China inasaidia vipi wahitimu wa vyuo kupata ajira na kujiajiri?

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,036
VCG111280014322.jpg

Kiwango cha ukosefu wa ajira kwa vijana wenye umri wa miaka 16 hadi 24 ambacho kimekuwa kikiongezeka sana duniani kinaleta changamoto kubwa kwa hivi sasa. Kwa mujibu wa ripoti ya Kamisheni ya Ulaya, mwaka 2021 kiwango cha vijana wasiokuwa na ajira barani Ulaya kilipanda hadi asilimia 16.6. Vijana ndio kundi la watu wanaoathirika vibaya zaidi kwa kupoteza kazi katika kipindi cha janga la UVIKO-19.

Mwaka huu nchini China, idadi ya wahitimu waliomaliza chuo kikuu imekuwa kubwa na kufikia milioni 10.76, ambayo imefanya ushindani wa kupata ajira kuwa mkubwa zaidi kuliko hapo awali. Kwa mujibu wa Idara ya Takwimu ya Taifa ya China, mwezi Juni mwaka huu, vijana wasiokuwa na ajira wenye umri wa kuanzia miaka 16 hadi 24 wanachukua asilimia 19.3, ambayo inaonekana kuwa mbali sana na kiwango cha wastani cha mijini kikiwa kimepungua hadi asilimia 5.5.

Kwa maana hiyo ni wazi kwamba vijana wanakabiliwa na changamoto kubwa sana hasa linapokuja swala la kutafuta ajira. Kuna mambo kadhaa yanayochangia kufanya changamoto hizi za kutafuta ajira kuwa kubwa kwa vijana wa China hasa katika miaka ya karibuni. Mambo hayo ni pamoja na athari za janga la UVIKO-19, ujuzi usiolingana kwenye soko la ajira, lakini jambo kubwa na la msingi zaidi linaloathiri ajira kwa vijana ni ukuaji wa uchumi, kwani tunafahamu kuwa watu wengi wanaweza kupata kazi endapo uchumi wa nchi utakuwa.

Ili kukabiliana na changamoto hizi, je China inafanya nini? Kwa hapa China, Pato la Taifa likiongezeka kwa asilimia moja tu basi zitapatikana nafasi za ajira karibu milioni 1.5. Ndio maana kwanza mwaka huu China imetilia maanani zaidi katika kutuliza uchumi.

Mwaka 2021, katika mkutano mkuu wa kazi za kiuchumi unaofanyika kila mwaka, China ilisisitiza kuwa kuna haja ya kuboresha ukuaji wa uchumi ili kuongeza nafasi za ajira katika mwaka 2022. Hivyo mwezi Mei China ilitoa kifurushi chenye hatua 33 za kutuliza uchumi, kikiangalia maeneo ya fedha, matumizi na ugavi. Katika mwezi huohuo, Baraza la Taifa la China lilitangaza hatua za kina za kuongeza ajira kwa vijana, zikigusia sekta mbalimbali ikiwemo ya makampuni madogo na ya kati.

Kwa sasa, hapa China makampuni milioni 140 yakiwemo madogo na ya kati yanatoa zaidi ya asilimia 85 ya fursa za ajira. Kwa hiyo makampuni haya ni muhimu sana katika soko la ajira. Lakini swali la kujiuliza hapa ni je, makampuni haya yanahamasika vipi kuajiri vijana wahitimu? Tukirudi kwenye hatua za kina za kuongeza ajira kwa vijana zilizotangazwa na China, katika sehemu ya kwanza imeonesha kwamba inataka kuongeza ajira kwa kutoa njia imara na madhubuti zaidi, kama vile kuyasaidia makampuni madogo na ya kati ambayo yataajiri wahitimu wa vyuo vikuu, kwa kuyapa ruzuku au kupunguziwa kodi. Lakini tunaona kwamba haya yote yanaweza kutimia hadi pale makampuni haya yatakapokuwa makubwa na kutengeneza fedha zaidi. Kwa hiyo serikali bado inahitaji kufanya juhudi zaidi ili kuyasaidia makampuni haya kufufuka kutokana na athari za UVIKO-19, na kurejesha uzalishaji wake wa kawaida.

