SEHEMU YA 91
“Kumbe ndiyo hivyo! Sawa. Sasa fanyeni kitu kimoja,” alisikika mwanaume huyo.
“Ndiyo bosi!”
“Muueni na muuache mwili wake hapohapo,” alisikika mwanaume huyo.
“Sawa. Hakuna tatizo!”
Jamaa yule akarudi ndani ya gari na kuwapa ishara wenzake juu ya kile kilichotakiwa kufanywa. Juma hakujua lakini kwa namna wanaume wale walivyokuwa wamebadili mikao yao akajua tu kwamba kulikuwa na kitu kinataka kutokea.
“Jamani! Nimewaambia ukweli! Naomba mniruhusu niondoke,” alisema Juma.
“Boka! Kazi kwako!” alisema mwanaume mmoja, mwenzake aliyeitwa Boka akatoa kitambaa kutoka mfukoni mwake na kumkamata Juma na kumziba pua na mdomo kwa kutumia kitambaa kile.
*** Moyo wa Rosemary ukawa na amani tena, alifurahia lakini kilichokuwa kikimsumbua ni juu ya mwanaume huyo aliyekuwa ameahidi kumsaidia, hakumfahamu, hakujua alikuwa nani lakini kwa mawazo yake, akagundua kwamba alikuwa Rais Bokasa ambaye hakutaka kugundulika kama alikuwa akimsaidia.
Hakuacha kumpigia simu, alipoona haipatikani, akamtumia ujumbe mfupi wa kumshukuru kwa kile alichokuwa amemfanyia kwani alikata tamaa na kuamini kama ndiyo ungekuwa mwisho wake lakini kwa kutumia fedha zake aliweza kumsaidia kulimaliza suala la nyumba.
Kila siku alikuwa akitumiwa kiasi cha fedha, hakujua kilipotoka lakini kila alipokuwa akiangalia kwenye akaunti yake benki, aliona akiwa ameingiziwa kiasi kikubwa cha fedha.
Hicho ndicho kilichoyaendeleza maisha yake, hakutaka kuona watoto wake wakipata tabu, alitaka kuona wakiendelea kusoma katika shule nzuri na za gharama kwa kuwa tu alikuwa na fedha ambazo aliamini kwamba zilitoka kwa Rais Bokasa.
Siku zikaendelea kukatika, baada ya miezi miwili ya msaada wa kifedha, ghafla msaada huo ukakatika, hakukuwa na fedha zilizoingizwa katika akaunti yake. Hakujua sababu iliyomfanya Rais Bokasa kuchukua uamuzi huo, akajipa moyo kwamba labda kulikuwa na vitu vimeingilia hivyo kusubiri na kusubiri lakini hali haikubadilika, hakikuingia kiasi chochote cha fedha katika akaunti yake.