mkuu umemsoma Lissu au umeandika tu?
YA KAIMU JAJI MKUU
Mheshimiwa Spika,
Mahakama ya Tanzania haina kiongozi wake kamili, yaani Jaji Mkuu. Hii ni kwa sababu, tangu Jaji Mkuu Mohamed Chande Othman astaafu tarehe Mosi Januari ya mwaka huu, Rais John Pombe Magufuli hajateua Jaji Mkuu mpya kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na Jaji Mkuu Chande Othman. Badala yake, Rais Magufuli amemteua Jaji wa Rufaa Prof. Ibrahim Hamisi Juma kuwa Kaimu Jaji Mkuu.
Mheshimiwa Spika,
Ibara ya 118(4) ya Katiba yetu, Rais anaruhusiwa kuteua Kaimu JAji Mkuu iwapo itatokea kiti cha Jaji Mkuu kitakuwa wazi; au Jaji Mkuu hayupo Tanzania; na au Jaji Mkuu atashindwa kutekeleza kazi yake kwa sababu yoyote, na Rais ataona kuwa kwa muda wa tukio lolote kati ya hayo matatu inafaa kumteua Kaimu Jaji Mkuu. Kaimu Jaji Mkuu aliyeteuliwa kwa utaratibu huu “... atatekeleza kazi za Jaji Mkuu mpaka atakapoteuliwa Jaji Mkuu mwingine....”
Mheshimiwa Spika,
Pamoja na kuwapo kwa ibara ya 118(4), Kambi Rasmi ya Upinzani ya Bunge lako tukufu inaamini kwamba Rais Magufuli anavunja Katiba ya nchi yetu kwa kushindwa kuteua Jaji Mkuu kamili takriban miezi mitano tangu kustaafu kwa Jaji Mkuu Chande Othman. Hii ni kwa sababu, ibara ya 118(4) haikutungwa kwa lengo la kumwezesha Rais kuteua Kaimu Jaji Mkuu bila kikomo cha muda.
Kama ilivyo kwa sheria zote, ibara ya 118(4) ina sababu yake maalum. Ibara hiyo imewekwa kwa makusudi ya kuhakikisha kwamba kwa muda wote kunakuwa na kiongozi wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania pamoja na kiongozi wa Mahakama ya Tanzania, wakati Jaji Mkuu kamili anasubiriwa kuteuliwa. Kaimu Jaji Mkuu ni sawa ni kile kinachoitwa na wanasheria ‘interlocutory position.’ Kaimu Jaji Mkuu ni nafasi ya muda inayoshikiliwa na mtu mwenye sifa za kuwa Jaji Mkuu kabla nafasi hiyo haijajazwa na Jaji Mkuu kamili.
Swali halali linahitaji majibu ni, je, Kaimu Jaji Mkuu anastahili kuwapo madarakani kwa muda gani? Hili ni suala la tafsiri ya Katiba linalohitaji kujibiwa na Mahakama. Kwa maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, miezi mitano ni muda mrefu mno wa kuwa na Kaimu Jaji Mkuu.
Mheshimiwa Spika,
Bunge lako tukufu, kama mmojawapo wa mihimili mikuu ya dola ya Tanzania, lina kiongozi wake mkuu muda wote: Spika au Naibu Spika. Serikali, kama mhimili mwingine mkuu, ina kiongozi wake mkuu muda wote: Rais au Makamu wa Rais. Kwa Mahakama ya Tanzania, mhimili mkuu wa tatu wa dola ya Tanzania, kutokuwa na kiongozi wake kamili miezi mitano baada ya kustaafu kwa Jaji Mkuu Chande Othman, kunatoa taswira potofu kwamba Mahakama ina hadhi hafifu au ya chini ikilinganishwa na mihimili mingine mikuu ya dola ya Tanzania.
Kitendo hiki vile vile kinatoa taswira potofu kwamba pengine Kaimu Jaji Mkuu wa sasa hatoshelezi nafasi hiyo; au kwamba miongoni mwa Majaji wote wa Rufaa au wa Mahakama Kuu ya Tanzania au mawakili na wanasheria wengine wa nchi hii pamoja na wale wa nchi za Jumuia ya Madola hakuna hata mmoja wao mwenye uwezo au sifa za kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania.
Kambi Rasmi ya Upinzani ya Bunge lako tukufu inamtaka Mheshimiwa Waziri amshauri Rais Magufuli, kwa heshima zote anazostahili, amthibitishe Kaimu Jaji Mkuu Prof. Juma katika nafasi hiyo au, vinginevyo, ateue mwanasheria mwingine anayemwona ana sifa za kuwa Jaji Mkuu kamili wa Tanzania. Hali ilivyo hivi sasa inawatia aibu wanasheria wote wa Tanzania na inaitia aibu nchi yetu katika jumuia ya kimataifa.