Hiki ndio kitu ambacho serikali imekuwa ikizingatia zaidi tangu mwaka jana. Matokeo yake hatua nyingi mfululizo zikiwemo kutoa fedha za uokoaji au kupunguza gharama ya uendeshaji na kodi zimetangazwa sasa.

Mbali na hapo hatua hizi za kuwanusua vijana na changamoto za ajira, pia zina kipengele cha wahitimu kujishughulisha na ujasiriamali, ambapo serikali imetenga fedha kwa ajili wahitimu hawa kuanzisha biashara zao, kuwapa punguzo la mikopo na kuwapa maeneo ya kuanzisha ofisi kwa bei nafuu au hata bure.

Hivi karibuni Shirika Kuu la Utangazaji la China CMG likishirikiana na wizara na idara saba za taifa ikiwemo Wizara ya Elimu ya China zimezindua "Hatua ya Kitaifa ya Ajira", ili kuwasaidia wahitimu wa vyuo vikuu kupata ajira sahihi mtandaoni. Kwa mtazamo wangu, mpango huo wa "Hatua ya Kitaifa ya Ajira" unaweza kuhamasisha rasilimali zaidi za serikali, nguvu za kijamii, makampuni, na vyuo vikuu kujiunga na kutoa urahisi kwa wanaotafuta kazi.

Tukitupia jicho barani Afrika, ingawa takwimu zilizotolewa na Shirika la Kazi Duniani (ILO), ambazo zinaonesha kwamba Afrika ina kiwango kidogo cha ukosefu wa ajira duniani kwa vijana wenye umri kati ya miaka 15 na 24, ambacho ni asilimia 10.6, lakini tunaona kuwa wengi wao wanafanya kazi zisizo rasmi na wengi hawana ajira ama wanakuwa masikini kutokana na kufanya kazi zenye mshahara mdogo sana na kuwepo kwa sulala la ukosefu wa usalama kwenye jamii. Hivyo inafanya iwe vigumu kulinganisha soko la ajira la nchi za Afrika na nchi zilizoendelea kiuchumi.

Kwa hiyo serikali za Afrika na washirika wa maendeleo wamejaribu kushughulikia changamoto ya ajira, hasa kwa kutekeleza programu za kukuza ujuzi wa kupata ajira katika sekta zilizopewa kipaumbele kama vile kilimo na viwanda, na kukuza ujasiriamali katika maeneo haya. Vijana waliojiandikisha katika programu hizo hujifunza ujuzi wa kiufundi na ufundi stadi, pamoja na stadi nyingine za maisha ili kuwasaidia kupata ajira na kuendesha biashara zao wenyewe.

Lakini kujikita kwenye suluhisho hili pekee, kutawatenga vijana ambao hawana mwelekeo wa ujasiriamali, pamoja na wale walio na ujuzi na uwezo mwingine ambao unaweza kukuzwa kwa njia mbadala za usaidizi. Msukosuko wa ajira kwa vijana barani Afrika ni wa muda mrefu.

Hivyo suluhisho linalofaa kuondoa tatizo hili ni kushughulikia mzizi wake, ambao kama nilivyotaja hapo awali kuhusu China inavyoshughulikia tatizo la ajira, ni muhimu kusimamia ukuaji wa uchumi pamoja kutuliza uchumi. Kama inavyofanya China, naona hata na nchi za Afrika pia zinahitaji kuhakikisha zinakuza na kutuliza uchumi wake ili kuwakwamua vijana wengi zaidi ambao wanateseka wanapokwenda kutafuta ajira.
 
Back
Top Bottom