Ziara ya Bw. Wang Yi barani Afrika na Latin Amerika yaonesha kuwa China inaendelea kupanua ushirikiano wa kunufaishana duniani

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,036
1706076942060.png

Waziri wa mambo ya nje wa China Bwana Wang Yi, amemaliza ziara ya kidiplomasia ya mwaka huu kwa kuzitembelea Misri, Tunisia, Togo na Cote d'Ivoire, ikiwa ni sehemu ya desturi ya zaidi ya miongo mitatu kwa waziri wa mambo ya nje wa China kufanya ziara ya kwanza barani Afrika. Lakini safari hii Bwana Wang Yi pia amefanya ziara nchini Brazil na Jamaica, na kufanya baadhi ya watu waanze kuwa na maswali, kwenye ongezeko hili ambapo huko nyuma halikuwepo.

Kuanzia Januari 13 hadi 22, waziri wa mambo ya nje wa China Bwana Wang Yi alifanya ziara yake ya kwanza akitembelea bara la Afrika na nchi za Latin Amerika. Hii ni mara ya kwanza kwa waziri wa mambo ya nje wa China kufanya ziara ya kwanza kwa mtindo huu, na kuacha maswali kwa baadhi ya watu.

Ikumbukwe kuwa katika miaka ya hivi karibuni hadhi ya China kwenye jukwaa la kimataifa imeendelea kuinuka, na inaendelea kuwa na ushawishi thabiti kwenye siasa za kimataifa. Tunakumbuka kuwa uhasama kati ya Saudi Arabia na Iran ambao ulikuwa na hatari ya kubadilika kuwa mgogoro, umekwisha na hata nchi hizo mbili kurudisha uhusiano wa kibalozi kutokana na juhudi za China.

Kinachofuatiliwa zaidi na wachambuzi wa mambo ya kidiplomasia kuhusu ziara ya safari ya Bwana Wang Yi, ni diplomasia ya uchumi inayoendeshwa na China. Mara nyingi ziara za maofisa wakubwa kama waziri wa mambo ya nje wa nchi kubwa, huwa zinafanyika kwenye nchi kubwa, lakini kwenye nchi ndogo mara nyingi tunaona maofisa wa ngazi za chini wakifanya ziara kwenye nchi hizo. Mara zote China imekuwa ikisema inaheshimu nchi zote na kuzichukulia nchi hizo kwa usawa, ndio maana tunaweza kuona kuwa Waziri Mkuu Wang Yi amefanya ziara nchini Togo na Jamaica.

Inatakiwa ikumbukwe kuwa baadhi ya nchi kutokana na hali za kijiografia, kidemografia, na hata kiuchumi zinawekwa pembezoni na nchi kubwa duniani, lakini kutokana na ukaribu na China, nchi hizo zinakuwa na fursa ya kutembelewa na maofisa waandamizi wa China na hata kupanga mipango ya maendeleo na hata kujadili mambo ya ushirikiano na maofisa wakubwa. Ziara ya Waziri Wang Yi inatakiwa kuangaliwa kwenye muktadha huu na malengo ya kidiplomasia ya China kwa mwaka huu, ambayo ni kuhimiza maendeleo.

Pamoja na nchi za Afrika na Latin Amerika kuwa na ushirikiano wa muda mrefu sana na nchi za magharibi, hasa nchi za Ulaya, hali halisi ni kuwa nchi za magharibi kutokana na changamoto mbalimbali za sasa, hazijawa na msaada mkubwa kwa nchi za Afrika, na badala yake zimekuwa zikileta changamoto kwa nchi hizo. Lakini China inaendelea kuwa mdau mkubwa wa maendeleo kwa hizo, ikiwa ni chanzo muhimu cha mikopo na fedha za maendeleo, uwekezaji na hata masoko.

Lakini pia tukumbuke kuwa China ikiwa ni nchi kubwa zaidi na yenye maendeleo zaidi kati ya nchi za kusini, ina wajibu wa asili wa kuzishika mkono nchi za kusini. Kwa sasa nchi nyingi za kaskazini zinaonekana kuwa katika wingu la mgogoro Russia na Ukraine, suala la maendeleo ni kama limewekwa pembeni. Kama nchi za Kusini zingetegemea nchi za kaskazini pekee kuwa wadau wake wa maendeleo, basi ina maana kuwa maendeleo yao yangesubiri hadi mgogoro huo umalizike ndipo zikumbukwe. Uwepo wa China na sera yake ya kidiplomasia, inaweza kuwa jambo la bahati nzuri kwa nchi nyingi za kusini.
 
Back
Top Bottom