Geofrey Nyang'oro
AFYA ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari, Dk Steven Ulimboka imeanza kuimarika ingawa bado amelazwa katika Chumba cha Wanaohitaji Uangalizi Maalumu (ICU).
Dk Ulimboka alipelekwa Afrika Kusini Juni 30, mwaka huu baada ya jopo la madaktari lililokuwa likimtibu, likiongozwa na Profesa Joseph Kahamba kutoa taarifa za kubadilika ghafla kwa afya yake na kupendekeza apelekwa nje ya nchi kwa ajili ya vipimo na matibabu zaidi.
Jana, Katibu wa Jumuiya ya Madaktari, Dk Edwin Chitage alisema taarifa walizokuwa nazo zinasema: "Afya mwenyekiti wetu imeanza
kuimarikia, lakini bado yupo katika chumba cha wagonjwa mahututi kwani alikuwa naumwa sana."
Katika hatua nyingine, Dk Chitage alisema madaktari na wananchi wa kawaida wanaendelea kutoa mchango wa awamu ya pili
unaolenga kukusanya Dola za Marekani 30,000 kwa ajili ya kulipia gharama za matibabu za Dk Ulimboka.
"Sijapata kiwango sahihi kilichokusanywa hadi sasa, lakini michango inaendelea vizuri. Madaktari na wananchi wanaendelea kukusanya na tunawashukuru," alisema Dk Chitage.
Madaktari na ndugu wa Dk Ulimboka kwa pamoja, walikataa ofa iliyokuwa itolewe na Serikali ya kulipia gharama za matibabu za
mgonjwa huyo wakiishutumu kuhusika na tukio la kutekwa, kupigwa na kutupwa katika Msitu wa Pande kwa mwenyekiti huyo wa jumuiya ya madaktari.
Madaktari pia wamepinga tume ya polisi iliyoundwa na Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa
Polisi, Suleman Kova wakitaka kuundwa kwa tume huru kuchunguza tukio hilo. Hilo ni miongoni mwa madai matano ya madaktari yaliyomo katika tamko la pamoja baina yao na viongozi wa dini na wanaharakati.
Madai mengine ni pamoja na Serikali kurejea katika meza ya majadiliano na madaktari, kufuta kesi iliyofungua mahakamani dhidi ya madaktari hao, kuwarejesha kazini waliofukuzwa na Rais Jakaya Kikwete kukutana na viongozi hao kujadili chanzo cha mgogoro huo.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk. Stephen Ulimboka
Hali ya Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk. Stephen Ulimboka, aliyelazwa nchini Afrika Kusini, imeendelea kuimarika, ingawa bado yuko chumba cha wagonjwa mahututi (ICU).
Akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu jana, Katibu wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk. Edwin Chitage, alisema pamoja na kwamba bado Dk. Ulimboka yuko ICU, lakini hali yake inaendelea kuimarika.
"Tunasubiri ripoti kutoka kwa daktari anayemtibu Dk. Ulimboka ili tufahamu ni kitu gani kinachomsumbua... ingawa daktari wake amesema hajapata ridhaa kutoka kwa mgonjwa wake ya kutoa ripoti hiyo kwa jumuiya yetu," alisema Dk. Chitage.
Mapema wiki iliyopita, baadhi ya vyombo vya habari pamoja na mitandao ya kijamii, viliripoti kuwa hali yake ni mbaya na kwamba amelazwa ICU.
Kutokana na taarifa hizo kutofautiana, NIPASHE lilikwenda nyumba kwa wazazi wa Dk. Ulimboka eneo la Ubungo Kibangu, jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kupata taarifa za hali yake.
Hata hivyo, mama mzazi wa Dk. Ulimboka, alipoulizwa kuhusu hali ya mwanaye aliyepelekwa Afrika Kusini, hakuwa tayari kusema chochote kwa kudai kuwa tukio lililompata mwanaye hawezi kulizungumzia.
Mama huyo ambaye alikataa kutaja jina lake, alikuwa na hali ya wasiwasi hasa anapokwenda mtu yeyote ambaye familia haimfahamu.
Usiku wa kuamkia Juni 25, mwaka huu, Dk. Ulimboka alitekwa na watu wasiojulikana wakiwa na silaha za moto, ambao walimjeruhi vibaya ikiwemo kumngoa meno na kucha.
Kufuatia tukio hilo, madaktari wenzake walichangishana fedha, ambapo Jumamosi ya wiki iliyopita, waliamua kumpeleka nchini Afrika Kusini kwa matibabu zaidi.
WanaJF
Taarifa kutoka Afrika Kusini hospitalini alikolazwa Dr Ulimboka ni nzuri sana na za kutia matumaini.Kwa mujibu wa Katibu wa Jumuiya ya Madaktari Dr Edwin Chitage ni kwamba kwa sasa Dr Ulimboka anaweza kula chakula mwenyewe.