu wa kawaida, ili kummaliza na wewe ulitakiwa kujipanga sana.
Akapigwa na mshangao baada ya vishindo hivyo kuacha, sasa akawa anaangalia macho kwa macho na fisi mmoja mkubwa aliyesimama mbele yake, akaanza kuhesabu sasa ungekuwa mwisho wa maisha yake.
“Hapa ni kukimbia kwanza,” alijisemea.
Hakutaka kubaki mahali hapo, ilikuwa ni lazima kuyaokoa maisha yake, akageuka na kuanza kukimbia, fisi yule aliyekuwa amesimama mbele yake kama hatua ishirini, akaanza kumkimbiza.
Aliruka vipande vya miti, alikimbia kwa kasi kubwa, hakutaka kuangalia nyuma lakini alijua fisi yule alikuwa akija kwa kasi kule alipokuwa akienda, kama angesema asimame basi ilikuwa ni lazima kushambuliwa.
Akakimbia mpaka alipofika sehemu iliyokuwa na ukuta mkubwa kwa mbele, ulikuwa ni mrefu kwa kwenda juu, kama mita ishirini hivi, asingeweza kuupanda, alijiuliza ni kwa namna gani ukuta huo ulijengwa pale porini na wakati hapakuwa na makazi ya watu? Nani alithubutu kufanya kitu kama hicho?
Huku akiwa anajiuliza maswali mengi, fisi aliyekuwa akimkimbiza akamsikia akiwa amefika hapo alipokuwa, umbali kama wa hatua kumi kutoka aliposimama, japokuwa kulikuwa na giza totoro lakini aliweza kuyaona macho ya fisi huyo, yalikuwa makubwa na yaliyong’aa sana.
“Hapa ni kupambana tu!” alijisemea huku akiwa na hofu, alipojiangalia mkononi, kisu chake kilishikwa vyema, sasa alikuwa na jukumu la kupambana na fisi huyo, akiwa amejiandaa vilivyo, akashangaa kuona fisi wengine watatu wakiongezeka mahali hapo, sasa wakawa fisi wanne ambao alitakiwa kupambana nao.
“Mh! Nitaweza kweli? Ila acha, nitapambana kiume,” alijisemea, sasa fisi wale wakaanza kumsogelea. Naye akajiandaa vilivyo.


