ELNIN0
JF-Expert Member
- Nov 26, 2009
- 4,161
- 1,460
Fred Mpendazoe: Vita ya ufisadi ni endelevu
Kulwa Karedia
TANGU Bunge la Jamhuri wa Muungano wa Tanzania lilipoanza mkutano wa 16 mjini Dodoma, tumeshuhudia wabunge hasa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wakisimama na kutoa hoja nzito dhidi ya serikali. Mmoja wa wabunge waliotoa mchango na kusisimua Bunge ni Mbunge wa Kishapu, Fred Mpendazoe (CCM).
Kutokana na hali hiyo, gazeti hili liliamua kumtafuta kufanya naye mahojiano yaliyolenga zaidi katika utekelezaji wa ilani ya uchaguzi, hali ya kisiasa kwenye Jimbo la Kishapu na masuala ya kitaifa pamoja na changamoto anazozikabili. Yafuatayo ni mahojiano kati ya mgunge huyo na mwandishi wetu
Swali: Imebaki miezi 15 kabla ya uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2010 kufanyika, unasemaje kuhusu utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi Jimboni kwako.
Jibu: Ninashukuru kunipa nafasi ya kunihoji juu ya utekelezaji wa ahadi tulizozitoa kwa wananchi wakati tunaomba kura. Utekelezaji wa ahadi hizo ambazo zipo kwenye Ilani ya Uchaguzi CCM hadi sasa utekelezaji unaendlea vizuri. Kwenye sekta ya barabara tumefanikiwa kujenga barabara ya Bunambiyu hadi Mhunze yenye umbali wa kilomita 24, zimebaki kilomita 34, barabara ya kwenda Kijiji cha Ngwanhiri, na barabara ya kwenda Lubaga kutoka Mhunze.
Kwa upande wa sekta ya afya ujenzi wa hospitali ya wilaya unaendelea vizuri. Pia tumeweza kupata fedha kutoka Japan kwa ujenzi wa Zahanati ya kijiji cha Igaga na Itilima.
Katika sekta ya elimu ujenzi wa sekondari za kata umekwenda vizuri kwa kushirikiana na wasani ambao wamekuwa wakisaidia kwa hali na mali. Kuhusu sekta ya maji tumefanikiwa kujenga mabwawa katika vijiji vya Seke- Ididi kwa sh kwa milioni 340, bwawa la Bupigi na bwawa la Mwamashimba.
Kwa upande wa kilimo tumefanikiwa kwenye ukarabati wa mradi wa umwagiliaji wa Itilima, mradi ambao ulikuwa umesimama kwa kipindi kirefu, umegharimu kiasi cha sh milioni 200.
Vile vile tunayo matumaini ya kufanikiwa kupata usajili wa serikali za Vijiji nane katika mwaka wa fedha unaoisha Juni 2009 na pia tumedhamiria ujenzi wa makao makuu ya wilaya na Halmashauri Kishapu unaendelea sambamba na suala la kupeleka umeme makao makuu linaendelea vizuri, natarjia fedha kiasi cha milioni 300 zinaweza kutolewa.
Swali: Kuna changamoto zipi unazoziona katika utekelezaji wa ahadi au Ilani ya Uchaguzi?
Jibu: Katika utekelezaji wa ilani ya uchaguzi zipo changamoto mbalimbali tulizokutana ambazo ni pamoja na serikali kuu kuchelewa kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya kutoka Kolandoto hadi Meatu kupitia Mhunze na barabara ya kutoka Mwigumbi hadi Maswa. Mpaka sasa ujenzi haujaanza. Tatizo jingine ni miradi mingi ya kilimo kupitia ASDP imechelewa kuanza, mfano Mradi wa Umwagiliaji Ngeme, Jijongo na Bulekela – utekelezaji bado lakini unasababishwa zaidi na urasimu wa serikali hivyo unasababisha wananchi kukata tama. Changamoto nyingine ni kwamba vijiji vingi, kata na tarafa ni vikubwa hivyo watendaji wa vijiji na kata hizo hupata shida kuwafikia watu na kuwahamasisha juu ya kushiriki miradi ya maendeleo. Kuna vijiji vyenye kaya zaidi ya 600 wakati kijiji kinatakiwa kiwe na kaya 250 tu. Hivyo kutokana na ukubwa wa vijiji uhamasishaji wa maendeleo unakuwa mgumu.
Changamoto nyingine ni uchangiaji wa miradi ya maendeleo. Uchangiaji huo ni hafifu na pia tatizo kubwa ni wananchi kutosomewa mapato na matumizi ya michango yao. Vile vile serikali za vijiji zinashindwa kufanya mikutano kama inavyotakiwa. Hivyo ushiriki wa wananchi katika miradi ya maendeleo ni hafifu, ndiyo maana kuna fedha zilizotolewa mwaka 2008 hazijatumika. Jimbo lake linakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na mgogoro wa muda wa zaidi ya miaka miwili kati ya menejimenti ya Halmashauri ya Kishapu na Mwenyekiti wa Halmashauri. Mgogoro huu umeathiri sana utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi.
Anasema tatizo jingine ni swala la la kuwa na migodi ya madini. Maeneo yote yenye migodi ya madini ikiwemo Wilaya ya Kishapu yana malalamiko ya wananchi wanaoishi karibu na migodi juu ya fidia ndogo waliyolipwa au kutolipwa fidia kabisa na mahusiano hafifu kati ya Migodi na wananchi.
Swali: Hali ya kisiasa ikoje kwenye Jimbo la Kishapu ukizingatia kuna taarifa ya vipeperushi vya kukukashifu vinatawanywa jimboni kwako?
