SEHEMU YA 87
Wakati Juma akiondoka, wanaume wale hawakutaka kumfuatilia kwa ukaribu, walichokifanya ni kutulia ndani ya gari lao kisha kumwacha mpaka atakapoingia ndani ya gari lake, alipofanya hivyo, wakaanza kumfuata.
“Kuna kitu!” alisema jamaa mmoja.
“Hata mimi nahisi! Hebu tumfuatilie, atatuambia ni kitu gani kinaendelea!” alisema jamaa mwingine.
Juma hakuwa na habari kama alikuwa akifuatiliwa kwa nyuma, akaingia kwenye barabara ya lami na kuondoka huku akielekea maeneo ya Namanga huku lengo lake likiwa ni kutaka kuelekea Kinondoni alipokuwa akiishi.
Wakati akiwa amekwishafika maeneo hayo ya Namanga, karibu na kona ya kuelekea ubalozi wa Marekani, akashtukia gari moja aina ya Range SUV jekundu likija na kusimama mbele yake.
“Kuna nini?’ alijiuliza lakini hata kabla hajajijibu, milango miwili ya gari lile ikafunguliwa, wanaume wawili waliokuwa na bastola mikononi mwao wakateremka na kumfuata Juma.
“Shuka chini,” alisema jamaa mmoja huku akiwa amevunja kioo.
“Nimefanya nini?”
“Paaa…” risasi ikapigwa hewani, watu wote waliokuwa wakishangaa huku wakitamani kujua kitu gani kinaendelea, wakaanza kukimbia.
“Jamani msiniue!”
“Basi teremka.”
“Sawa!” alisema Juma huku akitetemeka.
Akateremka, wakamchukua, wakamuingiza ndani ya gari lao na kuondoka naye mahali hapo. Watu wote waliokuwa wamejificha, wakaanza kujitokeza huku wengine wakilaumu kwamba kwa nini polisi wa Kituo cha Osterbay hawakutokea na wakati hawakuwa mbali na mahali ambapo risasi ilipigwa?
“Wale sio majambazi?” aliuliza jamaa mmoja.
“Majambazi! Majambazi gani wanavaa suti?” aliuliza jamaa mwingine, wakati huo gari lile lilifika ubalozini, likakata kulia na kuanza kuelekea Mikocheni huku muda wote huo Juma akilia kuomba msamaha japokuwa hakujua alifanya nini.
*** Bilionea Adam Matiku alikuwa nyumbani kwake ametulia, alichokuwa akikisubiri ni ripoti kutoka nyumbani kwa Mapoto ambapo nyumba ya marehemu huyo ilikuwa ikipigwa mnada huku akiwa amemuandaa rafiki yake, Othman Ngolisho kwa ajili ya kuinunua nyumba hiyo.