nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Caption Meneja Mkuu wa Kiwanda cha Viberiti cha Kibo Match Group Ltd, cha mjini Moshi, Sheriff Babu akitoa taarifa kwa mbunge wa viti maalumu kupitia Chadema Lucy Owenya, ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Viwanda, Biashara na Masoko aliyetembelea kiwanda hicho. (Picha na Daniel Mjema)
Daniel Mjema, Moshi
RAIA wa India, Sheriff Babu ameshangazwa na hatua ya viwanda vilivyojengwa kwa mabilioni ya dola za Marekani mkoani Kilimanjaro kufa wakati utafiti alioufanya unaonyesha vinaweza kufufuliwa na kuchangia uchumi wa nchi.
Babu ambaye ni Meneja wa Kiwanda pekee cha viberiti nchini cha Kibo Match Group, cha mjini Moshi alitoa somo kwa serikali namna ya kuviwezesha viwanda hivyo kufufuliwa kama wawekezaji waliouziwa wana dhamira ya dhati ya kuvifufua.
Raia huyo wa kigeni alisema kama atakabidhiwa viwanda hivyo ana uwezo wa kuvifufua na kuanza uzalishaji ndani ya mwaka mmoja ili mradi tu serikali ikubali nayo kubeba jukumu lake la kujenga mazingira mazuri ya uwekezaji.
Moja ya mambo ambayo raia huyo wa India alitaka serikali ifanye ni kubadili sera ya uwekezaji ili msamaha wa kodi wa miaka mitano (tax holiday) wanaopewa wawekezaji wapya nchini ili uwanufaishe pia wale wanaotaka kufufua viwanda.
"Kwa viwanda hivi vya mkoani Kilimanjaro, wala sihitaji msamaha wa kodi wa miaka mitano wanipe miaka miwili tu, viwanda vyote hivi vilivyokufa vitafufuka, nchi imelalia mabilioni ya dola hapa Kilimanjaro,"alisema kwa uchungu raia huyo wa India.
Sharti lingine ni kwa serikali kutoa mtaji wa uanzishaji uzalishaji na kubeba mzigo wa madeni yote ya nyuma ya viwanda hivyo ikiwamo michango ya NSSF na mafao ya watumishi ili viweze kuanza upya katika mazingira ya sasa.
Babu alikuwa akitoa taarifa ya changamoto zinazokikabili kiwanda cha viberiti cha Kibo Match kwa Waziri kivuli wa Viwanda, Biashara na Masoko, Lucy Owenya aliyetembelea viwanda kabla ya Bunge la bajeti mwezi ujao.
Mbali na mapendekezo yake hayo, Babu alisema kama serikali haitakuwa na uwezo wa kutoa mtaji basi, iwezeshe kupitia Benki ya Rasilimali (TIB) viwanda vikopeshwe mkopo wenye masharti nafuu utakaolipwa kwa muda mrefu.
Miongoni mwa viwanda alivyosema vinaweza kuanza uzalishaji sasa ni Interchem Pharm Limited (IPL) ambacho kina uwezo wa kuzalisha asilimia 60 ya mahitaji yote ya dawa nchini ambacho sasa kimefilisika na kimetangazwa kuuzwa kwa zabuni.
Viwanda vingine ni Kilimanjaro Machine Tools (KMT), Pestside Industries na Kiwanda cha Magunia (TBC) ambacho baadhi ya mitambo yake imeondolewa kiwandani.