Jibu: Nashukuru sana kwa swali hili. Ningependa kueleza kwamba mimi kama Mbunge ambaye nimetokana na Chama cha Mapinduzi ninashirikiana vizuri na viongozi wa chama kwenye wilaya na sina tatizo lolote. Nimefanya ziara kadhaa na kila ninapofanya ziara mara kwa mara ninakuwa na viongozi wa chama. Pia nimechangia mambo mengi kwenye chama na ndiyo maana mwaka 2008 niliweza kutunukiwa cheti juu ya uchangiaji wa maendeleo katika chama. Cheti hicho kilitolewa mwezi Februari 2008. Kati ya waliotunukiwa ni pamoja na aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya, E. Mlaki. Hivyo kwa ujumla sina matatizo na chama wilayani. Aidha, sina mgogoro na uongozi wa chama wa mkoani. Ni kweli kumekuwepo vipeperushi vinavyotupwa sehemu za minada kwenye Wilaya ya Kishapu na vilianza kutupwa Mei 20, 2009 nilipokuwa na ziara Maganzo na baadae vilitupwa Mhunze, Nyasamba, Mwamishoni, Mipa na Mwigumbi, labda (nieleze) baadhi ya maneno yaliyoandikwa kwenye vipeperushi na baadae nieleze wanaotupa vipeperushi hivyo ni akina nani. Vipeperushi hivyo vilikuwa vinasomeka hivi: Unazungumzia juu ya ufisadi hatujakutuma na yanadhalilisha chama. Kulikuwa na vipeperushi vingi, lakini vipeperushi vingi vilikuwa na maneno hayo hayo. Naomba nijibu kwa muhtasari tu vipeperushi hivyo.
Ukisoma maneno yaliyopo kwenye vipeperushi hivyo utaweza kupata mwanga waliotayarisha vipeperushi ni kina nani. Nadhani wananchi wa Jimbo la Kishapu wameisha pata mwanga ni nani walioandika vipeperushi hivyo na kwa maslahi ya akina nani. Gazeti moja la kila siku (si Tanzania Daima), Mei 18, 2009 lilikuwa na habari juu ya mafisadi kutenga bilioni 2 kwa ajili ya kuhakikisha wabunge wanaopinga ufisadi wanaondolewa kwenye Ubunge katika uchaguzi mkuu ujao mwaka 2010. Kwenye habari hiyo yalitajwa majina na jina langu lilikuwemo. Mei 20, 2009 nilikuwa na ziara Maganzo, tukakuta vipeperushi vimetupwa na moja ya vipeperushi vilisema "Mbunge usitutenganishe wananchi na wawekezaji" na kingine kikasema "Hotuba zako juu ya ufisadi zinakithalilisha chama cha Mapinduzi", ni dhahiri utaona walioandika ni watu wa aina gani.
Katiba ya CCM inapinga masuala ya rushwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inapiga vita rushwa na utajiri wa taifa kuwa mikononi mwa watu wachache. Hivyo hawa wanaotaka kuondoa wabunge wa wanaopiga vita ufisadi ni adui wa CCM na pia ni adui wa demokrasia, kwani wanataka kuua demokrasia. Hawa wanaochukia vita dhidi ya ufisadi wanataka kuweka watu wao ambao watatetea maslahi yao na si maslahi ya wananchi wanyonge.
Moja ya mambo ambayo nimekuwa nikisisitiza kwenye mikutano wakati wa ziara zangu jimboni ni suala la kuwataka wananchi waelewe kwamba maendeleo ya Kishapu yataletwa na Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu kama itasimamiwa vizuri. Serikali inapeleka fedha nyingi za miradi ya maendeleo kwenye halmashauri zetu ikiwamo Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, lakini hali ya matumizi si nzuri, Hivyo ipo haja ya wananchi kujua kinachoendelea kwenye halmashauri zao.
Maendeleo ya wilaya yatategemea mno utendaji mzuri wa halmashauri na si kutokana na ufadhili wa mtu mmoja mmoja kama watu wengi walivyozoea.
Niliwaeleza wananchi wangu wahakikishe migogoro kwenye halmashauri inaisha na badala yake uwepo ushirikiano kati ya Madiwani na watendaji au wataalamu wa Halmashauri, bahati mbaya kwenye halmashauri kulikuwa na mgogoro wa muda mrefu na wananchi wanafahamu chanzo chake kwani tume ziliishatumwa kufuatilia.
Kwa mfano, kata anayotoka vijiji vya Seke Bugoro, Ididi, Mipa, Mwashinonghela vimekataa kuchanga hadi wasomewe matumizi wa michango yao. Hivyo si msimamo wangu tu ni msimamo wa wananchi wote. Nimechukua hatua ya kuieleza kamati ya Hesabu ya Serikali za Mitaa na imeahidi kufuatilia suala hilo.
Swali: Unawashauri nini wananchi juu ya vipeperushi hivyo?
Jibu: Mimi nasema wananchi wanafahamu utendaji wangu, uwezo wangu na nia ya dhati ya kuhakikisha wilaya yetu inapiga hatua kimaendeleo. Nawaomba wananchi wafahamu kwamba kuna watu wangependa kupata mbunge ambaye hatatetea wananchi bali atakuwa ni kibaraka wa wale watakaomweka ili maslahi yao yalindwe na wananchi wakose wa kuwatetea. Haya yote yanayotokea kutokana na msimamo wangu wa kutaka wananchi wasionewe na kupiga vita ufisadi. Haya ni mapambano, nawaomba wananchi waendelee kuniunga mkono kwani ni watu wachache wenye ubinafsi ndio wanaoshiriki kusambaza vipeperushi hivyo, ili tuweze kuinua jimbo letu.