Date::12/2/2008
Masha atetea Magereza kuhusu Mramba, Yona
Na Ramadhan Semtawa
Mwananchi
KITENDO cha mawaziri wawili wa zamani kutolewa gerezani bila ya hati ya kuitwa mahakamani kimezua mjadala mkubwa kwa wadau mbalimbali, lakini Waziri wa Mambo ya Ndani, Lawrence Masha amelitetea Jeshi la Magereza kuwa halikuwapeleka mahakamani watuhumiwa hao.
Hakimu Hezron Mwankenja juzi alikataa kushughulikia dhamana ya mawaziri hao, Basil Mramba na Daniel Yona akidai kuwa walipelekwa mahakamani bila ya amri ya dharura ya kupelekwa mahakamani kwa ajili ya kushughulikiwa dhamana yao na hivyo kuwafanya vigogo hao kurejeshwa gerezani.
Wakati Hakimu Mwankenja akikataa kushughulikia dhamana hiyo, Mramba na Yona walikuwa kwenye gari lililokuwa nje ya mahakama wakisubiri kuitwa ndani, lakini wakajikuta wakirejeshwa tena rumande, hali iliyozua majadala juu ya nani aliwatoa vigogo hao Gereza la Keko na kuwasafirisha hadi Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Kisutu.
Jana, Waziri Masha, ambaye alitembelea gereza la Keko siku moja baada ya mawaziri hao kulazwa humo akisema kuwa alikuwa kwenye moja ya shughuli zake za kikazi licha ya kwamba alitumia gari binafsi, alisema watuhumiwa hao walikwenda Kisutu kuunganishwa na wenzao ili warudishwe Keko.
"Naomba ieleweke wazi kwamba, watuhumiwa hawakuwa wamepelekwa Kisutu kupandishwa kizimbani, walifikishwa pale ili waunganishwe na wenzao kurejea Keko... ninachosema magereza iko makini, ina mfumo imara haiwezi kutoa watuhumiwa bila taratibu," alifafanua Masha.
Waziri Masha alikiri kwamba watuhumiwa hao hawakuwa na kibali cha kuwafikisha mahakamani Kisutu kwani haikuwa siku ya kusikilizwa dhamana yao.
Hata hivyo, akifafanua zaidi alisema watuhumiwa hao walikuwa na kibali cha kufikishwa Mahakama Kuu kwa ajili ya taratibu za kumaliza dhamana zao.
"Kama mnavyojua, bado kuna taratibu za dhamana zilikuwa hazijakamilika Mahakama Kuu, sasa wao walikuwa na kibali cha Mahakama Kuu na si Kisutu," alifafanua waziri huyo.
Waziri Masha alisema uamuzi wa hakimu (Hezron Mwaikenja), kusema hakukuwa na kibali cha kuwafikisha watuhumiwa hao mahakamani hapo, ulikuwa sahihi.
"Ndiyo maana hakimu akasema hakukuwa na kibali cha kuwafikisha watuhumiwa hao mahakamani hapo, ni sahihi kwani hawakuwa wamekwenda kupandishwa kizimbani," alisisitiza Masha.
Afisa habari wa Magereza, Omar Mtiga alisema uamuzi wa kuwapeleka akina Mramba na Daniel Yona, si mpya.
Mtiga alifafanua kuwa kutokana na uhaba wa magari, si rahisi kumsafirisha kila mtuhumiwa ndiyo maana waliwachukua watuhumiwa hao na kuwapeleka Kisutu ili wakaunganishwe na wenzao ambao wanatuhumiwa kama mtandao wa wizi katika mabenki.
"Si mara ya kwanza, wakati mwingine watuhumiwa wa Kinondoni wanaletwa Kisutu kusubiri wenzao, sasa sijui hii imechukuliwaje lakini hawa hawakwenda kupanda kizimbani," alifafanua.
Aliongeza kwamba ndiyo maana watuhumiwa hao walikuwa katika chumba maalumu si kizimbani na hata hakimu hakusema kizimbani.
Wakati Masha na Magereza wakijisafisha, duru huru za habari kutoka serikalini zilisema suala hilo lilitikisa ndani ya serikali hadi Ikulu kutaka ufafanuzi.
Kwa mujibu wa duru hizo, Magereza ilipaswa kutoa maelezo kuhusu nini hasa kilitokea katika shitaka hilo.
"Hapa Ikulu imehitaji taarifa, wakuu wa Magereza wanaandaa kuipeleka Ikulu kueleza nini hasa kilitokea," zilisema duru huru.
Alipoulizwa Katibu Mkuu Kiongozi Philemon Luhanjo hakuwa tayari kuzungumzia na kuongeza: "Mimi siwezi chochote."
Mramba, ambaye alishika wizara nyeti katika serikali za awamu zote nne, na Yona, ambaye alikuwa waziri wa Wizara ya Madini katika serikali ya awamu ya tatu, wanatuhumiwa kutumia vibaya ofisi kwa kuipa kampuni ya M/S Alex Stewart ya Uingereza mkataba wa kudhibiti madini ya dhahabu kinyume cha sheria.
Kutokana na tuhuma hizo, wawili hao wanadaiwa kulisababishia taifa hasara ya Sh11.9 bilioni.
Wakati maofisa hao wa serikali wakitetea kitendo hicho, wadau mbalimbali wametoa maoni yao kuhusu uamuzi wa kuwapeleka mahakamani bila ya hati hiyo ya kuitwa (remove order).
Baadhi ya wananchi waliongea na Mwananchi walionyeshwa kushangazwa na kitendo hicho na kusema kuwa hali hiyo inaashiria kuna jambo fulani dhidi ya watuhumiwa hao.
Ninavyojua mimi ni kwamba mahabusu hawezi kutolewa nje bila kibali hata kama ni kwa ajili ya kupelekwa mahakamani. Utaratibu ni kwamba askari anayekwenda kumtoa ni lazima awe na kibali cha mahakama ambacho anatakiwa kukionyesha kwanza kwa mkuu wa gereza, alisema Clement Msumi mkazi wa Mabibo Makuburi.
Msumi alisema askari Magereza ni watu makini sana na kwamba hata mtoto mdogo hawezi kuelewa kuwa watuhumiwa walitolewa kimakosa, huku akisisitiza kuwa kwa vyovyote vile aliyetoa agizo la kutolewa kwao rumande na kupelekwa mahakamani atakuwa ni mtu mzito.
Naye Jackson Lyimo alisema askari wasingeweza kuwatoa mahabusu hao bila kibali kwa kuwa hata wao wanajua kuwa kitendo hicho ni hatari kwani ikitokea bahati mbaya wakapata ajali ama wakafa au wakatoroka mzigo huo unakuwa juu yao.