SEHEMU YA 51
Hapo alipokaa kwenye ndege alikuwa na mwanaume mmoja, alikuwa mtu mzima kidogo, walianza kupiga stori na kuzungumza mambo mengi. Walichangamkiana na mzee yule aliposikia kwamba alikuwa mwandishi wa habari, alifurahi zaidi.
“Nitataka kuanzisha gazeti langu la siasa, nadhani nitafanya mawasiliano na wewe ili uje kunipa mawazo juu ya nini cha kufanya,” alisema mzee huyo huku akiwa kwenye tabasamu pana.
Wakakubaliana, walipofika Dar es Salaam, ndege ikaanza kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere. Iliposimama, wakainuka na kuanza kuelekeea nje.
“Nina mizigo mingi sana, unaweza kunibebea mmoja hadi nje?” aliuliza mzee huyo.
“Hakuna shida.”
Wakaelekea sehemu ya kuchunguzia mizigo yao, walipoichukua, mzee yule akampa begi lake Matamshi ili amsaidie mpaka nje ambapo angechukua teksi na kuelekea nyumbani.
Huku akiwa na begi lile na kupiga hatua nje, ghafla akashtuka akisimamishwa na polisi wawili waliokuja mbele yake. Mzee yule hakusimama, aliendelea kupiga hatua kwenda mbele, na hata alipoitwa, hakugeuka.
“Simama hapo,” alisema polisi mmoja.
“Kuna nini?”
“Tunahitaji kukuchunguza!”
“Ili?”
“Tunahisi umebeba madawa yya kulevya!”
“Nimebeba madawa ya kulevya?”
“Ndiyo! Twende kwenye chumba kile,” alisema polisi mmoja na polisi wengine watatu kuongezeka.
Matamshi hakuonekana kuwa na hofu, alijua kabisa kwamba hakuwa muuzaji wa madawa ya kulevya, hakuwahi kuyatumia, hakutaka kupinga, akaondoka nao na kwenda kwenye chumba kimoja na kukaa huko.
Polisi wale wakaanza kuangalia mizigo yake, hakukuwa na kitu. Hapo ndipo walipoanza kulipekua begi lile alilopewa na mzee yule. Muda wote Matamshi alikuwa akitabasamu, alijijua kwamba alikuwa mtu msafi na hakuhusika kabisa na biashara hiyo haramu.
“Umejitetea sana kwamba hujabeba madawa ya kulevya, na haya ni nini?” aliuliza polisi mmoja huku akitoa mfuko wa madawa ya kulevya, Matamshi akapigwa na mshtuko, hakuamini kuona mzigo wa madawa ya kulevya ukitolewa ndani ya begi.
“Hapana! Huo mzigo siyo wangu! Ni wa mzee aliyeniambia nimbebee,” alijitetea huku macho yakiwa yamemtoka.