Je, nini kitaendelea
 
NYEMO CHILONGANI
UCHAWI WA BILIONEA BAZOKA
0718069269

SEHEMU YA 20

Wale fisi waliendelea kumsogelea Bazoka hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya mahali hapo, alikuwa akiogopa lakini ghafla huku akiwa hajui ni kitu gani kimetokea, mwanga kama wa radi ukapiga, fisi mmoja akapigwa na kubabuliwa, akaanguka chini, akafa.
Akashangaa kuhusu radi hilo, likapiga jingine, hapohapo likatokea jitu kubwa mfano wa nguzo ya umeme, lilikuwa na mwili mkubwa, mikono yake ilikuwa mikubwa huku akiwa na makucha marefu.
Mwili wake ulikuwa na manyoya, alitisha na sura yake ilikuwa kama ya Mbweha, meno yalitokeza kwa nje, wale fisi badala ya kumsogelea Bazoka, sasa wakageuka na kuliangalia hilo dudu lililosimama pembeni yao.
Kwa kutumia mikono yake mirefu, hapohapo akaanza kupambana na hao fisi, kwake wala haikuwa kazi kubwa hata kidogo, aliwashambulia mara moja tu, fisi wawili walipigwa na kufa na mmoja alikwanguliwa ubavuni na makucha ya jitu lile, akaanguka chini, akaugulia maumivu na kukimbia mahali hapo kuelekea porini.
Bazoka alibaki akitetemeka, hakuamini kile alichokuwa akikiona mahali hapo, alihisi kama alikuwa kwenye njozi moja ya kutisha sana, iliyomfanya kusisimka mwili wake wote. Sasa akawa anaangaliana na jitu lile, alitamani kukimbia lakini miguu ilikosa nguvu kabisa.
Halikuzungumza, likageuka na kuondoka zake huku akimwacha Bazoka akimwangalia. Hakujua nini kilitokea lakini ghafla akajikuta akiwa ndani ya chumba cha Bi. Semeni, mwanamke huyo alikuwa palepale kitandani, alikuwa akitoka damu nyingi ubavuni mwake, hapo akili ya Bazoka ikamwambia kwamba ndiye yule fisi aliyekuwa amekimbia.
“Siwezi kukucha,” alisema Bazoka, haraka sana akamsogelea, akamchoma kisu tumboni, mara mbili, akakichomoa, akaufungua mlango na kuondoka nyumbani hapo kupitia kulekule ukutani uani.
Damu zilikuwa zimetapakaa kitandani, Bi. Semeni aliuawa vibaya, japokuwa alikuwa mchawi wa kutisha lakini alikutana na mtu aliyekuwa na nguvu zaidi yake.
Watu hawakujua kilichokuwa kimetokea, ilikuwa ni usiku na kubwa zaidi waliogopa kuingia ndani ya nyumba hiyo. Siku iliyofuata kulikuwa na misiba mitatu mtaani, kulikuwa na wanaume wawili na mwanamke mmoja walikufa wakiwa kitandani.
Kila mmoja alishangaa, vilikuwa ni vifo vya ghafla ila kilichowashangaza wengi ni kufa kwa siku moja, tena wote walikufa wakiwa usingizi, watu hao ndiyo walikuwa wale fisi waliofika kwa ajili ya kumsaidia Bi. Semeni.
Mwanamke huyo hakuonekana, watu walikuwa wakijiuliza sababu zilizofanya kutokuonekana lakini hapakuwa na yeyote aliyejua chochote kile. Walizoea kumuona akiwa nje akisuka ukili lakini hakuwa akionekana tena.
Baada ya siku ya tatu kuingia ndipo wakaanza kusikia harufu kali ya mzoga ikitokea ndani ya nyumba ile. Kila mmoja alishangaa, hawakujua ulikuwa mzoga wa nini, ilikuwa ni rahisi kusema wa paka ama panya lakini kila walipokuwa wakiijadili harufu ile, haikuwa ya kawaida.
Kuingia ndani ya nyumba hiyo waliogopa, halikuwa jambo la kawaida kuingia kichwa kichwa ndani ya nyumba ya mwanamke mchawi kama Bi. Semeni, ulitakiwa kujipanga vilivyo.
Watu hao wakatoa taarifa katika ofisi ya serikali ya mtaa ambao hao ndiyo waliofika mahali hapo na kuingia ndani kuona kulikuwa na nini. Nje ya nyumba hiyo kulikuwa na watu zaidi ya mia moja, kila mmoja alitaka kujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea ndani.
Wengi walisema kulikuwa na maiti, inawezekana Bi. Semeni aliamua kumuua mtu na mwili huo kuuacha humo. Mwenyekiti wa serikali ya mtaa alipoingia na watu wake mpaka chumbani mule, hawakuamini walichokiona.
Mwili wa Bi. Semeni ulikuwa kitandani, kulikuwa na damu zilizoganda, mwili uliharibika na nzi walikuwa wakiuzingira tu. Hawakuugusa wala kugusa chochote kile, wakapiga simu polisi ambao walifika hapo baada ya dakika kadhaa.
Wakaingia ndani, wakaupiga picha, wakafanya mambo yao na kuuchukua. Watu waliposikia kwamba ni Bi. Semeni ndiye aliyekuwa amekufa ndani ya chumba chake, kila mmoja alishangilia kwa furaha, hapakuwa na mtu aliyeamini kama mwanamke huyo alifariki dunia.
Hawakuwa wakimpenda, aliwafanya kutokuwa na amani hata kidogo, kila mtu alitamani kuona siku moja anakufa, na siku hiyo ndiyo iliwadia, hatimaye yule mchawi aliyekuwa akiwatesa alikufa, inasemekana mwili wake ulichomwa kisu.
Kila mmoja alibaki akiwa na mshangao, hawakujua ni nani alimchoma kisu, wengine walisema inawezekana alijichoma mwenyewe kama kujimaliza lakini hilo likatoka vichwani mwao kwa sababu kisu hakikuwepo.
“Huyu ameuliwa!” alisema jamaa mmoja.
“Na nani? Kuna mtu anaweza kumuua? Atakuwa amejimaliza mwenyewe,” alisema mwanaume mwingine.
“Hapana! Angekuwa amejichoma kisu na kujiua, kisu kingeonekana,” alimwambia.
“Ila kweli!”
