Fungueni kwa kuona mwezi, nyie mmeona mwezi au mmepewa taarifa, kwanini mnatumia vyombo vya habari kusikia kuhusu mwezi ulioandama nchi tofauti na yako?
Waislamu wa dunia nzima wote ni ndugu.
Waislamu waliopo mashariki mwa Dunia na waliopo magharibi, kusini na kaskazini wote ni ndugu.
Mungu wao ni mmoja, mtume wao ni mmoja, kitabu chao ( Qurani ) ni kimoja na kibla Chao ni kimoja.
Ni jambo jema wakifunga na kufungua pamoja.
Mipaka kati ya nchi moja na nyingine imewekewa na wanasiasa kwa faida na maslahi ya kisiasa .( Nchi nyingi barani Afrika mipaka yake imewekwa na wakoloni)
Na mipaka hii hubafilika mara kwa mara kwa maslahi na faida za kisiasa.
Kwa msimamo wa kwamba KILA NCHI NA MWEZI WAKE! hadi tarehe 25 April 1964 waislamu wa Tanganyika walikuwa na mwezi wao na waislamu wa Zanzibar walikuwa na mwezi wao.
Mara baada ya muungano April 26 , 1964 mwezi mmoja ukazamishwa baharini ukapotea ( sina uhakika kama mwezi uliopotea ni ule wa Tanganyika au mwezi wa Zanzibar ndio uliopotea!)
Hadi mwaka 2010 waislamu wa Sudani ya kusini na kaskazini walikuwa wanafunga kwa mwezi mmoja kwa kuwa Sudani ilikuwa moja tu bila kujali kwamba kuna kusini na kaskazini.
Kutokana na migogoro ya kisiasa mwaka 2011 Sudani ya kusini ikajitenga toka Sudani ya kaskazini.
Kwa msimamo wa KILA NCHI NA MWEZI WAKE waislamu wa Sudani kusini ikabidi watafute mwezi wao kwakuwa hawawezi kufunga kwa mwezi ulioandama Sudani ya kaskazini wakati hiyo ni nchi tafauti.
Kwa maslahi na faida za WANASIASA yaliyotokea Sudani siku moja yaweza yakatokea Tanzania.
Kwa maslahi na faida za WANASIASA haitashangaza siku moja kuwa na Tanzania ya mashariki na Tanzania ya magharibi, au Tanzania ya kusini na Tanzania ya kaskazini . Je itakuwa kila nchi zikitengana tunatafuta mwezi mpya na zikiungana mwezi mmoja tunauzika?!