Aliyemburuza mbunge kortini achomewa gari

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Monday, 12 December 2011 20:37


Hawa Mathias, Mbeya

MWENYEKITI wa Kijiji wilayani Mbarali Mkoa wa Mbeya, (jina linahifadhiwa) ametiwa mbaroni kwa tuhuma za kuchoma moto gari la Ofisa Mtendaji wa Kata ya Ruiwa, Jordan Masweve.

Ofisa Mtendaji aliyechomewa gari ni yule aliyemshtaki mbunge wa Mbarali kupitia CCM, Dickison Kilufi kwa kutishia kumuua.Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Advocate Nyombi, alisema polisi walimkamata mwenyekiti huyo Desemba 11, mwaka huu kijijini hapo baada ya kuhusishwa na tukio la kuchoma moto gari hilo.

Nyombi alisema pamoja na kumkamata Polisi wanaendelea kumhoji mtuhumiwa huyo kwa tuhuma hizo.
Alisema mbali ya mtuhumiwa huyo, polisi wanapeleleza zaidi ili kuwakamata watuhumiwa wengine waliohusika katika tukio hilo.Kilufi alihukumiwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Mbeya kulipa faini ya Sh500,000 baada ya kupatikana na hatia na kunusurika kwenda jela miezi 10.

Kamanda wa Polisi alisema gari la Ofisa Mtendaji lililochomwa moto ni aina ya Canter lenye namba za usajili T 57 BFD

Inadaiwa kuwa Desemba 10, mwaka huu, watu watatu wasiojulikana walivamia nyumbani kwa ofisi huyo usiku wa manane na kulichoma moto gari hilo.

Moto huo ulizimwa na majirani waliosikia kelele za yowe kuomba msaada zilizopigwa nyumbani kwa Ofisa Mtendaji huyo_Ofisa Mtendaji alisema familia yake ilishtuka mlio mkubwa wa kupasuka kwa tairi lililokuwa likiwaka na kwamba ndipo walipoamka na kulikuta gari likiungua.

Majirani walifanikiwa kuzima moto kabla ya kusambaa na kuunguza nyumba.Wakati huohuo, mkazi wa Kijiji cha Mahango, Kata ya Ruiwa wilayani Mbarali, Bariki Sanga (30), amekutwa ndani ya shimo la choo huku maiti yake ikiwa imenyofolewa viungo vikiwamo sikio, ulimi na sehemu za Siri.

Maiti hiyo ilikutwa ikiwa imeharibika vibaya na kuuzikwa kando ya nyumba iliyo karibu na choo hicho.
Maiti ya Sanga ambaye alikuwa ametoweka kwa kipindi cha zaidi ya wiki mbili nyumbani kwake, ilikutwa kwenye choo hicho Desemba 11, mwaka huu majira ya saa 10 jioni ikiwa imewekwa kwenye gunia na kufungwa na nguo.

Mwenyekiti wa kijiji hicho, Witson Kazimoto aliwataka wananchi kushirikiana na Jeshi la Polisi kumkamata mtu anayedaiwa kuonekana kwa mara ya mwisho na Sanga ambaye walikubaliana kwenda kulangua mpunga.

Alisema kabla ya kuuawa, Sanga alikuwa na Sh600,000 ambazo hazijulikani zilipo. Kamanda wa polisi Mkoa, Nyombi amethibitisha kutokea kwa mauaji hayo na kusisitiza kuwa polisi wanawashikilia watu wawili kwa tuhuma za kuhusika nalo.



 
Back
Top Bottom