• Yamuomba akaokoe jahazi Nzega
na Kulwa Karedia
CHAMA chama Mapinduzi (CCM), kimegeuka kuwa kigeugeu baada ya kumwangukia aliyekuwa Mjumbe wa Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM) na Mjumbe wa Halmashauri Kuu (NEC), Hussein Bashe, kikimtaka akasaidie kukipigia kampeni katika jimbo la Nzega mkoani Tabora. Habari za kuaminika zilizopatikana kutoka Nzega na Dar es Salaam jana, zinasema CCM imeteua zaidi ya makada 20 katika jimbo hilo, kwa ajili ya kukinadi chama hicho ambacho kinaonekana kupata wakati mgumu.
Bashe ambaye alitangazwa na CCM hivi karibuni na kuvuliwa nyadhifa zote na Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), kisha kutangazwa na Katibu wa Itikadi na Uenezi Taifa wa chama hicho, Kapteni John Chiligati, kuwa si raia, kunaibua maswali mengi kama uamuzi huo, ulikuwa sahihi.
Bashe ambaye alishinda kura za maoni kwenye jimbo la Nzega, lililokuwa likishikiliwa na Lucas Selelii, (CCM) na ushindi wake kupewa Dk. Hamisi Kigwangala ambaye amepitishwa rasmi kupeperusha bendera ya chama katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Akitangaza uamuzi huo, baada ya kumalizika kwa kikao cha NEC cha mchujo wa wagombea ubunge na Baraza la Wawakilishi, Chiligati, alisema CCM imeamua kumtimua Bashe uanachama na kumuengua kuwania ubunge katika jimbo la Nzega, baada ya kubaini kuwa ni raia wa Somalia.
Alisema uchunguzi uliofanywa na chama hicho kwa kushirikiana na Idara ya Uhamiaji, umebaini kuwa Bashe licha ya kuzaliwa nchini, ni raia wa Somalia na hajaukana uraia wake.
"Bashe sio raia wa Tanzania, alikuwa akiishi kwa mazoea tu. Tulipojaribu kutafuta uraia wake kwa kuwashirikisha watu wa Uhamiaji, walituthibitishia kuwa sio raia, licha ya kuzaliwa nchini na alikuwa akiishi kwa mazoea tu. Hii ni kama iliyowahi kumtokea Jenerali Ulimwengu na ndivyo ilivyo kwa Bashe," alisema Chiligati.
Kwa mujibu wa barua ya Agosti 30, mwaka huu iliyosainiwa na Bagaile B. Lumola na nakala kupelekwa kwa Katibu wa CCM Mkoa wa Tabora, inasoma hivi "Nachukua fursa hii kukupongeza kwa dhati kuwa Kamati ya Siasa ya Halmashauri Kuu CCM Wilaya imekuteua kuwa mpiga kampeni za ubunge kama ulivyopangiwa.
Kwa barua hii nakuomba uwe tayari kupokea maagizo yatakayokuwa yakitolewa kutoka ngazi mbalimbali, pia uzingatie ratiba ya jimbo ulilopangiwa. Pia nakuomba ufike ofisi ya CCM Wilaya Septemba mosi, mwaka huu kwa ajili ya uzinduzi wa kampeni jimbo la Nzega, aidha jimbo la Bukene itakuwa Septemba 4, mwkaa huu.
Nakutakia afya njema na familia yako kwa ujumla ili tukijenge chama chetu na "ushindi ni lazima".
Habari zaidi zinasema mbali ya Bashe, kujumuishwa kwenye kampeni hizo, wamo pia makada 19 pamoja na aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, aliyebwagwa kwenye kura za maoni, Lucas Selelii.
Katibu Mkuu wa CCM, Yusuf Makamba, alipotakiwa kutoa ufafanuzi na gazeti hili, alisema yeye anatambua wazi Bashe bado ni mwanachama wao halali, hivyo viongozi wa mkoa wa Tabora wana haki ya kumtumia pale panapohitajika.
"Kama Katibu wa Mkoa wa Tabora amemteua, ana haki ya kufanya hivyo, anatambua mchango wake ndani ya chama… hata kama kuna makada 20, kumbuka ndugu yangu hata kanisani utasikia kuna askofu, padri, mchungaji, shemasi, katekista na wazee wa kanisa… hivyo hata CCM tunao wa aina hii,
… kama hilo suala limefikiwa basi ni jema, nadhani wamegundua namna mchango wake unavyotambulika ndani ya chama," alisema Makamba.
Kwa upande wake, Bashe alipotafutwa kwa njia ya simu na gazeti, alikiri kusikia tetesi hizo ingawa barua rasmi haijamfikia mkononi mwake.
"Duh kaka hamniachi? Hiyo ndiyo nasikia kwako sijapata barua, lakini ufahamu huu ni wajibu wangu kukisaidia chama nikiwa mwanachama kimeniomba lazima nikisaidie kwa kuwa hilo ni jukumu langu, kwa hiyo tunasuburi barua ikinifikia nitaenda kukisaidia, kuhusu kauli ya mzee Makamba nashukuru alichokisema ndiyo ukweli siku zote nimekuwa mwanachama na nitaendelea kuwa mwanachama mwaminifu na mkweli wa CCM," alisema Bashe.