Fred Katulanda
JF-Expert Member
- Apr 1, 2011
- 374
- 509
Nchini Tanzania ni kama maeneo mbalimbali barani Afrika, kumekuwa na ufugaji wa nyuki kwa ajili ya uvunaji wa mazao yake ili kujipatia fedha lakini bahati mbaya kumekuwa na uvunaji wa mazao machache huku mazao mengine yakiwa hayajulikani.
Kwa ufugaji wa kisasa Nyuki huvunwa mazao sita ambayo ni Asali (Honey), Nta (Wax), Chavua (Pollen), Gundi ya Nyuki (Propolis), maziwa ya nyuki (Royal Jelly) pamoja na Sumu ya nyuki (Bee Venom). Hapa katika makala haya, nitazungumzia zaidi uvunaji wa zao la Sumu ya Nyuki kwa kirefu ambao ninaufanya katika shamba langu (Nyuki Farming).
Ukweli zao hili halifahamiki sana kwa wafugaji wengi kutokana na kukosa maarifa ya uvunaji sambamba na mazao ya Asali na Nta ambayo yamezoeleka zaidi.
Sumu ya Nyuki huvunwa kwa wiki moja mara mbili yaani unapovuna mzinga moja siku moja hunauacha mpaka siku ya nne unarudia tena kuuvuna. Mfano ukivuna leo (Jumapili), unauacha mpaka Jumatano kisha Alhamisi unarudia kuvuna, wakati Asali huvunwa kwa mwaka mara mbili tu.
Sasa ili kuivuna sumu mfugaji hulazimika kuwa na mashine maalumu kwa ajili hiyo ambayo sehemu ya kifaa chake kiitwacho Plate hutegeshwa katika mlango wa mzinga au juu yake baada ya kuondoa mfuniko wa mzinga kuwashawishi nyuki kutoka kushambulia wakiamini ni adui hivyo kuacha sumu hiyo ambayo baadaye hukusanywa kwa utaratibu maalum na kuhifadhiwa tayari kwa kuuzwa.
Katika mzinga mmoja mfugaji anaweza kuvuna kiasi cha 0.20 hadi 0.85 ya gramu mmoja lakini ikitegemea ukubwa wa kundi la nyuki waliomo ndani yake na namna ya uvunaji.
Wakati Asali huuzwa kwa kipimo cha kilo moja (sawa na gramu 1,000), sumu huuzwa kwa kipimo cha gramu mmoja kwa zaidi ya bei ya asali.
Sumu ya Nyuki ni nini?
Sumu ya nyuki ni kemikali asili au tindikali isiyo na rangi, ambayo hutengenezwa na kuhifadhiwa ndani ya mwili wa nyuki na wao huitumia kwa kujilinda na maadui wao kwa kuwashambulia pale wanapohisi kuvamiwa.
Sumu hii hutolewa na nyuki kwa njia ya mwiba wake (Stingers) uliopo nyuma ya mwili wake wakati wanaposhambulia maadui baada ya kuvamiwa. Sumu hii inapoingia kwenye mwili wa adui husababisha maumivu makali kutokana na vichochezi ilivyonavyo
ambavyo ni Phospholipase A2, Enzyme na Allergen kuu ambayo husababisha huathiri kwa kushambulia seli za adui.
Hata hivyo kulingana na tafiti mbalimbali kiasi cha vichochezi vilivyomo ndani ya sumu licha ya kuwa na athari inayosababisha maumivu hasa kwa binadamu anapoumwa na nyuki, ilibainika vimekuwa mali ya faida kwa binadamu hivyo kuifanya sumu ya nyuki kuwa bidhaa muhimu kwa matumizi ya kibinadamu. Umuhimu huu pia umechochea kuongezeka kwa matumizi yake na hivyo
kuwalazimu watalaamu kubuni teknolojia ya kuvuna sumu hiyo.
Uvunaji wa Sumu hufanyikaje?:
Ili kuvuna sumu ni lazima mfugaji awe na mizinga ya nyuki yenye makundi makubwa na waliyokaa ama kuishi ndani yake muda mrefu walau isiwe chini ya miezi mitatu, awe na mashine ya kuvunia, chupa ya kutunzia pamoja na jokofu kwa ajili ya kuhifadhi sumu hiyo kabla ya kuiuza au kuipeleka sokoni. Sumu hii pamoja na kwamba hutolewa ikiwa kimiminika (Liquid) lakini inapovunwa huwa hutoka ikiwa unga (Powder) ambao unapaswa kutunzwa kwa makini kwa kuukinga na joto kali, mwanga wa jua na maji, hivyo sumu hii hutunzwa kwenye chupa maalumu isiyoruhusu mwanga wa jua na huihifadhi kwenye jokofu kwa muda ambao kusafirishwa au kupelekwa sokoni. Ikitunzwa vyema kwa kuzingatia utaratibu hukaa muda mrefu hata zaidi ya mwaka.
Sifa za Sumu ya Nyuki:
Mfugaji anapoivuna sumu hii anapaswa kuhakikisha inakuwa safi na alazima ajiepushe na kuichanganya na kitu chochote na ili kuweza kuiuza ni lazima iwe na rangi nyeupe au brownish. Sumu ikiwa na rangi nyeusi wala majimaji huwa imeharibika hivyo kupoteza sifa sokoni.
Matumizi ya Sumu ya Nyuki:
Hutumika katika tiba ya kuzuia magonjwa na maumivu (API Therapy), ingawa hivi karibuni imepata umaarufu zaidi, tiba ya sumu ya nyuki imekuwa ikitumika katika mazoea ya dawa za jadi kwa miaka mingi. Kwa sasa sumu hii hutayarishwa sindano za kinga za mwili kwa magonjwa ambazo zimekuwa zikisimamiwa na wataalamu wa huduma za afya na pia zimekuwa ikiongezwa katika utayarishaji wa bidhaa kama vile Moisturizers, Lotions na Lozenges ikiwa sehemu ya virutubisho na viboreshaji.
Unaweza kusoma moja ya makala zangu zingine hapa jamiiforums kama; Fahamu mbinu ya kugawa makundi ya nyuki uliyonayo kujaza mizinga mipya isiyo na nyuki
Utegaji Nyuki waingie kwenye mzinga