“Itakuwa mtu aliingia, akamuua na kutokomea zake!” alisema mwanaume huyo.
“Sasa atakuwa nani? Yaani uingie kwa Bi. Semeni, umuue na yeye anakuangalia tu!” alisema jamaa huyo.
“Sijajua! Ngoja tusikilize polisi watasemaje,” alisema.
Kamanda Masumbuko akapelekewa taarifa ya mauaji hayo, alichanganyikiwa, hakujua ni kitu gani hasa kilichotokea mpaka mtu aingie ndani ya nyumba ya mwanamke huyo na kumuua.
Ripoti aliyopelekewa mezani kwake aliambiwa pia kwamba mwanamke huyo alikuwa mchawi mkubwa, hakupendwa na kifo chake kiliwafanya watu wengi kushangilia, inawezekana kulikuwa na mtu aliyejitoa na kumuua.
Kichwa cha Kamanda Masumbuko kikamkumbuka mtu mmoja tu, Maganza, akampigia simu na kutaka kuonana naye ofisini kwake, hilo halikuwa tatizo, baada ya dakika kadhaa, mwanaume huyo alikuwa humo.
“Kuna taarifa nimeletewa!” alisema huku akimwangalia.
“Taarifa ipi mkuu?”
“Kuna mwanamke ameuawa hapo Magomeni!”
“Mwanamke gani?”
“Sijajua ni yupi ila kwa taarifa hizo zinasema alikuwa akichukiwa na mtaa mzima!” alimwambia.
“Kwa sababu gani?”
“Ulozi! Nasikia alikuwa anapaa usiku!”
“Na ndiyo sababu iliyopelekea watu washangilie?”
“Kabisa. Sasa ninahitaji ulifuatilie hili suala!” alimwambia.
“Haina shida. Na mwili upo wapi?”
“Hospitali ya Mwananyamala!”
“Sawa. Acha nikauone kwanza,” alisema.
Maganza hakutaka kupoteza muda, haraka sana akaondoka na kuelekea huko hospitalini. Kichwani mwake kulikuwa na mambo mengi, hakuwa amemalizana na suala la mtoto Yusufu, tayari mezani kwake kulipelekwa kiesi nyingine kabisa.
Kwa maelezo ya bosi wake alimwambia kifo cha mwanamke huyo kiliibua furaha sana mtaani kwa sababu alikuwa mchawi, kwa maana hiyo inawezekana kabisa kulikuwa na mtu aliyeingia ndani ya nyumba hiyo na kumuua kwa makusudi kabisa kwa sababu hakupendwa.
Alichukua dakika kadhaa akafika huko hospitalini, akateremka na kumfuata mkunga mkuu na kumwambia kilichompeleka hapo, akachukuliwa na kupelekwa mpaka mochwari na kuonyeshwa mwili wa Bi. Semeni.
Aliuangalia, aliangalia jeraha la kisu kwa umakini, lilikuwa kubwa, hilo lilimuonyesha hakuwa amechomwa mara moja, hapakuwa na kisu kilichokuwa na uwezo wa kuchoma na kuacha tundu kubwa namna hiyo.
“Huyu alichomwa mara kadhaa,” alisema huku akimwangalia daktari.
“Kwa sababu gani?”
“Angalia tundu! Na mtu aliyemchoma anatumia mkono wa kulia,” alisema.
“Umejuaje?”
“Kama angekuwa antumia mkono wa kushoto, angemchoma upande huu wa kulia, ukiona mtu amechomwa tumboni, upande kidogo wa kushoto, jua muuaji anatumia mkono wa kulia,” alimwambia, daktari akashangaa.
“Ila pia ana jeraha ubavuni!” aliambiwa.
“Jeraha? Hebu tulione,” alimwambia, daktari akafungua zaidi shuka, ni kweli mwili wa Bi. Semeni ulikuwa na majeraha kama ya kucha mbili kubwa zilizopita ubavuni mwake.
“Kwa jinsi ninavyoona ni kama kucha!” alisema daktari.
“Kucha? Kuna kucha zinazoweza kujeruhi pakubwa kama hivi?” aliuliza huku tayari akiwa na majibu kwamba hazikuwa kucha.
“Sasa tutasemaje? Ama alichanwa na kisu pia?”
“Hapana! Hizi si alama za kuchanwa na kisu! Hebu subiri niende kwake, naweza kupata majibu,” alisema na kuondoka mahali hapo.
Sasa akachanganyikiwa! Hakujua kilichokuwa kimetokea, kuhusu jeraha la kuchomwa na kisu ilikuwa ni rahisi sana kujua kilichotokea lakini yale majeraha ya ubavuni yalimuweka kwenye wakati mgumu sana.
Akaondoka na kuelekea Magomeni, alipofika, haraka sana akateremka na kuifuata nyumba hiyo. Majirani walikuwa wakimwangalia, kwa jinsi alivyokuwa akitembea, kila mmoja alijua alikuwa polisi.
Akaingia mpaka ndani, akaanza kuangalia huku na kule, alikuwa makini kabisa. Akaingia mpaka ndani ya chumba alichouawa Bi. Semeni na kuanza kuangalia huku na kule, kulikuwa na harufu kali ya dawa iliyopulizwa na polisi kuondoa harufu mbaya ya mzoga.
“Alichomwa kisu akiwa kitandani,” alijisemea huku akiendelea kuangalia chumbani mule.
“Ile mikwaruzo ubavuni aiipatia wapi?” alijiuliza huku akiendelea kukikodolea macho chumba kile.
Aliporidhika, akatoka na kusimama ukumbini. Sasa akaanza kujiuliza ni kwa namna gani muuaji huyo aliingia chumbani humo. Kuingia kwa mlango wa mbele, alikataa hilo, mara nyingi wauaji wanaokwenda sehemu fulani kufanya mauaji huwa hawapitii mlango wa mbele kwa sababu hawakutaka kuonekana.
“Labda alipitia mlango wa nyuma,” alijisemea na kuelekea uani.
Akaanza kuangalia huku na kule, kwa jinsi mazingira yalivyokuwa alikuwa na uhakika hapakuwa na mtu yeyote aliyeingia lakini kwenye kuangalia akauona ukuta ukiwa na alama fulani nyeusi, ilikuwa kubwa.
“Muuaji alipitia ukutani! Hii ni alama ya kiatu alipokuwa akiuparamia ukuta huu,” alijisemea huku akiwa ameusogelea ukuta na kuiangalia alama ile.

Je, nini kitaendelea
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom