SEHEMU YA 32
Ofisini hakukukalika tena, Mapoto alichanganyikiwa, kwa simu aliyopigiwa, alihisi kabisa kulikuwa na tatizo shuleni hasa kwa mtoto wake Irene. Akachukua koti lake, hata kuuweka mkonga wa simu sehemu husika hakukumbuka, akatoka, hakumuaga ‘secretary’ wake, akatoka na kwenda nje ambapo akaingia ndani ya gari lake.
Dereva hakuwemo garini, alikuwa katika mgahawa uliokuwa hapo ofisini akinywa kahawa. Hakutaka kusubiri na wala hakutaka kumuita, akachukua ufunguo mwingine aliokuwanao, akaliwasha na kuondoka mahali hapo.
Alichanganyikiwa, hata uondokaji wake haukuwa wa kawaida, watu wote waliouona uondokaji ule wakawa na wasiwasi kwamba kulikuwa na kitu kimetokea.
Njiani, aliendesha kwa mwendo wa kasi, akaingia katika barabara iliyokuwa ikiruhusu magari kwenda kwa mwendokasi kuanzia 90 na kuendelea, akakanyaga mafuta kwa kasi, alichokuwa akikihitaji ni kuwahi huko, alitaka kuona ni kitu gani kilitokea.
Alichukua dakika kumi mpaka kufika shuleni ambapo geti likafunguliwa, hata hakuzima gari, akateremka na kuelekea katika ofisi ya mwalimu mkuu, alitaka kujua ni kitu gani kilitokea.
Alipofika huko, macho yake yakatua kwa mtoto wake, Godwin ambaye baada ya kumuona, akainuka kitini, akamkimbilia na kumkumbatia huku akilia mno.
“Kuna nini?” alimuuliza lakini Godwin hakujibu zaidi ya kuendelea kulia tu.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo akamkaribisha, hakutaka kuzungumza kitu chochote kuhusu Irene, alimwangalia Mapoto, kwa jinsi alivyoonekana, alionekana kuwa na hofu kubwa.
“Mtoto wangu yupo wapi?” aliuliza Mapoto.
“Kuna kitu inabidi tuzungumze,” alisema mwalimu mkuu.
“Kitu gani? Kwanza niambieni mtoto wangu yupo wapi,” alisema Mapoto kwa sauti kubwa iliyowafanya walimu wawili kuingia humo kwani walihisi kwamba kulikuwa na fujo.
“Ndiyo tunahitaji kuzungumza kuhusu hilo,” alisema mwalimu mkuu.
“Ila yupo hai?”
“Ndiyo! Yupo hai! Cha msingi nisikilize kwanza,” alisema mwalimu huyo.
Hakutaka kumficha, alimwambia ukweli kwamba mtoto wake, Irene hakuwa kwenye hali nzuri.
Wakati wakiwa darasani, alipanda juu ya kiti huku akicheza na wenzake lakini kwa bahati mbaya alidondoka baada ya viatu vyake kuteleza.