Dunia haijawahi kuwa na upendeleo na mtu. Wale watafutao hupata, nao hutakiwa kutafuta usiku na mchana wakibisha na kuomba. Hata kwenye falsafa ya kiti, hutoruhusiwa kwenda kukalia kiti si cha mbele wala cha nyuma bila ya kuwa na mwaliko, mwaliko ambao umeuchangia kwa namna moja ama nyingine. Ukielewa falsafa hii kiundani zaidi hakuna siku utatoka mbele za watu na kulalamika kuwa hali imekuwa ngumu.
Hakuna Taifa duniani ambalo kiongozi wake anapochaguliwa anapaswa kwenda wapa watu wake maendeleo bali kwa kuwatumia watu hao hao kuwaonyesha dira ya kule wanakopaswa kwenda na kwa kutumia rasilimali walizonazo wenyewe, awakusanye ili wajenge miundombinu sahihi kwa ajili ya maendeleo yao na shughuli zao.
Na hili ni agizo ambalo hata ulimwengu wa roho unalisisitiza. Pesa, magari, majumba, nk nk, havikuumbwa bali viliachwa kwa mwanadamu ili kwamba yeye atakayechukua hatua na kufanya basi atafanikiwa. Watu wote tuliumbwa tu uchi na tukapewa akili na utashi kuja kuvitumia vitu vya duniani kwa mustakabali wetu. Na zaidi tukaambiwa alaaniwe yeye amtegemeaye mwanadamu mwenzake. Itupase sasa kuacha kuhamisha lawama kwa mapungufu yetu wenyewe.
Tuhamishe lawama ikiwa rasilimali zetu na jitihada zetu zitatumiwa vibaya na wachache kwa manufaa yao binafsi, lakini pia tukubali ukweli kwamba katika maisha kuna wakati yatupasa kufunga mikanda kwa ajili ya maisha yetu ama mustakabali wa vizazi vyetu. Sio kila mti utakaoupanda basi utapaswa kula matunda yake.
Hata ulaya wanaoifaidi sio wale walioijenga.